Sunday, January 29, 2012

Mwandishi Shafi Adam Shafi

Tanzania tuna waandishi wengi maarufu katika lugha ya ki-Swahili. Mmoja wao ni Shafi Adam Shafi, kutoka Zanzibar, ambaye anaonekana nami pichani hapa kushoto. Tulikuwa New Africa Hotel, Dar es Salaam mwaka 2004 wakati wa tamasha la vitabu.







Shafi Adam Shafi anafahamika sana kwa riwaya zake. Riwaya aliyoichapisha kwanza ni Kasri Ya Mwinyi Fuad (Tanzania Publishing House, 1978). Ilikuwa maarufu tangu mwanzo. Sikupata muda wa kuisoma. Halafu, mwaka 1980 niliondoka Tanzania, kuwenda masomoni Marekani, hadi mwaka 1986.

Baada ya kukaa Marekani miaka sita hiyo, nilivyorejea Tanzania nilifanya juhudi ya kujipatia vitabu vya ki-Swahili. Nilinunua nakala ya Kasri Ya Mwinyi Fuad tarehe 28 Oktoba, 1987, ikasainiwa na Shafi Adam Shafi tarehe 29. Nina risiti ya kununulia kitabu, kutoka Tanzania Publishing House. Kwa hivyo, nina ushahidi kuwa nimeonana na Shafi Adam Shafi mara mbili.

Ingawa mara kwa mara ninapoongelea vitabu katika blogu zangu huwa naandika kuhusu yaliyomo, na uchambuzi wangu, leo nimependa tu kuchangia kumtangaza Shafi Adam Shafi na kazi zake. Nitakapokuwa nimezisoma kazi zake, Insh'Allah, nitaweza kuandika kwa undani zaidi.

Shafi Adam Shafi ameandika pia Kuli (Dar es Salaam: Tanzania Publishing House, 1979) , Vuta N'kuvute (Dar es Salaam: Mkuki na Nyota Publishers, 1999), na Haini (Nairobi: Longhorn Publishers, 2003).

Kuna taarifa ya mahojiano ya kina baina ya Shafi Adam Shafi na Freddy Macha ambayo unaweza kuyasoma hapa.

Thursday, January 26, 2012

Africonexion: Kampuni Chipukizi

Mwaka 2002 nilisajili kampuni katika jimbo la Minnesota ambayo niliita Africonexion. Nilichagua aina ya usajili iitwayo "sole proprietorship." Yaani mmiliki na mhusika mkuu ni mimi.

Nilianzisha Africonexion kama chombo cha kushughulikia elimu kuhusu tamaduni duniani, kwa kuandika, kuchapisha, na kuuza vitabu, na kutoa mihadhara na ushauri kwa watu binafsi, mashirika, taasisi, makampuni, na kadhalika, kama ninavyoripoti mara kwa mara katika blogu zangu.


Africonexion ni kampuni ndogo sana kwa wakati huu, kwa maana kwamba sina timu ya wafanyakazi au washiriki. Lakini nimeitumia vizuri kama fursa ya kujielimisha, kwa kuzingatia kuwa elimu ni mtaji bora kuliko hata fedha. Shughuli zote ninazofanya, iwe ni kuandika au kutoa mihadhara au ushauri kwa watu binafsi, ni kama shule kwangu. Hii picha hapa kushoto ilipigwa wakati wa maonesho fulani Brooklyn Park, Minnesota.



Ninataka kuipeleka kampuni hii Tanzania na kwingineko. Nimeshaendesha warsha Dar es Salaam, Zanzibar na Pemba, Tanga, na Arusha. Pia nilishiriki maonesho ya elimu na ajira yaliyofanyika Diamond Jubilee Hall, Dar es Salaam. Hapa kushoto naonekana na wadau kwenye meza yangu. Nilishiriki maonesho hayo ili kuwapata wadau wa kujiunga nami, kwani nimejenga msingi mzuri wa uzoefu, na mtandao thabiti, huku Marekani. Lakini, kutokana na shughuli zangu, watu hao inabidi wawe wapenda vitabu na elimu kwa ujumla.

Wednesday, January 25, 2012

Mfanya usafi akamatwa akimlawiti mtoto msikitini

Habari hii inahuzunisha, nikizingatia jinsi mtoto huyu alivyohujumiwa maisha yake na haki zake za kibinadamu, nikizingatia uchungu wa mama yake, ndugu, jamaa, marafiki na wapenda haki. Habari hii inapaswa kutangazwa, ijulikane, ili angalau iwe faraja kwa mtoto huyu na mama yake, kwamba tuko tunaojali utu na haki, na tuko pamoja nao.

Habari hii imetokea msikitini. Hivi juzi, wanafunzi wa ki-Islam walipoandika waraka wakiorodhesha hujuma walizosema wanafanyiwa wa-Islam mashuleni, niliandika ujumbe kuwaunga mkono katika kulaani hujuma hizo. Soma hapa. Nilisukumwa na maadili ya kuzingatia haki, niliyofundishwa katika imani yangu ya u-Katoliki.

Sasa basi, ni muhimu wa-Islam, wa-Kristu, na wengine wote tuungane kumpigania mtoto huyu aliyelawitiwa msikitini, na watoto wengine wanaotendewa vitendo hivi, na wengine wote wanaohujumiwa haki zao. Tuungane kukemea maovu yote na kupigania haki za wote.

Ni lazima tufanye hivyo, ili angalau kumpunguzia mtoto huyu matatizo ya kisaikolojia ambayo yatamwandama maishani. Akiwa ni mtoto mu-Islam, atakuwa anasikiliza mahubiri yanayosisitiza kwamba wa-Islam wanahujumiwa na wa-Kristu, hasa wa-Katoliki. Atakuwa anasikiliza mihadhara ambayo inawaongelea wa-Islam kama watu wasio na dosari, watu wasio na ubaya na mtu, bali wenye dosari ni wa-Kristo, na katika wa-Kristo, hasa wa-Katoliki. Ataambiwa adui yake mkuu ni mfumo Kristo. Hatasikia kuwa wa-Islam ni sawa na wa-Kristu katika uwezo wa kufanya mema au mabaya. Hatasikia kuhusu hujuma zinazoweza kufanywa na wa-Islam, hata dhidi ya wa-Islam wengine, kama ilivyomtokea yeye.

Hapa ndipo ninaposema pana hatari kubwa ya kumbebesha mtoto huyu mzigo wa machungu kisaikolojia. Kutokumweleza kuwa wa-Islam nao wanaweza kuwa wabaya itakuwa ni kumwongezea kejeli juu ya machungu. Tuungane kumwepusha na hayo, kwa kadiri iwezekanavyo. Labda kwa njia hii ya kuyatangaza na kuyakemea maovu yanayotokea nchini mwetu, tutayapunguza au kuyatokomeza.

--------------------------------------------------

Chanzo: MWANANCHI


Mfanya usafi akamatwa akimlawiti mtoto msikitini
Tuesday, 24 January 2012 20:40

Hamisi Mwesi, Dodoma
POLISI mkoa hapa inamshikilia mkazi wa Bahi Road, Manispaa ya Dodoma, kwa tuhuma za kumlawiti mtoto mwenye umri wa miaka tisa baada ya kumpa Sh500 ili kumfichia siri.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Zelothe Stephen, alisema mtuhumiwa huyo ambaye ni mfanya usafi wa Msikiti wa Ghazal uliopo eneo la Majengo, alitenda kosa hilo juzi saa 12:00 jioni.

Stephen alisema baada ya polisi kupewa taarifa na wananchi wa eneo hilo, walifika msikitini hapo na kumkamata mtuhumiwa akiwa ndani ya choo cha wanawake alipokuwa akifanyia mtoto kitendo hicho cha kinyama.

“Polisi walijulishwa na wananchi waliokuwapo eneo hilo kwamba mtuhumiwa alimuingiza mtoto huyo kwenye choo cha wanawake na kujifungia ndani, watu waliokuwa jirani na eneo hilo walifuatilia kwa makini ndipo waliposhuhudia mtuhumiwa akimlawiti mtoto huyo na kutoa taarifa polisi,” alisema Stephen.

Alisema mtoto huyo amelazwa Hospitali Kuu ya Mkoa wa Dodoma kutokana na maumivu, kutokana na kitendo hicho na hali yake inaendelea vizuri na uchunguzi juu ya afya yake unafanyika kubaini athari zaidi.

Alisema mama mzazi wa mtoto huyo, alimg’ata sikio la kulia mtuhumiwa huyo kwa hasira na kunyofoka nusu ya sikio lake na kwamba, hivi sasa wanashikiliwa.

Inadaiwa mtuhumiwa amekuwa na tabia hiyo muda mrefu na waumini wa msikiti huo waliwahi kumuonya, baada ya kutiliwa shaka kuhusu kujihusisha na vitendo hivyo ambavyo hawakuwa na ushahidi, ndipo walipoamua kuanza upelelezi dhidi yake.

“Waumini walishamshtukia mtuhumiwa, wakaanza kufuatilia nyendo zake kwani yeye muda mwingi hukaa msikitini kwa ajili ya kufanya usafi, wakati mwingine kutoa adhana kwa ajili ya swala, leo (juzi) amenaswa na mtego baada ya kumtanguliza mtoto choo cha wanawake na yeye kumfuata,” alisema mmoja wa waumini wa msikiti huo.

Tuesday, January 24, 2012

Maandamano ni Mpango wa Makafiri--'Allaamah al-Fawzaan

Video hii imenisisimua akili. Sikujua kuwa maandamano ni mpango wa makafiri na kwamba hakuna maandamano katika u-Islam

Monday, January 23, 2012

Mwandishi Lazima Awe Msomaji Sana

Yule mwandishi maarufu sana, Ernest Hemingway, alikuwa na mawazo ya kusisimua kuhusu masuala mbali mbali, likiwemo suala la uandishi. Aliandika sana kuhusu uandishi: mbinu za uandishi, uandishi bora, changamoto za uandishi na namna ya kuzikabili, raha na machungu ya kuandika. Aliongelea kazi za waandishi mbali mbali, na hakuficha hisia na mtazamo wake kuhusu ubora au mapungufu ya waandishi hao.

Kuna mengi sana ya kuongelea, kuhusu suala hilo la Hemingway na uandishi. Lakini hapa nataka kutaja jambo moja tu, nalo ni kauli ya Hemingway kwamba mwandishi ana wajibu wa kusoma kazi za waandishi wote waliomtangulia, ili ajue kazi inayomkabili ya kuwafunika hao waandishi.

Napenda kunukuu maneno ya Hemingway aliyomjibu kijana kutoka Minnesota aliyemfuata Hemingway umbali mkubwa ili kuuliza masuali kuhusu uandishi. Kiutani, Hemingway alimpa kijana huyo jina la Mice.

Mice alimwuliza Hemingway masuali mengi, ila suali ninalotaka kulileta hapa ni, "What books should a writer have to read?" Hemingway akajibu, "He should have read everything so he knows what he has to beat."(Ernest Hemingway, By-Line, New York: Touchstone, 1998, p. 217)

Kwa tafsiri ya juu juu, suali lilikuwa, "Je, mwandishi anapaswa asome vitabu gani?" Na Hemingway alijibu kwamba awe amesoma kila kitu ili afahamu kazi inayomkabili ya kuwashinda waliomtangulia.

Tuangalie kauli hizi kwa kuzingatia hali ya Tanzania. Kila mchunguzi anakubali kuwa utamaduni wa kusoma vitabu unazidi kufifia au umefifia Tanzania. Taarifa zinaeleza kuwa hata uwezo wa kusoma na kuandika unazidi kufifia. Asilimia ya waTanzania wasiojua kusoma na kuandika inaongezeka. Kwa maneno mengine, Tanzania inazidi kuwa nchi ya ngumbaru.

Katika hali hiyo, na kwa kuzingatia kauli ya Hemingway, tutawezaje kutegemea kuwa na waandishi wa kiwango cha juu kabisa? Kwa mujibu wa Hemingway, mwandishi m-Tanzania, ambaye labda tuseme anaandika kwa ki-Swahili, anapaswa kuwa amesoma waandishi wote waliotangulia. Kwa mfano awe amesoma Tambuka, Al-Inkishafi, Mwana Kupona, Miraji, Masahibu, Ngamia na Paa, Muyaka bin Haji, Rasi l'Ghuli, Shufaka, Fumo Liyongo, Maisha ya Tippu TIp, vitabu vyote vya Shaaban Robert, na kadhalika. Anapaswa afahamu jadi hiyo vizuri, apambane kiuandishi ili awe juu zaidi, aweze kweli kutoa mchango unaotupeleka mbele.

Sitaki kudanganya. Lazima nikiri kuwa Hemingway alitoa mtihani mkubwa sana. Kwa mfano, sijui kama kuna mtu leo anayeweza kumfikia Muyaka, au Mgeni bin Faqihi. Lakini Hemingway alifanya vizuri kuweka kigezo cha juu kabisa, hata kama kukifikia ni taabu sana au haiwezekani. Ni vibaya sana kujiwekea viwango vya chini na kisha kujipongeza kwa kufikia viwango hivyo. Naamini hili ndilo tatizo letu: tunajiwekea viwango vya chini, au tunababaisha bila viwango, na bado tunajipongeza au tunapongezana.

Sunday, January 22, 2012

Naikumbuka Matema Beach

Tanzania ina sehemu nyingi zinazopendeza sana, nami nimebahatika kuziona baadhi ya sehemu hizo. Mwaka jana, kwa mfano, nilipata bahati ya kufika Matema Beach, pwani ya kaskazini ya Ziwa Nyasa. Ni sehemu nzuri sana kwa mapumziko. Imetulia na haina msongamano na misuguano kama ya Dar es Salaam. Hapa kushoto naonekana nimetulia kwenye bembea, nikifaidi upepo mwanana. Huyu binti ni mmoja wa wanafunzi wawili niliowaleta hapo kwenye ziara ya kuifahamu nchi.

Ukifika ufukweni hapo, unaweza kujikalia mahali chini ya mti, unapiga mbonji, kama wasemavyo watoto wa vijiweni, au ukawa unasoma kitabu, kupiga michapo na wenyeji, au kuangalia Ziwa na mitumbwi ipitayo humo.

NImeandika mara kadhaa kuhusu Matema Beach katika blogu zangu, kwa mfano hapa na hapa, na napangia kuendelea kuandika.

Friday, January 20, 2012

Kitabu cha m-Tanzania Kuhusu Usimamizi wa Fedha

Hatimaye, nimejipatia na kusoma nakala ya kitabu kiitwacho Taking Control of Your Money, kilichoandikwa na Juanita Puja Kilasara. Huyu ni binti m-Tanzania ambaye amejipambanua katika fani ya uhasibu na masuala ya fedha kwa ujumla. Habari za kitabu chake hiki niliziona kwanza katika tovuti ya wavuti, kwani kwenye ukurasa wa mbele pana sehemu inayotangaza vitabu vya wa-Tanzania.

Kitabu hiki kinaeleza kwa njia rahisi masuala mbali mbali ya kuzalisha fedha na matumizi ya fedha kwa namna ya kumsaidia mtu kuwa mwangalifu na kumfanya asonge mbele kimaisha. Kuna mawaidha mengi ya manufaa, hata katika masuala ya kuanzisha na kuendesha biashara na shughuli zingine za kujipatia kipato.

Kwa kuzingatia mabadiliko ya dunia, hasa katika tekinolojia ya mawasiliano, kitabu hiki kinatoa dokezo mbali mbali za kumwezesha mtu kutumia fursa zilizopo mtandaoni. Ingekuwa vijana wa Tanzania wana mazoea ya kusoma vitabu, wakawa wanasoma vitabu kama hiki, hata suala la ajira wangeliangalia kwa upeo tofauti, kwani ni aina ya kitabu kinachofungua milango ya ujasiriamali. Nina jambo moja tu la kushauri, kwamba ingefaa kitafsiriwe pia katika ki-Swahili.

Unaweza kumsikiliza Juanita akiongelea kitabu chake hapa. Kitabu hiki kinapatikana sehemu mbali mbali, kama ilivyoelezwa hapa.