Tuesday, February 27, 2018

Freeman Mbowe: Kiongozi wa Mfano

Kwa miezi kadhaa nimekuwa nikiwazia kuandika ujumbe kuelezea kuwa ninamkubali Freeman Mbowe kuwa ndiye kiongozi wa kitaifa wa kupigiwa mfano. Nina sababu zangu, ambazo nitazieleza hapa.
Kabla sijafanya hivyo, nataka nifafanue kuwa mimi si mwanachama wa chama chochote cha siasa. Baadhi ya watu wamekuwa wakinibambikiza uanachama wa CHADEMA. Ukweli ni kwamba sijawahi kukanyaga katika ofisi yoyote ya CHADEMA, wala sijawahi kuiona hata kadi ya CHADEMA, isipokuwa katika picha mitandaoni. Sijawahi kuhudhuria mkutano wa CHADEMA. 
Watu hao wanaonibambikiza chama sijui akili yao ikoje. Mimi ni mtu huru ninayetambua na kutumia haki yangu ya kutoa maoni na kujieleza kuhusu masuala yoyote, yakiwemo ya siasa. Nikisema jambo kuikosoa CCM, kwa mfano, sifanyi hivyo kwa sababu ya kuwa katika chama tofauti. Akili yangu haihitaji chama ili iweze kufikiri.
Baada ya ufafanuzi huo, napenda kurejea kwenye mada. Kwa nini ninamwenzi Freeman Mbowe kama kiongozi wa kupigiwa mfano? Si suala la mihemko au ushabiki. Ni suala la hoja.
Leo, katika taaluma ya saikolojia, tunaambiwa kuwa kuna aina nyingi za akili. Suala hilo kitaaluma linaongelewa chini ya kichwa cha "multiple intelligence" au "multiple intelligences."
Kufuatana na ufuatiliaji wangu wa mada hiyo, nimejifunza kwamba uongozi unahitaji aina ya akili iitwayo "emotional intelligence." Labda kwa ki-Swahili niseme akili hisia. Kwa maneno mengine, mtu mwenye akili hiyo ndiye anaumudu uongozi. Anakuwa kiongozi wa kweli.
Mtu huyo anakuwa mwenye kujitambua. Anatambua hisia zake na hisia za wengine. Kutokana na hilo, anazimudu hisia zake na hisia za wengine, kwa maana kwamba anajitawala vizuri, na anajali hisia za wenzake. Hana mihemko. Anakuwa msikivu. Watu wakitofautiana, yeye anakuwa msuluhishi. Anajenga umoja na maelewano. Anavutia watu. Watu wa kila aina wanamkubali kama kiongozi.
Mtu huyu anajiamini. Wale anaowaongoza wanakuwa huru kung'ara katika maeneo ya ujuzi wao. Yeye hawi mtu wa kutaka sifa, aonekane yeye ndio zaidi. Wenzake waking'ara kumzidi, kwake ni sawa. Vipaji vya kila moja anaviona ni mtaji wa manufaa kwa wote. Anachofanya si kuzuia vipaji hivyo visijitokeze, bali anaviratibisha kwa manufaa ya wote. Hii kwa ki-Ingereza huitwa "leveraging."
Nikirejea kwa Freeman Mbowe, ninaona anakidhi vigezo hivyo. Kuna watu wanambeza Mbowe, eti hana elimu ya kutosha. Wengine wanasema huyu ni DJ. Watu hao ni wajinga, kwa namna mbili. Kwanza hawaelewi kuwa elimu si ya shuleni na vyuoni tu. Inapatikana pia nje ya shule na vyuo. Pili hawaelewi hiyo dhana "emotional intelligence" kama kigezo na msingi wa uongozi.
Wangejua, wasingeshangaa kwa nini huyu Mbowe wanayemsema hana elimu ya kutosha, lakini ndiye kiongozi wa maprofesa, wanasheria maarufu, na kadhalika. Ni kwa sababu yeye hatingishiki na kung'ara kwa hao wenye kisomo zaidi yake. Hatingishiki na umaarufu wa wenzake, akina Tundu Lissu, Msigwa, Lema, au Halima Mdee. Wote wako naye, naye yuko nao. Hiyo ndio tabia ya mtu anayejiamini.
Kutokan na akili yake hiyo na busara zitokanazo, Mbowe amefanikiwa kuijenga CHADEMA mwaka hadi mwaka, hadi leo imekuwa ni chama kikuu cha upinzani, chenye kuongoza majimbo na miji mikubwa. Ingekuwa kuna fursa na uhuru sawa kwa kila chama kufanya shughuli zake kama inavyoelekezwa na katiba na sheria, nina hakika CHADEMA ingekuwa mbali zaidi.
Jambo jingine la muhimu sana linalonivutia kwa Freeman Mbowe ni uzalendo wake. Hata pamoja na magumu yote ambayo chama chake kinawekewa na utawala, daima anaongelea mustakabali wa Taifa. Hata mimi ambaye si mwana CHADEMA ninaguswa na hilo, kwamba anatuwazia wa-Tanzania, na nchi yetu sote, si wana CHADEMA pekee. Huyu ndiye Mbowe ninayemwona mimi.
Nimesema kuwa mimi si mwanachama wa chama chochote cha siasa. Ila napenda kusema kuwa kutokana na kwamba mimi ni mwanataaluma na mwalimu, kama ingekuwa ni lazima kuwa na chama, ningekuwa CHADEMA. Ninaona jinsi CHADEMA inavyopigania uhuru na haki zilizomo katika katiba, ikiwemo uhuru na haki ya kutoa mawazo na kujieleza, na uhuru wa mikutano. 
Uhuru wa fikra ni msingi wa kustawi yale ninayofanya kama mwanataaluma na mwalimu. Elimu haistawi bila uhuru wa kutoa mawazo na kujieleza. Elimu inaihusu jamii nzima. Mikutano ni sehemu ya hiyo elimu ya jamii. Kwa hivyo, ni wazi kwangu kuwa kama ingekuwa lazima kuwemo katika chama, ningekuwa CHADEMA. Ningekuwa huko si kwa sababu CHADEMA inakidhi mategemeo yangu yote kuhusu masuala yote ya kitaifa, bali kwa sababu hii moja ambayo nimeelezea. Kama mwanataaluma ninayehitaji uhuru wa kufikiri na kutoa mawazo, na ninayetaka elimu ishamiri katika nchi yetu, ningejisikia huru kuwa na kiongozi Freeman Mbowe.

Wednesday, February 21, 2018

Maana ya Uzalendo

Kwa kuzingatia jinsi dhana ya uzalendo inavyovurugwa na watu mbali mbali, nimeona nilete tamko la Ilhan Omar, Msomali Mmarekani ambaye ameweka historia hapa Marekani kwa kuchaguliwa kuwa mwakilishi katika bunge la jimbo la Minnesota. Anafafanua kwa lugha rahisi maana ya uzalendo. Anachosema ni kuwa uzalendo si kutetea uongozi au kiongozi wa nchi, bali ni kutetea na kuzingatia maslahi ya nchi, katiba yake, na watu wake. Anasema ni kosa kufikiri kwamba mkuu wa nchi asikosolewe. Anasema kwamba katika nchi ya kidemokrasia, na katiba inayotambua uhuru wa watu kutoa mawazo na kujieleza, watu wana haki ya kumkosoa mkuu wa nchi, kumshinikiza afanye mambo ya manufaa, na kumwajibisha, bila wasi wasi au woga wa kueleweka kwamba si wazalendo.

Saturday, February 17, 2018

Ripoti ya Mhadhara wa Red Wing

Nashukuru nimeweza kwenda leo Red Wing na kutoa mhadhara juu ya "African Storytelling," kama ilivyotangazwa. Barabara zilikuwa na theluji, kwa hivyo ilibidi niendeshe gari kwa uangalifu. Lakini nilifika salama, saa tatu na dakika hamsini. Mhadhara ulipangiwa kuanza saa nne, na ndivyo ilivyokuwa.

Nilipokelewa vizuri na wahudumu wa maktaba ya Red Wing, hasa Lindsey Rindo ambaye ndiye aliyefanya mawasiliano nami tangu mwanzo, mwaka jana, kuniulizia kama ningeweza kwenda kutoa mhadhara, akafuatilia na kufanya mipango yote hadi kufanikisha shughuli ya leo.

Walikuwepo watu wa kila rika, kuanzia watoto wadogo hadi wazee. Nilianza kwa kuelezea umuhimu wa Afrika kama chimbuko la binadamu, tekinolojia, lugha, na usimuliaji wa hadithi. Nilielezea jinsi falsafa na maadili yalivyohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi hadi kizazi katika aina za fasihi simulizi kama vile methali. Nilitoa mifano ya methali.

Kisha nilisimulia hadithi ya "Spider and the Calabash of Knowledge," na "The Lion's Advice," kutoka katika kitabu cha West African Folktales cha Jack Berry, na hadithi ya "The Chief's Daughter," kutoka katika kitabu cha West African Folktales cha Steven H. Gale. Hizo hadithi mbili za mwanzo sikuzifahamu hadi jana. Ndipo nilizisoma, nikaamua kwenda kuzisimulia leo. Hiyo ya tatu niliifahamu, na niliwahi kuisimulia.

Dakika kumi za mwisho zilikuwa za masuali na majibu. Kwa tathmini yangu, mhadhara wa leo umekuwa moja wa mihadhara bora ambayo nimewahi kutoa. Nilivutiwa kuona wazazi wamekuja na watoto wao. Inapendeza kuona jinsi watoto wadogo wa Marekani wanavyozoeshwa kutumia muda maktabani.

Lindsey alikuwa ameniambia kuwa nilete vitabu vyangu, nikitaka, kwa ajili ya kuuza, nami nilifanya hivyo. Nilichukua nakala za kutosha za Matengo Folktales na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Wakati wa kunua na kusainiwa vitabu, niliguswa kumwona mama moja alivyokuwa na ari ya kununua kitabu cha "Africans and Americans." aliniambia kuwa ni mfanya usafi katika maktaba hiyo. Kwa hapa Marekni, ni jambo la kawaida watu wa aina zote kupenda vitabu.

Friday, February 16, 2018

Mrejesho Kuhusu Kitabu

Ni furaha na faraja kwangu kama mwandishi kupata mrejesho kutoka kwa wasomaji. Leo asubuhi, nilipoamka, niliona ujumbe kutoka kwa mwalimu wa chuo cha St. Lawrence. Ameandika:

Mimi ni ndugu Kitito. Tulikuwa wageni wako katika kongamano la African network. Mimi na Robin tunashukuru mno kwa kitabu chako "Africans and Americans." Tunakitumia darasani mwetu. Wanafunzi wamefaidika mno...

Huyu mwalimu Robin anayetajwa nilishaandika habari zake katika blogu hii. Baada ya mimi kusoma ujumbe wake, mwalimu Kitito amenipigia simu, akanielezea zaidi kuhusu kitabu kinavyotumiwa. Nami nilimwelezea nilivyokiandika, baada ya miaka mingi ya kukabiliana na maisha ya Marekani. Nilimweleza kwa nini nilitumia mtindo ambao si kawaida kwa wanataaluma.

Nimefarijika kupata mrejesho kutoka kwa waalimu hao ambao wanatumia kitabu changu, nami nimeona niweke kumbukumbu hii hapa, kama ilivyo kawaida yangu.

Monday, February 12, 2018

Nasubiri Mhadhara wa Red Wing

Tarehe 17 mwezi huu, nitakwenda Red Wing kutoa mhadhara, kama nilivyoripoti katika blogu hii. Mada itakuwa "African Storytelling" yaani jadi ya hadithi za Afrika. Maandalizi yamefanyika kikamilifu, kama inavyoonekana katika tangazo la mhadhara.

Hii si shughuli ya kwenda kusimulia hadithi tu. Ni kuelimisha kuhusu misingi, maana, na dhima ya hadithi za jadi katika utamaduni wa Afrika. Jadi ya kusimulia hadithi ni sanaa yenye kugusa vionjo na hisia za binadamu, pia ni nia ya kuhifadhi elimu na kuelimisha. Hadithi zinayotafakari maisha, tabia na mahusiano ya binadamu, na masuala ya maadili.

Hadithi zimefungamana na aina zingine za sanaa ya maneno kama vile methali na nyimbo. pia zimefungamana na mila, desturĂ­, na imani. Ni kioo cha jamii, lakini pia ni kichocheo cha mwenendo wa jamii. Upana huo wa mtazamo kuhusu hadithi nimeubainisha katika kitabu changu, Matengo Folktales ambacho kina hadithi kumi, pamoja na uchambuzi wangu wa kila hadithi. Pia kina insha juu ya padithi kwa mtazamo wa kitaaluma, lakini kwa lugha rahisi.

Mhadhara wangu wa Red Wing utaelimisha kuhusu mchango wa wa-Afrika katika utamaduni wa ulimwengu. Nitaelezea kuwa sanaa ya usimuliaji hadithi ilianzia Afrika, sambamba na kutokea kwa binadamu na lugha. Nitaelezea kuwa falsafa haikuanzia Ulaya, kwa akina Socrates na Plato, bali ilikuwepo Afrika, katika hadithi na aina nyingine za fasihi simulizi. Mafundisho ya hadithi na fasihi simulizi kwa ujumla kuhusu maisha na mahusiano ya binadamu bado yana maana na umuhimu
katika ulimwengu wa leo na kesho.

Ninatoa shukrani kwa uongozi wa Red Wing Public Library na Goodhue County Historical Society kwa kunialika kwenda kutoa mhadhara huu. Nafurahi pia kuwa sitaenda kuzungumza tu, bali pia, k kuoutakuwa na shughuli ya watu kununua na kusainiwa kusaini vitabu vyangu. Vitabu vitadumisha ujumbe wangu katika maisha ya watakaovisoma.

Tuesday, February 6, 2018

Mteja Anapokupigia Debe

Tarehe 3 Februari, nilipata ujumbe wa barua pepe kutoka kwa dada au mama ambaye amejitambulisha kwa jina la Cynthia, ila simjui. Ameandika kuulizia kitabu changu namna hii:

Hello,

I am planning a trip to Tanzania and someone recommended your book about cultural differences between Africans and Americans. How can I purchase your book? Thank you very much.

Kwa wasiojua ki-Ingereza, tafsiri yake ni hii:

Habari

Ninapanga safari ya kwenda Tanzania na mtu fulani alikipendekeza kitabu chako juu ya tofauti za tamaduni za wa-Afrika na wa-Marekani. Nitakinunuaje kitabu chako? Shukrani sana.

Kwa mwandishi, habari ya aina hii ni habari njema. Kwamba mtu fulani ambaye alitumia hela zake kununulia kitabu chako alikisoma akaridhika au kufurahi kiasi cha kukipendekeza kwa mwingine, si jambo jepesi. Mtu anapopendekeza kitu kwa mwingine namna hii, anajiweka katika hali ya kueleweka vibaya, iwapo kile anachopendekeza hakitamridhisha huyu mwingine. Tunapendekeza vitu kwa marafiki zetu tukiwa na uhakika na hicho tunachopendekeza.

Sisi wote ni wateja wa hiki au kile, iwe ni vitu au huduma. Muda wote tunawashawishi wenzetu wakanunue kitu fulani au wanapohitaji huduma, tunawaelekeza sehemu ambayo tunaiamini. Tunapopendekeza kitu au huduma tunatoa tamko kuhusu ubora wa kile tunachopendekeza. Nimekuwa nikielezea masuala haya katika blogu hii.

Muda wote sisi binadamu tunafanya hii shughuli ya kupiga debe bila malipo. Tunafanya hiki kibarua kisicho na malipo bila hata kujitambua. Ni sehemu ya mazungumzo yetu na marafiki au watu wengine. Mwenye kuuza bidhaa au kutoa huduma anafaidika bila kutumia hela kulipia matangazo.

Hayo ni baadhi ya mawazo yangu wakati huu ninapotafakari suala la huyu mpiga debe asiyejulikana ambaye amekipendekeza kitabu changu kwa mtu huyu aitwaye Cynthia, ambaye naye simjui. Nimemjibu Cynthia nikamwambia sijui mahali alipo, lakini kitabu anaweza kukipata mtandaoni.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...