Wednesday, October 15, 2008

Mwalimu Nyerere na Elimu


Mwalimu Julius Nyerere alikuwa mwalimu. Naamini ni sahihi kusema kuwa silika ya ualimu iliathiri siasa na matendo ya Mwalimu Nyerere kama kiongozi wa Tanganyika na hatimaye Tanzania. Aliiona nchi yake kama darasa, na daima alikuwa anafundisha.

Ninachotaka kuongelea hapa ni mchango wa Mwalimu Nyerere katika uwanja wa elimu. Elimu ni suala mojawapo ambalo Mwalimu Nyerere alilishughulikia sana. Katika kuelezea suala la elimu, Mwalimu aliweka na kufuata misingi kadhaa muhimu.

Tanganyika ilipopata Uhuru, Mwalimu Nyerere alikuwa ameshajizatiti kubadilisha mfumo wa elimu uliokuwepo wakati wa ukoloni, ambao ulikuwa mfumo wa kibaguzi. Kulikuwa na shule za wazungu, za Wahindi, na za watu weusi. Mara tulipopata Uhuru, Nyerere alifuta ubaguzi na kuwachanganya wanafunzi mashuleni. Tangu mwanzo, Mwalimu Nyerere aliamini dhana ya usawa wa binadamu.

Mwalimu Nyerere aliamini kuwa elimu ni haki ya kila mtu. Alifanya kila juhudi kutoa elimu kwa watu wote, kuanzia watoto hadi watu wazima. Mwalimu alijitahidi kujenga mfumo wa elimu ambao ulitoa nafasi kwa yeyote kutokana na uwezo wa akili yake, bila kujali kama alikuwa maskini au tajiri. Kwa msingi huu, watu wengi ambao hawangeweza kulipia masomo walisoma hadi vyuo vikuu.

Mwalimu Nyerere alitaka elimu iwe inamjenga mwanafunzi kuwa mdadisi wa mambo na mwenye kiu ya kutafuta elimu. Yeye mwenyewe alikuwa mwanafalsafa, mtu wa kutafakari mambo. Na hivyo ndivyo alivyotaka elimu iwe. Mwalimu alitaka elimu iwe nyenzo ya kumkomboa mwanadamu, tofauti na elimu ya kikoloni, ambayo ilikuwa inaendeleza fikra tegemezi, fikra za kujidhalilisha, fikra za kitumwa. Alitaka elimu ijenge tabia ya kuheshimiana, sio kiburi cha usomi.

Mwalimu Nyerere alitaka elimu ijumlishe nadharia na vitendo, na ijenge tabia ya kushirikiana, si kushindana na ubinafsi. Vijana mashuleni alitaka wawe pia wanajishughulisha na kazi za mikono, kama vile kulima au kufuga na useremala. Hii nayo ni elimu, na ni fursa ya kufahamu mengi ambayo hayapatikani darasani. Kazi za mikono aliziona ni njia moja ya shule kujenga msingi wa kujitegemea kwa mahitaji yake.

Mwalimu Nyerere alifundisha kuwa elimu haina mwisho. Aliwahimiza watu kujibidisha katika kutafuta elimu. Mbali ya kushughulikia elimu ya watoto na vijana mashuleni, alianzisha mpango wa elimu ya watu wazima. Vijijini na mijini watu walihimizwa na walipata fursa ya kujiongezea elimu, kuanzia kujifunza kusoma na kuandika hadi kujipatia ujuzi na maarifa katika fani na taaluma mbali mbali.

Kwa utaratibu ulioitwa kisomo chenye manufaa, wavuvi, wakulima, seremala, wafugaji, na wengine katika shughuli mbali mbali, walihimizwa kujiongezea ujuzi kwenye fani na shughuli zao. Vitabu vilichapishwa katika fani za aina aina, ambavyo viliwapa watu fursa ya kujifunza kusoma na pia kujiongezea maarifa na ujuzi.

Kama Watanzania tungefuata mawazo ya Mwalimu, leo tungekuwa mbali kimaendeleo, na tungekuwa na mategemeo ya kufanikiwa zaidi. Katika dunia ya leo ya utandawazi, elimu, ujuzi na maarifa ndio msingi wa mafanikio. Lakini, Tanzania tuna matatizo makubwa, kwani ari ya kujielimisha imepungua sana, na watu wanatafuta vyeti badala ya elimu. Wengi wanaamini kuwa njia ya mafanikio ni kutumia mambo ya ushirikina, badala ya kujiongezea maarifa katika fani na shughuli mbali mbali, iwe ni kilimo, uvuvi, au biashara.

Nimeona jinsi Wamarekani wanavyojali elimu. Wanatumia fedha kununua vitabu, kulipia semina, na fursa nyingine kadha wa kadha za kujiongezea elimu, ujuzi na maarifa, ili wapate mafanikio katika shughuli zao, kama vile biashara. Watanzania tungekuwa tumefuata nyayo za Mwalimu Nyerere tungefanya hivyo hivyo: tungeona umuhimu wa kutumia fedha kununulia vitabu na kulipia warsha za kujiongezea ujuzi na maarifa katika shughuli mbali mbali. Imani ya kuwa maendeleo na mafanikio yanatokana na mambo ya kishirikina ni dalili za kuanguka kwa ule msingi aliokuwa anaujenga Mwalimu Nyerere. Je, Watanzania tutaweza kushindana katika dunia ya leo na kufanikiwa bila elimu, ujuzi na maarifa? Hilo wimbi la ushindani wa kimataifa tutaliweza au litatuzamisha? Hilo ni suala la kulitafakari.

Kuufahamu mchango wa Mwalimu Nyerere katika elimu ni sherti kuyapitia maandishi yake na hotuba zake. Baadhi ya maandisho hayo na hotuba hizo zilihusu elimu moja kwa moja, na baadhi ya kazi zake hizo ni hazina ambayo inatuwezesha kukusanya dondoo mbali mbali za kutuwezesha kuielewa falsafa na sera ya Mwalimu Nyerere kuhusu elimu. Kwa bahati nzuri, kuna kitabu kimechapishwa, kinachokusanya maandishi muhimu ya Mwalimu Nyerere kuhusu elimu. Kinaitwa Nyerere on Education/ Nyerere Kuhusu Elimu. Ni kitabu muhimu sana ambacho kinapatikana hapa: http://msupress.msu.edu/bookTemplate.php?bookID=3032

Wednesday, October 8, 2008

Watoto wa Marekani














Ingawa kazi yangu kuu hapa Marekani ni kufundisha katika kiwango cha chuo kikuu, kufanya utafiti katika taaluma zangu, na kutoa mchango wa mawazo na uzoefu kwa walimwengu kwa ujumla, napenda sana kukutana na kuongea na watoto, kuwasilimulia hadithi za Afrika, na kuwaeleza kuhusu maisha ya Afrika na masuala mengine ya maisha kwa ujumla, katika nchi yao na duniani.





Nimeshaongea na watoto kwenye miji mbali mbali, katika mikoa ya Colorado, Minnesota, Pennyslvania, na Wisconsin. Watoto ni watoto. Kitu kimoja wanachopenda ni hadithi. Nami nimekuwa na fursa nyingi za kuwasimulia hadithi za Kiafrika. Kitu kimoja kinachofurahisha ni jinsi watoto walivyo na akili ya kufuatilia hadithi na kuzichambua. Hata watoto wanaodhaniwa kuwa hawana akili sana au hawana moyo wa kupenda masomo, wanaonyesha msisimko wanaposimuliwa hadithi. Hapa kuna taarifa kuhusu nilivyokutana na watoto wa shule ya LeTort, Pennsylvania. Soma hapa














Jambo hili limenifanya nikumbuke habari moja niliyosoma kuhusu mwanasayansi maarufu Einstein. Inasemekana aliulizwa na wazazi kuhusu mkakati bora wa kuwaandaa watoto kuwa wanasayansi makini. Wazazi walidhani kuwa angeshauri watoto wafundishwe sana masomo ya sayansi tangu utotoni. Lakini Einstein aliwajibu kuwa watoto wasimuliwe hadithi. Alipoulizwa nini kifanyike baada ya hizo hadithi, yeye alilisitiza kuwa watoto wasimuliwe hadithi zaidi.














Habari hii niliisoma nilipokuwa masomoni katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, katika kujisomea mwenyewe vitabu. Mwanzoni sikuelewa kwa nini Einstein alikuwa na mawazo hayo. Lakini baada ya miaka mingi, nilipojaribu kusoma zaidi mawazo ya Einstein, nilianza kufahamu alikuwa na maana gani. Yeye aliamini kabisa kuwa kitu cha maana kwa mtoto ni kumhamasisha awe mbunifu. Ubunifu--dhana ambayo Waingereza wanaita "imagination"--ndio msingi, kwa mujibu wa Einstein. Nilivyozidi kufuatilia habari za Einstein, nilikuja kuelewa kuwa yeye mwenyewe kama mwanasayansi alikuwa anatagemea sana ubunifu, sio tu majaribio katika maabara. Alikuwa na ubunifu wa hali ya juu; hata baadhi ya nadharia zake wataalam wenzake waliziona kuwa ni ndoto. Lakini miaka mingi baadaye, kutokana na kuwepo vifaa vya uchunguzi, nadharia zake zimethibitishwa kuwa kweli.

Watoto wa Marekani ni sawa na watoto wengine. Wana dukuduku, na wanapenda kujua mambo. Wana masuali mengi. Sehemu kadhaa nilipoenda kuongea na hao watoto, walimu wao walikuwa na wasi wasi kuwa labda watoto wataniuliza masuali ya kijinga. Lakini mimi niliwaambia walimu kuwa watoto wana haki ya kuuliza masuali, hata yawe ya aina gani.

Watoto wanaoonekana katika picha hizi hapa walikuwa wanafunzi kwenye shule za mji wa Faribault, Minnesota. Mwalimu wao alikuwa ameniomba awalete hao watoto ili niwape mawaidha na motisha. Hakufafanua zaidi, bali mimi nilichukulia hii kama fursa ya kuwaeleza hao watoto jinsi dunia ilivyo pana na yenye fursa nyingi kwao, jinsi dunia ilivyo na nchi nyingi, kila moja ikiwa na mazuri yake. Ilikuwa ni siku nzuri kwa watoto hao na kwangu.

Saturday, October 4, 2008

Wasomaji wa Maandishi Yangu

Uandishi ni shughuli inayohitaji juhudi na ustahimilivu. Inaweza kuleta mema au mabaya katika jamii. Kwa hivi, mwandishi anapaswa kuwa makini. Uandishi unaweza kuwa na manufaa mengi, kwa mwandishi mwenyewe na kwa jamii. Kuandika kunatupa fursa ya kutumia akili katika kupanga mawazo na lugha. Ni zoezi la kuchangamsha na kuboresha akili. Kitu kimoja kinachonipa faraja sana na motisha pia, ni kufahamiana na watu mbali mbali, kwa njia ya maandishi yangu. Najifunza mengi kutokana na maoni ya wasomaji. Napenda kwenda sehemu mbali mbali kuwaonyesha watu maandishi yangu na kuongelea shughuli zangu za ufundishaji, utafiti, na uandishi. Napenda pia kuelezea ninavyojishughulisha katika kutoa ushauri kwa wageni mbali mbali, hasa Wamarekani, wanaokwenda Afrika, kama wanafunzi, watafiti, watalii, na washiriki katika shughuli za kujitolea. Baadhi ya picha zinazoonekana hapa zilipigwa Minneapolis, tarehe 4 Oktoba, 2008, wakati wa sherehe za kumbukumbu ya Uhuru wa Nigeria. Nilipata fursa ya kushiriki, nikiwa na meza yangu ya vitabu na maandishi mengine. Mama anayeonekana pichani na binti yake walikuwa miongoni mwa wengi waliokuja kuongea nami na kuangalia vitabu, au kuvinunua. Nilifurahi kuona wazazi wakiwa na watoto wao. Kwa vile mimi ni mwalimu, naamini hii ni namna bora ya kuwalea watoto. Utamaduni huu uko sana hapa Marekani. Kwenye maduka ya vitabu, ninawaona wazee, vijana, watoto, wake kwa waume wakiangalia vitabu, wakivisoma, na kuvinunua. Hata watoto wadogo kabisa wanaletwa humo na wazazi wao, na hivi kujengewa tabia ya kusoma. Majumbani, utamaduni wa wazazi kuwasomea vitabu watoto wao wadogo umejengeka. Inakuwa kama vile hao wenzetu ndio wanafuata ule ushauri wa wahenga kwamba samaki mkunje angali mbichi. Utamaduni huu kwa kiasi kikubwa hauonekani Tanzania. Kwenye maduka ya vitabu, ambayo ni machache sana, na kwenye matamasha ya vitabu, watu wazima ni nadra kuonekana. Hii ni dalili ya tatizo kubwa katika jamii yetu. Tutawezaje kustahimili ushindani wa dunia ya leo, au kustawi na kufanikiwa katika dunia ya leo, ambayo inategemea elimu na maarifa? Hapo juu niko na mama moja na mume wake. Huyu mama ni mratibu wa mpango wa uhusiano baina ya jimbo moja la kanisa na kiLuteri hapa Marekani na Waluteri wa Malawi. Baada ya kusoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, http://www.lulu.com/content/105001, amekuwa akiwasiliana nami mara kwa mara, akitafakari vipengele mbali mbali vya vinavyojitokeza katika mahusiano baina ya Wamarekani na Waafrika. Masuali yake mengi kuhusu vipengele vya maisha ya watu wa Malawi yamenipa changamoto ya pekee. Hapo juu naonekana na akina mama wawili kutoka Ethiopia, ambao wanaishi Marekani. Wote wamesoma kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Huyu mama wa kushoto alinieleza kuwa laiti angekuwa amesoma kitabu hiki kabla hajaja Marekani, angekuwa amejiandaa kwa mengi aliyoyapitia hapa Marekani. Niliguswa sana na hii kauli yake. Nayasikia maoni ya aina hiyo muda wote, kutoka kwa Waafrika wanaoishi Marekani. Nami nawashukuru, kwani ni changamoto kwangu, niongeze juhudi ya kutafakari masuala na kuandika zaidi. Hapo juu niko na vijana wa Mto wa Mbu, Tanzania, wanaoshughulika na utalii unaolenga kwenye utamaduni. Waliniambia kuwa wamesoma Matengo Folktales, http://www.lulu.com/content/136624, na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na wanavitumia katika shughuli zao. Vimewapa uwezo wa kuelezea fasihi simulizi ya Mtanzania. Hicho cha pili kimewapa mawazo mengi ya kuelezea utamaduni wa Mtanzania na Mwafrika kwa ujumla. Pia kimewapa mwanga wa kuuelewa utamaduni wa watalii wanaowakaribisha Mto wa Mbu, hasa Wamarekani. Nilifurahi na kufarijika kuwasikia vijana hao wakinieleza kuwa vitabu hivi vimewapa moyo wa kujiamini katika kutekeleza majukumu yao. Ninafurahi kuwa nao bega kwa bega. Kama nilivyosema, Wamarekani wengi wanakwenda Afrika, kama watalii, wanafunzi, watu wa kujitolea, watafiti, na kadhalika. Nimekuwa na bahati ya kuwa bega kwa bega na watu wa aina hiyo. Hapo kulia kuna hao wazungu wawili ambao wanashughulika na miradi ya elimu, afya na kadhalika huko Kenya na Tanzania. Huyu aliye kushoto ni Mkenya ambaye wanashughulika wote kule Kenya. Huyu mama, baada ya kusoma Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, amekuwa na mawasiliano ya mara kwa mara nami, akitaka kujua zaidi vipengele vya maisha ya Waafrika, ili aweze kuishi na kufanya nao kazi vizuri bila mikwaruzano wala vipingamizi. La msingi ni kuwa nashukuru kuwa nimepata fursa ya kuwa karibu na watu wengi namna hiyo, na fursa ya kutoa mchango katika maisha na shughuli zao. Sitasahau ujumbe niliopata kutoka kwa mama mmoja Mwamerika, ambaye sijawahi kumwona. Aliniambia alikuwa anakamilisha mipango ya kufunga ndoa na mwanamme Mwafrika, lakini kwa muda mrefu walikuwa na mikwaruzano, ambayo hakuelewa kwa nini ilikuwa inatokea. Aliongeza kuwa katika kusoma Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, aligundua mizizi ya mikwaruzano yao. Taarifa kama hizi ni changamoto kwangu. Nawajibika kuendelea kuandika. Vitabu vilivyotajwa hapa juu vinapatikana Dar es Salaam, simu namba 0754 888 647.

Friday, October 3, 2008

Mwalimu Julius Nyerere

Nimeona kuwa andiko la kwanza liwe juu ya Mwalimu Julius Nyerere. Mwalimu Nyerere ni mtu maarufu katika historia ya Tanzania. Katika ukumbi huu athari za mawazo na siasa za Mwalimu Nyerere zitajitokeza mara kwa mara, kwani alichangia kuiwezesha Tanzania kupitia hatua ilizopitia, akishirikiana na wazalendo wenzake, ambao nao watakuwa wanatajwa hapa ukumbini, kila itakapobidi.

Mwalimu Nyerere anastahili kukumbukwa, kwa mchango wake mkubwa, sio tu kwa nchi yetu bali kwa dunia. Tunapaswa kusoma maandishi yake na kuyajadili, kuyatathmini, na kuyakarabati inapobidi, ili yaendelee kuwa mwongozo wetu.

Mwalimu Nyerere alikuwa mtu wa fikra, ambaye daima alikuwa anaangalia maslahi ya nchi yetu, na jitihada alizofanya katika kubadilisha siasa, uchumi, utamaduni, na vipengele vingine vya nchi yetu ilikuwa ni kwa nia ya kuikomboa na kuijenga katika misingi ya uhuru, usawa, haki, na kujitegemea. Yako makosa ambayo alifanya, lakini alikuwa mzalendo, aliyeamini kuwa aliyokuwa anafanya ni kwa maslahi ya nchi. Makosa yake yanahitaji kuwekwa katika mkabala huo. Huu ndio mtazamo nitakaokuwa nao katika kuelezea na kujadili mchango wa Mwalimu Nyerere kwa Tanzania na dunia.

Karibu, hapa kwetu

Karibu. Hapa ni kwetu--Watanzania, Waafrika, na wengine wanaotumia kiSwahili. Ninategemea kuwa huu utakuwa ukumbi wa masuala yanayotuhusu: katika siasa, uchumi, utamaduni, na jamii kwa ujumla. Namshukuru sana ndugu Freddy Macha, ambaye alinipa wazo la kuanzisha blogu. Freddy ni Mtanzania mwenye uwezo wa pekee katika fani mbali mbali, hasa muziki na uandishi. Anafanya kazi kubwa ya kuwaelisha na kuwaunganisha walimwengu. Namshukuru sana pia ndugu Jeff Msangi kwa kunihamasisha kwa namna mbali mbali. Jeff ni hodari katika kuelimisha umma kwa namna mbali mbali.

Karibuni.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...