Saturday, October 4, 2008

Wasomaji wa Maandishi Yangu

Uandishi ni shughuli inayohitaji juhudi na ustahimilivu. Inaweza kuleta mema au mabaya katika jamii. Kwa hivi, mwandishi anapaswa kuwa makini. Uandishi unaweza kuwa na manufaa mengi, kwa mwandishi mwenyewe na kwa jamii. Kuandika kunatupa fursa ya kutumia akili katika kupanga mawazo na lugha. Ni zoezi la kuchangamsha na kuboresha akili. Kitu kimoja kinachonipa faraja sana na motisha pia, ni kufahamiana na watu mbali mbali, kwa njia ya maandishi yangu. Najifunza mengi kutokana na maoni ya wasomaji. Napenda kwenda sehemu mbali mbali kuwaonyesha watu maandishi yangu na kuongelea shughuli zangu za ufundishaji, utafiti, na uandishi. Napenda pia kuelezea ninavyojishughulisha katika kutoa ushauri kwa wageni mbali mbali, hasa Wamarekani, wanaokwenda Afrika, kama wanafunzi, watafiti, watalii, na washiriki katika shughuli za kujitolea. Baadhi ya picha zinazoonekana hapa zilipigwa Minneapolis, tarehe 4 Oktoba, 2008, wakati wa sherehe za kumbukumbu ya Uhuru wa Nigeria. Nilipata fursa ya kushiriki, nikiwa na meza yangu ya vitabu na maandishi mengine. Mama anayeonekana pichani na binti yake walikuwa miongoni mwa wengi waliokuja kuongea nami na kuangalia vitabu, au kuvinunua. Nilifurahi kuona wazazi wakiwa na watoto wao. Kwa vile mimi ni mwalimu, naamini hii ni namna bora ya kuwalea watoto. Utamaduni huu uko sana hapa Marekani. Kwenye maduka ya vitabu, ninawaona wazee, vijana, watoto, wake kwa waume wakiangalia vitabu, wakivisoma, na kuvinunua. Hata watoto wadogo kabisa wanaletwa humo na wazazi wao, na hivi kujengewa tabia ya kusoma. Majumbani, utamaduni wa wazazi kuwasomea vitabu watoto wao wadogo umejengeka. Inakuwa kama vile hao wenzetu ndio wanafuata ule ushauri wa wahenga kwamba samaki mkunje angali mbichi. Utamaduni huu kwa kiasi kikubwa hauonekani Tanzania. Kwenye maduka ya vitabu, ambayo ni machache sana, na kwenye matamasha ya vitabu, watu wazima ni nadra kuonekana. Hii ni dalili ya tatizo kubwa katika jamii yetu. Tutawezaje kustahimili ushindani wa dunia ya leo, au kustawi na kufanikiwa katika dunia ya leo, ambayo inategemea elimu na maarifa? Hapo juu niko na mama moja na mume wake. Huyu mama ni mratibu wa mpango wa uhusiano baina ya jimbo moja la kanisa na kiLuteri hapa Marekani na Waluteri wa Malawi. Baada ya kusoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, http://www.lulu.com/content/105001, amekuwa akiwasiliana nami mara kwa mara, akitafakari vipengele mbali mbali vya vinavyojitokeza katika mahusiano baina ya Wamarekani na Waafrika. Masuali yake mengi kuhusu vipengele vya maisha ya watu wa Malawi yamenipa changamoto ya pekee. Hapo juu naonekana na akina mama wawili kutoka Ethiopia, ambao wanaishi Marekani. Wote wamesoma kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Huyu mama wa kushoto alinieleza kuwa laiti angekuwa amesoma kitabu hiki kabla hajaja Marekani, angekuwa amejiandaa kwa mengi aliyoyapitia hapa Marekani. Niliguswa sana na hii kauli yake. Nayasikia maoni ya aina hiyo muda wote, kutoka kwa Waafrika wanaoishi Marekani. Nami nawashukuru, kwani ni changamoto kwangu, niongeze juhudi ya kutafakari masuala na kuandika zaidi. Hapo juu niko na vijana wa Mto wa Mbu, Tanzania, wanaoshughulika na utalii unaolenga kwenye utamaduni. Waliniambia kuwa wamesoma Matengo Folktales, http://www.lulu.com/content/136624, na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na wanavitumia katika shughuli zao. Vimewapa uwezo wa kuelezea fasihi simulizi ya Mtanzania. Hicho cha pili kimewapa mawazo mengi ya kuelezea utamaduni wa Mtanzania na Mwafrika kwa ujumla. Pia kimewapa mwanga wa kuuelewa utamaduni wa watalii wanaowakaribisha Mto wa Mbu, hasa Wamarekani. Nilifurahi na kufarijika kuwasikia vijana hao wakinieleza kuwa vitabu hivi vimewapa moyo wa kujiamini katika kutekeleza majukumu yao. Ninafurahi kuwa nao bega kwa bega. Kama nilivyosema, Wamarekani wengi wanakwenda Afrika, kama watalii, wanafunzi, watu wa kujitolea, watafiti, na kadhalika. Nimekuwa na bahati ya kuwa bega kwa bega na watu wa aina hiyo. Hapo kulia kuna hao wazungu wawili ambao wanashughulika na miradi ya elimu, afya na kadhalika huko Kenya na Tanzania. Huyu aliye kushoto ni Mkenya ambaye wanashughulika wote kule Kenya. Huyu mama, baada ya kusoma Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, amekuwa na mawasiliano ya mara kwa mara nami, akitaka kujua zaidi vipengele vya maisha ya Waafrika, ili aweze kuishi na kufanya nao kazi vizuri bila mikwaruzano wala vipingamizi. La msingi ni kuwa nashukuru kuwa nimepata fursa ya kuwa karibu na watu wengi namna hiyo, na fursa ya kutoa mchango katika maisha na shughuli zao. Sitasahau ujumbe niliopata kutoka kwa mama mmoja Mwamerika, ambaye sijawahi kumwona. Aliniambia alikuwa anakamilisha mipango ya kufunga ndoa na mwanamme Mwafrika, lakini kwa muda mrefu walikuwa na mikwaruzano, ambayo hakuelewa kwa nini ilikuwa inatokea. Aliongeza kuwa katika kusoma Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, aligundua mizizi ya mikwaruzano yao. Taarifa kama hizi ni changamoto kwangu. Nawajibika kuendelea kuandika. Vitabu vilivyotajwa hapa juu vinapatikana Dar es Salaam, simu namba 0754 888 647.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...