Hebu fikiria: sikukuu ya Idd el Fitr au Krismasi imewadia na unataka kuwapa zawadi ndugu na marafiki zako, wa-Tanzania wenzako. Unaamua kwenda kwenye duka la vitabu, na unawanunulia nakala za kitabu kama Kufikirika cha Shaaban Robert, au Binadamu na Maendeleo cha Mwalimu Nyerere, au kwa wanaojua ki-Ingereza, The Tempest cha Shakespeare. Unawafungia vizuri, kisha unawapelekea. Je, watajisikiaje hao wa-Islam na wa-Kristu wa Tanzania? Miaka ya tisini na kitu, katika jumuia ya mawasiliano ya mtandaoni iitwayo Tanzanet, ambayo wanachama wake ni wa-Tanzania na marafiki wa Tanzania, niliwahi kuandika, kiutani, kwamba siku za usoni huenda nikaamua kwamba, kwenye mialiko ya arusi nisipeleke kreti ya bia, bali kreti ya vitabu. Ingawa ulikuwa ni mchapo, nilikuwa na jambo muhimu kichwani, kwani ni kweli kuwa vitabu ni hazina, na ni bora kuliko bia. Hapa Marekani, ni kawaida watu kutoa au kupokea zawadi ya vitabu. Msimu kama huu wa Krismasi, watu wengi wananunua vitabu ili kuwapa zawadi wenzao