Tuesday, December 27, 2011

Hadithi za wa-Matengo Zatamba Ughaibuni

Hivi karibuni, nilipata ujumbe kutoka kwa Profesa Paschal Kyoore wa Chuo cha Gustavus Adolphus kuwa anatunga kozi mpya, "The African Trickster," akaomba ushauri wangu, kwani mada hiyo ya "trickster" nimeifanyia utafiti na kuandika makala kwa miaka mingi.

Hatimaye, Profesa Kyoore ameniletea ujumbe kuwa ameshaagiza nakala za kitabu cha Matengo Folktales kwa ajili ya darasa hilo. Kisha angependa siku moja niende kuongea na wanafunzi wake, nami nimekubali.

Ninafurahi sana ninapoona watu wa ughaibuni wakipata fursa ya kujifunza mambo ya kwetu, na hadithi za jadi ni hazina mojawapo kubwa, kama nilivyoelezea hapa. Ni fursa kwetu na kwa walimwengu kutambua mchango wa wahenga wetu kwa utamaduni wa dunia, kwani katika hadithi zao, wahenga waliongelea na kutafakari kila aina ya suala linalomkabili binadamu, sawa na watu walivyofanya watu wa mataifa mengine.

Hadithi za wa-Matengo zinatumika katika vyuo mbali mbali hapa Marekani, kama nilivyoelezea hapa. Yapata miaka miwili iliyopita, nilipata pia ujumbe kutoka kwa mwalimu mmoja Uingereza, ambaye alikuwa anatafuta nakala ya Matengo Folktales kwa ajili ya kufundishia. Nilimpelekea.

Tunawajibika kuzirekodi hadithi hizi na masimulizi mengine, kwani vijana wa leo hawazielewi, na wanatekwa na tamaduni za nje, zinazoenezwa kwetu hasa kwa njia ya machapisho, televisheni, na mtandao wa kompyuta. Mimi nilirekodi hadithi za wa-Matengo nilipokuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, miaka yapata 40 iliyopita. Halafu nilitumia miaka yapata 23 kuzishughulikia hadithi zilizomo katika Matengo Folktales, kwa maana ya kuzitafsiri na kuziandikia uchambuzi, ndipo nikachapisha kitabu. Lakini, shughuli hii haina mwisho, na kitabu kimoja hakitoshi. Ni kama changamoto tu. Kwa walioko Tanzania, kitabu kinapatikana Dar es Salaam, simu namba 0754 888 647 na 0717 413 073.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...