Friday, December 23, 2011

Maongezi na Wanafunzi Waendao Tanzania

Profesa Barbara Zust, wa Chuo cha Gustavus Adolphus, amenialika kwenda kuongea na wanafunzi anaowaandaa kwa safari ya Tanzania. Anafundisha masomo ya uuguzi, na mwezi Januari anawapeleka wanafunzi Tanzania kujifunza masuala ya afya na matibabu katika utamaduni tofauti na ule wa Marekani.

Profesa Zust ameshawapeleka wanafunzi Tanzania mara kadhaa. Katika kuwaandaa, hutumia kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na pia hunialika nikaongee nao. Anajisikia vizuri sana ninapokutana na wanafunzi wake kujibu masuali yao na kuwapa maelezo mbali mbali, nami huwa nafurahi kukutana na wanafunzi hao wanaosomea taaluma ambayo sikusomea, ila ni wazi kuwa wanafaidika na mawazo yangu kuhusu jinsi tofauti za tamaduni zinavyohusika katika taaluma yao.

Hapa kushoto ni picha tuliyopiga na wanafunzi waliokuwa wanaenda Tanzania mwaka 2009. Tulikuwa kwenye chumba cha mkutano cha kanisa la Shepherd of the Valley, mjini Apple Valley. Habari za mkutano wetu niliziandika hapa.








Hapa kushoto ni picha tuliyopiga na wanafunzi waliokuwa wanakwenda Tanzania mwaka 2010. Tulikutana Mount Olivet Retreat Center, mjini Lakeville. Habari zaidi niliziandika hapa.

Wanafunzi hao na profesa wao wanapata fursa ya kuona sehemu mbali mbali za Tanzania, kama vile hospitali ya Ilula, kijiji cha Tungamalenga, na hifadhi ya Taifa ya Ruaha. Sehemu zote tatu ziko Iringa. Wanafunzi hao wanaguswa sana na ziara yao Tanzania. Nimeshasoma baadhi ya maoni yao.

Mwaliko wa sasa ni wa kuongea na wanafunzi tarehe 2 Januari. Insh'Allah, nitaleta picha na taarifa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...