Thursday, December 29, 2016

Vitabu Tulivyosoma Mwaka 2016

Zikiwa zimebaki siku mbili tu kabla ya kwisha mwaka 2016, nimeona wa-Tanzania kadhaa wakijitokeza katika mtandao wa Facebook na kutaja vitabu walivyosoma mwaka huu. Jambo hili limenifurahisha, nikizingatia kuwa nimekuwa nikihamasisha usomaji wa vitabu, kwa kutumia blogu yangu hii, blogu za wengine, na pia katika kitabu changu, CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Ninawapongeza watu hao kwa kuonyesha mfano mzuri. Ninawapongeza pia wasomaji waliojitokeza na kuchangia suala hili kwa namna mbali mbali, kama vile kuvijadili vitabu hivyo, kuulizia upatikanaji wake, au kupendekeza vitabu vingine. Kuhusu upatikanaji wa vitabu, watu wamepeana taarifa za maduka ya vitabu, na pia upatikanaji wa vitabu pepe mtandaoni. Ni jambo la kuvutia kwamba kuna wa-Tanzania wanaotambua matumizi ya manufaa ya tekinolojia ya mtandao.

Mazungumzo haya yameonyesha mambo kadhaa. Jambo moja ni kuwa wako wa-Tanzania wanaojibidisha kusoma vitabu. Jambo jingine ni kuwa wanasoma vitabu vya aina mbali mbali, kama vile vya siasa, ujasiriamali, fasihi, na maendeleo ya jamii au ya mtu binafsi. Vile vile wanasoma vitabu vya waandishi wa mataifa mbali mbali, vya ki-Swahili na vya ki-Ingereza. Jambo jingine ni kuwa wahusika wameonyesha moyo mkubwa wa kusaidiana, kama vile kwa kufahamishana vitabu bora na hata kuazimishana vitabu.

Ninawaenzi watu hao. Huenda wakawa chachu ya kustawisha utamaduni wa kusoma vitabu nchini Tanzania. Laiti watu wengi zaidi wangejumuika katika safari hii. Laiti kama watu maarufu nchini mwetu, kama vile wanasiasa na wasanii, wangejiunga na kuwa wahamasishaji wa usomaji wa vitabu. Kutokana na mvuto wa wasanii wetu, kwa mfano, wangeweza kuwa wahamasishaji wa watoto na vijana katika kupenda kusoma vitabu.

Kwa upande wangu, naona sihitaji kuorodhesha vitabu nilivyosoma mwaka 2016. Mara kwa mara, katika blogu hii au blogu ya ki-Ingereza, ninaandika taarifa za baadhi ya vitabu ninavyosoma. Vingine ni vile ninavyofundisha chuoni St. Olaf, na vingine ni vile ninavyojisomea mwenyewe. Ninapoandika  taarifa, ninajitahidi kuelezea upekee au ubora wa vitabu hivyo.

Tuesday, December 27, 2016

Nimejutia Kusoma "Hamlet" Wakati wa Sikukuu

Siku kadhaa zilizopita, nilianza kusoma Hamlet, tamthilia ya Shakespeare, kama nilivyoandika katika blog ya ki-Ingereza. Tamthilia hii haikuwa ngeni kwangu. Ni moja ya tungo za Shakespeare ambazo nimezifahamu au kuzisoma tangu ujana wangu.

Lakini kuna jambo ambalo sikulizingatia nilipoamua kusoma Hamlet wakati huu, ambao ni wa sikukuu ya Krismasi. Ulikuwa si wakati muafaka wa kusoma Hamlet, hadithi yenye matukio ya kusikitisha. Mkondo mkuu wa hadithi hii ni jinsi baba ya Hamlet alivyouawa na ndugu yake, mfalme Claudius, ambaye miezi miwili tu kufuatia msiba huo alimwoa mama yake Hamlet. Mambo haya yanampa Hamlet msongo mkubwa wa mawazo.

Mzimu wa marehemu baba yake unamtokea Hamlet na kumweleza ufedhuli uliofanyika na kisha kumwelekeza alipize kisasi. Hamlet anatafakari afanye nini. Hasira na huzuni zake anazieleza kwa hisia na ufasaha tena na tena, kwa mfano katika tamko hili:

Ham. O that this too too solid flesh would melt
Thaw and resolve itself into dew!
Or that the Everlasting had not fixed
His canon 'gainst self-slaughter! O God! God!
How weary, stale, flat, and unprofitable
Seem to me all the uses of this world!
Fie on't! ah, fie! 'Tis an unweeded garden
That grows to seed; things rank and gross in nature
Possess it merely. That it should come to this!
But two months dead--nay, not so much, not two!
So excellent a king, that was to this
Hyperion to a satyr; so loving to my mother
That he might not beteem the winds of heaven
Visit her face too roughly. Heaven and earth!
Must I remember? Why, she would hang on him
As if increase of appetite had grown
But what it fed on; and yet, within a month--
Let me not think on't! Frailty, thy name is woman!
....
              Act I. Sc. II

Tafakari yake inamfanya hata ajiulize kama aendelee kuishi na kupambana na masaibu ya maisha kwa mategemeo ya kuyamaliza, au atoe uhai wake, kama tunavyomsikia katika tamko hili maarufu sana:

Ham. To be, or not to be, that is the question:
Whether 'tis nobler in the mind to suffer
The slings and arrows of outrageous fortune
Or to take arms against a sea of troubles,
And by opposing end them. To die--to sleep--
No more; and by a sleep to say we end
The heartache, and the thousand natural shocks
That flesh is heir to. 'Tis a consummation
Devoutly to be wished. To die--to sleep.
To sleep--perchance to dream: ay, there's the rub!
For in that sleep of death what dreams may come
When we have shuffled off this mortal coil,
Must give us pause....
                                              Act. III. Sc. I

Ili kuzipata vizuri hisia za Hamlet, tushuhudie jinsi Laurence Olivier alivyoliigiza tamko hili la pili, katika filamu ya mwaka 1948, ambayo niliiangalia kwa mara ya kwanza mwaka 1971, nilipokuwa Mkwawa High School, Tanzania:

Tuesday, December 20, 2016

Zawadi ya Krismasi

Siku tatu zilizopita, jirani yangu m-Marekani, mama mwenye umri zaidi yangu, aliniomba nimsainie nakala za kitabu cha Africans and Americans Embracing Cultural Differences. Alikuwa amevinunua kwa ajili ya kuwapelekea rafiki zake, wa-Marekani wenzake, kama zawadi ya Krismasi.

Jambo hili lilitosha kunifanya niandike ujumbe katika blogu yangu, kwani linadhihirisha jadi ninayoiona hapa Marekani, kama nilivyowahi kudokeza katika blogu hii. Lakini nimehamasika kuandika baada ya kusoma makala ambayo ameichapisha Christian Bwaya katika blogu yake. Ameelezea umuhimu wa zawadi kwa watoto na mambo ya kuzingatia katika kutoa zawadi kwa watoto.

Kati ya mifano ya zawadi alizotaja ni vitabu. Ni jambo muhimu, nami kama mwalimu ninaliafiki moja kwa moja. Nimejionea jinsi watoto wanavyopenda vitabu, sio tu hapa Marekani, bali pia Tanzania. Nimeandika mara kwa mara umuhimu wa kuwasomea watoto vitabu na kuwajenga watoto katika utamaduni wa kusoma vitabu. Huwa ninafarijika ninaposoma taarifa za uhamasishaji wa suala hilo.

Tutakuwa tumepiga hatua kubwa iwapo tutajijengea utamaduni wa kuwanunulia watoto vitabu kama zawadi, kwani wanavipenda vitabu. Tutakuwa tumepiga hatua iwapo vijana wetu na watu wa kila rika watakuwa na utamaduni wa kuthamini zawadi ya vitabu.

Friday, December 16, 2016

Dunia Yetu ya Maigizo

Shakespeare alisema, tena na tena, kuwa dunia ni jukwaa la maigizo ambapo kila mtu hujitokeza na kuigiza nafasi yake na kisha hutoweka zake. Maelezo haya naona ni kianzio muafaka cha kutafakari mambo ya dunia yetu. Ili kuchangia tafakari hiyo, nanukuu Hamlet, tamthilia maarufu ya Shakespeare, kutoka onyesho la 2, sehemu ya 2, ambapo tunasikia maongezi baina ya Polonius na Hamlet:

   Pol. My lord, I have news to tell you.
   Ham. My lord, I have news to tell you: when Roscius was an actor in Rome--
   Pol. The actors are come hither, my lord.
   Ham. Buzz, buzz!
   Pol. Upon my honor--
   Ham. Then came each actor on his ass--
   Pol. The best actors in the world, either for tragedy, comedy, history, pastoral, pastoral-comical, historical pastoral, tragical-historical, tragical-comical-historical-pastoral; scene individable, or poem unlimited, Seneca cannot be too heavy, nor Plautus too light. For the law of writ and the liberty, these are the only men.

Tangu zamani, nimevutiwa na ufafanuzi wa Polonius wa aina za maigizo. Kwa upande moja, naona kama analeta dhihaka nyepesi au kejeli, ingawa siwezi kudai kuwa ninaweza kuthibitisha jambo hilo. Ila kwa kweli anasisimua akili yangu.

Katika taaluma ya fasihi, inaeleweka kuwa ni juu ya kila msomaji kutumia ufahamu wake kuchambua kazi ya fasihi. Ufahamu huo unaweza kujumlisha mambo mengi, kama vile ufahamu wa fasihi, falsafa, na saikolojia. Matokeo ya kuchambua kazi ya fasihi hayabashiriki, na kwa kuwa kila msomaji ana upeo tofauti wa ufahamu, ni wazi kuwa kila msomaji wa kazi ya fasisi ataielewa kwa mtazamo tofauti.

Ukiwauliza wasomaji mbali mbali maana ya kazi fulani ya fasihi, utegemee kusikia majibu na maelezo tofauti, isipokuwa kama hao wasomaji wanafanya ukasuku. Kwa bahati mbaya, ukasuku huu umeshamiri miongoni mwa wengi. Hata katika blogu hii ya hapakwetu, wanajitokeza watu wanaoulizia maana ya kazi ya sanaa. Wanategemea niwape uchambuzi, kwa imani kwamba fasihi ni kama dini, ambamo kuna imamu au padri mwenye majawabu ya masuali ya waumini.

Baada ya maelezo haya, narejea tena kwenye ujumbe wangu wangu wa awali hapo juu, pamoja na nukuu niliyoiweka kutoka katika tamthilia ya Hamlet. Ninaona ni changamoto na kichocheo murua cha fikra.


Wednesday, December 14, 2016

Wosia wa Rabindranath Tagore Kuhusu Uhuru wa Kutoa Maoni

Rabindranath Tagore ni mmoja wa waandishi maarufu kabisa waliowahi kuishi. Alizaliwa mwaka 1861 Calcutta na kufariki 1941. Aliheshimika duniani kote wakati wa uhai wake na bado anaheshimika. Aliandika mashairi, tamthilia, insha, riwaya, hadithi fupi, na pia maelfu ya barua. Niliwahi kufundisha utungo wake maarufu Gitanjali, hapa chuoni St. Olaf.

Tagore alikuwa mwalimu aliyetukuka, kioo cha ubinadamu wa kweli ("humanism"), mwenye fikra pevu na nzito juu ya maisha na maadili. Watu maarufu kama W.B. Yeats, Mahatma Gandhi na Albert Einstein, walimmwenzi sana. Mwaka 1913 alipata tuzo ya Nobel katika fasihi. Nina vitabu vyake vitatu, kimojawapo kikiwa Rabindranath Tagore: An Anthology.

Kutoka katika kitabu hiki nimenukuu sehemu ya ujumbe wa tarehe 25 Septemba, 1930, kwa gazeti la Izvestia la Urusi. Ni ujumbe unaopaswa kutafakariwa na kuzingatiwa, tunaposhuhudia ukandamizaji wa uhuru wa watu kujieleza. Ili kuufikisha ujumbe kwa watu wasiojua ki-Ingereza, nimejaribu kuutafsiri.

     There must be disagreement where minds are allowed to be free. It would not only be an uninteresting but sterile world of mechanical regularity if all our opinions were forcibly made alike. If you have a mission which includes all humanity, you must, for the sake of that living humanity, acknowledge the existence of differences of opinion. Opinions are constantly changed and re-changed only through the free circulation of intellectual forces and moral persuasion. Violence begets violence and blind stupidity. Freedom of mind is needed for the reception of truth; terror hopelessly kills it. The brute cannot subdue the brute. It is only the man who can do it.

Tafsiri

     Lazima pawepo na kutokubaliana mahali ambapo akili zinaruhusiwa kuwa huru. Dunia itakuwa sio tu haipendezi bali tasa yenye kwenda kwa mwendo ule ule kama mashine, iwapo maoni yetu yote yatalazimishwa kufanana. Kama watu mna malengo yanayowahusu wanadamu kwa ujumla wao, sherti, kwa manufaa ya uhai wa jamii hiyo ya wanadamu, kutambua uwepo wa tofauti za maoni. Maoni hubadilishwa bila ukomo pale tu panapokuwa na mzunguko huru wa nguvu za akili na ushawishi wa mwenendo wa kimaadili. Mabavu huzaa mabavu na ujinga mithili ya upofu. Uhuru wa akili unahitajika ili ukweli upokelewe, na vitisho huua kabisa ukweli huo. Hayawani hawezi kumdhibiti hayawani. Ni binadamu tu ndiye anaweza.

Monday, December 12, 2016

Leo Nimemaliza Kufundisha Muhula wa Kwanza

Leo nimemaliza kufundisha muhula wa kwanza. Nilikuwa ninafundisha kozi tatu: "First Year Writing," "African Literature," na "Muslim Women Writers." Nilihitimisha ufundishaji wa "First Year Writin"g wiki iliyopita, ili kuwapa wanafunzi muda wa kuandika insha kuu ya mwisho. Katika kozi hii, ninafundisha uandishi bora wa ki-Ingereza, na uangalifu unaotakiwa katika vipengele vyote , kuanzia neno, hadi sentensi, hadi insha.

Katika African Literature tumemalizia muhula tukisoma riwaya ya Mia Couto, The Tuner of Silences. Mia Couto ni mwandishi wa Msumbiji, ambaye ni maarufu sana. Amepata sifa na tuzo kem kem, ikiwemo tuzo ya Neustadt. The Tuner of Silences ni riwaya inayosisimua akili kwa jinsi ilivyosheheni ubunifu wa kisanaa na kifikra.

Kuna mengi ya kutafakari katika riwaya hii, hasa yatokanayo na dini, fasihi linganishi, historia, falsafa kama vile "existentialism," na mikondo ya falsafa ya sanaa kama vile "surrealism."  Vile vile, taaluma ya saikolojia, kama vile mkondo wa "psychoanalysis," inasaidia kutafakari dhamira zilizomo. Kuisoma na kuufaidi utajiri wa riwaya kama The Tuner of Silences kunahitaji upeo mpana wa mawazo ambao unatokana na kusoma kwingi, sio tu fasihi bali taaluma mbali mbali.

Katika kuiongelea The Tuner of Silences darasani, nimesisitiza jambo hilo, Nimefundisha wanafunzi umuhimu wa kuzingatia nadharia za usomaji kama zilivyoelezwa na Cleanth Brooks katika insha yake, "The Language of Paradox," na pia zilivyoelezwa na Roland Barthes katika kitabu chake kiitwacho S/Z: An Essay.

Katika kozi ya "Muslim Women Writers," tumemalizia muhula tukisoma riwaya ya Monica Ali, Brick Lane. Ni riwaya ndefu, inayoelezea maisha ya watu wa Bangladesh ambao wanaishi Uingereza. Ni jamii ya ki-Islam, na tunaiona inavyojitahidi kustahimili na kustawi katika mazingira ya ugenini.

Hii ni jamii kama jamii zingine, yenye watu wenye maadili mema na ari ya kuwa mfano kwa wengine, na pia wako ambao tabia zao zina walakini. Wanapenda kufuatilia habari za wenzao, na ni wapiga majungu. Tofauti baina ya utamaduni wao na ule wa wa-Ingereza zinajitokeza, na pia tofauti baina ya vijana na watu wazima au wazee. Vijana wanaonekana kuiga mambo ya vijana wa kizungu, yakiwemo ambayo si mazuri.

Kufundisha kazi ya fasihi kutoka Bangladesh imekuwa ni fursa ya kuelezea historia ya fasihi ya nchi hiyo, ukiwemo mchango mkubwa wa Rabindranath Tagore, mwandishi wa mashairi, tamthilia, riwaya, na insha, ambaye aliitwaa tuzo ya Nobel mwaka 1913. Kwa bahati nzuri, Tagore ametajwa katika Brick Lane, kwa jinsi alivyo hazina kwa watu wa Bangladesh. Lakini jambo la kuzingatia ni kuwa Tagore ni mwamba katika fasihi ya ulimwengu, aliyeheshimiwa na miamba wenzake kama vile W.B. Yeats wa Ireland, aliyekuwa na urafiki na mawasiliano na Tagore.

Leo, katika kuhitimisha kozi yetu ya "Muslim Women Writers," nimewaomba wanafunzi ushauri juu ya kuitumia tena riwaya hii siku za usoni, nitakapofundisha kozi hii. Wameniambia kuwa ni riwaya muhimu sana, ingawa inachukua muda sana kuisoma. Wameshauri kwamba nitakapofundisha tena kozi hii, Brick Lane iwe mwanzoni, wakati wanafunzi wakiwa bado hawajachoka na masomo. Riwaya zingine, ambazo ni fupi fupi, zije baadaye. Nimewashukuru kwa ushauri huo wa wanafunzi ambao wamepitia kozi yangu, nikizingatia kuwa adhabu ya kaburi aijuaye maiti.

Friday, December 9, 2016

The Rime of the Ancient Mariner: Samuel Taylor Coleridge

Jana na leo nimesoma The Rime of the Ancient Mariner, utenzi maarufu wa Samuel Taylor Coleridge, ambao ni moja ya tungo za ki-Ingereza nilizokuwa ninazipenda wakati wa ujana wangu, kama nilivyoandika katika blogu hii. Nimefurahi kuusoma tena, baada ya miaka mingi, wakati ambapo akili yangu imepevuka zaidi kutokana na kusoma tungo nyingi za fasihi.

Katika kusema hivi, ninakumbuka kauli ya mshairi William Wordsworth, katika shairi lake maarufu, "Lines Written a Few Miles Above Tintern Abbey," anavyoongelea namna alivyotembelea, katika utu uzima wake, eneo ambalo alilizoea alipokuwa kijana. Matokeo ya kufanya hivyo ni kwamba, ingawa hawezi tena kuyaona mazingira yale kwa hisia za ujanani, sasa anayaona kwa kutumia akili ya kiutu uzima. Aina zote mbili za maono anazienzi, ingawa zinatofautiana.

Nami ninajisikia hivyo hivyo katika kusoma wakati huu The Rime of the Ancient Mariner. Nimeweza kuuweka utungo huu katika mkabala wa tungo nilizosoma kwa miaka ya baina ya ujana wangu na umri nilio nao sasa. Ninawazia hadithi ya kale ya Misri iitwayo, "The Tale of the Shipwrecked Sailor," utenzi wa Odyssey wa Homer, hadithi za baharia Sindbad, riwaya ya Daniel Defoe, Robinson Crusoe; riwaya ya Herman Melville, Moby Dick; na Utenzi wa Masaibu.

Papo hapo, kutokana na utafiti na ufundishaji wa somo la "Folklore," nimetilia maanani vipengele vya The Rime of the Ancient Mariner kama usimuliaji wa hadithi, imani mbali mbali ambazo tunaziita ushirikina. Kuna imani kama vile juu ya macho kuwa na nguvu ya kichawi. Dhana hiyo inajitokeza mara kadhaa katika utenzi huu. Kwa mfano, mwanzoni kabisa mwa utenzi tunasoma:

It is an ancient Mariner,
And he stoppeth one of three.
'By thy long grey beard and glittering eye,
Now wherefore stopp'st thou me?

'The Bridegroom's doors are opened wide,
And I am next of kin;
The guests are met, the feast is set:
May'st hear the merry din.'

He holds him with his skinny hand,
'There was a ship,' quoth he.
'Hold off! unhand me, grey-beard loon!'
Eftsoons his hand dropt he.

He holds him with his glittering eye--
The Wedding-Guest stood still,
And listens like a three years' child:
The Mariner hath his will.

Kuanzia hapo, huyu baharia mkongwe anamsimulia kijana yaliyomsibu katika safari baharini, yeye na mabaharia wenzake. Ni kisa cha mikosi, majanga na vifo vya wenzake wote akasalimika yeye, na tangu hapo katika maisha yake, hupatwa na maumivu fulani nafsini mwake ambayo suluhu yake ni kumnasa mtu wa kumsimulia kisa chake.

The Rime of the Ancient Mariner ni kisa cha kusisimua. Coleridge anazisukuma hisia zetu kupitia hali mbali mbali: mshangao, hofu, masikitiko, na huruma. Pamoja na kwamba hatimaye tunafarijika kwa jinsi mzee huyu alivyonusurika, tunabaki na majonzi kwa vifo vya mabaharia wenzake. Baada ya kuelewa kisa kizima, tunaelewa kwa nini mzee huyu anamteka kwa uchawi wa macho yake kijana anayekwenda arusini na kumfanya asikilize kisa chake hadi mwisho.


Thursday, December 8, 2016

Tamko la CUF Kuelekea Maadhimisho ya Uhuru wa Tanganyika


Kesho, Alhamisi, tarehe 9 Disemba, 2016 ni siku ya maadhimisho ya miaka 55 ya Uhuru wa Tanganyika, Watanzania tunaadhimisha miaka 55 ya kuwa huru baada ya harakati za miaka mingi ya kudai uhuru wa nchi yetu kutoka kwa wakoloni waliotutawala.

The Civic United Front (CUF-Chama Cha Wananchi) kinaungana na wananchi wote katika kuadhimisha siku hii muhimu katika historia ya nchi yetu, na kutoa wito kwao kuendelea kusimamia malengo, dhamira, na nia za viongozi wetu katika kupigania Uhuru kama yalivyowahi kusema na kuainishwa kuwa ni kupambana na maadui wakubwa watatu ambao ni Umasikini, Ujinga, na Maradhi.

Sambamba na siku ya uhuru wa Tanganyika, tarehe 9 Disemba, ni siku ya maadhimisho ya kimataifa kuhusiana na waathirika wa mauaji ya halaiki na kuzuia jinai zake, (International Day of Commemoration and Dignity of the Victims of the Crime of Genocide and of the Prevention of this Crime) kama ilivyotangazwa na Umoja wa Mataifa (UN) kwa tamko lake namba (A/RES69/363). Tarehe hii ya 9 Disemba pia ni siku ya kimataifa kuadhimisha juhudi za kupinga na kupambana na rushwa, (Internatinal Anti Corruption Day) kama ilivyotangazwa na Umoja wa Mataifa (UN) kwa tamko lake namba (A/RES/58/4).

THE CIVIC UNITED FRONT (CUF-Chama Cha Wananchi) kinaungana na mataifa yote duniani kuadhimisha siku hizi na kuiahidi Jumuiya ya Kimataifa kuwa itaipa kila aina ya ushirikiano ili kufikia malengo ya kuanzishwa kwa maadhimisho ya siku hizo. Kwa kutumia mifano michache ya maadhimisho ya siku kama hizi za kimataifa juu ya jinai dhidi ya ubinadamu na kutamalaki kwa rushwa, na kufuatilia mwenendo wa matukio yanayoendelea kutokea katika nchi yetu kwa pande zote mbili za Muungano (Tanganyika na Zanzibar), inabainika kuwa malengo halisi ya mapambano ya kudai uhuru hayajafikiwa kama ilivyodhamiriwa na viongozi na majemedari walioongoza harakati za kudai uhuru na ukombozi wa nchi yetu. Kwa hakika, mapambano ya kudai Uhuru yamefanikiwa kwa kiwango kidogo mno cha kumuondosha mkoloni mzungu, na badala yake ndugu zetu na wananchi wenzetu wamejiweka katika nafasi hiyo kwa kuendeleza yaleyale aliyokuwa akiyafanya Mkoloni kwa takribani nchi zote za kiafrika. 

Wakati huu nchi yetu ikiwa inatimiza miaka 55 ya kuwa huru, kumeshuhudiwa uvunjifu mkubwa wa Haki za binaadamu, Ukandamizaji wa demokrasia uliochupa mipaka ikiwa ni pamoja na kupuuzwa na kuminywa kwa maamuzi ya kidemokrasia ya wananchi kuchagua viongozi wanaowataka, uvamizi, ushambuliaji na utekaji wa viongozi wa kisiasa, na utawala usiozingatia matakwa ya kisheria katika kuongoza kwake.

Katika siku za hivi karibuni hali imeendelea kuwa mbaya zaidi ambapo vyombo vya Ulinzi na Usalama, vyenye wajibu na jukumu la kulinda Raia na Mali zao, vimekuwa vikikubali kupokea amri na kutumiwa na wanasiasa wa Chama tawala na vibaraka wao kushiriki jinai mbalimbali kama vile kunyanyasa na kudhalilisha wananchi wasio na hatia kwa kuwabambikizia kesi, kuvamia, kupiga na kujeruhi wananchi na au kutoa ulinzi na kufanikisha njama za matukio hayo, kama inavyofanywa na kikosi cha askari kinachojulikana kwa jina la ‘Mazombi’ kisiwani Zanzibar na kushindwa kwa vyombo hivyo kuchukuwa hatua zozote za kisheria kwa wahusika wa uratibu na utekelezaji wa jinai hizi zinazofanywa wazi wazi.

Vitendo vyote hivi vinaashiria namna Viongozi wa CCM na Serikali yake walivyoshindwa kusimamia nia, dhamira na malengo ya Viongozi wetu waliopigania Uhuru. Bila ya shaka haya yote ni dalili na mwelekeo mbaya wa kuvurugika kwa amani ndani ya nchi yetu. The Civic United Front (CUF-Chama Cha Wananchi) inatowa wito kwa Serikali na viongozi wa CCM, kuheshimu na kuzingatia misingi ya HAKI, USAWA, DEMOKRASIA NA KUFATA UTAWALA WA SHERIA ili kuiepusha nchi yetu kuingia katika majanga yanayoweza kuepukika.

HAKI SAWA KWA WOTE

SALIM BIMANI

MKURUGENZI WA HABARI, UENEZI NA MAHUSIANO NA UMMA

MAWASILIANO: 0777 414 112 / 0752 325 227

Saturday, December 3, 2016

Msikilize Rais Yahya Jammeh Anavyokubali Ushindi wa Mpinzani

Msikilize Rais Yahya Jammeh wa Gambia anavyokubali matokeo ya uchaguzi wa urais ambayo mpinzani ameshinda. Rais Jammey, bila kusita, anasema kuwa kwa kura zao, wananchi wa Gambia wamenena, naye anayapokea matokeo. Anampongeza mpinzani kwa ushindi wake, na anaahidi kumpa ushirikiano kuanzia kipindi hiki cha mpito. Anamwombea baraka za Allah katika kuiongoza nchi ya Gambia, na anawashukuru watu wa Gambia.

Friday, December 2, 2016

Ndugu wa Uganda Anataka Kitabu

Kama ilivyo kawaida katika blogu hii, ninapenda kujiwekea kumbukumbu mbali mbali. Jana niliwatembelea akina mama wawili wa-Kenya waishio Brooklyn Park, Minnesota, ambao walitaka tukutane ili niweze kuwapa ushauri kuhusu fursa za kujiendeleza kielimu ya juu na katika ajira. Wakati tulipokuwa katika maongezi, waliwasiliana na bwana mmoja wa kutoka Uganda, wakamwita kuja kuungana nasi.

Tulizungumza kuhusu masuala mbali mbali, yakiwemo masuali waliyoniuliza juu ya ufundishaji na uandishi wangu. Mmoja wa hao akina mama nilikuwa nimemwahidi kumpa nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Huyu jamaa wa Uganda aliniulizia namna ya kukipata kitabu kile, nikamweleza kuwa anaweza kukipata mtandaoni Amazon.com au lulu.com/spotlight/mbele, au kutoka kwangu. Nikamshauri kwamba kwa upnde wa gharama, ni rahisi zaidi kukinunua Amazon.com. Lakini yeye alisisitiza kuwa nimpelekee, akanipa na anwani yake.
,
M-Ganda huyu amenikumbusha wa-Ganda wengine niliokutana nao hapa Minnesota, wakajiptia kitabu changu. Mmoja ni Steven Kaggwa ambaye alikuwa anamiliki mgahawa wa Tam Tam. Baada ya kukisoma kitabu hiki, aliniambia kuwa aliwaelezea wafanya kazi wake. Mmoja wao, Sally, hakuishia tu kujinunulia nakala, bali alinunua nakala nyingine ambayo aliniambia alikuwa anampelekea mkuu wake wa kazi, ambaye ni m-Marekani. Niliguswa na taarifa ya huyu mama, kama nilivyoguswa miaka michache baadaye, wakati mama mmoja kutoka Togo alivyonunua nakala za kitabu hiki kwa ajili ya wakuu wa kazini kwake, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

M-Ganda mwingine ninayemkumbuka nilikutana naye katika tamasha la vitabu ambalo nilikuwa ninashiriki. Alikuwa amefika kikazi hapa Minnesota, lakini alikuja kwenye tamasha hilo, na ndipo tulipofahamiana. Bila kusita alinunua kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differenes, akaenda zake. Yeye na hao wengine wameniacha nikitafakari jinsi hao wenzetu walivyo. Ninaona kuwa sio tu wameenda shule, bali wameelimika, kwani uthibitisho wa kuelimika ni kuwa na hamu ya kutafuta elimu hata baada ya kumaliza shule.

Thursday, December 1, 2016

Maandalizi ya Wanachuo wa Gustavus Adolphus Waendao Tanzania

Jana nilipata ujumbe kutoka kwa Profesa Barbara Zust wa Chuo cha Gustavus Adolphus akiulizia iwapo nitaweza kwenda kuongea na wanafunzi wanaojiandaa kwenda naye Tanzania kwa safari ya kimasomo. Ameniambia kuwa watakuwa na kikao cha maandalizi ya safari tarehe 2 na 3 Januari, katika kituo cha mikutano cha Mount Olivet. Nimefanya mazungumzo hayo tena na tena miaka iliyopita.

Katika ujumbe wake, Profesa Zust amekumbushia kuwa, kama ilivyo jadi, wanafunzi hao watakuwa wameshasoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Pia amekumbushia jinsi wanafunzi wanavyoshukuru na kufurahia kwamba wanapokuwa Tanzania wanakutana na yale ambayo ninakuwa nimewaeleza kitabuni na katika mazungumzo.

Taarifa hii ni muhimu kwangu, na ndio maana ninaiweka hapa katika blogu yangu, kama kumbukumbu. Kwa kuzingatia umuhimu wa suala hili, nimeitika mwaliko wa Profesa Zust na kumwambia kuwa nitakwenda kukutana nao tarehe 2 Januari. Kama kawaida, panapo majaliwa, nitaandika taarifa katika blogu hii.

Wednesday, November 30, 2016

Kitabu cha Historia ya Chai

Leo nimenunua kitabu, A Brief History of Tea, cha Roy Moxham, nilichokiona jana katika duka la vitabu la hapa chuoni St. Olaf. Nilivutiwa na taarifa kwenye jalada la nyuma:

Behind the wholesale image of the world's most popular drink lies a strangely murky and often violent past. When tea began to be imported into the West from China in the seventeenth century, its high price and heavy taxes made it an immediate target for smuggling and dispute at every level, culminating in international incidents like the notorious Boston Tea Party. In China itself the British financed their tea dealings by the ruthless imposition of the opium trade. Intrepid British tea planters soon began flocking to Africa, India and Ceylon, setting up huge plantations. Workers could be bought and sold like slaves.

Maelezo haya yalinisisimua nikaona sherti nikinunue kitabu hiki. Niliona wazi kuwa kitanielimisha kuhusu mengi tusiyoyajua juu ya chai, kinywaji ambacho wengi tunakitumia. Mambo hayo ni pamoja na uchumi, historia, siasa, na mahusiano ya jamii, na mahusiano ya mataifa.  Kitabu hiki kimenikumbusha kitabu cha Sidney Mintz. Sweetness and Power: The Place of Sugar in Modern History, ambacho kinahusu sukari. Iwe ni chai au sukari, ni msingi wa kutafiti na kuelewa masuala mengi. Tafakari ya aina hii inanikumbusha pia Karl Marx, ambaye alitafakari kitu kinachoitwa bidhaa ("commodity"), akathibitisha jinsi bidhaa inavyobeba mambo mbali mbali ya jamii, ikiwemo mahusiano ya binadamu.

Nimeanza kusoma A Brief History of Tea na kujionea jinsi mwandishi alivyo na kipaji cha kujieleza. Ameanzia na maelezo ya maisha yake, alivyokuwa kijana u-Ingereza, akawa amechoshwa na maisha ya kule. Katika kutafuta fursa nje ya nchi yake, aliweka tangazo gazetini, na hatimaye akaajiriwa kuwa afisa katika shamba la chai Nyasaland, ambayo leo ni Malawi. Hapo ndipo yanapoanzia masimulizi ya kusisimua na kuelimisha yaliyomo katika kitabu hiki.

Thursday, November 24, 2016

"A Far Cry From Africa," Shairi la Derek Walcott

Tangu nilipoanza kufundisha katika chuo cha St. Olaf, mwaka 1991, nimepata fursa ya kusoma na kufundisha fasihi iliyoandikwa kwa ki-Ingereza kutoka sehemu mbali mbali ulimwenguni, kwa kiwango kikubwa kuliko ilivyowezekana nilipokuwa ninafundisha katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mwandishi mmojawapo ambaye kazi zake nimezishughulikia sana ni Derek Walcott wa St. Lucia, pande za Caribbean, maarufu kwa utunzi wa mashairi na tamthilia, ambaye alipata tuzo ya Nobel mwaka 1992.

Nimesoma na kufundisha mashairi yake mengi na tamthilia zake kadhaa. Moja ya mashairi hayo ni "A Far Cry From Africa," ambalo lilichapishwa mwaka 1962. Linaelezea mahuzuniko juu ya vita ya Mau Mau nchini Kenya iliyodumu kuanzia mwaka 1952 hadi 1960. Masetla wazungu walipigana na wa-Afrika waliotaka kuchukua ardhi yao iliyoporwa. Kwa kuwa Derek Walcott ni chotara, damu ya kizungu na ki-Afrika, alihisi vita hiyo ikitokea ndani ya nafsi yake. Uhasama na ukatili wa pande hizo mbili aliuhisi mithili ya sumu katika mishipa ya damu yake. Alijihisi kama mateka aliyekosa namna ya kujinasua.

Walcott anaimudu lugha ya ki-Ingereza kwa namna inayonikumbusha umahiri wa Shakespeare. Nitafurahi iwapo nitapata ujasiri wa kujaribu kulitafsiri shairi kwa ki-Swahili.
-------------------------------------------------------------------------------

A Far Cry From Africa

Derek Walcott


A wind is ruffling the tawny pelt 
Of Africa, Kikuyu, quick as flies, 
Batten upon the bloodstreams of the veldt. 
Corpses are scattered through a paradise. 
Only the worm, colonel of carrion, cries: 
'Waste no compassion on these separate dead!' 
Statistics justify and scholars seize 
The salients of colonial policy. 
What is that to the white child hacked in bed? 
To savages, expendable as Jews?

Threshed out by beaters, the long rushes break 
In a white dust of ibises whose cries 
Have wheeled since civilizations dawn 
From the parched river or beast-teeming plain. 
The violence of beast on beast is read 
As natural law, but upright man 
Seeks his divinity by inflicting pain. 
Delirious as these worried beasts, his wars 
Dance to the tightened carcass of a drum, 
While he calls courage still that native dread 
Of the white peace contracted by the dead. 

Again brutish necessity wipes its hands 
Upon the napkin of a dirty cause, again 
A waste of our compassion, as with Spain, 
The gorilla wrestles with the superman. 
I who am poisoned with the blood of both, 
Where shall I turn, divided to the vein? 
I who have cursed 
The drunken officer of British rule, how choose 
Between this Africa and the English tongue I love? 
Betray them both, or give back what they give? 
How can I face such slaughter and be cool? 
How can I turn from Africa and live?

Tuesday, November 22, 2016

Ninaendelea Kusoma "Hamlet"

Miaka miwili iliyopita, niliandika katika blogu hii kuwa nina tabia ya kusoma vitabu kiholela. Wakati wowote nina vitabu kadhaa ninavyovisoma, bila mpangilio maalum, na pengine bila nia ya kufikia mwisho wa kitabu chochote.

Kusoma kwa namna hii hakuna ubaya wowote, bali kuna manufaa. Nilipokuwa mwanafunzi wa sekondari, katika seminari ya Likonde, mwalimu wetu, Padri Lambert OSB alituhimiza tuwe na mazoea ya kusoma sana vitabu, na pia mazoea ya kuvipitia vitabu kijuu juu, ambayo kwa ki-Ingereza huitwa "browsing."

Nikiachilia mbali vitabu ninavyofundisha, wakati huu nimezama zaidi katika kusoma Hamlet, kama nilivyoandika katika blogu hii. Ninasoma Hamlet pole pole, ili kuyanasa vizuri akilini yaliyomo, hasa maudhui kuhusu maisha, maadili, na tabia za binadamu. Kusoma pole pole kunaniwezesha kukifurahia ki-Ingereza cha Shakespeare, ingawa si rahisi kama ki-Ingereza tunachotumia leo.

Tofauti kati ya ki-Ingereza cha leo na kile cha Shakespeare ninaifananisha na tofauti kati ya ki-Swahili cha leo na kile cha mashairi ya zamani kama yale ya Muyaka au Utenzi wa Rasi lGhuli. Kwa msingi huo, kusoma utungo kama Hamlet ni chemsha bongo inayoboresha akili, sawa na mazoezi ya viungo yanavyoboresha afya ya mwili.

Mwandishi maarufu Ernest Hemingway alielezea vizuri thamani ya vitabu aliposema, "There is no friend as a loyal as a book," yaani hakuna rafiki wa kweli kama kitabu. Ujumbe uko wazi, nami sina la kuongeza. Kitabu bora ukishakinunua, ni rafiki wa kudumu.


  

Saturday, November 19, 2016

"Ozymandias:" Shairi la Shelley na Tafsiri Yangu

Percy Bysshe Shelley ni mmoja kati ya washairi maarufu kabisa katika ki-Ingereza, ambaye nilimtaja jana katika blogu hii. Alizaliwa mwaka 1792 akafariki mwaka 1822. Ni mmoja wa washairi wanaojumlishwa katika mkondo uitwao "Romanticism," ambamo wanaorodheshwa pia washairi wa ki-Ingereza kama William Blake, William Wordsworth, Samuel Taylor Coleridge, na Lord Byron. "Romanticism" ni mkondo uliojitokeza katika mataifa na lugha zingine pia, kama vile Ujerumani na Ufaransa. Kwa waandishi wa Afrika au wenye asili ya Afrika waliotumia ki-Faransa, "Romanticism" ilijitokeza kama "Negritude," jambo ambalo nimeelezea katika mwongozo wa Song of Lawino.

"Ozymandias" ni shairi mojawapo maarufu la Shelley. Ninakumbuka kuwa nililisoma kwa mara ya kwanza nilipokuwa sekondari, miaka ya kuanzia 1967. Kitu kimoja kinacholitambulisha shairi hili kuwa ni la mkondo wa "Romanticism" ni ule mtazamo wake ambao Edward Said aliuita "Orientalism." Lengo langu hapa si kuongelea "Romanticism" wala "Orientalism," bali kutaja mambo mawili matatu yanayohusu shairi la "Ozymandias" na suala la tafsiri.

Suala la kutafsiri kazi za fasihi nimeliongea tena na tena katika blogu hii. Pamoja na ugumu wake, ninaona kuwa baada ya mahangaiko yote, inakuja raha ya aina yake. Sio raha au furaha inayotujia tunaposhinda shindano au mtihani, kwani katika kutafsiri hakuna ushindi. Kinachotokea ni kuwa mtu unafanikiwa kuuzalisha upya utungo unaowania kuutafsiri.

"Ozymandias" ni shairi ambalo ninalielewa vizuri kabisa lilivyo katika ki-Ingereza. Lakini, nilivyojaribu kulitafsiri, tangu jana, limenihangaisha. Nimejionea jinsi ufahamu wangu wa ki-Swahili unavyopwaya. Nimejikuta nikijiuliza iwapo madai yetu wa-Tanzania kuwa tunakifahamu vizuri ki-Swahili ni ya kweli au ni porojo. Nilipata taabu zaidi kutafsiri mstari wa tano na mistari mitatu ya mwisho. Pamoja na kwamba nimeweka tafsiri yangu hapa, siridhiki nayo.

Kuhusu dhamira, shairi la "Ozymandias" lina mengi ya kujadiliwa. Kwa mtazamo wa fasihi linganishi, dhamira ya kisa cha msafiri inajitokeza katika tungo nyingi za tangu zamani. Mfano moja ni hadithi ya Misri ya kale iitwayo "The Tale of the Shipwrecked Sailor." Kuna pia hadithi za baharia Sindbad. Pia kuna shairi la Samuel Taylor Coleridge, "The Rime of the Ancient Mariner." Tungo zote hizi zina mambo ya ajabu na mtazamo juu ya ulimwengu na tabia za binadamu.

Vile vile, "Ozymandias" ni shairi lenye ujumbe mzito. Ni onyo kwa wanadamu kuwa utukufu wa hapa duniani, uimara wa himaya au udikteta ni vitu ambavyo vina mwisho. Ujumbe huu umo pia katika tungo zingine maarufu, kama vile utenzi wa Al Inkishafi. Naishia hapo.
--------------------------------------------------------------------------------------------------------

Ozymandias

Percy Bysshe Shelley, 1792-1822

I met a traveller from an antique land,
Who said: "Two vast and trunkless legs of stone
Stand in the desert.... Near them, on the sand,
Half sunk, a shattered visage lies, whose frown,
And wrinkled lip, and sneer of cold command,
Tell that its sculptor well those passions read
Which yet survive, stamped on these lifeless things,
The hand that mocked them, and the heart that fed;
And on the pedestal, these words appear:
'My name is Ozymandias, King of Kings;
Look on my Works, ye Mighty and despair!'
Nothing beside remains. Round the decay
Of that colossal Wreck, boundless and bare
The lone and level sands stretch far away."

Tafsiri

Nilimkuta msafiri kutoka nchi ya kale
Ambaye alisema, "Miguu miwili ya mawe mikubwa sana isiyo na kiwiliwili
Imesimama jangwani....Karibu nayo, mchangani,
Ukiwa umezama nusu, uso uliopasuka vipande umelala, mnuno wake,
Na mdomo uliokunyata, na dhihaka ya mamlaka yabisi
Vyabainisha kwamba mchongaji alizifahamu sawasawa hisia zile
Ambazo bado zimedumu, zikiwa zimebandikwa katika vitu hivi visivyo hai,
Mkono uliovidhihaki, na moyo uliovilisha,
Na kwenye sehemu ya kusimamia yanaonekana maneno haya:
'Jina langu ni Ozymandias, Mfalme wa Wafalme:
Yaoneni niliyofanikisha, enyi wenye mamlaka makuu, mkate tamaa!'
Hakuna kilichosalia, pembeni mwa uharibifu
Wa ile sanamu kuu iliyoporomoka, bila upeo bila chochote
Mchanga mpweke umetanda hadi mbali kabisa."

Friday, November 18, 2016

Mashairi Mazuri ya Ki-Ingereza

Tangu ujana wangu, nimebahatika kusoma na kuyafurahia mashairi mazuri ya ki-Ingereza. Ninakumbuka nilivyoingia kidato cha tano, Mkwawa High School, mwaka 1971, nikakutana na Mugyabuso Mulokozi na Kulikoyela Kahigi ambao nao walikuwa wanafunzi. Walikuwa na kitabu cha mashairi ya ki-Ingereza, tukawa tunayasoma na kuyafurahia. Mifano ni shairi la Thomas Hardy, "An Ancient to Ancients."

Mashairi ya Shakespeare yaitwayo "sonnets" yalituvutia. Mfano ni "Sonnet 18" ambayo mstari wake wa kwanza ni "Shall I compare thee to a summer's day?" Shairi la Samuel Taylor Coleridge, "The Rime of the Ancient Mariner," lilikuwa daima mawazoni mwetu. Shairi la W.B. Yeats, "The Second Coming," ni moja ya mashairi yaliyonigusa sana, kama nilivyoandika katika blogu hii. Shairi la Walter de la Mare, "The Listeners," limeng'ang'ania akili mwangu tangu enzi zile.

Mashairi mengine tulisoma darasani, kama vile yale ya Percy Bysshe Shelley na Alfred Lord Tennyson, ambao ni wa-Ingereza, na pia waandishi wa ki-Afrika kama vile Wole Soyinka, John Pepper Clark, Dennis Brutus, na Keorapetse Kgositsile. Hiyo ilikuwa ni miaka ya sabini na kitu.

Baada ya kuja masomoni katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, mwaka 1980, niliendelea kukutana na mashairi yenye mvuto mkubwa kwangu. Mifano ni shairi la William Wordsworth, "Lines Composed a Few Miles Above Tintern Abbey.'' Hilo tulilisoma kwa makini katika kozi ya "Poetry" iliyofundishwa na Profesa John Brenkman. Profesa Brenkman alitufundisha pia mashairi ya washairi wengine, kama vile Wallace Stevens.

Baada ya kuja kufundisha katika Chuo cha St. Olaf, mwaka 1991, nimepata fursa ya kusoma na kufundisha mashairi ya watunzi wengi zaidi, kuanzia wa Australia, kama vile Judith Wright na Oodgeroo Noonuccal hadi wa Marekani, kama vile Carl Sandburg na Lawrence Ferlinghetti, hadi wa Caribbean, kama vile Derek Walcott. Derek Walcott ni mshairi mojawapo ninayemwenzi sana, kwa uhodari wake wa kutumia lugha, kusisimua akili. na kuelezea hali halisi ya tabia na hisia za binadamu kwa upeo mpana wa historia na tamaduni mbali mbali.

Ninaendelea kusoma mashairi ya ki-Ingereza, ili kutajirisha akili yangu, na wakati mwingine ninayatafsiri kwa ki-Swahili. Kwa mfano nimetafsiri shairi la Stanley Kunitz, "The Layers," na shairi la Edmund Spencer, "Ye Tradefull Merchants." Ninajiona mwenye bahati kwa hizi fursa nilizo nazo za kufurahia kazi za watunzi maarufu. Jana, kwa mfano, nimesoma shairi la William Savage Landor, "To Wordsworth," nikaguswa sana.

Kuhitimisha ujumbe wangu, ninawazia ingekuwaje kama ningejua lugha nyingi zaidi, kama vile ki-Faransa, ki-Jerumani, ki-Hispania, na ki-Arabu, nikawa ninasoma tungo maarufu zilizomo katika lugha hizo.

Monday, November 14, 2016

Ninajikumbusha "Hamlet"

Wiki hii, pamoja na majukumu ya kawaida ya kufundisha, nimeamua kujikumbusha enzi za ujana wangu kwa kusoma Hamlet, tamthilia mojawapo maarufu kabisa ya Shakespeare. Kila ninapokumbuka tamthilia hii, ninakumbuka nilivyoangalia filamu yake yapata mwaka 1971, Mkwawa High School, Iringa.  Sir Laurence Olivier aliigiza nafasi ya Hamlet, kama nilivyogusia katika blogu hii.

Miaka ile ya ujana, tulifahamu ki-Ingereza vizuri hadi kusoma maandishi ya Shakespeare na kuyafurahia. Shakespeare ni kipimo kizuri cha ufahamu wa ki-Ingereza. Umahiri wake katika kutumia maneno na kutunga sentensi unadhihirika katika tungo zake zote. Ninanukuu hapa hotuba ya Claudius, mfalme wa Denmark, kwa Hamlet, ambayo ni kielelezo cha umahiri huo:

Tis sweet and commendable in your nature, Hamlet,
To give these mourning duties to your father;
But you must know, your father lost a father;
That father lost, lost his, and the survivor bound
In filial obligation for some term
To do obsequious sorrow. But to persever
In obstinate condolement is a course
Of impious stubborness. 'Tis unmanly grief;
It shows a will most incorrect to heaven,
A heart unfortified, a mind impatient,
An understanding simple and unschooled;
For what we know must be, and is as common
As any the most vulgar thing to sense,
Why should we in our peevish opposition
Take it to heart? Fie! 'tis a fault to heaven,
A fault against the dead, a fault to nature,
To reason most absurd, whose common theme
Is death of fathers, and who still hath cried,
From the first corse till he that died today,
"This must be so." We pray you throw to earth
This unprevailing woe, and think of us
As of a father; for let the world take note
You are the most immediate to our throne,
And with no less nobility of love
Than that which dearest father bears his son
Do I impart toward you. For your intent
In going back to school in Wittenberg,
It is most retrograde to our desire;
And we beseech you, bend you to remain
Here in the cheer and comfort of our eye,
Our chiefest courtier, cousin, and our son.


Sunday, November 13, 2016

Nimeteuliwa Kwenye Bodi ya Rochester International Association

Mwezi huu nimeteuliwa kujiunga na bodi ya Rochester International Association, ambayo makao yake ni mjini Rochester, Minnesota. Rochester International Association inashughulika na program mbali mbali za kujenga mahusiano mema miongoni mwa watu wa mataifa na tamaduni mbali mbali.

Moja ya programu hizo ni tamasha liitwalo World Festival, linalofanyika kila mwaka. Nimewahi kushiriki tamasha hili mara mbili, nikaelezea habari zake katika blogu yangu ya ki-Ingereza, na blogu hii ya hapakwetu.

Shughuli za bodi ni za kujitolea. Kwa miaka yote niliyoishi hapa Marekani, nimejionea jinsi wa-Marekani wanavyozijali shughuli za kujitolea, nami nimekuwa nikishiriki shughuli za aina hiyo, kama vile katika programu zinazowapeleka wanafunzi Afrika. Kujitolea kwa manufaa ya jamii kunaleta faraja na furaha moyoni.

Kushiriki kwangu katika Rochester International Association kutaniwezesha kuchangia mawazo katika masuala ya tamaduni kama nilivyoyaelezea katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kwa bahati nzuri, baadhi ya wanabodi wa Rochester International Association wamesoma kitabu hiki na ndio maana wamenipokea kwa msisimko.

Kushiriki shughuli za Rochester International Association ni jambo la manufaa kwangu katika kujijenga katika shughuli zangu za kutoa ushauri ambazo ninafanya chini ya mwavuli wa kampuni ndogo ya Africonexion: Cultural Consultants. Vile vile ni fursa ya kuiwakilisha Tanzania na Afrika huku mbali Marekani.

Sunday, November 6, 2016

Buriani Mwandishi John Calvin Rezmerski

Leo hapa Minnesota zimeenea taarifa za kufariki kwa mwandishi John Calvin Rezmerski. Taarifa moja imechapishwa katika Minneapolis Star Tribune. Nilipata bahati ya kuonana naye miaka michache iliyopita mjini Mankato, Minnesota, kwenye tamasha la vitabu, Deep Valley Book Festival. Tuliongea, nikanunua kitabu chake cha mashairi kiitwacho What Do I Know?: New & Selected Poems, ambacho alikisaini hivi:

for Joseph Mbele--
Wonderful to talk with you at Deep Valley Book Festival,
John Calvin Rezmerski

Taarifa tulizopata leo zinaelezea mambo mema mengi ya bwana Rezmerski: alikuwa mwandishi makini wa mashairi, msimuliaji hadithi, mwalimu aliyependwa, mkarimu kwa watu. Kuhusu falsafa ya ushairi ya Rezmerski, Bill Holm, ambaye ni mwandishi maarufu hapa Minnesota, aliwahi kuandika: "John Rezmerski believes that poetry lives inside the daily speech of ordinary people, that the ear and the mouth are connected to the imagination and the heart."

Dhana hiyo ya ushairi inanikumbusha falsafa ya Shaaban Robert na pia William Wordsworth kuhusu ushairi. Inaendana hasa na falsafa ya Wordsworth, ambaye aliamini kuwa lugha ya watu wa kawaida ndio chimbuko la ushairi halisi na ndio inapaswa kutumiwa na washairi, tofauti na lugha ya urasimi, ambayo haikuendana na hisia halisi za binadamu bali ilikuwa lugha tasa.

Mara baada ya kusikia taarifa za kifo cha Rezmerski, nimetafuta nakala yangu ya What Do I Know?: New & Selected Poems, ili kusoma mashairi yaliyomo, kama njia ya kumkumbuka mwandishi huyu ambaye nilibahatika kumwona, ingawa ni mara moja tu. Shairi lake moja ni hili:

THE FUGITIVE

What if after all these years
in the same body,
I turn out to be somebody else?
What a new thing
to decide which pair of pants.
How sweet to have grapefruit
and like it for the first time.
I would burn old letters,
buy a new toothbrush,
learn to like the closeness
of cold on my clean skin.
I would pronounce every word
as though it were fine glass.
It is an old story
I tell the mirror
while I gape at my teeth
looking for someone else's cavities.

Nimelipenda shairi hili kwa jinsi linavyotumia mbinu mbali mbali za kuchezea akili ya msomaji, kuanzia kejeli hadi ubunifu wa mambo yasiyowezekana, hadi kuangalia mambo tuliyoyazoea kwa mtazamo wa kuyafanya yawe ya ajabu. Shairi limejaa mawazo na kauli tusizotegemea. Ili kulisoma na kulitafakari shairi hili kwa umakini, makala maarufu ya Cleanth Brooks, The Language of Paradox, inaweza kusaidia sana.

Saturday, November 5, 2016

Mteja wa Uingereza Kanunua Kitabu

Leo kwenye tovuti ninapochapisha vitabu vyangu nimeona kuwa mteja aliyeko Uingereza amenunua nakala ya Notes on Achebe's Things Fall Apart. Uzuri wa uchapishaji wa namna hii ninayotumia ni kuwa mwandishi unaweza kufuatilia taarifa kama hizi za mauzo, ukajua kitabu kimenunuliwa sehemu gani ya dunia, nakala ngapi, na malipo yako ni kiasi gani.

Kwa miaka yote tangu nilipoanza kuchapisha vitabu kwenye tovuti ya lulu.com maelfu ya wateja walionunua vitabu vyangu wamefanya hivyo kutokea hapa Marekani. Nilikuwa na hisia kuwa hii ni kwa kuwa utamaduni wa kununua vitu mtandaoni ulikuwa bado kujengeka sehemu zingine za dunia.

Ninahisi kuwa huyu mteja aliyenunua Notes on Achebe's Things Fall Apart ni mwalimu wa fasihi. Kama ni hivyo, ninafurahi kuwa atapata mawazo mapya juu ya Things Fall Apart. Ingawa kuna miongozo mingi ya Things Fall Apart, mwongozo wangu umepata umaarufu hata ukateuliwa kama mwongozo kwa wanafunzi katika chuo kikuu cha Cornell, ambacho kina jina kubwa katika masomo ya lugha na fasihi ya ki-Ingereza.

Vile vile, hivi karibuni, nilipohudhuria mkutano wa Africa Network, profesa Eric Michael Washington wa chuo cha Calvin aliniambia jinsi anavyotumia mawazo yaliyomo katika mwongozo huo, katika ufundishaji wake wa Things Fall Apart. Alisema anavutiwa zaidi na jinsi ninavyomwelezea mhusika aitwaye Unoka.

Mambo hayo yananipa hamasa ya kuendelea kuandika miongozo ya kazi za fasihi, azma ambayo niliwahi kuielezea katika blogu hii. Mimi kama mwalimu wa fasihi ninafarijika kuyaweka hadharani mawazo yangu kuhusu fasihi, ambayo yatadumu. 

Wednesday, November 2, 2016

Nimenunua Webster's Concise Dictionary and Thesaurus

Jana nilinunua nakala ya Webster's New World Concise Dictionary and Thesaurus, iliyochapishwa mwaka 2014. Hili ni toleo jipya la kitabu hiki ambacho kimekuwa kikichapishwa kwa miaka mingi. Kitabu hiki ni hazina ya pekee kwa kuwa kinajumlisha kamusi na "thesaurus."

Kwa wale wasiofahamu tofauti za vitu hivi viwili, napenda kusema kwa kifupi kwamba kamusi hutoa tafsiri za maneno. "Thesaurus," badala ya kutoa tafsiri ya neno, huorodhesha maneno ambayo maana zake zinafanana au kukaribiana na neno hilo.

Kwa mfano, katika kitabu nilichonunua leo, sehemu ya thesaurus, neno "docile" limewekewa maneno yafuatayo: "meek, mild, tractable, pliant, submissive, accommodating, adaptable, resigned, agreeable, willing, obliging, well-behaved, manageable, tame, yielding, teachable, easily influenced, easygoing, usable, soft, childlike."

Mfano huu unaonyesha wazi ubora na upekee wa "thesaurus." Kwa kuyaorodhesha maneno yenye maana zinazofanana au kukaribiana, mtu unakumbushwa msamiati wa lugha. Kama ni mzoefu wa kusoma unayeyatambua maneno hayo na unapenda kuchagua neno la kulitumia, kazi yako inakuwa imerahisishwa. Inatakiwa uwe na ufahamu wa tofauti ndogo ndogo za maana au msisitizo zilizomo katika maneno kama zile ambazo kwa ki-Ingereza huitwa "denotation" na "connotation" ili uweze kuchagua neno lifaalo kuliko mengine katika muktadha wa uandishi wako.

Nimenunua Webster's New World Concise Dictionary and Thesaurus ingawa ninazo "thesaurus" tangu zamani, nilipokuwa sekondari, ambapo niliifahamu Roget's Thesaurus. Kwa nini nimenunua "thesaurus" nyingine leo? Ni kwa kuwa ni toleo jipya. Vile vile, mara kwa mara ninanunua kitabu ambacho nakala yake ninayo, kama nilivyowahi kueleza katika blogu hii.

Nakala za ziada za vitabu muhimu ni baraka. Ninapokwenda Tanzania, huwa sikosi kuchukua vitabu kadhaa kuzigawa kwenye maktaba za jamii au vyuo. Kwa miaka mingi, nimekuwa na wazo kwamba ukipeleka kamusi ya ki-Ingereza, kwa mfano, kwenye shule yoyote, ni kama unaanzisha mapinduzi katika ufundishaji wa somo la ki-Ingereza katika shule hiyo. Unakuwa umemwezesha mwalimu kufahamu uandishi sahihi wa maneno ya ki-Ingereza. Vile vile, kwa kuwa kamusi kwa kawaida hutoa pia mifano ya matumizi ya maneno, unakuwa umemjengea mwalimu fursa ya kujiongezea ufahamu wa lugha. Unakuwa umeweka msingi wa kuboresha somo la ki-Ingereza kwa wanafunzi.

Kitabu ni rasilimali na pia ni mtaji. Kupeleka kitabu muhimu popote nchini kikasomwe ipasavyo ni aina ya uwekezaji. Hilo ni jambo linaloeleweka kwa yeyote anayefahamu kuwa dunia inaingia zaidi na zaidi katika enzi za uchumi unaoendeshwa na elimu na maarifa. Hiyo ndiyo dhana ya "knowledge economy." 

Monday, October 31, 2016

Black African Voices: Tungo za Afrika

Pamoja na kwamba fasihi ya Afrika, kama ilivyo ulimwenguni kote, inastawi kwa kasi kadiri miaka inavyopita, na waandishi wapya hujijokeza na kujipambanua, ni lazima pia kukumbuka na kusoma uandishi wa zamani. Kwa yeyote anayependa fasihi, awe ni mwanafunzi, mwalimu au msomaji wa kawaida, usomaji wa aina hii ni jambo lisilohitaji mjadala. Fasihi inahitaji usomaji usio na kikomo, sio tu kwa kuwa ina historia ndefu, bali pia kwa kuwa inastawi ulimwenguni kote na daima inaendelea kuchanua kama maua.

Mimi, mwalimu wa fasihi, ninazingatia umuhimu wa kufundisha kazi za tangu zamani hadi leo. Fasihi ya kila taifa au sehemu yoyote ya dunia ina historia, na fasihi inayoandikwa leo ni mwendelezo wa mkondo ulioanza zamani.

Katika siku hizi chache, nimekuwa ninasoma Black African Voices, kitabu kilichohaririwa na James E. Miller na wenzake. Sikumbuki ni lini nilikinunua kitabu hiki, lakini mara kwa mara katika kuangalia vitabu vyangu, nilikuwa ninakichungulia kitabu hiki, nikawa ninakumbuka kwa furaha enzi za ujana wangu, kuanzia miaka ya sitini na kitu, nilipokuwa ninasoma badhi ya tungo zilizomo. Kuna hadithi kadhaa na nyimbo za fasihi simulizi, mashairi, hadithi fupi na maandishi mengine ya waandishi mbali mbali.

Baadhi ya waandishi ambao tungo zao zimo katika kitabu hiki ni Ezekiel Mphahlele, Raphael Armatoe, Peter Abrahams, Birago Diop, David Diop, Cyprian Ekwensi, Richard Rive, Wole Soyinka, John Pepper Clark, James D. Rubadiri, na Grace Ogot. Ni furaha isiyoelezeka kuzisoma tena hadithi zilizonisisimua tangu miaka ile ya sitini na kitu, nilipokuwa mwanafunzi katika seminari ya Likonde, 1967-70 na Mkwawa High School, 1971-72.

Baadhi ya hadithi hizo ni "No Room at Solitaire," ya Richard Rive; "The Dignity of Begging," ya Bloke Modisane, "The Rain Came," ya Grace Ogot. Baadhi ya mashairi yaliyonisisimua miaka ile ni "Stanley Meets Mutesa" (James D. Rubadiri), "Africa" na "Listen Comrades" (David Diop), na "Prayer to Masks" (Leopold Sedar Senghor). Kuna pia tamthilia ya Edufa ya Efua Sutherland.

Katika Black African Voices kuna pia tungo za waandishi ambao sikuwafahamu miaka ile ya ujana wangu, kama vile J, Benibengor Blay (Ghana), Tshakatumba (Congo), Rui Nogar (Mozambique). Siwezi kuwataja waandishi wote ambao kazi zao zimo katika kitabu hiki, bali ninapenda tu kusisitiza kuwa ninaguswa sana na uandishi huu wa kuanzia miaka ya kabla ya kuzaliwa kwangu hadi ujana wangu. Wahariri walifanya kazi nzuri kuzikusanya tungo hizi katika kitabu kimoja.

Wednesday, October 26, 2016

Miaka 80 ya "The Snows of Kilimanjaro"

Kwa mara nyingine tena, ninaandika ujumbe kuhusu kutimia kwa miaka 80 tangu hadithi ya Ernest Hemingway, 'The Snows of Kilimanjaro" ilipochapishwa kwa mara ya kwanza. Niliandika ujumbe wa aina hiyo katika blogu hii. Leo nimesoma tena ujumbe wangu, nikajiridhisha kwamba niliyosema ndiyo ninayoamini hadi sasa.

Jambo moja kubwa kabisa ni kuwa wa-Tanzania tunajipotezea fursa za wazi za kutumia hazina kama hii hadithi ya Hemingway kuitangaza nchi yetu. Niliandika katika ujumbe wangu baadhi ya mambo ambayo tungeyafanya mwaka huu wa kumbukumbu. Lakini mwaka unaelekea ukingoni, na hakuna tulichofanya. Hii ni hasara ya kukosa utamaduni wa kusoma vitabu. Tunashindwa hata kutumia fursa zilizo wazi.

Nimeona niandike ujumbe huu leo kwa sababu wiki hii, hapa katika Chuo cha St. Olaf ninapofundisha, litatokea jambo la pekee linalohusiana na Ernest Hemingway. Keshokutwa, tarehe 28, pataonyeshwa kwa mara ya kwanza filamu ya "Papa's Shadow," ambayo niliwahi kuielezea katika blogu hii.

Hiyo ni filamu iliyotokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwaka 2013 iitwayo Hemingway in East Africa. Nilisafiri na wanafunzi 29 wa Chuo cha St. Olaf, tukazunguka maeneo kadhaa ya Tanzania kaskazini, ambamo alipita Ernest Hemingway mwaka 1933-34. Katika safari hiyo, tulikuwa tunasoma maandishi ya Hemingway kuhusu maeneo hayo na maeneo mengine ambayo alipitia mwaka 1953-54.

Maandishi hayo ni pamoja na Green Hills of Africa na Under Kilimanjaro, ambavyo ni vitabu, kadhalika hadithi fupi mbili: "The Short Happy Life of Francis Macomber" na "The Snows of Kilimanjaro." Pia aliandika makala katika magazeti na barua nyingi akielezea aliyoyaona na kufanya katika safari zake. Kwa ujumla wake, maandishi haya ya Ernest Hemingway yanaitangaza nchi yetu na Afrika Mashariki kwa ujumla kwa namna ambayo sisi wenyewe hatujaweza kujitangaza.

Hiyo filamu ya "Papa's Shadow" inawasilisha vizuri mambo muhimu ya uhusiano wa Ernest Hemingway na Afrika Mashariki. Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway. Tunajadili kwa kina na mapana fikra za Ernest Hemingway kuhusu Afrika, uandishi, na maisha kwa ujumla.

Kwa kuwa hiyo filamu inaonyesha sehemu mbali mbali za Tanzania na maelezo kuhusu mambo yanayoifanya Tanzania kivutio kwa watalii, kama vile Mlima Kilimanjaro, na kwa kuwa filamu hii imejengeka katika maandishi ya Ernest Hemingway, mwandishi maarufu sana ulimwenguni, ni wazi kuwa filamu hii itakuwa chachu ya kuitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Taarifa zaidi Kuhusu "Papa's Shadow," zinapatikana kwenye tovuti ya Ramble Pictures.

Monday, October 24, 2016

Ninarekebisha Kitabu Nilichochapisha Mtandaoni

Mara kwa mara, ninaongelea suala la kuchapisha vitabu mtandaoni, kutokana na uzoefu wangu. Ninatarajia kuwapa wengine uzoefu wangu wa kutumia tekinolojia za uchapishaji mtandaoni, ambazo zinatoa fursa tele kwa yeyote kujikomboa na taabu na vikwazo vya uchapishaji wa jadi.

Faida mojawapo ya uchapishaji wa aina ninayotumia kuchapishia vitabu vyangu ni fursa isiyo na mipaka ya kurekebisha kitabu chako wakati wowote uonapo dosari ndani yake au fursa ya kukiboresha. Hilo linawezekana kwa kuwa mswada wako unakuwa umehifadhiwa kama faili la kielektroniki mtandaoni, hata kama hukuuhifadhi katika kompyuta, disketi, au kifaa kingine.

Mimi ninatumia mtandao wa lulu.com. Hapo, ukishachapisha kitabu, nakala ya mswada inahifadhiwa hapo hapo mtandaoni. Unapotaka kurekebisha kitabu chako, unachofanya ni kuuingiza "(down-loading") mswada katika "flash drive" na kuufanyia marekebisho. Kisha unaurudisha ("up-loading") sehemu ya kuchapishia. Yeyote atakayekinunua baada ya hapo atakuwa ananunua kitabu kilichoboreshwa.

Hatua zote hizi zinafanyika bila mtu yeyote kutambua kinachotokea, bali wewe mhusika tu. Na wakati wote, unaporekebisha mswada, kitabu hakitoweki hapo mtandaoni. Kinakuwa kama kilivyokuwa mwanzo, na yeyote anaweza kukinunua, wakati wewe unaendelea na marekebisho. Unapomaliza marekebisho na kukiingiza tena mtandaoni ("up-loading"), ndipo kitabu kilichoboreshwa kinachukua nafasi ya kile cha awali.

Sasa hivi, niko katika kurekebisha kitabu changu, Notes on Okot p'Bitek's Song of Lawino. Hakuna anayetambua kuwa kinafanyiwa marekebisho, kwani kinaonekana hapo mtandaoni kama kawaida. Nitakapomaliza marekebisho na kukichapisha tena, itakuwa kama vile hakuna lililotokea.

Urahisi huu wa kurekebisha kitabu hauko katika uchapishaji wa jadi, ambapo inabidi kungoja hadi wakati wa kutoa toleo jipya la kitabu. Aghalabu, wachapishaji huwa hawana uwezo wa kifedha wa kutoa toleo jipya. Nakala zikiisha, huwa ndio mwisho wa kuchapishwa kitabu.

Lakini tatizo hili haliko katika uchapishaji wa mtandaoni kama huu ninaotumia. Kitabu hakiwezi kutoweka, yaani kuwa "out of print," labda mtu uamue kukiondoa wewe mwenyewe hapo mtandaoni. Ukibadili mawazo ukataka kukirudisha tena ulimwenguni, ni hiari yako kufanya hivyo, wakati wowote. 

Sunday, October 23, 2016

Siku ya Mashujaa wa Kenya, Rochester, Minnesota

Jana nilikwenda mjini Rochester, Minnesota, kuhudhuria sherehe ya siku ya Mashujaa wa Kenya. Hii ni sikukuu ambayo wa-Kenya huifanya kila mwaka tarehe 20 Oktoba, kuwakumbuka mashujaa wa tangu enzi za kupigania uhuru hadi leo. Sherehe ya jana iliandaliwa na jumuia ya wa-Kenya waishio Rochester.

Nilipata taarifa ya sikukuu hii kutoka kwa Olivia Njogu, m-Kenya aishiye Rochester, na mwanabodi wa Rochester International Association. Anaonekana pichani hapa kushoto, wa pili kutoka kulia. Chama hiki huandaa tamasha la kimataifa kila mwaka, na Olivia tulifahamiana niliposhiriki tamasha hilo mwaka huu, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Baada ya tamasha, Olivia alisoma kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na kisha akaniandikia kunielezea alivyokipenda. Taarifa hiyo niliiandika katika blogu hii.

 .


Hii haikuwa mara yangu ya kwanza kuhudhuria sherehe za wa-Kenya hapa Marekani. Daima nimependezwa kujumuika nao, kama nilivyowahi kuandika katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Hali ilikuwa hivyo hivyo jana. Nilivyokuwa ninapaki gari kwenye eneo la sherehe, walikuja wa-Kenya kadhaa kunipokea, ingawa hatukuwa tunafahamiana. Tulitambulishana na hima tukazama katika maongezi ya dhati na michapo.













Hii ilikuwa ni sherehe iliyojumuisha watoto vijana na watu wazima. Pamoja na maongezi yasiyo kikomo, vicheko na chereko, kulikuwa na vyakula tele na muziki. Nilivutiwa kwa namna ya pekee na muziki wa Kenya, nikakumbuka safari zangu za Kenya kuanzia mwaka 1989, za utafiti juu ya tungo za zamani na utamaduni wa wa-Swahili.














Picha hapa kushoto ni ushahidi wa hali ya furaha iliyotawala.






























Wengi waliohudhurua sherehe ya jana sikuwa nimefahamiana nao kabla, ingawa wachache walinikumbuka kwa kuwa waliniona katika tamasha la kimataifa la Rochester la mwaka huu.

Sherehe hii haikuwa ya wa-Kenya pekee. Ingawa sikuweza kuongea na kila mtu, nilipata fursa ya kuongea na watu wawili wa mataifa mengine: mmoja kutoka Nigeria na mwingine kutoka Uganda.




Katika kuishi kwangu hapa Minnesota, nimeweza kufahamiana na wa-Afrika wengi waishio Minneapolis, St. Paul, na maeneo ya jirani. Sasa ninafurahi kuweza kujenga mtandao wa aina hiyo maeneo ya Rochester.

Wanadiaspora wa Afrika tuna wajibu wa kujenga mshikamano miongoni mwetu, kama msingi wa ushirikiano katika bara letu. Waliotutangulia huku ughaibuni, kama akina Peter Abrahams, Jomo Kenyatta, na Kwame Nkrumah walifanya hivyo. Kwangu kama mwandishi na mwalimu, hizi zote ni fursa za kielimu. Darasa ni popote, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.


Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...