Showing posts with label Africonexion: Cultural Consultants. Show all posts
Showing posts with label Africonexion: Cultural Consultants. Show all posts

Friday, January 17, 2020

Mwaliko wa African Travel Seminars

Nimepata mwaliko kutoka African Travel Seminars wa kushiriki shughuli itakayofanyika tarehe 22 Februari. Mada siku hiyo itakuwa "Celebrating Black Culture Through Travel." Kutakuwa na chakula, maonesho na michezo mbali mbali kuhusu Afrika.

Nimealikwa kuongelea kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho African Travel Seminars hutumia kwa watalii wanaoenda Afrika.

African Travel Seminars inaelimisha na kujenga mahusiano baina ya watu kupitia utalii. Hivi karibuni, tumeamua kushirikiana. Malengo ya kampuni hiyo yanafanana kwa namna fulani na ya kampuni yangu ndogo ninayojaribu kuikuza iitwayo Africonexion: Cultural Consultants.

Saturday, November 30, 2019

Wadau wa Utalii wa Kielimu Tumekutana

Tarehe 2 Novemba nilikutana na mama Georgina, ambaye anatoka Ghana na ni mmiliki wa kampuni iitwayo African Travel Seminars. Anapeleka wasafiri kwenda nchi za Afrika, kuanzia kaskazini, hadi kusini, mashariki hadi magharibi, na Tanzania imo. Mbali ya kuwaonesha vivutio vya utalii, anawaelimisha kuhusu maisha na tamaduni za waAfrika.

Niliifahamu kuhusu kampuni yake kuanzia miaka ya tisini na kitu, nikaona jinsi shughuli zake zinavyofanana na zangu, ambazo zimeelezwa katika tovuti ya Africonexion. Hivi karibuni nilianza kuwasiliana na huyu mama, na tukapanga kukutana.

Kabla hatujakutana, mama huyu alisoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ameamua awe anawapa wageni anaowapelea Afrika. Yeye nami tunafahamu kuwa hii itawawezesha wageni kuelewa mwenendo na tabia za waAfrika na pia kujielewa namna wao wenyewe wanavyoeleweka kwa mtazamo wa waAfrika.

Tumejithibitishia kuwa malengo yetu yanafanana. Tunapenda kuendeleza elimu kuhusu Afrika kwa waMarekani na tunapenda kujenga maelewano baina ya waMarekani na waAfrika. Yeye nami tuna uzoefu wa kuongelea masala haya hapa Marekani, kwa wanafunzi na walimu, watu wanaoenda Afrika kwa shughuli za kujitolea, watalii, nakadhalika.

Sunday, February 12, 2017

Nimemaliza Kusoma The Highly Paid Expert

Leo nimemaliza kusoma The Highly Paid Expert, kitabu kilichotungwa na Debbie Allen, ambacho nilikitaja katika blogu hii. Nimekifurahia kitabu hiki, kwa jinsi kilivyoelezea misingi na mbinu za kumwezesha mtu kuwa mtoa ushauri mwenye mafanikio kwake na kwa wateja.

Mambo anayoelezea mwandishi Debbie Allen yananihusu moja kwa moja katika ya kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants. Kwa hivi, kitabu hiki kimekuwa na mvuto wa pekee kwangu. Nimevutiwa na namna mwandishi anavyoelezea mbinu za mtu kujijenga katika uwanja wake hadi kufikia kileleni. Anaelezea mategemeo ya wateja na namna ya kushughulika nao. Anaelezea umuhimu wa kujifunza kutoka kwa wataalam wengine, matumizi ya tekinolojia katika kuwasiliana na wateja, kuendesha mikutano, na kujitangaza. Vile vile anasisitiza uaminifu na uwajibikaji.

Ameelezea vizuri namna wengi wetu tunavyoshindwa kujitangaza na tunavyoshindwa au kusita kutambua umaarufu na umuhimu wetu na thamani ya ujuzi wetu, jambo ambalo linatufanya tusitegemee malipo yanayoendana na ubingwa wetu. Tunaridhika na malipo hafifu, wakati tulistahili malipo makubwa.

Sura ya 24 ya The Highly Paid Expert inaelezea uandishi wa kitabu. Mwandishi anasema kuwa kitabu ni nyenzo muhimu ya mtaalam katika fani yake. Kitabu kinamjengea sifa na kuonekana. Kinamfanya mtaalam aaminike. Mwandishi anaeleza wazi kuwa kitabu hakileti utajiri, bali kinafungua milango ya fursa.

Hayo nimejionea mwenyewe. Kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimenifungulia fursa nyingi. Nimepata mialiko ya kwenda kutoa mihadhara au ushauri katika taasisi na jumuia mbali mbali, kama vile makanisa, vyuo, na makampuni.

Nimevutiwa na mambo anayoelezea mwandishi wa The Highly Paid Expert kuhusu uandishi na uuzaji wa kitabu. Yanafanana na yale ambayo nami nimekuwa nikieleza katika blogu hii. Kwa mfano, anasema kuwa jukumu kubwa la kutangaza na kuuza kitabu ni la mwandishi.

The Highly Paid Expert ni kati ya vitabu ambavyo nimevifurahia kwa dhati. Mawaidha yake mengi ni ya kukumbukwa daima. Mfano ni msisitizo wake juu ya kushirikiana na wengine. Mtu hufanikiwi kwa uwezo wako mwenyewe tu na kutojihusisha na wengine wenye utaalam, hata kama ni washindani wako.

Monday, January 30, 2017

Kitabu Nilichonunua Leo: "The Highly Paid Expert"

Leo nilikwenda Minneapolis na wakati wa kurudi, nilipita Mall of America, kuangalia vitabu katika duka la Barnes & Noble. Nilitaka hasa kuona kama kuna vitabu vipya juu ya mwandishi Ernest Hemingway.

Niliangalia scheme vinapowekwa vitabu vya fasihi, nikakuta kitabu kipya juu ya Ernest Hemingway, Everybody Behaves Badly: The Backstory to 'The Sun Also Rises.' kilichoandikwa na Lesley M.M. Blume. Kwa kuwa nimezama sana katika uandishi wa Hemingway, maisha na falsafa yake, na kwa kuwa nimeshasoma The Sun Also Rises, nilitamani kukinunua kitabu hiki, ambacho, kwa maelezo niliyoyaona, kinazungumzia yaliyo nyuma ya pazia.

Sikuwa na hela za kutosha, kwa hivyo nikaamua kuangalia vitabu vingine. Nilitumia muda zaidi katika sehemu ya "Business/Management." Huwa ninapenda sana kununua na kusoma vitabu vya taaluma hii, kwani vinanifundisha mengi kuhusu mambo ya ujasiriamali na biashara. Taaluma hii inanisaidia katika kuendesha shughuli za kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants.

Hatimaye, nilikiona kitabu kilichonivutia kwa namna ya pekee, The Highly Paid Expert, kilichoandikwa na Debbie Allen.  Kwa mujibu maelezo nyuma ya kitabu, huyu mwandishi ni mtaalam maarufu katika mambo ya biashara na ujasiriamali. Niliangalia ndani, nikaona mada anazoongelea ni za kuelimisha kabisa, kama vile matumizi ya tekinolojia za mawasiliano na mitandao.

Niliona anatoa ushauri wa kusisimua. Kwa mfano, anasema kuwa ni lazima mtu unayetaka mafanikio katika shughuli zako, uwasaidie wengine kufanikiwa. Unavyowasaidia wengine wafanikiwe, unajijengea mtandao wenye manufaa kwako pia. Ubinafsi na uchoyo wa maarifa haukuletei mafanikio. Kitabu hiki kinavutia kwa jinsi mwandishi anavyothibitisha mawazo yake, ambayo kijuu juu yanaonekana kama ya mtu anayeota ndoto.

Kwa bahati niliweza kuimudu gharama ya kitabu hiki, nikakinunua na kuondoka zangu, kwani nilikuwa sina hela iliyosalia. Sijutii kununua vitabu. Vitabu vinavyoelimisha ni mtaji, kwani hakuna mtaji muhimu zaidi ya elimu. Kwa wajasiriamali, wafanya biashara, watoa huduma, na kwa kila mtu, elimu ni tegemeo na nguzo muhimu. Ulazima wa kununua vitabu ni sawa na ilivyo lazima kwa mkulima kununua pembejeo.

Sunday, November 13, 2016

Nimeteuliwa Kwenye Bodi ya Rochester International Association

Mwezi huu nimeteuliwa kujiunga na bodi ya Rochester International Association, ambayo makao yake ni mjini Rochester, Minnesota. Rochester International Association inashughulika na program mbali mbali za kujenga mahusiano mema miongoni mwa watu wa mataifa na tamaduni mbali mbali.

Moja ya programu hizo ni tamasha liitwalo World Festival, linalofanyika kila mwaka. Nimewahi kushiriki tamasha hili mara mbili, nikaelezea habari zake katika blogu yangu ya ki-Ingereza, na blogu hii ya hapakwetu.

Shughuli za bodi ni za kujitolea. Kwa miaka yote niliyoishi hapa Marekani, nimejionea jinsi wa-Marekani wanavyozijali shughuli za kujitolea, nami nimekuwa nikishiriki shughuli za aina hiyo, kama vile katika programu zinazowapeleka wanafunzi Afrika. Kujitolea kwa manufaa ya jamii kunaleta faraja na furaha moyoni.

Kushiriki kwangu katika Rochester International Association kutaniwezesha kuchangia mawazo katika masuala ya tamaduni kama nilivyoyaelezea katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kwa bahati nzuri, baadhi ya wanabodi wa Rochester International Association wamesoma kitabu hiki na ndio maana wamenipokea kwa msisimko.

Kushiriki shughuli za Rochester International Association ni jambo la manufaa kwangu katika kujijenga katika shughuli zangu za kutoa ushauri ambazo ninafanya chini ya mwavuli wa kampuni ndogo ya Africonexion: Cultural Consultants. Vile vile ni fursa ya kuiwakilisha Tanzania na Afrika huku mbali Marekani.

Sunday, August 2, 2015

Bendera ya Tanzania Katika Tamasha la Afrifest 2015

Jana, tarehe 1 Agosti, tamasha la Afrifest lilifanyika mjini Brooklyn Park, Minnesota. Hili ni tamasha ambalo huandaliwa mara moja kwa mwaka na bodi ya Afrifest Foundation ambayo mimi ni mwenyekiti wake. ili kuwakutanisha wa-Afrika, watu wenye asili ya Afrika waishio Marekani ya Kaskazini, Kati, na Kusini, pamoja na Caribbean, na pia watu wa mataifa mengine. Lengo kubwa ni kufahamiana, kuelimisha, na kuuenzi mchango wa watu weusi duniani kote, katika nyanja mbali mbali.

Hiyo jana ilikuwa ni mara ya kwanza kwa bendera ya Tanzania kupepea kwenye tamasha la Afrifest. Baada ya kushiriki matamasha na kujionea wenzetu wanavyotumia fursa kuzitangaza nchi zao, nilijiuliza kwa nini nisitafute bendera ya Tanzania, kama nilivyoeleza katika blogu hii.

Hatimaye, nilifanya uamuzi wa kununua bendera, niwe ninaipeperusha kwenye matamasha ninayoshiriki, maadam fursa zipo. Hapo kushoto naonekana na binti zangu Assumpta na Zawadi kwenye meza yetu, hiyo jana.
Sawa na kuweka vitabu mezani katika tamasha, ambavyo huwavutia watu waje kuulizia habari zake, sawa na kutundika bendera ya kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants, ambayo nayo huwavutia watu waje kuulizia maana ya Africonexion, bendera hiyo nayo ni kivutio na kianzio cha mazungumzo kuhusu Tanzania.

Miaka yote, nimekuwa nikishiriki matamasha chini ya kivuli cha kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants. Hata hivi katika kuelezea shughuli zangu, sikujiwekea mipaka, kwani utafiti wangu, ufundishaji, uandishi na utoaji ushauri katika masuala ya athari za tofauti za tamaduni, nagusia dunia yote, ikiwemo Tanzania. Lakini kuitundika bendera ya Tanzania kama nilivyofanya jana kunaongeza mwonekano wa nchi katika nchi za dunia.

Kwa kuwa bendera hiyo ilipepea hapo uwanjani siku nzima, kila mtu katika umati wa waliohudhuria tamasha aliiona. Wengi wa waliohudhuria walipiga picha hapo uwanjani, na haikwepeki bendera kuonekana katika baadhi ya picha.

Thursday, January 26, 2012

Africonexion: Kampuni Chipukizi

Mwaka 2002 nilisajili kampuni katika jimbo la Minnesota ambayo niliita Africonexion. Nilichagua aina ya usajili iitwayo "sole proprietorship." Yaani mmiliki na mhusika mkuu ni mimi.

Nilianzisha Africonexion kama chombo cha kushughulikia elimu kuhusu tamaduni duniani, kwa kuandika, kuchapisha, na kuuza vitabu, na kutoa mihadhara na ushauri kwa watu binafsi, mashirika, taasisi, makampuni, na kadhalika, kama ninavyoripoti mara kwa mara katika blogu zangu.


Africonexion ni kampuni ndogo sana kwa wakati huu, kwa maana kwamba sina timu ya wafanyakazi au washiriki. Lakini nimeitumia vizuri kama fursa ya kujielimisha, kwa kuzingatia kuwa elimu ni mtaji bora kuliko hata fedha. Shughuli zote ninazofanya, iwe ni kuandika au kutoa mihadhara au ushauri kwa watu binafsi, ni kama shule kwangu. Hii picha hapa kushoto ilipigwa wakati wa maonesho fulani Brooklyn Park, Minnesota.



Ninataka kuipeleka kampuni hii Tanzania na kwingineko. Nimeshaendesha warsha Dar es Salaam, Zanzibar na Pemba, Tanga, na Arusha. Pia nilishiriki maonesho ya elimu na ajira yaliyofanyika Diamond Jubilee Hall, Dar es Salaam. Hapa kushoto naonekana na wadau kwenye meza yangu. Nilishiriki maonesho hayo ili kuwapata wadau wa kujiunga nami, kwani nimejenga msingi mzuri wa uzoefu, na mtandao thabiti, huku Marekani. Lakini, kutokana na shughuli zangu, watu hao inabidi wawe wapenda vitabu na elimu kwa ujumla.

Wednesday, March 9, 2011

Mteja ni Mfalme

Kwamba mteja ni mfalme ni dhana inayojulikana, hata kama wengi wenye biashara hawaifuati. Mantiki ya usemi kuwa mteja ni mfalme iko wazi, kwamba mteja akiridhika anakuwa ndio mpiga debe wako, bila wewe kumlipa chochote. Kwa hivi, kama wewe ni mfanyabiashara, ukiwa na tabia ya kumridhisha kila mteja, utafanikiwa.

Kwa kawaida nadharia ni rahisi, ila utekelezaji unaweza kuwa mtihani mgumu. Hayo ninayaona wakati huu ninapoandika makala hii. Kuna mtu ameanza mawasiliano nami, kunialika nikazungumze kwenye kampuni anapofanyia kazi, kuhusu masuala ninayoongelea katika kitabu changu cha Africans and Americans.

Ingawa nimethibitisha kuwa shughuli hii itafanyika, nimeona kuwa huyu mhusika hana uzoefu mzuri katika kupanga mipango ya aina hii. Nimeanza kupata usumbufu fulni, kwani wakati fulani anasema kitu nami nikadhani nimemwelewa, kumbe baadaye inaonekana hatukuelewana. Hata tarehe aliyopangia tufanya hiyo shughuli ameniambia kuwa imebidi waibadili.

Ninajua kabisa kuwa hatimaye nitaenda kutoa huo mhadhara, lakini usumbufu unanikera. Sasa hapo ndipo suala la mteja ni mfalme linapoingia. Mimi ninatoa huduma ya ushauri katika masuala kama haya niliyoongelea katika kitabu changu. Nimesajili kijikampuni kiitwacho Africonexion hapa Minnesota na huduma nazitoa chini ya kivuli cha kampuni hiyo. Huduma hizo ni pamoja na ushauri, warsha, na vitabu.

Sasa basi, kwa mujibu wa dhana ya kwamba mteja ni mfalme, ni wazi kuwa nawajibika kuwa sambamba na huyu jamaa anayenisumbua, nimsikilize vizuri muda wote na kuongea naye kwa uchangamfu, kama vile hakuna kinachonikera. Kero zake nizione kuwa ni fursa ya mimi kujiongezea uzoefu katika kuwashughulikia wateja na kuimarisha sifa ya kikampuni changu.

Najua kuwa pamoja na yote, kikampuni changu kitafaidika. Kwanza, malipo tumeshapatana, na maandalizi yake yameanza. Siku itakapofika, nitaenda kutoa mhadhara wa kusisimua na kuelimisha. Wao watafaidika, nami nitajipatia wapiga debe wengi.
(Katuni ni ya Nathan Mpangala)

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...