Showing posts with label ujasiriamali. Show all posts
Showing posts with label ujasiriamali. Show all posts

Sunday, May 14, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo nilikwenda tena Apple Valley, kwa muda mfupi, nikaingia katika duka la Half Price Books. Niliangalia kwanza sehemu vinapowekwa vitabu vya Hemingway au juu ya Hemingway. Kitabu cha pekee nilichokiona, ambacho nimekifahamu kwa miezi kadhaa ila sijakinunua, ni Hemingway's Boat: Everything He Loved in Life, And Lost, kilichotungwa na Paul Hendrickson.

Nilielekea sehemu ambapo huwekwa vitabu vya bei rahisi kabisa. Kwa kuwa sikuwa na muda mwingi, niliangalia haraka haraka, nikaona kitabu cha Matigari cha Ngugi wa Thiong'o, kilichotafsiriwa kwa ki-Ingereza na Wangui wa Goro. Ngugi alikuwa amekiandika kwa Kikuyu. Nilivutiwa kuona kuwa ni nakala ya jalada gumu, iliyochapishwa na Africa World Press. Nilichukua. Wasomaji wa Ngugi wanakumbuka kuwa tafsiri hii ilichapishwa kwanza na Heinemann.

Kisha, sehemu hiyo hiyo, katika kuchungulia chungulia, niliona kitabu Contagious Success: Spreading High Performance Throughout Your Organization, kilichoandikwa na Susan Lucia Annunzio. Nilivyoona kuwa kinahusu mbinu za kusambaza ufanisi katika makampuni na mashirika nilikichukua hima. Dhana ya maambukizi ya mafanikio ilinivutia.

Ninapenda kusoma vitabu vinavyohusu ujasiriamali na biashara, kwa sababu mimi mwenyewe ninajiona kama mjasiriamali jamii ("social enterpreneur"). Vile vile, ninavipenda vitabu hivi vinahusu masuala yenye uhusiano na taaluma ambazo nimezizoea, hasa saikolojia.

Monday, January 30, 2017

Kitabu Nilichonunua Leo: "The Highly Paid Expert"

Leo nilikwenda Minneapolis na wakati wa kurudi, nilipita Mall of America, kuangalia vitabu katika duka la Barnes & Noble. Nilitaka hasa kuona kama kuna vitabu vipya juu ya mwandishi Ernest Hemingway.

Niliangalia scheme vinapowekwa vitabu vya fasihi, nikakuta kitabu kipya juu ya Ernest Hemingway, Everybody Behaves Badly: The Backstory to 'The Sun Also Rises.' kilichoandikwa na Lesley M.M. Blume. Kwa kuwa nimezama sana katika uandishi wa Hemingway, maisha na falsafa yake, na kwa kuwa nimeshasoma The Sun Also Rises, nilitamani kukinunua kitabu hiki, ambacho, kwa maelezo niliyoyaona, kinazungumzia yaliyo nyuma ya pazia.

Sikuwa na hela za kutosha, kwa hivyo nikaamua kuangalia vitabu vingine. Nilitumia muda zaidi katika sehemu ya "Business/Management." Huwa ninapenda sana kununua na kusoma vitabu vya taaluma hii, kwani vinanifundisha mengi kuhusu mambo ya ujasiriamali na biashara. Taaluma hii inanisaidia katika kuendesha shughuli za kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants.

Hatimaye, nilikiona kitabu kilichonivutia kwa namna ya pekee, The Highly Paid Expert, kilichoandikwa na Debbie Allen.  Kwa mujibu maelezo nyuma ya kitabu, huyu mwandishi ni mtaalam maarufu katika mambo ya biashara na ujasiriamali. Niliangalia ndani, nikaona mada anazoongelea ni za kuelimisha kabisa, kama vile matumizi ya tekinolojia za mawasiliano na mitandao.

Niliona anatoa ushauri wa kusisimua. Kwa mfano, anasema kuwa ni lazima mtu unayetaka mafanikio katika shughuli zako, uwasaidie wengine kufanikiwa. Unavyowasaidia wengine wafanikiwe, unajijengea mtandao wenye manufaa kwako pia. Ubinafsi na uchoyo wa maarifa haukuletei mafanikio. Kitabu hiki kinavutia kwa jinsi mwandishi anavyothibitisha mawazo yake, ambayo kijuu juu yanaonekana kama ya mtu anayeota ndoto.

Kwa bahati niliweza kuimudu gharama ya kitabu hiki, nikakinunua na kuondoka zangu, kwani nilikuwa sina hela iliyosalia. Sijutii kununua vitabu. Vitabu vinavyoelimisha ni mtaji, kwani hakuna mtaji muhimu zaidi ya elimu. Kwa wajasiriamali, wafanya biashara, watoa huduma, na kwa kila mtu, elimu ni tegemeo na nguzo muhimu. Ulazima wa kununua vitabu ni sawa na ilivyo lazima kwa mkulima kununua pembejeo.

Wednesday, March 23, 2016

Watu Wanaofanikiwa na Wale Wasiofanikiwa

Katika vitabu vinavyohusu mafanikio na maendeleo binafsi na pia kuinufaisha jamii, kuna mambo yanayoelezwa tena na tena. Mambo hayo tunaweza kuyaita mbinu au siri za mafanikio.

Picha nilizoweka hapa zinaorodhesha mambo hayo. Kwa upande mmoja kuna mambo wanayofanya watu wenye mafanikio au wanaotaka mafanikio. Ni mambo ambayo ni sehemu ya tabia ya watu hao.

Kwa upande wa pili, yanatajwa mambo wafanyayo watu wasio na mafanikio, au wasiofahamu njia au siri ya mafanikio. Hao ni watu wa kushindwa.

Mambo wanayofanya watu wenye mafanikio au wanaotaka mafanikio ni kama kusoma kila siku, kuwa wepesi wa kuyapokeo mabadiliko, wepesi wa kuwasamehe wenzao, wanaongelea fikra na mawazo, wanajifunza muda wote, ni wenye shukrani, wanajiwekea malengo na wanayatekeleza, wanawatakia wenzao mafanikio, wanayasifia mafanikio ya wenzao.

Watu wasio na mafanikio au wasiofahamu siri ya mafanikio ni wakosoaji wakubwa na walalamishi,  wanaogopa mabadiliko, wana visirani, wanawaongelea watu, wanajiona wajuaji, wanawalaumu wengine kwa lolote, wanadhani wanastahili kila watakacho, hawajiwekei malengo, hawakiri udhaifu wao au makosa yao, hawatambui mazuri ya wenzao, wanataka sifa hata wasipostahili, wanaangalia televisheni kila siku.

Katika kuyatafakari mambo hayo, nimeona wazi matatizo ya wa-Tanzania wengi. Wengi wamo katika hili kundi la wasiofanikiwa. Tabia ya kukaa vijiweni na kulumbana kuhusu vilabu vya mpira vya Ulaya, kuhusu vituko vya mastaa, kulalamikia hili au lile, ni tabia iliyoshamiri. Muda wanaokaa vijiweni wangeweza kuutumia kwa kusoma vitabu. Lakini huwaoni wakifanya hivyo, wala nyumbani, wala maktabani. Wasipofanikiwa, hawajitathmini na kutambua dosari zao, bali wanatafuta visingizio na wachawi.

Tuesday, March 15, 2016

Kutana na Fundi Abdallah Ramadhani

Leo ninapenda kumtambulisha Abdallah Ramadhani, ambaye nimefahamiana naye siku chache tu zilizopita katika mtandao wa Facebook. Ilikuwa bahati tu kuwa nilianzisha mawasiliano naye, na ndipo nikaweza kujua habari zake. Nilivutiwa na shughuli za ufundi anazofanya.




Nilimwambia kuwa ningeweza kuzitangaza shughuli zake katika blogu yangu. Nilitambua tangu miaka iliyopita kuwa ninaweza kuitumia blogu yangu hii kutangazia shughuli za wa-Tanzania ninaokutana nao au ninaopata habari zao na kuvutiwa na namna wanavyojishughulisha. Ninawaunga mkono. Kwa mfano, niliwahi kuandika juu ya wajasiriamali wa Duka Asili na Super Muhogo.



Abdallah Ramadhani alizaliwa Temeke, Dar es Salaam, mwaka 11 Mei,1979.  Anatengeneza viatu vizuri kama inavyoonekana pichani katika ukurasa huu. Ufundi huu alijifunza kwa baba yake, ambaye alijifunza kwa wa-Hindi.

Wa-Tanzania tujijengee utamaduni wa kuvithamini vipaji vya wa-Tanzania wenzetu, na huduma wanazotoa. Tuwe na utamaduni wa kuzithamini kazi zao. Tuzithamini bidhaa zinazozalishwa nchini mwetu, kama nilivyowahi kuelezea katika blogu hii, na katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Manufaa yake ni kwa hao wahusika na kwa Taifa.

Unaweza kuwasiliana na Abdallah kwa simu, namba  255-682-588-583 au 255-719-588-583


Friday, May 8, 2015

Going Visual: Kitabu Kuhusu Mawasiliano Kwa Taswira

Leo napenda kukiongelea kitabu kiitwacho Going Visual: Using Images to Enhance Productivity, Decision-Making and Profits, kilichoandikwa na Alexis Gerard na Bob Goldstein. Nilikinunua kitabu hiki miaka michache iliyopita. Kama ilivyo kawaid yangu ninaponunua kitabu, sikiweki katika maktaba yangu bila kukipitia angalau juu juu, ili nijue kinahusu nini.

Hivi ndivyo nilivyofanya niliponunua Going Visual. Niliona ni kitabu kinachoelezea maendeleo katika utumiaji wa taswira katika mawasiliano, kitabu kinachoelezea matokeo ya utafiti na uzoefu na mikakati ya matumizi ya taswira katika biashara na ujasiriamali. Kitabu kinaelezea jinsi tekinolojia ya kuzalisha, kuhifadhi, kuandaa, na kusambaza taswira, kuanzia za digitali hadi video, zinavyowezesha ufanisi katika biashara na ujasiriamali katika ulimwengu wa leo.

Wakati nilipokinunua kitabu hiki, nilikipitia juu juu, nikaelewa haya niliyoelezea. Lakini leo nimekitoa maktabani ili nikisome ipasavyo. Mada yake inanivutia, na ukweli kwamba sina ufahamu wa masuala yaliyomo umenipa shauku ya kufahamu.

Suala la mawasiliano tunalishughulikia katika usomaji na ufundishaji wa fasihi, kwani fasihi hutumia lugha, ambayo ni chombo mahsusi cha mawasiliano. Nadharia za lugha na fasihi zinatueleza mengi kuhusu mawasiliano. Mvuto wa kitabu cha Going Visual kwangu, na duku duku inayonisukuma kukisoma, ni hiyo mikakati na mbinu za kutumia taswira ambazo waandishi wa kitabu wanasema zinawanufaisha wafanya biashara na wajisiriamali wa leo.

Ninajiuliza: hizi mbinu ni zipi? Na hiyo mikakati ni ipi? Kwa hivi, ninaona ni muhimu nikisome kitabu hiki nielimike, ingawa siwezi kujiita mfanyabiashara au mjasiriamali. Elimu haina mwenyewe, haina mipaka, wala haina mwisho.

Wednesday, February 15, 2012

Maskat: Mbunifu wa Mitindo

Katika pita pita zangu mtandaoni, nilikumbana na taarifa kwenye blogu ya Swahili na Waswahili kuhusu mwanamitindo Maskat, m-Tanzania ambaye jina lake jingine ni Hayakuhusu. Nilivutiwa na taarifa hiyo, nikaifuatiliza zaidi, nikaona jinsi dada huyu alivyo mjasiriamali makini.













Sio tu anajibidisha katika fani hii ya mitindo, bali anazitumia vilivyo tekinolojia za mawasiliano ya kisasa. Utamkuta sehemu kama Youtube, Facebook na blogu yake. Anwani yake ni maskatdehaan@hotmail.com. Napenda kusoma habari za watu wa aina hii na pia kuzitangaza katika blogu yangu, kwani ni changamoto kwa wengine, hasa watoto na vjiana wetu. Wanasema kuwa picha inajeleza sawa na maneno elfu. Kwa kuangalia picha za Dada Maskat, napata hisia kuwa ni dada anayejipenda na kujiamini, anayejua anachofanya na anakoelekea. Hili ni fundisho muhimu kwa watoto wetu, na sisi wenye mabinti tuna sababu ya ziada ya kuuenzi mfano wa dada Maskat.

Friday, February 25, 2011

SUPER MUHOGO: Unga Safi wa Muhogo

Katika pita pita zangu, nimeona tangazo kwenye blogu ya Lady JayDee la wajasiriamali wa Chanika, Dar es Salaam, wanaouza unga wa muhogo. Wamemwomba Lady JayDee awawekee tangazo hilo kwenye blogu yake, naye amefanya hivyo.

Nimevutiwa na jambo hili. Njia madhubuti ya kujenga uchumi wa nchi yetu ni kuzalisha bidhaa na kuziuza nje, ili tupate fedha za kigeni. Kuuza bidhaa zetu nje kunaleta ajira nchini.

Hili ni jambo rahisi kulielewa. Hata mimi ambaye sikusomea somo la uchumi nimeandika kuhusu suala hili katika kitabu changu cha CHANGAMOTO, nikielezea namna mbali mbali jinsi wa-Tanzania tunavyohujumu uchumi wa nchi yetu. Mfano moja ni jinsi tunavyozishabikia bidhaa za kutoka nchi za nje, bila kutambua kuwa tunawapa ajira watu wa nchi zingine. Wakati huo huo, wa-Tanzania wanalalamikia uhaba wa ajira nchini. Tunapaswa kuuza bidhaa na huduma kwa wengine.

Kutokana na yote hayo, nimevutiwa na hao wajasiriamali wanaouza unga wa muhogo. Nimeamua kusaidia kutangaza biashara yao hapa kwenye blogu yangu. Nawatakia mafanikio tele katika kuboresha maisha yao na kuinua uchumi wa nchi.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...