
Picha nilizoweka hapa zinaorodhesha mambo hayo. Kwa upande mmoja kuna mambo wanayofanya watu wenye mafanikio au wanaotaka mafanikio. Ni mambo ambayo ni sehemu ya tabia ya watu hao.
Kwa upande wa pili, yanatajwa mambo wafanyayo watu wasio na mafanikio, au wasiofahamu njia au siri ya mafanikio. Hao ni watu wa kushindwa.

Watu wasio na mafanikio au wasiofahamu siri ya mafanikio ni wakosoaji wakubwa na walalamishi, wanaogopa mabadiliko, wana visirani, wanawaongelea watu, wanajiona wajuaji, wanawalaumu wengine kwa lolote, wanadhani wanastahili kila watakacho, hawajiwekei malengo, hawakiri udhaifu wao au makosa yao, hawatambui mazuri ya wenzao, wanataka sifa hata wasipostahili, wanaangalia televisheni kila siku.
Katika kuyatafakari mambo hayo, nimeona wazi matatizo ya wa-Tanzania wengi. Wengi wamo katika hili kundi la wasiofanikiwa. Tabia ya kukaa vijiweni na kulumbana kuhusu vilabu vya mpira vya Ulaya, kuhusu vituko vya mastaa, kulalamikia hili au lile, ni tabia iliyoshamiri. Muda wanaokaa vijiweni wangeweza kuutumia kwa kusoma vitabu. Lakini huwaoni wakifanya hivyo, wala nyumbani, wala maktabani. Wasipofanikiwa, hawajitathmini na kutambua dosari zao, bali wanatafuta visingizio na wachawi.
No comments:
Post a Comment