Friday, May 8, 2015

Going Visual: Kitabu Kuhusu Mawasiliano Kwa Taswira

Leo napenda kukiongelea kitabu kiitwacho Going Visual: Using Images to Enhance Productivity, Decision-Making and Profits, kilichoandikwa na Alexis Gerard na Bob Goldstein. Nilikinunua kitabu hiki miaka michache iliyopita. Kama ilivyo kawaid yangu ninaponunua kitabu, sikiweki katika maktaba yangu bila kukipitia angalau juu juu, ili nijue kinahusu nini.

Hivi ndivyo nilivyofanya niliponunua Going Visual. Niliona ni kitabu kinachoelezea maendeleo katika utumiaji wa taswira katika mawasiliano, kitabu kinachoelezea matokeo ya utafiti na uzoefu na mikakati ya matumizi ya taswira katika biashara na ujasiriamali. Kitabu kinaelezea jinsi tekinolojia ya kuzalisha, kuhifadhi, kuandaa, na kusambaza taswira, kuanzia za digitali hadi video, zinavyowezesha ufanisi katika biashara na ujasiriamali katika ulimwengu wa leo.

Wakati nilipokinunua kitabu hiki, nilikipitia juu juu, nikaelewa haya niliyoelezea. Lakini leo nimekitoa maktabani ili nikisome ipasavyo. Mada yake inanivutia, na ukweli kwamba sina ufahamu wa masuala yaliyomo umenipa shauku ya kufahamu.

Suala la mawasiliano tunalishughulikia katika usomaji na ufundishaji wa fasihi, kwani fasihi hutumia lugha, ambayo ni chombo mahsusi cha mawasiliano. Nadharia za lugha na fasihi zinatueleza mengi kuhusu mawasiliano. Mvuto wa kitabu cha Going Visual kwangu, na duku duku inayonisukuma kukisoma, ni hiyo mikakati na mbinu za kutumia taswira ambazo waandishi wa kitabu wanasema zinawanufaisha wafanya biashara na wajisiriamali wa leo.

Ninajiuliza: hizi mbinu ni zipi? Na hiyo mikakati ni ipi? Kwa hivi, ninaona ni muhimu nikisome kitabu hiki nielimike, ingawa siwezi kujiita mfanyabiashara au mjasiriamali. Elimu haina mwenyewe, haina mipaka, wala haina mwisho.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...