Friday, May 8, 2015

Vitabu vya Moyez Vassanji

Siku chache zilizopita niliandika taarifa kuhusu vitabu nilivyonunua hivi karibuni. Kati ya vitabu kilikuwepo kimoja cha Moyez Vassanji, The Gunny Sack. Wakati huo, nilikuwa navingojea vitabu vingine viwili vya Moyez Vassanji, ambavyo nilikuwa nimeshavilipia. Vimefika.

Kimoja ni Uhuru Street, mkusanyo wa hadithi za kubuniwa,ambazo zinatokea katika mtaa wa Uhuru, mjini Dar es Salaam. Nasikitika kuwa kitabu hiki sijakisoma ingawa nimetamani kukisoma kwa miaka mingi. Kutokana na taarifa, nilijua kuwa kwa yeyote anayeijua Dar es Salaam, hiki ni kitabu kinachogusa hisia. Nimeanza kukisoma na ninajionea mwenyewe ukweli huo.

Kitabu cha pili ambacho kimewasili ni The Book of Secrets, ambacho, kama nilivyosema, niliwahi kukifundisha katika semina ya walimu katika Chuo cha Colorado. Mtu akisoma kitabu hiki, naamini atapata hamu ya kusoma vitabu vingine vya Moyez Vassanji.

Kitabu cha tatu ambacho kimewasili ni The In-Between World of Vikram Lall. Sijaanza kukisoma, ila nimekuwa nikisoma habari zake.

Kitabu kingine nilichokitaja siku chache zilizopita ni Amriika, ambacho nilikinunua zamani kidogo, ila sijakisoma. Moyez Vassanji ameshaandika vitabu karibu kumi hadi sasa. Ambavyo sijavitaja ni The Assasin's Song, No New Land, The Magic of Saida, A Place Within, na  And Home Was Kariakoo. Orodha haiishii hapo, na kuvisoma vyote itakuwa kazi kubwa. Kwa vyo vyote, baadhi nitavitumia katika kozi yangu ya Post-colonial Literature.

Moyez Vassanji ni mwandishi maarufu, nasi wa-Tanzania tuna haki ya kusema ni mtu wetu, kwani mnali ya kukulia Tanzania, amekuwa akiipeperusha vizuri sana bendera ya nchi yetu katika ulimwengu wa fasihi. Ninaamini tunawajibika kuwa naye bega kwa bega kwa kusoma vitabu vyake.

Ninakiri kuwa si jambo la kuridhisha kwamba vitabu vingi vilivyovitaja hapo juu ambavyo vilichapishwa miaka iliyopita, sikuvisoma na bado sijavisoma. Hiyo ni dosari. Ninapaswa kumfahamu mwandishi kama Moyez Vassanji kama ninavyowafahamu waandishi ninaowasoma katika ki-Ingereza kama Wole Soyinka, Nadine Gordimer, Derek Walcott, J.M. Coetzee, Anita Desai, Athol Fugard, Ngugi wa Thiong'o, Chinua Achebe, Sembene Ousmane, Salman Rushdie, na kadhalika.

Panapo majaliwa, nitaandika katika blogu hii juu ya Abdulrazak Gurnah na Tololwa Mollel, ambao ni waandishi wengine maarufu wa ki-Tanzania huku ughaibuni wanaoandika kwa ki-Ingereza. Tuwe nao bega kwa bega. Ni aibu kwetu kwamba waandishi hao wanasifika nchi za ng'ambo lakini si nyumbani Tanzania.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...