Wednesday, May 6, 2015

Leo Nimepata Bendera ya Tanzania

Leo nimepata bendera ya Tanzania. Niliwahi kuandika katika blogu hii kuwa mara kwa mara ninashiriki matamasha hapa Marekani ambapo watu huja na bendera za nchi zao, nami nilijisikia vibaya kwa kutokuwa na bendera kubwa ya nchi yangu. Nilifanya uamuzi muafaka, nikaagiza, na leo nimeipata.

Mwaka jana, nilipoandika ujumbe wangu, nilikuwa napeleleza katika tovuti kadhaa zinazouza bendera. Lakini safari hii, kwa kubahatisha tu, nimeingia katika tovuti ya Amazon nikaona bendera ziko, tena kwa bei rahisi sana.




Nimejionea hapa Marekani jinsi wa-Kenya walivyo hodari kwa suala hilo, na hapa naleta picha niliyopiga katika tamasha la Afrifest, tarehe 2 Agosti, mwaka jana, mjini Brooklyn Park, Minnesota. Inamwonyesha m-Kenya akitamba na bendera ya nchi yake.

Jiulize mwenyewe, ungejisikiaje kuwepo mahali ambapo wenzako wanatamba na bendera za nchi zao, nawe huna. Kwa nini ukae mahali hivyo, kama vile huna nchi? Hisia hizi ni kubwa unapokuwa ughaibuni. Sikutaka kuendelea kudhalilika namna hiyo.



Picha nyingine, inayoonekana hapa kushoto, nilipiga tarehe 11 Aprili, 2015, mjini Rochester, Minnesota, kwenye tamasha la tamaduni za ulimwengu. Inaonyesha meza ya wa-Kenya na bendera yao.

Kuna matamasha yanayokuja ambayo nitashiriki, kama vile tamasha la Afrifest, tarehe 1 Agosti, 2015. Nitakapokuwa naandika taarifa za matamasha hayo na maonesho, wadau mtajionea wenyewe bendera ya Tanzania ikipepea kwenye eneo la meza ya vitabu vyangu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...