Thursday, May 14, 2015

Hadithi za Luis Bernardo Honwana wa Msumbiji

Leo nimeagiza mtandaoni kitabu cha hadithi za Luis Bernardo Honwana wa Msumbiji kiitwacho We Killed Mangy Dog and Other Stories. Kwa wiki kadhaa, nimemwazia sana mwandishi huyu, ambaye kitabu chake hiki nilikipenda sana nilipokuwa mwanafunzi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuanzia mwaka 1973. Nilivutiwa na jinsi alivyoielezea maisha nchini Msumbiji, ambayo ilikuwa daima mawazoni mwetu kutokana na vita vya ukombozi vilivyoongozwa na FRELIMO.

Nimeamua kununua kitabu hiki wakati huu kwa sababu katika wiki hizi nimeandaa orodha ya vitabu vya kufundishia kozi yangu ya "Post-colonial Literature" muhula wa kiangazi, mwezi Julai na Agosti. Kwa mara ya kwanza tangu nianze kufundisha hapa Chuoni St. Olaf, nimeamua kuingiza kazi ya fasihi kutoka Msumbiji.

Sitafundisha We Killed Mangy Dog and Other Stories, ingawa ningeweza kufanya hivyo kwa furaha kabisa. Badala yake, nitafundisha riwaya ya mwandishi mwingine maarufu Mia Couto iitwayo The Tuner of Silences, ambayo sijaisoma. Hata hivyo nimeona nijipatie hiki kitabu cha hadithi za Honwana, nilichokipenda enzi za ujana wangu, nikisoma tena wakati nangojea kufundisha The Tuner of Silences,

Ninangojea kwa hamu kusoma na kufundisha The Tuner of Silences. Ninangojea kwa hamu  kujikumbusha na kuwaeleza wanafunzi kuhusu Msumbiji, historia yake, historia ya utamadini na fasihi yake. Ninapangia kuandika zaidi kuhusu hayo katika blogu hii wakati utakapowadia.

2 comments:

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Hata mimi huwa nazikubali kazi na Honwana kusema ule ukweli. Ni nguli katika nyanja yake. Nimefaidika na kazi zake nyingi pamoja na za professor Francis Nyamnjoh wa Kameruni anayefundisha chuo kikuu Afrika ya Kusini.

Joseph said...

Nimesoma kidogo sana maandishi ya Francis Nyamnjoh, ingawa jina lake nimelisikia kwa miaka mingi kidogo.

Huyu ni kijana. Lakini nchi yake, Cameroon, imetoa waandishi wengi maarufu sana, kama vile Mongo Beti na Ferdinand Oyono, ambao tulianza kuwasoma tulipokuwa wanafunzi Chuo Kikuu Dar, mwaka 1973. Kuna pia akina Mbella Sonne Dipoko na Bate Bisong, Bole Butake, na Guillaume Oyono Mbia, Francis Namnjoh na wengine.

Inasikitisha kuwa haiwezekani kuwasoma waandishi maarufu wote wa Afrika, hata tu wale wanaoandika kwa ki-Ingereza, kuanzia Somalia hadi Gambia, kuanzia Afrika Kusini hadi Ethiopia.

Kinachosikitisha pia ni jinsi jamii ya wa-Tanzania ilivyogubikwa na uzembe, kiasi kwamba hata waandishi maarufu wetu, kama vile Moyez Vassanji na Abdulrazak Gurnah hawafahamiki Tanzania.

Hicho tunachoita mfumo wa elimu ni mzaha na dhihaka. Wanafunzi hawajengewi utamaduni wa kusoma sana vitabu, na watu wazima nao wanaonyesha mfano mbaya wa utamaduni wa kutosoma.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...