Showing posts with label St. Olaf College. Show all posts
Showing posts with label St. Olaf College. Show all posts

Thursday, May 18, 2017

Vitabu Nilivyonunua Jana

Jana nilinunua vitabu vitatu katika duka la vitabu la chuoni St. Olaf. Viwili, Two Years Eight Months and Twenty-Eight Nights cha Salman Rushdie na A Strangeness in my Mind cha Orhan Pamuk, niliviona juzi. Cha tatu, Why Homer Matters, kilichotungwa na Adam Nicolson, nilikiona hiyo hiyo jana.

Nilipoingia dukani, nilikumbuka makala niliyoisoma juzi usiku, kuhusu vitabu halisi na vitabu pepe. Makala hii, sawa na nyingine nyingi, inatafakari iwapo vitabu vya jadi vitasalimika katika himaya hii ya vitabu pepe. Lakini inahitimisha kuwa hakuna ushahidi kuwa vitabu vya jadi vitapoteza mvuto au kufifia.

Mimi ni mmoja wa wale ambao hatujabadilika. Bado tumezoea vitabu halisi, yaani vitabu vya jadi, na ndio maana sisiti kuvinunua, wala sisiti kuelezea tabia yangu hiyo. Hapa nitaelezea kifupi kwa nini nimenunua vitabu hivi vitatu.

Kitabu cha Salman Rushdie kilinivutia kwa sababu ya umaarufu wa mwandishi huyu. Bila shaka wengi watakumbuka kitabu chake, Satanic Verses, ambacho kilipigwa marufuku katika nchi nyingi kwa madai kuwa kinaukashifu u-Islam. Ayatollah Khomeini wa Iran alitangaza fatwa kuwa Salman Rushdie anapaswa kuuawa.

Duniani kote, na hata miongoni mwa wa-Islam wenyewe hukumu hii ilizua mjadala. Baadhi walisema kuwa fatwa haikupaswa kutolewa kabla ya Salman Rushdie kupewa fursa ya kujieleza na kukiri kosa lake. Watu wengine walisema kuwa zogo hili lilimpa Salman Rushdie umaarufu ambao hakustahili kwa kigezo cha ubora wa uandishi wake.

Ninavyo baadhi vitabu vya Salman Rushdie, kikiwemo hiki cha Satanic Verses. Nimemewahi kufundisha riwaya yake maarufu, Midnight's Children. Ninavutiwa na ubunifu wake katika kuelezea mambo, na uhodari wake wa kutumia lugha. Uandishi wake unasisimua na kufikirisha.

Orhan Pamuk ni mwandishi ambaye nimewahi kumtaja katika blogu hii. Nina vitabu vyake kadhaa, na nimekuwa na hamu ya kuvisoma, ila bado sijapata wasaa. Huyu amenivutia si tu kwa kuwa alipata tuzo ya Nobel, bali pia kwa sababu ninafahamu kiasi fulani kuhusu fasihi simulizi ya Uturuki, kama vile hadithi za Nasreddin Hodja na Dede Korkut.

Why Homer Matters nimekipenda kwa kuwa taaluma ya tendi nimeipenda na kuishughulikia kwa miaka mingi. Homer, ingawa taarifa zake hazijulikani vizuri, ndiye anayehusishwa na tendi maarufu za u-Griki ya kale, The Iliad na The Odyssey. Kwa kuangalia juu juu, niliona kuwa mwandishi wa Why Homer Matters ana uwezo mkubwa wa kuelezea masuala ya Homer na hizi tendi.

Wednesday, March 15, 2017

Maktaba ya Chuo Kikuu cha Minnesota

Mara kwa mara, ninaandika kuhusu maktaba ninazozitembelea, hapa Marekani na Tanzania. Mifano ni maktaba ya John F. Kennedy,  ya Brookdale, ya Southdale, ya Moshi, ya Tanga, ya Iringa, ya Dar es Salaam, na ya Songea.

Jana, nilikuwa Minneapolis kwa shughuli binafsi. Baadaye niliingia katika maktaba ya Wilson. Nimezoea kwenda kusoma katika maktaba hii, ambayo ni moja ya maktaba za Chuo Kikuu cha Minnesota. Kati ya hizo, hii ndio inayonihusu zaidi, kwa sababu humo ndimo kuna majarida, vitabu, na hifadhi za lugha na fasihi.

Ingawa chuoni St. Olaf ninapofundisha pana maktaba kubwa, ambayo imeunganishwa na maktaba ya chuo cha Carleton, maktaba ya Wilson ni kubwa zaidi.

Picha zinazoonekana hapa nilipiga jana. Hiyo ya juu ni ubavuni mwa maktaba, na hiyo ya chini ni sehemu ya mbele, kwenye mlango. Ardhini inaonekana theluji, kwani ni bado kipindi cha baridi.


Thursday, November 24, 2016

"A Far Cry From Africa," Shairi la Derek Walcott

Tangu nilipoanza kufundisha katika chuo cha St. Olaf, mwaka 1991, nimepata fursa ya kusoma na kufundisha fasihi iliyoandikwa kwa ki-Ingereza kutoka sehemu mbali mbali ulimwenguni, kwa kiwango kikubwa kuliko ilivyowezekana nilipokuwa ninafundisha katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mwandishi mmojawapo ambaye kazi zake nimezishughulikia sana ni Derek Walcott wa St. Lucia, pande za Caribbean, maarufu kwa utunzi wa mashairi na tamthilia, ambaye alipata tuzo ya Nobel mwaka 1992.

Nimesoma na kufundisha mashairi yake mengi na tamthilia zake kadhaa. Moja ya mashairi hayo ni "A Far Cry From Africa," ambalo lilichapishwa mwaka 1962. Linaelezea mahuzuniko juu ya vita ya Mau Mau nchini Kenya iliyodumu kuanzia mwaka 1952 hadi 1960. Masetla wazungu walipigana na wa-Afrika waliotaka kuchukua ardhi yao iliyoporwa. Kwa kuwa Derek Walcott ni chotara, damu ya kizungu na ki-Afrika, alihisi vita hiyo ikitokea ndani ya nafsi yake. Uhasama na ukatili wa pande hizo mbili aliuhisi mithili ya sumu katika mishipa ya damu yake. Alijihisi kama mateka aliyekosa namna ya kujinasua.

Walcott anaimudu lugha ya ki-Ingereza kwa namna inayonikumbusha umahiri wa Shakespeare. Nitafurahi iwapo nitapata ujasiri wa kujaribu kulitafsiri shairi kwa ki-Swahili.
-------------------------------------------------------------------------------

A Far Cry From Africa

Derek Walcott


A wind is ruffling the tawny pelt 
Of Africa, Kikuyu, quick as flies, 
Batten upon the bloodstreams of the veldt. 
Corpses are scattered through a paradise. 
Only the worm, colonel of carrion, cries: 
'Waste no compassion on these separate dead!' 
Statistics justify and scholars seize 
The salients of colonial policy. 
What is that to the white child hacked in bed? 
To savages, expendable as Jews?

Threshed out by beaters, the long rushes break 
In a white dust of ibises whose cries 
Have wheeled since civilizations dawn 
From the parched river or beast-teeming plain. 
The violence of beast on beast is read 
As natural law, but upright man 
Seeks his divinity by inflicting pain. 
Delirious as these worried beasts, his wars 
Dance to the tightened carcass of a drum, 
While he calls courage still that native dread 
Of the white peace contracted by the dead. 

Again brutish necessity wipes its hands 
Upon the napkin of a dirty cause, again 
A waste of our compassion, as with Spain, 
The gorilla wrestles with the superman. 
I who am poisoned with the blood of both, 
Where shall I turn, divided to the vein? 
I who have cursed 
The drunken officer of British rule, how choose 
Between this Africa and the English tongue I love? 
Betray them both, or give back what they give? 
How can I face such slaughter and be cool? 
How can I turn from Africa and live?

Wednesday, October 26, 2016

Miaka 80 ya "The Snows of Kilimanjaro"

Kwa mara nyingine tena, ninaandika ujumbe kuhusu kutimia kwa miaka 80 tangu hadithi ya Ernest Hemingway, 'The Snows of Kilimanjaro" ilipochapishwa kwa mara ya kwanza. Niliandika ujumbe wa aina hiyo katika blogu hii. Leo nimesoma tena ujumbe wangu, nikajiridhisha kwamba niliyosema ndiyo ninayoamini hadi sasa.

Jambo moja kubwa kabisa ni kuwa wa-Tanzania tunajipotezea fursa za wazi za kutumia hazina kama hii hadithi ya Hemingway kuitangaza nchi yetu. Niliandika katika ujumbe wangu baadhi ya mambo ambayo tungeyafanya mwaka huu wa kumbukumbu. Lakini mwaka unaelekea ukingoni, na hakuna tulichofanya. Hii ni hasara ya kukosa utamaduni wa kusoma vitabu. Tunashindwa hata kutumia fursa zilizo wazi.

Nimeona niandike ujumbe huu leo kwa sababu wiki hii, hapa katika Chuo cha St. Olaf ninapofundisha, litatokea jambo la pekee linalohusiana na Ernest Hemingway. Keshokutwa, tarehe 28, pataonyeshwa kwa mara ya kwanza filamu ya "Papa's Shadow," ambayo niliwahi kuielezea katika blogu hii.

Hiyo ni filamu iliyotokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwaka 2013 iitwayo Hemingway in East Africa. Nilisafiri na wanafunzi 29 wa Chuo cha St. Olaf, tukazunguka maeneo kadhaa ya Tanzania kaskazini, ambamo alipita Ernest Hemingway mwaka 1933-34. Katika safari hiyo, tulikuwa tunasoma maandishi ya Hemingway kuhusu maeneo hayo na maeneo mengine ambayo alipitia mwaka 1953-54.

Maandishi hayo ni pamoja na Green Hills of Africa na Under Kilimanjaro, ambavyo ni vitabu, kadhalika hadithi fupi mbili: "The Short Happy Life of Francis Macomber" na "The Snows of Kilimanjaro." Pia aliandika makala katika magazeti na barua nyingi akielezea aliyoyaona na kufanya katika safari zake. Kwa ujumla wake, maandishi haya ya Ernest Hemingway yanaitangaza nchi yetu na Afrika Mashariki kwa ujumla kwa namna ambayo sisi wenyewe hatujaweza kujitangaza.

Hiyo filamu ya "Papa's Shadow" inawasilisha vizuri mambo muhimu ya uhusiano wa Ernest Hemingway na Afrika Mashariki. Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway. Tunajadili kwa kina na mapana fikra za Ernest Hemingway kuhusu Afrika, uandishi, na maisha kwa ujumla.

Kwa kuwa hiyo filamu inaonyesha sehemu mbali mbali za Tanzania na maelezo kuhusu mambo yanayoifanya Tanzania kivutio kwa watalii, kama vile Mlima Kilimanjaro, na kwa kuwa filamu hii imejengeka katika maandishi ya Ernest Hemingway, mwandishi maarufu sana ulimwenguni, ni wazi kuwa filamu hii itakuwa chachu ya kuitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Taarifa zaidi Kuhusu "Papa's Shadow," zinapatikana kwenye tovuti ya Ramble Pictures.

Wednesday, May 18, 2016

Muhula Unaisha; Umebaki Utafiti

Jana tumemaliza muhula wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Nilikuwa ninafundisha "Folklore," Muslim Women Writers, na "First Year Writing." Kwa utaratibu wa chuo hiki, masomo matatu kwa muhula ndio kiwango cha juu kabisa. Hatufundishi zaidi ya masomo matatu. Kwa hivi, nilitegemea ningekuwa nimechoka, lakini sisikii uchovu. Alhamdulillah.

Kwa wiki nzima inayokuja, tutakuwa na mitihani. Baada ya hapo tutaanza likizo ndefu ya miezi mitatu na kidogo. Inaitwa likizo, lakini maprofesa tunaona ni wakati muafaka wa kufanya shughuli za kitaaluma kama utafiti na uandishi.

Nami nimeamua kwenda Boston kwa siku chache kufanya utafiti juu ya Ernest Hemingway katika maktaba ya John F. Kennedy. Humo kuna hifadhi kubwa kuliko zote duniani ya vitabu, miswada, picha na  kumbukumbu zingine zinazomhusu Hemingway. Ingawa nimefika Boston mara kadhaa, sijawahi kwenda katika maktaba hiyo maarufu.

Nina bahati kuwa ninafahamiana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway ambaye bado yuko hai. Yeye ndiye mmiliki wa haki zote za urithi wa Hemingway. Nilipomwambia kwa mara ya kwanza kwamba napangia kwenda kufanya utafiti katika maktaba ya John F. Kennedy,  aliniambia nimfahamishe ni lini ili anitambulishe kwa wahusika. Wiki chache zilizopita, katika maongezi yetu, nilimwambia tena kuwa napangia kwenda kwenye maktaba ile, alikumbushia kuwa nimweleze ni muda upi nitakwenda ili awafahamishe.

Ninashukuru sana kwa hilo, kwani katika kusoma taarifa za maktaba ile, nimefahamu kuwa kuna masherti yanayohusu kuitumia hifadhi ya Ernest Hemingway. Mtu hukurupuki tu ukafika pale na kufanya utafiti. Kuna baadhi ya kumbukumbu ambazo zimefungiwa. Mtafiti unahitaji kibali maalum kuweza kuzifanyia utafiti. Sherti nichukue hatua hima.

Monday, January 4, 2016

Nawazia Dini na Uandishi wa Wanawake wa ki-Islam

Muhula ujao, kuanzia mwezi Februari hadi Mei, nitafundisha kozi mpya hapa chuoni St. Olaf ambayo nimeiita "Muslim Women Writers." Ni kozi ya fasihi kwa ki-Ingereza, ambamo tutasoma maandishi ya wanawake wa-Islam kutoka Bangladesh, India, Iran, Misri, Sudan, Senegal, na Marekani. Taarifa fupi ya kozi hiyo nimeandika hapa.

Wakati huu ninapongojea kufundisha kozi hii katika mazingira ya leo ambamo maelewano miongoni mwa waumini wa dini na madhehebu mbali mbali yanatatanisha, ninajikuta nikiwazia mara kwa mara masuala ya dini. Katika siku zijazo, labda kwa miezi kadhaa, ninategemea kuandika tena na tena katika blogu hii kuhusu dini na kozi yangu.

Nimeshaandika mara kadhaa kuhusu dini. Nimeandika kuhusu umuhimu wa mijadala ya dini, umuhimu wa kuziheshimu dini zote, na nilivyozuru nyumba za ibada za dini nyingine. Sioni mantiki kwa dini yoyote kuwafundisha waumini wake kwamba Muumba anawapenda wao zaidi kuliko watu wa dini nyingine. Msimamo wangu ni kwamba Mungu (Allah) hana ubaguzi.

Ninafurahi na kujivunia kwamba kanisa langu Katoliki linasimama katika msingi huo, kama ilivyodhihirishwa katika ziara na ujumbe wa Papa John Paul wa Pili nchini Nigeria, ziara ya Papa Francis katika msikiti Uturuki, na katika sala ya Papa Francis ya kuuombea ulimwengu. Na zaidi ni kuwa Kanisa Katoliki lina baraza la kujenga maelewano miongoni mwa dini mbali mbali liitwalo Pontifical Council for Inter-religious Dialogue.

Katika kujiandaa kwa kozi yangu, nimekuwa nikiwazia kuwa ingekuwa vizuri kama ningesoma Quran yote. Ninayo Quran takriban tangu mwaka 1982. Nimekuwa nikisoma visehemu hapa na pale, lakini si yote kikamilifu. Ingawa ninafahamu misingi ya u-Islam kiasi cha kuridhisha, wazo la kuisoma Quran linanivutia.

Kuna mambo mengine ambayo nimekuwa nikifanya, kama vile utafiti ili kufahamu misimamo na mitazamo ya wanawake wa-Islam kuhusu u-Islam na nafasi yao katika dini hiyo. Nimeanza pia kuwatafuta wanawake wasomi wa ki-Islam na kujitambulisha kwao, ili waweze kuniongezea elimu kwa manufaa yangu na ya wanafunzi wangu. Ninafurahi kwa mafanikio ya kutia moyo ambayo nimeanza kuyaona.

Nimeandika ujumbe huu kwa kuzingatia kuwa wengi wanaosoma blogu yangu ni waumini wa dini. Wana wajibu wa kuchangia mawazo, hasa wakiona nimepotosha jambo lolote. Kwa muumini yeyote, hili si  suala la hiari, bali ni wajibu.

Thursday, October 8, 2015

Wanafunzi Wangu wa Ki-Ingereza

Ni yapata mwezi sasa tangu tuanze muhula mpya wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Ninafundisha kozi mbili, South Asian Literature na "First Year Writing." Hii ya kwanza ni kozi ya fasihi ya ki-Ingereza kutoka India, Pakistan, na Sri Lanka. Ya pili ni kozi ya uandishi wa ki-Ingereza. Picha hii kushoto, ya darasa la ki-Ingereza (FYW), tulipiga leo. Mwanafunzi mmoja hayumo. Niliweka picha ya darasa kama hili katika blogu hii.

Nilipenda ualimu tangu utotoni. Ninawapenda wanafunzi. Ninawaambia hivyo tangu siku ya kwanza ya masomo, nao wanashuhudia hivyo siku zote. Wanajionea ninavyojituma kuwaelimisha kwa uwezo wangu wote na kwa moyo moja. Sina ubaguzi, dhulma, wala upendeleo. Hiyo imekuwa tabia yangu tangu nilipoanza kufundisha, mwaka 1976, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Ninajivunia jambo hilo.

Kwa miezi mingi, hasa mwaka jana, afya yangu haikuwa njema, na nilichukua likizo ya matibabu. Ingawa nimeanza tena kufundisha, inatokea mara moja moja kwamba sijisikii vizuri. Juzi ilitokea hivyo, ikabidi niwaambie wanafunzi hao waendelee kuandika insha niliyowaagiza kabla, nikawaaga.

Jana, nilipofika ofisini, nilikuta kadi mlangoni pangu, ambayo picha yake inaonekana hapa kushoto. Wanafunzi hao walikuwa wameniandikia hiyo kadi na ndani walikuwa wamesaini majina yao. Maneno yanayoonekana pichani yanatokana na michapo yangu darasani. Nilivyoipata kadi hii, niliguswa. Nimewaambia hivyo leo, tulipoanza kipindi.

Ualimu si kazi rahisi. Inahusu taaluma. Inahusu malezi. Inahusu kuwashauri na kuwasaidia wanafunzi katika hali mbali mbali za maisha. Lakini, hayo ndiyo mambo yanayonivutia katika ualimu. Mafanikio ya wanafunzi masomoni na maishani ndio mafanikio na furaha yangu.

Tuesday, August 25, 2015

Nimekikuta Kitabu Changu Kinameremeta Dukani

Mchana huu nimemaliza kusahihisha mtihani wa kumalizia muhula wa somo langu la "African Literature." Nimekwenda chuoni kuwarudishia wanafunzi daftari zao, nikiwa na furaha ya kuwa na wiki mbili tatu za "uhuru," kabla ya kuanza muhula mwingine.

Baada ya kurudisha daftari, niliingia katika duka la vitabu. Nilizunguka kidogo tu humo ndani nikaona kitabu changu cha Matengo Folktales kimewekwa mahali pa wazi, pamoja na vitabu vingine vichache. Kinaonekana pichani chenye rangi ya manjano na ramani ya Afrika.

Huu ni utaratibu wa duka letu la vitabu. Kila wakati wanachagua vitabu vichache na kuviweka sehemu hizo za wazi ili viweze kuonekana kirahisi kwa wateja. Kufuatana na utaratibu uliopo, kitabu kitakuwa hapo kwa siku kadhaa, na hata wiki kadhaa, kabla ya kurudishwa sehemu yake.

Katika duka hili la chuoni St. Olaf vinapatkana vitabu vyangu vyote. Mbali ya wanafunzi, waalimu, na wafanyakazi wengine wa chuo, wageni wanaokitembelea chuo hupenda kuingia katika hili duka la vitabu, ambalo huuza pia bidhaa mbali mbali, kama ilivyo kawaida katika maduka ya vitabu ya vyuo vya Marekani.

Kila ninapoviona vitabu vyangu katika duka hili, mawazo hunijia, hasa kuhusu namna vitabu hivi vinavyowafaidia wa-Marekani. Vinawafaidia kielimu, kwa kuwa vinatumika katika masomo. Vinawafaidia kibiashara, kwa kuviuza, na vinachangia ajira hata kama ni kiasi kidogo sana, kwa wachapishaji, wasafirishaji, na wahudumu wa duka kama hili la Chuo cha St. Olaf. Nawazia mambo ya aina hii.

Monday, June 1, 2015

Blogu Zangu Zimenisaidia

Hapa Chuoni St. Olaf kuna utaratibu unaomtaka kila mwalimu kuandika ripoti ya shughuli alizofanya katika mwaka wa shule unaoisha. Hizo ni shughuli za kitaaluma, yaani vitabu ulivyochapishwa, makala ulizochapisha, ushiriki wako katika mikutano ya kitaaluma, kazi ulizofanya katika uongozi wa vyama vya kitaaluma, kozi ulizotunga na kufundisha, uhariri katika majarida ya kitaaluma. Vile vile unaorodhesha huduma ulizotoa katika jamii nje ya chuo, kama vile ushauri ("consultancy"), na mihadhara katika mikutano ya vikundi na jumuia.

Nimekuwa na jadi ya kuandika mambo ya aina hiyo katika blogu hii ya hapakwetu na blogu ya ki-Ingereza. Katika kuandika ripoti yangu ya mwaka unaoisha, blogu zangu zimekuwa hazina ya kumbukumbu na taarifa nilizohitaji. Huu ni uthibitisho wa manufaa ya shughuli ninayofanya ya kublogu. Ninakumbuka kuwa niliwahi kuelezea namna blogu ilivyonisaidia darasani.

Watu wengine wanaandika kumbukumbu zao katika "diary." Lakini mimi kwa vile sina mazoea ya kufanya hivyo, nitaendelea kublogu kama ninavyofanya. Lengo ni kuhifadhi kumbukumbu. Tena, kwa kuwa nimezoea kuelezea shughuli zangu kwa upana, tangu chimbuko hadi matokeo, taarifa zangu zitaweza kutumika hata kwa kuandika kitabu. Ndoto ya kuandika kitabu cha aina hiyo nimekuwa nayo kitambo. Panapo majaliwa, nitaitekeleza.

Monday, May 18, 2015

Kitabu cha Dr. John C. Sivalon, M.M.

Leo nimejipatia kitabu cha Dr. John C. Sivalon, M.M. Kanisa Katoliki na Siasa ya Tanzania Bara 1953 Hadi 1985. kilichochapishwa na shirika la Kanisa Katoliki la wa-Benediktini, Ndanda. Kutokana na kutopatikana madukani hapa Marekani, nimekipata kupitia maktaba ya hapa Chuoni St. Olaf, kwa utaratibu wa uazimishanaji wa vitabu baina ya maktaba. Nimejitengenezea nakala kwa matumizi yangu, kama inavyoruhusiwa kisheria.

Hiki ni kitabu kinachojulikana Tanzania kwa kuwa kinatajwatajwa sana na viongozi wa wa-Islam wanaosema kwamba wa-Islam wamekuwa wakihujumiwa na bado wanahujumiwa na serikali ya Tanzania kwa manufaa ya kanisa na wa-Kristu.

Kutokana na madai hayo, kwa miaka yote hii nimekuwa na hamu ya kujisomea kitabu hiki. Sikuwahi kusema lolote juu yake, kwa vile sikuwa nimekisoma. Baada ya kukipata, kama saa mbili tu zilizopita, nimekipitia chote, ila bado sijakisoma kwa makini.

Hata hivi, nimeona kuwa mwandishi ameandika kitabu hiki kwa busara bila ushabiki, nikakumbuka kitabu cha Hamza Njozi, Mauaji ya Mwembechai, ambacho nacho amekiandika kwa busara bila ushabiki. Nimeangalia mtandaoni nikaona kuwa Dr. Sivalon ameandika pia kitabu kingine, God's Mission and Postmodern Culture: The Gift of Uncertainty. Hiki itakuwa rahisi kukinunua hapa Marekani.

Napenda kusema kila mmoja wetu ajisomee mwenyewe kitabu hiki cha Dr. Sivalon cha Kanisa Katoliki na Siasa ya Tanzania Bara 1953 Hadi 1985, ayatafakari yaliyomo. Kwa kuzingatia kuwa bado sijakisoma kwa umakini, napenda kutoa fursa kwa yeyote ambaye amekisoma aweze kutuletea maoni yake. Nami, baada ya kukisoma ipasavyo, nitatoa maoni yangu.

Thursday, May 14, 2015

Hadithi za Luis Bernardo Honwana wa Msumbiji

Leo nimeagiza mtandaoni kitabu cha hadithi za Luis Bernardo Honwana wa Msumbiji kiitwacho We Killed Mangy Dog and Other Stories. Kwa wiki kadhaa, nimemwazia sana mwandishi huyu, ambaye kitabu chake hiki nilikipenda sana nilipokuwa mwanafunzi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuanzia mwaka 1973. Nilivutiwa na jinsi alivyoielezea maisha nchini Msumbiji, ambayo ilikuwa daima mawazoni mwetu kutokana na vita vya ukombozi vilivyoongozwa na FRELIMO.

Nimeamua kununua kitabu hiki wakati huu kwa sababu katika wiki hizi nimeandaa orodha ya vitabu vya kufundishia kozi yangu ya "Post-colonial Literature" muhula wa kiangazi, mwezi Julai na Agosti. Kwa mara ya kwanza tangu nianze kufundisha hapa Chuoni St. Olaf, nimeamua kuingiza kazi ya fasihi kutoka Msumbiji.

Sitafundisha We Killed Mangy Dog and Other Stories, ingawa ningeweza kufanya hivyo kwa furaha kabisa. Badala yake, nitafundisha riwaya ya mwandishi mwingine maarufu Mia Couto iitwayo The Tuner of Silences, ambayo sijaisoma. Hata hivyo nimeona nijipatie hiki kitabu cha hadithi za Honwana, nilichokipenda enzi za ujana wangu, nikisoma tena wakati nangojea kufundisha The Tuner of Silences,

Ninangojea kwa hamu kusoma na kufundisha The Tuner of Silences. Ninangojea kwa hamu  kujikumbusha na kuwaeleza wanafunzi kuhusu Msumbiji, historia yake, historia ya utamadini na fasihi yake. Ninapangia kuandika zaidi kuhusu hayo katika blogu hii wakati utakapowadia.

Wednesday, July 2, 2014

Mandhari ya Mto wa Mbu na Ziwa Manyara

Mwezi Januari, 2013, katika mizunguko yangu Tanzania na wanafunzi wa Chuo cha St. Olaf, tukiwa tunafuatilia safari na maandishi ya Ernest Hemingway, niliamua tusimame kwenye mlima juu ya Mto wa Mbu, pembeni ya barabara iendayo Karatu.

Mkisimama hapo, mnauona mji wa Mto wa Mbu kule bondeni, na kwa mbali kule mbele mnaliona ziwa la Manyara.








Hata miaka iliyotangulia, wakati nasafiri na wanafunzi kutoka Chuo cha Colorado, tulifika mahali hapa. Mimi kama mwalimu naona ni muhimu kwa wanafunzi kufika sehemu hiyo na kuangalia sehemu hizi ambazo Hemingway alizielezea vizuri katika kitabu chake cha Green Hills of Africa. Inavutia kusoma maelezo ya Hemingway wakati mpo mahali hapa, anavyouelezea mji, mto unaopita hapo, duka la m-Hindu na uzuri wa Ziwa Manyara.

Nina imani kuwa sina haja ya kueleza kuwa anayeonekana hapo kushoto ni mimi.

Tuesday, July 1, 2014

Ngorongoro

Hapa ilikuwa ni mwezi Januari, 2013. Niko katika bonde la Ngorongoro, mmoja ya vivutio vikubwa vya utalii Tanzania. Nimebahatika kufika sehemu hiyo mara kadhaa. Kila wakati naguswa na uzuri na upekee wa mahali hapo.



Mara ya kwanza kufika hapo nilikuwa kiongozi wa wanafunzi na wazazi wao kutoka shule ya Shady Hill, Boston. Nilikuwa nimeombwa na kampuni ya Thomson Safaris kuongoza msafara huu.







Miaka iliyofuata nimefika hapo na wanafunzi kutoka vyuo vya Marekani vya Colorado na St. Olaf, tukiwa katika kozi ya "Hemingway in East Africa," ambayo niliitunga. Nimeandika makala kadhaa kuhusu kozi hiyo, na makala ya hivi karibuni kabisa ni hii hapa

Kila wakati naguswa na uzuri na upekee wa mahali hapo. Kuna wanyama wa aina aina, kama vile samba, pundamilia, twiga, tembo, vifaru na nyati.

Mara zote, tulitembelea pia hifadhi za Serengeti, Manyara, na Tarangire. Zote hizo ni utajiri mkubwa wa nchi yetu, kwa sasa na kwa vizazi vijavyo.

Tuesday, February 8, 2011

Blogu Imenisaidia Darasani

Leo wakati muhula mpya unaanza hapa Chuoni St. Olaf, nimekutana na wanafunzi nitakaowafundisha somo la kuandika kwa ki-Ingereza. Kama kawaida, siku ya kwanza huwa ni ya kujitambulisha, kuelezea habari za somo, maana yake, falsafa na maadili yangu kama mwalimu, maana na mikakati ninayotumia katika kufundisha.

Katika kujitambulisha, huwa nawaeleza wanafunzi kuhusu nyumbani kwangu, shule nilizosoma, na nilivyoingia katika kazi ya ualimu, na imani yangu kuwa Mungu alitaka niwe mwalimu.

Leo wakati naanza kuelezea habari za nyumbani kwangu, nilikumbuka kuwa nilishaandika kwenye blogu. Basi, niliwasha kompyuta iliyomo darasani nikafungua blogu na wao wenyewe wakasoma kwenye skrini kubwa habari za Litembo.

Blogu imenisaidia kufikisha ujumbe wangu kwa ufanisi, kwani mbali ya maelezo kuna picha. Picha zinajieleza vizuri kuliko pengine hata maneno, jambo linalosisitizwa katika ule usemi kuwa picha ni sawa na maneno elfu. Niliwaambia kuwa nina picha nyingi za nyumbani kwangu na Tanzania kwa ujumla. Ni wazi kuwa ninazo fursa tele za kuendelea kuwajulisha walimwengu habari za kwetu.

Wednesday, September 1, 2010

Nimepiga Picha Nyingi Tanzania

Kila mwaka, ninapokuwa Tanzania, napiga picha nyingi niwezavyo na kuja nazo huku Marekani. Mwaka huu nimepiga picha nyingi sehemu nilizopata fursa ya kuzitembelea: Arusha, Dar es Salaam, Lushoto, Morogoro, Moshi, na Tanga.

Watu ambao wameishi Tanzania tu wanaweza kuuliza kwa nini napiga picha hata sehemu ambazo si za pekee au muhimu. Siwezi kuwalaumu. Huku ughaibuni mambo ni tofauti, na napenda nitoe fununu kidogo.

Mbali na kufundisha hapa katika chuo cha St. Olaf, ninashughulika na programu zinazopeleka wanafunzi Tanzania na sehemu zingine za Afrika. Kazi yangu ni kuwaandaa hao wanafunzi, kwa kuwaeleza mambo ya utamaduni, maisha, elimu, na kadhalika yahusuyo nchi hizo wanakokwenda.

Picha zangu hizi ni hazina inayonisaidia katika shughuli hizi. Mbali ya kuwaelimisha, zinawahamasisha katika kupenda kuja Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Wiki iliiyopita, niliporejea hapa chuoni kutoka Tanzania, mkuu wa idara yangu ya ki-Ingereza aliomba nitundike picha za Tanzania kwenye ubao wetu wa matangazo. Niko katika harakati ya kuziandaa. Ni fursa ya kuitangaza Tanzania, nami nimeipokea kwa furaha. Picha hizi zitakaa hapo kwa wiki kadhaa, labda miezi.

Napangia kutundika picha za Chuo Kikuu Dar es Salaam, maeneo ya miji niliyoitembelea na vijiji mbali mbali. Nitatundika picha za matukio mbali mbali. Nitatundika picha za makanisa na misikiti, nikizingatia kuwa wa-Marekani hawajazoea kuona misikiti, na mbaya zaidi, wengi wana mawazo potofu kuhusu misikiti na u-Islam, kama nilivyogusia hapa. Hizi picha zitachangia kuwaelimisha.

Jambo la ziada ni kuwa ninazunguka sehemu mbali mbali hapa Marekani nikitoa mihadhara kuhusu masuala kama elimu na tamaduni, kama inavyoonekana katika blogu zangu. Basi, katika mizunguko hiyo, picha zangu ni hazina mojawapo na nyenzo ya kuelimishia.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...