Wednesday, May 18, 2016

Muhula Unaisha; Umebaki Utafiti

Jana tumemaliza muhula wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Nilikuwa ninafundisha "Folklore," Muslim Women Writers, na "First Year Writing." Kwa utaratibu wa chuo hiki, masomo matatu kwa muhula ndio kiwango cha juu kabisa. Hatufundishi zaidi ya masomo matatu. Kwa hivi, nilitegemea ningekuwa nimechoka, lakini sisikii uchovu. Alhamdulillah.

Kwa wiki nzima inayokuja, tutakuwa na mitihani. Baada ya hapo tutaanza likizo ndefu ya miezi mitatu na kidogo. Inaitwa likizo, lakini maprofesa tunaona ni wakati muafaka wa kufanya shughuli za kitaaluma kama utafiti na uandishi.

Nami nimeamua kwenda Boston kwa siku chache kufanya utafiti juu ya Ernest Hemingway katika maktaba ya John F. Kennedy. Humo kuna hifadhi kubwa kuliko zote duniani ya vitabu, miswada, picha na  kumbukumbu zingine zinazomhusu Hemingway. Ingawa nimefika Boston mara kadhaa, sijawahi kwenda katika maktaba hiyo maarufu.

Nina bahati kuwa ninafahamiana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway ambaye bado yuko hai. Yeye ndiye mmiliki wa haki zote za urithi wa Hemingway. Nilipomwambia kwa mara ya kwanza kwamba napangia kwenda kufanya utafiti katika maktaba ya John F. Kennedy,  aliniambia nimfahamishe ni lini ili anitambulishe kwa wahusika. Wiki chache zilizopita, katika maongezi yetu, nilimwambia tena kuwa napangia kwenda kwenye maktaba ile, alikumbushia kuwa nimweleze ni muda upi nitakwenda ili awafahamishe.

Ninashukuru sana kwa hilo, kwani katika kusoma taarifa za maktaba ile, nimefahamu kuwa kuna masherti yanayohusu kuitumia hifadhi ya Ernest Hemingway. Mtu hukurupuki tu ukafika pale na kufanya utafiti. Kuna baadhi ya kumbukumbu ambazo zimefungiwa. Mtafiti unahitaji kibali maalum kuweza kuzifanyia utafiti. Sherti nichukue hatua hima.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...