Wednesday, May 4, 2016

Tamasha la Kimataifa, Rochester, Aprili 30

Tarehe 30 April, nilihudhuria tamasha la kimataifa mjini Rochester ambalo nililizungumzia katika blogu hii. Nilipeleka vitabu vyangu, kwani ninashiriki matamasha kama mwalimu na mwandishi. Nilichukua pia bendera ya Tanzania. Meza yangu ilikuwa inavyoonekana pichani hapa kushoto, picha ambayo ilipigwa na mama mmoja kutoka China, mmoja wa watu walioniambia kuwa walipendezwa na mwonekano wa meza yangu, wakapiga picha.

Kwa kuiona bendera yangu, watu kadhaa wa Kenya na Uganda walikuja kuongea nami. Kwa utani na moyo wa ujirani, Wa-Kenya walitumia jina la Bongo muda wote.

Pichani hapa kushoto ni jamaa wawili kutoka Guatemala. Niliwapa makala yangu fupi, "Chickens in the Bus," tukaongea kuhusu tamaduni zetu, tukaona jinsi zinavyofanana. Ni kawaida kuwaona watu  Guatemala wakisafiri ndani ya basi wakiwa wamebeba kuku au hata nguruwe. Kwa mujibu wa mama mmoja Mmarekani aliyefika mezani pangu na kuiona makala hiyo, Mexico nako unaweza kuwaona watu ndani ya basi wakiwa na kuku au nguruwe.

Kwa kufahamu kwamba wa-Marekani wanashangaa mambo hayo, nimekumbushia katika makala yangu kuwa hapa Marekani ninawaona watu wakisafiri na mbwa katika magari yao.

Kama picha zangu zinavyoonyesha, tamasha lilihudhuriwa na watu wa tamaduni mbali mbali. Mji wa Rochester una watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Kutoka Afrika, kwa mfano, kuna wa-Somali wengi katika mji huu.

Kulikuwa na maonesho ya bidhaa, mavazi, kazi za sanaa, kama vile michoro na vinyago, na ala za muziki. Kulikuwa na burudani ya nyimbo na ngoma, na hata mchezo wa karate.


























Jumuia na taasisi mbali mbali za huduma za jamii ziliwakilishwa pia.





Pichani hapa kushoto ni meza iliyowakilisha Trinidad. Nilisogea hapo, nikaongea na huyu mama. Nilimwambia kuwa ninafahamu kiasi fasihi na utamaduni wa Trinidad, tukazungumza juu ya waandishi maarufu kama V.S. Naipaul, Sam Selvon, Shiva Naipaul, na Earl Lovelace.

Tulipomwongelea mwandishi Selvon, huyu mama aliniuliza kama nimesoma riwaya yake ya The Lonely Londoners, nami nikamweleza kuwa ni riwaya mojawapo ambayo naipenda sana, nimeifundisha mara nyingi.



Lengo la tamasha, kuwaleta watu wa mataifa na tamaduni za ulimwengu pamoja kwa ajili ya kufahamiana, kuelimishana, na kufurahia maonesho mbali mbali lilifanikiwa sana. Nimeandika taarifa ya tamasha hili katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Waandaji wa tamasha, Rochester International Association, wanastahili sifa na pongezi kwa kazi yao nzuri.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...