Showing posts with label jumuia. Show all posts
Showing posts with label jumuia. Show all posts

Sunday, February 12, 2017

Nimemaliza Kusoma The Highly Paid Expert

Leo nimemaliza kusoma The Highly Paid Expert, kitabu kilichotungwa na Debbie Allen, ambacho nilikitaja katika blogu hii. Nimekifurahia kitabu hiki, kwa jinsi kilivyoelezea misingi na mbinu za kumwezesha mtu kuwa mtoa ushauri mwenye mafanikio kwake na kwa wateja.

Mambo anayoelezea mwandishi Debbie Allen yananihusu moja kwa moja katika ya kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants. Kwa hivi, kitabu hiki kimekuwa na mvuto wa pekee kwangu. Nimevutiwa na namna mwandishi anavyoelezea mbinu za mtu kujijenga katika uwanja wake hadi kufikia kileleni. Anaelezea mategemeo ya wateja na namna ya kushughulika nao. Anaelezea umuhimu wa kujifunza kutoka kwa wataalam wengine, matumizi ya tekinolojia katika kuwasiliana na wateja, kuendesha mikutano, na kujitangaza. Vile vile anasisitiza uaminifu na uwajibikaji.

Ameelezea vizuri namna wengi wetu tunavyoshindwa kujitangaza na tunavyoshindwa au kusita kutambua umaarufu na umuhimu wetu na thamani ya ujuzi wetu, jambo ambalo linatufanya tusitegemee malipo yanayoendana na ubingwa wetu. Tunaridhika na malipo hafifu, wakati tulistahili malipo makubwa.

Sura ya 24 ya The Highly Paid Expert inaelezea uandishi wa kitabu. Mwandishi anasema kuwa kitabu ni nyenzo muhimu ya mtaalam katika fani yake. Kitabu kinamjengea sifa na kuonekana. Kinamfanya mtaalam aaminike. Mwandishi anaeleza wazi kuwa kitabu hakileti utajiri, bali kinafungua milango ya fursa.

Hayo nimejionea mwenyewe. Kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimenifungulia fursa nyingi. Nimepata mialiko ya kwenda kutoa mihadhara au ushauri katika taasisi na jumuia mbali mbali, kama vile makanisa, vyuo, na makampuni.

Nimevutiwa na mambo anayoelezea mwandishi wa The Highly Paid Expert kuhusu uandishi na uuzaji wa kitabu. Yanafanana na yale ambayo nami nimekuwa nikieleza katika blogu hii. Kwa mfano, anasema kuwa jukumu kubwa la kutangaza na kuuza kitabu ni la mwandishi.

The Highly Paid Expert ni kati ya vitabu ambavyo nimevifurahia kwa dhati. Mawaidha yake mengi ni ya kukumbukwa daima. Mfano ni msisitizo wake juu ya kushirikiana na wengine. Mtu hufanikiwi kwa uwezo wako mwenyewe tu na kutojihusisha na wengine wenye utaalam, hata kama ni washindani wako.

Monday, June 1, 2015

Blogu Zangu Zimenisaidia

Hapa Chuoni St. Olaf kuna utaratibu unaomtaka kila mwalimu kuandika ripoti ya shughuli alizofanya katika mwaka wa shule unaoisha. Hizo ni shughuli za kitaaluma, yaani vitabu ulivyochapishwa, makala ulizochapisha, ushiriki wako katika mikutano ya kitaaluma, kazi ulizofanya katika uongozi wa vyama vya kitaaluma, kozi ulizotunga na kufundisha, uhariri katika majarida ya kitaaluma. Vile vile unaorodhesha huduma ulizotoa katika jamii nje ya chuo, kama vile ushauri ("consultancy"), na mihadhara katika mikutano ya vikundi na jumuia.

Nimekuwa na jadi ya kuandika mambo ya aina hiyo katika blogu hii ya hapakwetu na blogu ya ki-Ingereza. Katika kuandika ripoti yangu ya mwaka unaoisha, blogu zangu zimekuwa hazina ya kumbukumbu na taarifa nilizohitaji. Huu ni uthibitisho wa manufaa ya shughuli ninayofanya ya kublogu. Ninakumbuka kuwa niliwahi kuelezea namna blogu ilivyonisaidia darasani.

Watu wengine wanaandika kumbukumbu zao katika "diary." Lakini mimi kwa vile sina mazoea ya kufanya hivyo, nitaendelea kublogu kama ninavyofanya. Lengo ni kuhifadhi kumbukumbu. Tena, kwa kuwa nimezoea kuelezea shughuli zangu kwa upana, tangu chimbuko hadi matokeo, taarifa zangu zitaweza kutumika hata kwa kuandika kitabu. Ndoto ya kuandika kitabu cha aina hiyo nimekuwa nayo kitambo. Panapo majaliwa, nitaitekeleza.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...