Showing posts with label wateja. Show all posts
Showing posts with label wateja. Show all posts

Tuesday, February 6, 2018

Mteja Anapokupigia Debe

Tarehe 3 Februari, nilipata ujumbe wa barua pepe kutoka kwa dada au mama ambaye amejitambulisha kwa jina la Cynthia, ila simjui. Ameandika kuulizia kitabu changu namna hii:

Hello,

I am planning a trip to Tanzania and someone recommended your book about cultural differences between Africans and Americans. How can I purchase your book? Thank you very much.

Kwa wasiojua ki-Ingereza, tafsiri yake ni hii:

Habari

Ninapanga safari ya kwenda Tanzania na mtu fulani alikipendekeza kitabu chako juu ya tofauti za tamaduni za wa-Afrika na wa-Marekani. Nitakinunuaje kitabu chako? Shukrani sana.

Kwa mwandishi, habari ya aina hii ni habari njema. Kwamba mtu fulani ambaye alitumia hela zake kununulia kitabu chako alikisoma akaridhika au kufurahi kiasi cha kukipendekeza kwa mwingine, si jambo jepesi. Mtu anapopendekeza kitu kwa mwingine namna hii, anajiweka katika hali ya kueleweka vibaya, iwapo kile anachopendekeza hakitamridhisha huyu mwingine. Tunapendekeza vitu kwa marafiki zetu tukiwa na uhakika na hicho tunachopendekeza.

Sisi wote ni wateja wa hiki au kile, iwe ni vitu au huduma. Muda wote tunawashawishi wenzetu wakanunue kitu fulani au wanapohitaji huduma, tunawaelekeza sehemu ambayo tunaiamini. Tunapopendekeza kitu au huduma tunatoa tamko kuhusu ubora wa kile tunachopendekeza. Nimekuwa nikielezea masuala haya katika blogu hii.

Muda wote sisi binadamu tunafanya hii shughuli ya kupiga debe bila malipo. Tunafanya hiki kibarua kisicho na malipo bila hata kujitambua. Ni sehemu ya mazungumzo yetu na marafiki au watu wengine. Mwenye kuuza bidhaa au kutoa huduma anafaidika bila kutumia hela kulipia matangazo.

Hayo ni baadhi ya mawazo yangu wakati huu ninapotafakari suala la huyu mpiga debe asiyejulikana ambaye amekipendekeza kitabu changu kwa mtu huyu aitwaye Cynthia, ambaye naye simjui. Nimemjibu Cynthia nikamwambia sijui mahali alipo, lakini kitabu anaweza kukipata mtandaoni.

Wednesday, October 25, 2017

Ninangojea Mwaliko Kuelezea Tamaduni

Nimeona tangazo la chuo kimoja cha hapa Minnesota kwamba wanajiandaa kuwapeleka wanafunzi kwenye nchi moja ya Afrika. Ni programu ambayo wamekuwa nayo kwa miaka kadhaa. Kila mara, wamekuwa wakitumia kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika maandalizi hayo, ili kufahamu mambo ya msingi ya tofauti za tamaduni. Wamekuwa wakinialika kuongea nao kabla ya safari.

Nilivyoona tangazo nilijisemea kuwa hawa watu lazima watatafuta kitabu changu tena, na watanitafuta tena, kutokana na nilivyoona siku zilizopita. Nimejifunza tangu zamani kuwa unapotoa huduma kwa mteja, toa huduma bora kiasi cha kumfanya mteja asiwe na sababu ya kutafuta huduma kwingine.

Kwa upande wangu, nilijenga uhusiano huu na wateja kwa awamu. Mwanzoni, nilikuwa ninatoa ushauri tu, hasa katika program za kupeleka wanafunzi Afrika, zinazoendeshwa na vyuo mbali mbali vya Marekani. Baadaye, nilichapisha kitabu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences,  na hicho kikawa kinawavutia wateja wapya. Si kwamba kitabu hiki kina kila kitu. Vile vile, wanaonialika hawanialiki nikawasomee hiki kitabu. Wanakuwa wameshakisoma, ila wanakuwa na shauku ya kujua zaidi kutoka kwangu mwandishi. Kitabu ni kama chambo na kianzio cha mazungumzo.

Ninaandaa kitabu kingine cha kuendeleza yaliyomo katika Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitakuwa na mwelekeo ule ule na mtindo ule ule, ila kitaibua mambo mapya. Tayari nimeshakipa jina, Chickens in the Bus, ambacho ni kichwa cha sura mojawapo katika kitabu hiki.

Sunday, February 12, 2017

Nimemaliza Kusoma The Highly Paid Expert

Leo nimemaliza kusoma The Highly Paid Expert, kitabu kilichotungwa na Debbie Allen, ambacho nilikitaja katika blogu hii. Nimekifurahia kitabu hiki, kwa jinsi kilivyoelezea misingi na mbinu za kumwezesha mtu kuwa mtoa ushauri mwenye mafanikio kwake na kwa wateja.

Mambo anayoelezea mwandishi Debbie Allen yananihusu moja kwa moja katika ya kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants. Kwa hivi, kitabu hiki kimekuwa na mvuto wa pekee kwangu. Nimevutiwa na namna mwandishi anavyoelezea mbinu za mtu kujijenga katika uwanja wake hadi kufikia kileleni. Anaelezea mategemeo ya wateja na namna ya kushughulika nao. Anaelezea umuhimu wa kujifunza kutoka kwa wataalam wengine, matumizi ya tekinolojia katika kuwasiliana na wateja, kuendesha mikutano, na kujitangaza. Vile vile anasisitiza uaminifu na uwajibikaji.

Ameelezea vizuri namna wengi wetu tunavyoshindwa kujitangaza na tunavyoshindwa au kusita kutambua umaarufu na umuhimu wetu na thamani ya ujuzi wetu, jambo ambalo linatufanya tusitegemee malipo yanayoendana na ubingwa wetu. Tunaridhika na malipo hafifu, wakati tulistahili malipo makubwa.

Sura ya 24 ya The Highly Paid Expert inaelezea uandishi wa kitabu. Mwandishi anasema kuwa kitabu ni nyenzo muhimu ya mtaalam katika fani yake. Kitabu kinamjengea sifa na kuonekana. Kinamfanya mtaalam aaminike. Mwandishi anaeleza wazi kuwa kitabu hakileti utajiri, bali kinafungua milango ya fursa.

Hayo nimejionea mwenyewe. Kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimenifungulia fursa nyingi. Nimepata mialiko ya kwenda kutoa mihadhara au ushauri katika taasisi na jumuia mbali mbali, kama vile makanisa, vyuo, na makampuni.

Nimevutiwa na mambo anayoelezea mwandishi wa The Highly Paid Expert kuhusu uandishi na uuzaji wa kitabu. Yanafanana na yale ambayo nami nimekuwa nikieleza katika blogu hii. Kwa mfano, anasema kuwa jukumu kubwa la kutangaza na kuuza kitabu ni la mwandishi.

The Highly Paid Expert ni kati ya vitabu ambavyo nimevifurahia kwa dhati. Mawaidha yake mengi ni ya kukumbukwa daima. Mfano ni msisitizo wake juu ya kushirikiana na wengine. Mtu hufanikiwi kwa uwezo wako mwenyewe tu na kutojihusisha na wengine wenye utaalam, hata kama ni washindani wako.

Tuesday, June 7, 2011

Mwaliko Nyumbani kwa Wateja Wangu

Jana jioni nilikuwa nyumbani kwa familia inayoonekana katika hii picha. Ni familia ya Shannon Gibney, mwandishi chipukizi ambaye tayari ni maarufu.

Miaka michache iliyopita, Shannon Gibney alisoma kitabu changu cha Africans and Americans, akaandika mapitio katika Minnesota Spokesman Recorder, kama nilivyosema hapa.

Siku chache zilizopita alinialika nyumbani kwake kwa chakula cha jioni, tukapanga hiyo tarehe ya jana. Aliniambia kuwa mume wake, ambaye anatoka Liberia, na bado ni mgeni hapa Marekani, amekuwa akisoma kitabu changu.

Nilifurahi kukutana na familia hii. Kwa zaidi ya saa mbili nilizokuwa nao, maongezi yetu yalihusu masuala niliyoongelea katika kitabu, yaani tofauti za tamaduni za wa-Marekani na wa-Afrika. Wote wawili wanakifahamu vizuri sana kitabu hiki, na walikuwa wananikumbusha mengi, ingawa mimi ndiye mwandishi.

Huyu bwana aliezea mshangao wake kwa jinsi maelezo ya kitabu hiki yanavyofanana na hali ya Liberia, ingawa mimi mwandishi sijafika kule. Niliguswa na furaha yake kwamba niliyoandika yamemwelewesha mambo ya wa-Marekani ambayo yalikuwa yanamtatiza. Nami nashukuru kwa hilo.

Familia hii ilinikarimu vizuri sana, nami nimebaki nashangaa kwa jinsi uandishi wa kitabu unavyoweza kukujengea urafiki na watu kiasi hicho.

Friday, March 11, 2011

Mteja Nimefurahi

Juzi niliandika makala fupi, "Mteja ni Mfalme". Leo napenda kuendelea na mada hiyo, kutokana na jambo lililonitokea.

Nilipeleka kigari changu kwenye kampuni ya CarTime, kubadilisha "oil." Kama kawaida, wakati fundi anaendelea na shughuli, nilikuwa kwenye sehemu ya mapumziko ambako wateja hungojea magari yao. Baada ya muda, niliitwa na kuambiwa kuwa gari yangu tayari, nikalipia na kuchukua ufunguo. Kama kawaida, mhudumu wa hapo mapokezi alinishukuru.

Nilienda nje fundi alikopaki gari nikafungua mlango. Kwenye kiti cha mbele alikuwa ameweka karatasi ambayo picha yake nimeiweka hapa juu. Fundi makenika alikuwa ameiweka hapo. Ujumbe wake ni huu: Asante kwa kuchagua CarTime. Tumefurahi kuhudumia gari lako. Kama vile hii haitoshi, fundi ameshukuru tena na kuandika jina lake, Eric.

Katika makala yangu ya juzi niliongelea umuhimu wa kumridhisha mteja. Sasa leo hapa nimeweka mfano hai. Mimi kama mteja nimefurahi kwa huduma niliyopata. Lakini kwa hapa Marekani, hili si jambo la ajabu, kwani wenye biashara wanazingatia suala la huduma kwa mteja. Niliwahi kusema hivyo hata kwenye mahojiano niliyofanyiwa na Radio Mbao.

Kwa vile wanablogu tunafahamu kuwa blogu ni kama shule, na kwa kuzingatia kuwa watu wengi nchini wanasoma hizi blogu, nimeona niweke taarifa hii na mawazo mawili matatu yanayotakiwa kuzingatiwa na wafanyabiashara na watoa huduma wa Tanzania, ambao mara nyingi tunawalalamikia.

Niliwahi kuhudhuria semina ya biashara hapa Minnesota ambapo baadhi ya mambo yaliyosisitizwa ni kuwa unapokuwa na mteja, uwe makini sana. Ujue kuwa mteja huyu akiridhika na kufurahi, atakwenda kukutangazia biashara au huduma yako kwa marafiki na watu wengine.

Sisi wenyewe tunafanya hivyo kila siku. Tukiwa tumevaa nguo nzuri, halafu marafiki wakatuuliza tumenunua wapi, tunawatajia duka. Au watu wakituuliza hoteli nzuri iko wapi, tunawatajia. Waulize watu Dar es Salaam kitimoto safi kinapatikana wapi, watakutajia. Tukiona filamu nzuri, tunawaambia watu wengine na kuwahamasisha nao wakaione. Kwa maana hiyo, tunawapelekea wafanyabishara wateja bila wao kuingia gharama ya matangazo.

Katika semina hiyo hiyo tulionywa kwamba mteja akiudhika, atakwenda kutangaza habari mbaya kuhusu yaliyompata. Habari hiyo itaenea. Wale watakaosikia watawaambia wenzao, na inakuwa kama sumu ambayo itahujumu biashara au huduma yako.

Mimi mwenyewe mwaka jana nilikumbana na wahudumu wa ovyo katika hoteli moja mjini Arusha. Ni hoteli nzuri, na niliiipenda. Nililipia nikapelekwa chumbani. Baada ya muda kidogo nilihitaji msaada wa kurekebishiwa taa. Hapo ndipo nilipokumbana na uzembe usio kifani. Wahudumu walichelewa sana, na huenda hata walisahau. Nikawakumbusha. Bado hawakuja, nimi nikaendelea kuwangoja. Hatimaye nilienda chini walikokuweko nikaanza kuwafokea. Bosi wao naye akaja, nami nikamjumlisha katika mhadhara wangu wa jazba, nikaendelea kutema cheche na kuwapa vidonge wote. Hawakuwa na sababu kabisa ya kushindwa kutekeleza nilichokuwa nimewaambia.

Basi, kutokana na usumbufu walionipa, hata wakati huu ninapoandika sipendi hata kuiwazia hoteli ile. Inakuwa kama vile natonoshwa kidonda. Sina hamu ya kufikia tena katika hoteli ile. Bahati yao ni kuwa hapa sitataja jina lao. Wangenikoma.

Haya ndio mambo ambayo wenye biashara wanapaswa kuyaelewa na kuyazingatia. Inashangaza kwamba wengi nchini mwetu wanaamini kuwa jambo la kufanya ni kwenda kwa waganga wakapate dawa ya kuwavutia wateja. Inakuwaje sisi tuzingatie imani hizo wakati wenzetu kama hao CarTime hawatumii dawa?

Wednesday, March 9, 2011

Mteja ni Mfalme

Kwamba mteja ni mfalme ni dhana inayojulikana, hata kama wengi wenye biashara hawaifuati. Mantiki ya usemi kuwa mteja ni mfalme iko wazi, kwamba mteja akiridhika anakuwa ndio mpiga debe wako, bila wewe kumlipa chochote. Kwa hivi, kama wewe ni mfanyabiashara, ukiwa na tabia ya kumridhisha kila mteja, utafanikiwa.

Kwa kawaida nadharia ni rahisi, ila utekelezaji unaweza kuwa mtihani mgumu. Hayo ninayaona wakati huu ninapoandika makala hii. Kuna mtu ameanza mawasiliano nami, kunialika nikazungumze kwenye kampuni anapofanyia kazi, kuhusu masuala ninayoongelea katika kitabu changu cha Africans and Americans.

Ingawa nimethibitisha kuwa shughuli hii itafanyika, nimeona kuwa huyu mhusika hana uzoefu mzuri katika kupanga mipango ya aina hii. Nimeanza kupata usumbufu fulni, kwani wakati fulani anasema kitu nami nikadhani nimemwelewa, kumbe baadaye inaonekana hatukuelewana. Hata tarehe aliyopangia tufanya hiyo shughuli ameniambia kuwa imebidi waibadili.

Ninajua kabisa kuwa hatimaye nitaenda kutoa huo mhadhara, lakini usumbufu unanikera. Sasa hapo ndipo suala la mteja ni mfalme linapoingia. Mimi ninatoa huduma ya ushauri katika masuala kama haya niliyoongelea katika kitabu changu. Nimesajili kijikampuni kiitwacho Africonexion hapa Minnesota na huduma nazitoa chini ya kivuli cha kampuni hiyo. Huduma hizo ni pamoja na ushauri, warsha, na vitabu.

Sasa basi, kwa mujibu wa dhana ya kwamba mteja ni mfalme, ni wazi kuwa nawajibika kuwa sambamba na huyu jamaa anayenisumbua, nimsikilize vizuri muda wote na kuongea naye kwa uchangamfu, kama vile hakuna kinachonikera. Kero zake nizione kuwa ni fursa ya mimi kujiongezea uzoefu katika kuwashughulikia wateja na kuimarisha sifa ya kikampuni changu.

Najua kuwa pamoja na yote, kikampuni changu kitafaidika. Kwanza, malipo tumeshapatana, na maandalizi yake yameanza. Siku itakapofika, nitaenda kutoa mhadhara wa kusisimua na kuelimisha. Wao watafaidika, nami nitajipatia wapiga debe wengi.
(Katuni ni ya Nathan Mpangala)

Tuesday, April 6, 2010

Huduma kwa Wateja: Nathan Mpangala

Suala la huduma bora kwa wateja ni muhimu katika biashara au sekta yoyote inayotoa huduma. Mchora katuni maarufu Nathan Mpangala amechora katuni nzuri, ambayo imenikumbusha makala niliyowahi kuandika kuhusu suala hilo, "Ubora wa Huduma, Msingi wa Mafanikio." Bofya hapa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...