Showing posts with label Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.. Show all posts
Showing posts with label Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.. Show all posts

Wednesday, October 25, 2017

Ninangojea Mwaliko Kuelezea Tamaduni

Nimeona tangazo la chuo kimoja cha hapa Minnesota kwamba wanajiandaa kuwapeleka wanafunzi kwenye nchi moja ya Afrika. Ni programu ambayo wamekuwa nayo kwa miaka kadhaa. Kila mara, wamekuwa wakitumia kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika maandalizi hayo, ili kufahamu mambo ya msingi ya tofauti za tamaduni. Wamekuwa wakinialika kuongea nao kabla ya safari.

Nilivyoona tangazo nilijisemea kuwa hawa watu lazima watatafuta kitabu changu tena, na watanitafuta tena, kutokana na nilivyoona siku zilizopita. Nimejifunza tangu zamani kuwa unapotoa huduma kwa mteja, toa huduma bora kiasi cha kumfanya mteja asiwe na sababu ya kutafuta huduma kwingine.

Kwa upande wangu, nilijenga uhusiano huu na wateja kwa awamu. Mwanzoni, nilikuwa ninatoa ushauri tu, hasa katika program za kupeleka wanafunzi Afrika, zinazoendeshwa na vyuo mbali mbali vya Marekani. Baadaye, nilichapisha kitabu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences,  na hicho kikawa kinawavutia wateja wapya. Si kwamba kitabu hiki kina kila kitu. Vile vile, wanaonialika hawanialiki nikawasomee hiki kitabu. Wanakuwa wameshakisoma, ila wanakuwa na shauku ya kujua zaidi kutoka kwangu mwandishi. Kitabu ni kama chambo na kianzio cha mazungumzo.

Ninaandaa kitabu kingine cha kuendeleza yaliyomo katika Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitakuwa na mwelekeo ule ule na mtindo ule ule, ila kitaibua mambo mapya. Tayari nimeshakipa jina, Chickens in the Bus, ambacho ni kichwa cha sura mojawapo katika kitabu hiki.

Friday, June 5, 2015

Ninaombwa Tafsiri ya Kitabu Changu

Mara kadhaa, wa-Marekani wameniuliza iwapo kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimetafsiriwa kwa ki-Swahili au wameniomba nikitafsiri. Hao ni watu ambao wameishi au wanaishi Afrika Mashariki, hasa kwa shughuli za kujitolea.

Tangu nilipoanza kupata maulizo au maombi hayo, nimekuwa na wazo la kukitafsiri kitabu hiki. Mwanzoni kabisa, kwa kuzingatia uwingi wa wa-Somali walioingia na wanaendelea kuingia hapa Minnesota, ambao nimekuwa nikiwasaidia katika kuufahamu utamaduni wa Marekani, niliwazia kumwomba mmoja wa marafiki zangu wa ki-Somali atafsiri kitabu hiki kwa ki-Somali. Ninao marafiki kadhaa wa ki-Somali ambao, sawa na wa-Afrika wengine, wamekisoma na wanakipenda kitabu hiki. Lakini bado sijalitekeleza wazo hilo.

Jana nimepata ujumbe wa aina hiyo kutoka kwa mama mmoja m-Marekani, ambaye simfahamu. Ninanukuu sehemu ya ujumbe wake, na nimeweka nukta nne mahali ambapo kuna maneno ambayo sijayanukuu:

....I hope one day that you will translate your wonderful book. It is such a wealth of knowledge for me, and I know my Tanzanian friends would feel the same. Of course most good people would never mean to hurt or offend a new acquaintance, but sometimes when we are lucky enough to make a friend from a different country, we can use a little guidance on how to be respectful of each others cultural differences. Your book has given me that gift, and so I thank you for that!....Last year I went to Africa for the wildlife, but I found it was the Tanzanian people who stole my heart. This year I will return and visit Eli's village and meet his family. I am so excited about my visit. That is why it is so important to me to do my best to not be the classic "UGLY AMERICAN". Thank you again for your response. I hope you will consider writing the Kiswahili version of your book in the future. I know there would be many people who would find it both helpful and fascinating, as I did....

Natafsiri ujumbe huu ifuatavyo:

....Natumaini siku moja utakitafsiri kitabu chako murua. Ni hazina kubwa ya maarifa kwangu, na ninajua kuwa marafiki zangu wa-Tanzania watakiri hivyo. Ni wazi kuwa watu wengi wenye roho nzuri hawanuii kumuumiza au kumkosea mtu pindi wanapofahamiana, lakini mara nyingine tunapobahatika kumpata rafiki kutoka nchi nyingine tunaweza kunufaika na mwongozo wa namna ya kuheshimiana kutokana na tofauti za tamaduni zetu. Kitabu chako kimekuwa tunu ya aina hiyo, na nakushuru kwa hilo....Mwaka jana nilikwenda Afrika kuwaona wanyama mbugani, lakini waliouteka moyo wangu ni wa-Tanzania. Mwaka huu nitaenda tena kijijini kwa Eli na kukutana na familia yake. Ninafurahi sana ninavyoingojea safari hiyo. Ndio maana ni muhimu sana kwangu kujitahidi kwa namna yoyote kutokuwa yule anayefahamika kama "M-MAREKANI WA OVYO." Narudia kukushukuru kwa jawabu lako. Ninatumaini utalichukulia maanani suala la kuandika toleo la ki-Swahili la kitabu chako siku zijazo. Ninajua kitabu hiki kitawasaidia na kuwasisimua wengi kama ilivyokuwa kwangu....

Kwa wale ambao hawafahamu, hii dhana ya "Ugly American" imejengeka sana katika mawazo ya wa-Marekani wanaoamini kuwa tabia ya wa-Marekani wanapokuwa nje za kigeni si nzuri. Dhana hiyo ilishamiri baada ya kuchapishwa kwa kitabu cha Eugene Burdick na William J. Lederer kiitwacho The Ugly American.

Sina la nyongeza la kusema kwa leo, bali kujiuliza: mimi ni nani niyapuuze maombi ya watu? Ninapaswa kuchukua hatua stahiki, nikizingatia ule usemi maarufu wa ki-Latini: "Vox Dei vox populi," yaani sauti ya umma ni sauti ya Mungu.

Saturday, April 4, 2015

Nimerejea Salama Kutoka Leech Lake Tribal College

Nilirejea jana jioni kutoka Leech Lake Tribal College, kwenye mkutano kuhusu "Narratives of Identity." Nilikuwa mmoja wa wanajopo wanne waliotoa mada, na mada yangu ilikuwa "Being African in America."

Niliongelea uzoefu wangu katika miaka mingi ya kuishi na kufundisha hapa Marekani, nikielezea kazi kubwa isiyoisha ya kujitambulisha kama mu-Afrika, ambaye ni tofauti na mu-Amerika Mweusi. Nilielezea jinsi suala hilo linavyosabisha mikanganyiko na kutoelewana baina ya wa-Marekani Weusi na wa-Afrika tuishio Marekani.

Nilisema wazi kuwa namna wanavyojiita na kujitambulisha wa-Marekani Weusi ni tofauti na namna tunavyojiita na kujitambulisha sisi wa-Afrika. Nilimnukuu Chimamanda Ngozi Adichie wa Nigeria ambaye katika mahojiano na katika riwaya yake maarufu ya Americanah, ameelezea vizuri suala hilo.

Nilimnukuu pia mwandishi Jamaica Kincaid wa Antigua, pande za Caribbean, ambaye pamoja na kuwa ni mweusi pia, hakuwahi kujiita kama wanavyojiita  wa-Marekani Weusi. Hayo mawazo yake niliyasoma katika mahojiano yaliyochapishwa mwaka 1991 katika jarida la Mississippi Review.

Nilisisitiza umuhimu wa kuheshimu haki ya kila jamii kujiita au kujitambulisha kwa majina wanayoyataka au yanayowaridhisha wenyewe. Watu wengine sherti wafuate njia hiyo badala ya kuwapachika watu majina ya utambulisho kama walivyofanya wakoloni.

Nilienda mbali zaidi na kuelezea suala la haki ya kila jamii kujieleza wenyewe, sio kuzimishwa kama walivyotuzimisha wakoloni, na wao wakawa wanaandika juu yetu.

Siwezi kuelezea hapa yote niliyosema. Nawazia kuendelea kutafakari suala hilo na kujisomea zaidi, na kuwasoma upya watu kama Frantz Fanon, Aime Cesaire, na Ngugi wa Thiong'o, ili hatimaye niandike makala kamili.

Hiyo jana, wakati nilipokuwa najitambulisha mkutanoni, nilisema kuwa nimeleta vitabu vyangu viwili kama zawadi kwa maktaba ya chuo cha Leech Lake Tribal College. Vitabu hivyo ni Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Matengo Folktales. Vitabu hivi vilipokelewa kwa furaha na shukrani tele.

Nina hakika kuwa mkutano ule umesisimua watu. Jana hiyo hiyo, katika ukurasa wa Facebook wa Leech Lake Tribal College iliandikwa taarifa hii:

We had some great speakers on campus today for the Narratives of Identity presentations. One of the many memorable remarks from today's visit was by Joseph Mbele, St Olaf College- “I am not a person of color. I am Tanzanian which is a concept of colonization. Only when I came to America was I referred to as black. Naming yourself, knowing yourself, is a right…Construction of identities are not fixed and it’s our right to identify ourselves.”

(Picha ya juu kabisa na ya katikati ni kutoka Leech Lake Tribal College)

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...