Showing posts with label Chimamanda Ngozi Adichie. Show all posts
Showing posts with label Chimamanda Ngozi Adichie. Show all posts

Saturday, April 4, 2015

Nimerejea Salama Kutoka Leech Lake Tribal College

Nilirejea jana jioni kutoka Leech Lake Tribal College, kwenye mkutano kuhusu "Narratives of Identity." Nilikuwa mmoja wa wanajopo wanne waliotoa mada, na mada yangu ilikuwa "Being African in America."

Niliongelea uzoefu wangu katika miaka mingi ya kuishi na kufundisha hapa Marekani, nikielezea kazi kubwa isiyoisha ya kujitambulisha kama mu-Afrika, ambaye ni tofauti na mu-Amerika Mweusi. Nilielezea jinsi suala hilo linavyosabisha mikanganyiko na kutoelewana baina ya wa-Marekani Weusi na wa-Afrika tuishio Marekani.

Nilisema wazi kuwa namna wanavyojiita na kujitambulisha wa-Marekani Weusi ni tofauti na namna tunavyojiita na kujitambulisha sisi wa-Afrika. Nilimnukuu Chimamanda Ngozi Adichie wa Nigeria ambaye katika mahojiano na katika riwaya yake maarufu ya Americanah, ameelezea vizuri suala hilo.

Nilimnukuu pia mwandishi Jamaica Kincaid wa Antigua, pande za Caribbean, ambaye pamoja na kuwa ni mweusi pia, hakuwahi kujiita kama wanavyojiita  wa-Marekani Weusi. Hayo mawazo yake niliyasoma katika mahojiano yaliyochapishwa mwaka 1991 katika jarida la Mississippi Review.

Nilisisitiza umuhimu wa kuheshimu haki ya kila jamii kujiita au kujitambulisha kwa majina wanayoyataka au yanayowaridhisha wenyewe. Watu wengine sherti wafuate njia hiyo badala ya kuwapachika watu majina ya utambulisho kama walivyofanya wakoloni.

Nilienda mbali zaidi na kuelezea suala la haki ya kila jamii kujieleza wenyewe, sio kuzimishwa kama walivyotuzimisha wakoloni, na wao wakawa wanaandika juu yetu.

Siwezi kuelezea hapa yote niliyosema. Nawazia kuendelea kutafakari suala hilo na kujisomea zaidi, na kuwasoma upya watu kama Frantz Fanon, Aime Cesaire, na Ngugi wa Thiong'o, ili hatimaye niandike makala kamili.

Hiyo jana, wakati nilipokuwa najitambulisha mkutanoni, nilisema kuwa nimeleta vitabu vyangu viwili kama zawadi kwa maktaba ya chuo cha Leech Lake Tribal College. Vitabu hivyo ni Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Matengo Folktales. Vitabu hivi vilipokelewa kwa furaha na shukrani tele.

Nina hakika kuwa mkutano ule umesisimua watu. Jana hiyo hiyo, katika ukurasa wa Facebook wa Leech Lake Tribal College iliandikwa taarifa hii:

We had some great speakers on campus today for the Narratives of Identity presentations. One of the many memorable remarks from today's visit was by Joseph Mbele, St Olaf College- “I am not a person of color. I am Tanzanian which is a concept of colonization. Only when I came to America was I referred to as black. Naming yourself, knowing yourself, is a right…Construction of identities are not fixed and it’s our right to identify ourselves.”

(Picha ya juu kabisa na ya katikati ni kutoka Leech Lake Tribal College)

Thursday, July 18, 2013

Kiu ya Kusoma Vitabu

Daima nina kiu ya kusoma vitabu.  Sio rahisi unikute sina kitabu. Hii sio tu kwa vile mimi ni mwalimu. Ni tabia ambayo nilijengeka nayo tangu nikiwa kijana mdogo.

Kuwa mwalimu kumenipa motisha zaidi ya kusoma sana vitabu. Wakati huu ninapoandika, wanafunzi wangu na mimi tumemaliza kusoma Half of a Yellow Sun kilichoandikwa na Chimamanda Ngozi Adichie. Sote tumekifurahia sana. Lakini, mwandishi huyu amechapisha hivi karibuni na kitabu kingine kiitwacho Americanah, ambacho tayari kinazungumziwa sana miongoni mwa wapenda vitabu. Kwa hivi, nami najipanga kujipatia kitabu hiki, nikisome.

Kitabu kingine ambacho tumekimaliza katika darasa tofauti siku chache zilizopita ni Midnight's Children cha Salman Rushdie.  Kitabu hiki ni kama chemsha bongo, kwa jinsi kilivyotumia mbinu mbali mbali za kuelezea maisha ya mhusika mkuu Saleem Sinai. Maisha hayo yamefungamana na historia ya India, tangu dakika ile India ilipopata uhuru, usiku wa manane, mwaka 1947. Rushdie amechanganya matukio ya historia na ubunifu wake wa ajabu katika kitabu hiki.

Midnight's Children ni kitabu kinachokutegemea msomaji uwe na ufahamu fulani wa mila, desturi na dini za India, hasa u-Hindu, u-Islam, u-Kristu, na u-Parsi. Uwe na ufahamu fulani wa historia ya India hasa katika karne ya ishirini, inayojumlisha viongozi maarufu kama Mahatma Gandhi, Jawaharlal Nehru, Muhammad Ali Jinnah, na Indira Gandhi. Ujue mazingira yaliysababisha kuzaliwa kwa nchi mbili za India na Pakistan, na mgogoro wa Kashmir, ambao bado unaendelea. Kwa bahati nzuri, katika miaka niliyofundisha hapa chuoni St. Olaf, nimefundisha sana fasihi ya India na hayo yote niliyoyataja.

Tulipofikia ukurasa wa mwisho wa kitabu hiki, tulijisikia kama washindi wa mashindano magumu. Kwa upande wangu, baada ya kupambana na Midnight's Children hadi mwisho, nimejawa na hamasa ya kusoma kitabu kingine cha Rushdie Satanic Verses, ambacho nilikinunua zamani, nikajaribu kukisoma, bila kufika mbali. Ninahisi kuwa kwa kusoma Midnight's Children nimejiandaa vilivyo kukabiliana na Satanic Verses. Au labda nianzie na kitabu chake kiitwacho The Enchantress of Florence, ambacho nimekuwa nacho kwa miaka kadhaa, bila kukisoma.

Ni jambo jema kujaribu kusoma maandishi mbali mbali ya mwandishi yeyote, sio kitabu kimoja tu. Kwa mfano, kwa upande wa Tanzania, utawakuta watu wakitaja kitabu cha Hamza Njozi kuhusu mauaji ya Mwembechai lakini hawajui kuwa mwandishi huyu amechapisha vitabu vingine pia, na makala nyingi, kuhusu u-Islam na fasihi.

Vile vile, wengi wakisikia jina la Salman Rushdie, wanalihusisha na kitabu cha Satanic Verses tu. Huu nao ni uzembe, kwani mwandishi huyu amechapisha vitabu vingi, kuanzia riwaya hadi insha kuhusu masuala mbali mbali ya sanaa, siasa na utamaduni. Kumtendea haki Rushdie ni lazima tusome maandishi yake mbali mbali.

Akili zetu zinapaswa ziwe na duku duku isiyoisha ya kujua mambo. Njia moja kuu ya kujaribu kukidhi kiu hii ni kusoma sana vitabu. Hapo utaona kwamba, tofauti na imani ya jamii yetu ya Tanzania, wajibu wa kusoma vitabu ni wa watu wote, sio wanafunzi tu.

Thursday, July 4, 2013

Tumemaliza Kusoma "Half of a Yellow Sun"

Kwa wiki hizi sita, katika kipindi hiki cha "summer," nimekuwa nikifundisha kozi juu ya fasihi ya Afrika. Jana tumemaliza kusoma Half of a Yellow Sun, riwaya ya Chimamanda Ngozi Adichie wa Nigeria.  Huyu ni mwandishi chipukizi, lakini tayari ameshajipatia umaarufu sana na nyota yake inazidi kung'ara.

Amechapisha vitabu kadhaa akianzia na Purple Hibiscus na The Thing Around Your Neck. Ninavyo vitabu hivyo, na nimeshawahi kufundisha Purple Hibiscus.  Hivi karibuni, amechapisha Americanah, kitabu ambacho kinaongelewa sana miongoni mwa wasomaji, walimu, na wahakiki.

Kilipochapishwa kitabu cha Half of a Yellow Sun, nilisoma taarifa zake. Taarifa hizi zilielezea kuwa kitabu hiki kinahusu vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini Nigeria, ambapo sehemu ya kusini mashariki ilijitenga na kutangaza kuwa imekuwa taifa huru la Biafra.

Mwaka 2008 Chimamanda Ngozi Adichie alikuwa mmoja wa waandishi walioalikwa kuhudhuria tamasha la vitabu Minneapolis. Alikuja kuzindua kitabu cha Half of a Yellow Sun. Nilihudhuria, nikasikiliza hotuba yake, kisha nikajumuika na umati wa watu waliokuwa wananunua nakala na kusainiwa na mwandishi. Nilipata pia fursa ya kupiga naye picha inayoonekana hapa kushoto.

Pamoja na kuwa nilinunua nakala ya Half of a Yellow Sun siku hiyo, sikupata fursa ya kukisoma. Lakini miaka yote hii nilikuwa na nia ya kufanya hivyo, na nimefanya hivyo katika kufundisha somo la fasihi ya Afrika.

Wote tumependezwa sana na Half of a Yellow Sun. Chimamanda Ngozi Adichie ana kipaji kikubwa sana cha kubuni na kusimulia hadithi. Yeyote anayesoma maandishi yake na anakijua ki-Ingereza vizuri, atakiri kuwa mwandishi huyu anaimudu vizuri sana lugha hiyo. Ni kweli kuwa kwa ujumla Half of a Yellow Sun inahusu vita ya Biafra, 1966-1970, lakini kwanza inaongelea maisha ya kila siku ya watu, hasa katika mazingira ya Chuo Kikuu cha Nsukka. Chimamanda alizaliwa na kukulia hapo, na katika maandishi yake hupenda kuongelea maisha ya wasomi na familia zao chuoni pale.

Hata katika mazingira ya vita, Half of a Yellow Sun inatuonyesha watu wakijitahidi kuendelea na shughuli zao za kawaida, kama vile kuelimisha watoto, hata kama ni chini ya mti. Tunawaona watu wakitafuta riziki za maisha. Na tunawaona watoto wakicheza michezo, pamoja na dhiki kubwa ya magonjwa na njaa. Pamoja na ukatili mkubwa uliojitokeza katika vita ya Biafra, Chimamanda Ngozi Adichie amejiepusha na kishawishi cha kuangalia suala zima kama suala la aina mbili tu ya watu, yaani wabaya na wema. Anaonyesha jinsi binadamu tulivyo na uwezo wa kuwa wabaya, sawa na wale ambao tunawaona ndio wabaya.

Half of a Yellow Sun imefuata vizuri mtiririko wa matukio yaliyotangulia vita na matukio ya vita yenyewe. Kwangu mimi kama m-Tanzania, nimeguswa na jinsi Chimamanda Ngozi Adichie alivyoelezea mchango wa Tanzania katika kuiunga mkono Biafra. Ameelezea furaha ya watu wa Biafra na heshima waliyokuwa nayo kwa Tanzania na Mwalimu Nyerere. Wakati nasoma kitabu hiki na suala hili la Tanzania, nilikumbuka kitabu kipya cha Chinua Achebe kiitwacho There Was a Country. Humo Achebe ameelezea vizuri sana jinsi msimamo wa Tanzania ulivyoshangiliwa na watu wa Biafra. Jina la Tanzania lilikuwa linatajwa kila mahali. Miziki ya Tanzania ilipigwa kila mahali. Katika Half of a Yellow Sun, kuna baa ambayo ilibadilishwa jina ikaitwa Tanzania Bar.

Kwa wasiofahamu napenda kusema kuwa sehemu iliyoitwa Biafra ni sehemu wanayoishi zaidi watu wa kabila la Igbo. Kutokana na siasa za Nigeria, ambamo ukabila una nafasi kubwa sana, dhuluma dhidi ya waIgbo, ikiwemo wengi kuuawa, hasa sehemu za kaskazini mwa Nigeria, ndio kitu kilichosababisha wakakimbilia kwao na kujitangaza kuwa ni taifa huru la Biafra. Chinua Achebe, ambaye alifariki hivi karibuni, na Chimamanda Ngozi Adichie ni wa kabila hilo.

Kwa kumalizia, bora niseme tu kwamba kuliko kusimuliwa, ni bora mtu ujipatie nakala ujisomee. Nasema hivyo nikijua fika kwamba ushauri huu hauna maana kwa jamii ya wa-Tanzania, kwani utamaduni wa kununua vitabu na kuvisoma haupo. Kuna uwezekano mkubwa kwamba ushauri wangu utazingatiwa na watu wa nchi zingine kama vile Kenya, ambayo ni makini kwa masuala ya aina hiyo.

Friday, December 17, 2010

Nimenunua Kitabu Kipya cha Chimamanda Ngozi Adichie

Leo nimenunua, The Thing Around Your Neck, kitabu kipya cha Chimamanda Ngozi Adichie. Huyu dada ni mwandishi wa ki-Nigeria, mwenye kipaji sana cha kuandika riwaya na hadithi fupi. Pia ana mawazo ya kusisimua na kufikirisha kuhusu simulizi. Umaarufu wake unakua kwa kasi. Amepata tuzo mbali mbali, ikiwemo ya Taasisi ya MacArthur

Riwaya yake ya kwanza, Purple Hibiscus, niliifundisha hapa chuoni St. Olaf. Inavutia sana kwa dhamira, maudhui, na matumizi ya lugha. Inaongelea maisha ya familia ya profesa wa chuo kikuu cha Nsukka, Nigeria, kwa namna ya kukufanya msomaji ujisikie uko sehemu hiyo. Matukio na migogoro baina ya wahusika imeelezwa kwa uhalisi wa kuvutia.

Mwaka 2006 nilipata bahati ya kumwona Chimamanda Ngozi Adichie, alipofika mjini Minneapolis kwenye tamasha la vitabu. Alikuja kuzindua kitabu chake cha pili, Half of a Yellow Sun. Nilinunua nakala, ambayo aliisaini, na tulipata muda wa kuzungumza kiasi, hata akaniambia kuhusu anavyoendesha blogu. Tulipiga picha inayoonekana hapa chini.
Bado sijapata muda wa kusoma Half of a Yellow Sun, ila ninayo hapa ofisini muda wote, na auala la kuisoma limo kwenye orodha yangu ya mambo muhimu ya kufanya.

The Thing Around Your Neck ni mkusanyo wa hadithi fupi. Nimeanza kusoma hadithi ya kwanza, ambayo inakumbusha Purple Hibiscus, kwa vile wahusika ni familia ya profesa katika chuo kikuu cha Nsukka. Lakini kwa kuangalia haraka haraka, nimeona kuwa kitabu hiki kina hadithi zinazohusu Nigeria na pia Marekani. Kwa maneno mengine, wahusika wa ki-Nigeria wako Nigeria na pia Marekani.

Hii imenikumbusha kitabu kingine cha hadithi kiitwacho Tropical Fish: Tales from Entebbe. Mwandishi ni Doreen Baingana wa Uganda, dada ambaye naye ana kipaji sana. Baadhi ya hadithi zilizomo katika kitabu hiki zinahusu matokeo yanayotokea Uganda na zingine zinahusu maisha ya wa-Ganda wakiwa Marekani.

Mpangilio huu wa hadithi za Adichie na Baingana unaendana na ukweli kwamba waandishi wote wawili wana uzoefu wa kuishi nchini kwao na pia Marekani. Ni katika kizazi kipya cha waandishi ambao wanailetea sifa sana Afrika.

Nina hamu ya kusoma The Thing Around Your Neck. Nina mategemeo ya kuandika makala katika blogu hii.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...