Friday, December 17, 2010

Nimenunua Kitabu Kipya cha Chimamanda Ngozi Adichie

Leo nimenunua, The Thing Around Your Neck, kitabu kipya cha Chimamanda Ngozi Adichie. Huyu dada ni mwandishi wa ki-Nigeria, mwenye kipaji sana cha kuandika riwaya na hadithi fupi. Pia ana mawazo ya kusisimua na kufikirisha kuhusu simulizi. Umaarufu wake unakua kwa kasi. Amepata tuzo mbali mbali, ikiwemo ya Taasisi ya MacArthur

Riwaya yake ya kwanza, Purple Hibiscus, niliifundisha hapa chuoni St. Olaf. Inavutia sana kwa dhamira, maudhui, na matumizi ya lugha. Inaongelea maisha ya familia ya profesa wa chuo kikuu cha Nsukka, Nigeria, kwa namna ya kukufanya msomaji ujisikie uko sehemu hiyo. Matukio na migogoro baina ya wahusika imeelezwa kwa uhalisi wa kuvutia.

Mwaka 2006 nilipata bahati ya kumwona Chimamanda Ngozi Adichie, alipofika mjini Minneapolis kwenye tamasha la vitabu. Alikuja kuzindua kitabu chake cha pili, Half of a Yellow Sun. Nilinunua nakala, ambayo aliisaini, na tulipata muda wa kuzungumza kiasi, hata akaniambia kuhusu anavyoendesha blogu. Tulipiga picha inayoonekana hapa chini.
Bado sijapata muda wa kusoma Half of a Yellow Sun, ila ninayo hapa ofisini muda wote, na auala la kuisoma limo kwenye orodha yangu ya mambo muhimu ya kufanya.

The Thing Around Your Neck ni mkusanyo wa hadithi fupi. Nimeanza kusoma hadithi ya kwanza, ambayo inakumbusha Purple Hibiscus, kwa vile wahusika ni familia ya profesa katika chuo kikuu cha Nsukka. Lakini kwa kuangalia haraka haraka, nimeona kuwa kitabu hiki kina hadithi zinazohusu Nigeria na pia Marekani. Kwa maneno mengine, wahusika wa ki-Nigeria wako Nigeria na pia Marekani.

Hii imenikumbusha kitabu kingine cha hadithi kiitwacho Tropical Fish: Tales from Entebbe. Mwandishi ni Doreen Baingana wa Uganda, dada ambaye naye ana kipaji sana. Baadhi ya hadithi zilizomo katika kitabu hiki zinahusu matokeo yanayotokea Uganda na zingine zinahusu maisha ya wa-Ganda wakiwa Marekani.

Mpangilio huu wa hadithi za Adichie na Baingana unaendana na ukweli kwamba waandishi wote wawili wana uzoefu wa kuishi nchini kwao na pia Marekani. Ni katika kizazi kipya cha waandishi ambao wanailetea sifa sana Afrika.

Nina hamu ya kusoma The Thing Around Your Neck. Nina mategemeo ya kuandika makala katika blogu hii.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...