Showing posts with label riwaya. Show all posts
Showing posts with label riwaya. Show all posts

Monday, November 13, 2017

Mwongozo wa Riwaya ya "Things Fall Apart"

Mimi mwalimu wa fasihi ya ki-Ingereza. Kati ya mambo ninayofanya ni kuandika miongozo ya fasihi. Nimeshaandika miongozo kadhaa, ikiwemo mwongozo wa Things Fall Apart, riwaya ya Chinua Achebe.

Nimeridhika kuwa mwongozo huu una mawazo muhimu ya kumwezesha mwalimu, mwanafunzi, na msomaji yeyote kuelewa mambo mapya juu ya Things Fall Apart na pia juu ya nadharia ya fasihi. Leo nimezipitia kurasa kadhaa, nikafurahia niliyoandika juu ya mhusika aitwaye Unoka.

Suali ni je, mwongozo huu unawafikia wanafunzi wa waalimu wa Tanzania? Ni wazi kuwa ningependa wafaidike nao, kama wanavyofaidika wanafunzi na wengine nje ya Tanzania, kama vile hapa Marekani. Ningekuwa na uwezo, ningepeleka nakala katika shule na vyuo vyote.

Kwa bahati nzuri, kitabu kinapatikana mtandaoni kama kitabu pepe. Ninafahamu kuwa kuna watu Tanzania ambao wanaweza kuagiza vitabu vya aina hiyo. Ninaamini kuwa kadiri siku zinavyokwenda na tekinolojia kuenea, wengi zaidi watakuwa na uwezo huo. Kwa hivi, nina matumaini makubwa kwa siku za usoni.

Njia nyingine ni kusafirisha vitabu. Mimi mwenyewe, kila ninapokwenda Tanzania, huchukua vitabu na kuvigawa kwenye maktaba na vyuo. Kuna wa-Tanzania wengi huku nje, ambao nao huenda Tanzania. Kama kungekuwa na nia ya kuchangia elimu, ingekuwa rahisi wao pia kuchukua vitabu. Vitu vingine wanachukua, kwa nini washindwe kuchukua vitabu?

Wednesday, September 6, 2017

Muhula wa Masomo Unaanza

Wiki hii hapa chuoni St. Olaf, tunaanza muhula mpya wa masomo. Nitafundisha madarasa matatu. Mawili ni ya "First Year Writing," na moja ni "Post-colonial Literature." Katika "First Year Writing," tunafundisha uandishi bora wa ki-Ingereza.

Kozi ninayotaka kuongelea hapa  ni "Post-colonial Literature." Niliajiriwa hapa chuoni St. Olaf kuanzisha kozi hiyo, na nilianza kufundisha mwaka 1991. Ni kozi inayohusu fasihi kutoka nchi zilizokuwa katika himaya ya u-Ingereza wakati wa ukoloni ila zilikuja kuwa huru.

Ninapofundisha kozi hii, huwa ninaamua waandishi wepi kutoka nchi zipi nifundishe. Kwa muhula huu, niliamua kufundisha fasihi kutoka Afrika Kusini. Nilichagua waandishi wawili: Alex la Guma na Nadine Gordimer. Wote ni waandishi wa hadithi fupi na riwaya.

Nadhani tangu nilipokuwa mwanafunzi Mkwawa High School, nilisoma hadithi za Alex la Guma katika kitabu cha hadithi fupi kiitwacho Quartet. Baadaye, nilipokuwa mwanafunzi katika idara ya Literature, chuo kikuu cha Dar es Salaam, Alex la Guma alikuja kutoka London akatufundisha kwa siku kadhaa. Alialikwa na mkuu wa idara, mwalimu Grant Kamenju wa Kenya.

Nilifahamu kuwa Alex la Guma alikuja kuwa mwakilishi Uingereza wa chama cha ukombozi cha African National Congress cha Afrika Kusini, (ANC), kisha akawa mwakilishi wa ANC nchini Cuba. Alipofariki, nchini Cuba, nilikuwa ninasoma katika Chuo Kikuu cha Wisconsin Madison.

Nadine Gordimer ni mzungu aliyejihusisha na ANC. Alikuwa mpinzani wa utawala wa makaburu. Baada ya kuja Marekani kufundisha, nimebahatika kumwona Nadine Gordimer kwenye mkutano fulani wa kitaaluma. Sikumbuki ulikuwa ni mwaka gani. Nimefundisha hadithi zake fupi zilizokusanywa katika kitabu Six Feet of the Country, na riwaya zake, The Conservationist, The Pickup, na July's People.

Kufundisha juu ya waandishi hao wawili ni fursa ya kutafakari historia na siasa, hasa ukaburu na harakati za ukombozi katika Afrika Kusini. Yote hayo yamefungamana na fasihi, hasa katika karne ya ishirini, ambayo ndiyo kozi yangu itashughulikia. Tutafakari mitazamo ya waandishi hao wawili kuhusu siasa, mahusiano ya jamii, utamaduni, na itikadi katika Afrika Kusini. Tutaangalia athari za fasihi ya ulimwengu katika maandishi ya waandishi hao wawili na tutatambua mchango wa waandishi hao katika fasihi ya Afrika na ulimwengu.

Friday, September 1, 2017

"Hope:" Shairi la Emily Bronte

Kwa wenye kuifahamu fasihi ya ki-Ingereza, jina la Emily Bronte linafahamika vizuri. Emily na dada zake Charlotte na Anne ni waandishi maarufu wa mashairi na riwaya. Emily anafahamika zaidi kwa riwaya yake, Wuthering Heights, na Charlotte anafahamika kwa riwaya yake, Jane Eyre. Katika kukua kwangu na kusoma fasihi Tanzania, nilikuwa ninawafahamu hao dada wawili, lakini si mdogo wao Anne, ambaye nimekuja kuelewa baadaye kwamba naye alikuwa mwandishi wa mashairi na riwaya. Hao dada watatu, maarufu kama "the Bronte Sisters," ni maarufu katika fasihi ya ki-Ingereza.

Hizo ni kumbukumbu za juu juu kuhusu hao dada watatu. Lakini leo ninaleta shairi moja la Emily, ambalo nimelisoma kwa mara ya kwanza wiki hii. Limenivutia sana kwa jinsi linavyofikirisha kutokana na mbinu zake za kuwasilisha mtazamo juu ya kitu kinachoitwa matumaini. Tofauti na ufahamu wetu wa kitu kiitwacho matumaini, shairi linayaelezea matumaini kama si kitu cha kuaminiwa au kutegemewa. Mshairi anayaelezea matumaini kama si rafiki wa imara wa kuaminiwa, bali ni kitu kisichojali hali yake ngumu, chenye mizengwe, na hatimaye chatoweka na kumwacha kwenye mataa, kama wasemavyo watu mitaani. Ili kulitendea haki shairi hili, bora kila mtu ajisomee na kutafakari.

Hope

Hope was but a timid friend;
She sat without the grated den,
Watching how my fate would tend,
Even as selfish-hearted men.

She was cruel in her fear;
Through the bars, one dreary
day, I looked out to see her there,
And she turned her face away!

Like a false guard, false watch keeping,
Still, in strife, she whispered peace;
She would sing while I was weeping;
If I listened, she would cease.

False she was, and unrelenting;
When my last joys strewed the ground,
Even Sorrow saw, repenting,
Those sad relics scattered round;

Hope, whose whisper would have given
Balm to all my frenzied pain,
Stretched her wings, and soared to heaven,
Went, and ne'er returned again!

Tuesday, July 18, 2017

Mhadhiri wa Algeria Amekifurahia Kitabu

Mimi kama mwandishi, ninaguswa na maoni ya wasomaji. Leo nimepata ujumbe kutoka kwa mhadhiri wa chuo kikuu kimoja cha Algeria, Samir, ambaye tumewasiliana kwa miaka michache, na nilimpelekea nakala ya kijitabu changu, Notes on Achebe's Things Fall Apart.

Nanukuu sehemu ya ujumbe wake:

I hope this finds you safe. I am so pleased to let you know that your book on Achebe's TFA is very helpful!! It really helped me. It is a pleasure also to inform you that I am citing you in my phd thesis on Gender in Ngugi's fiction. Your name will also be cited in my Acknowledgements and Dedications. Thank you so much....We love you much.

Kwa wale wasiojua ki-Ingereza, napenda kuelezea anachosema mhadhiri huyu kwa ujumla. Anasema kuwa anategemea ujumbe wake utanifikia nikiwa salama. Amefurahi sana kunifahamisha kuwa kitabu changu kuhusu riwaya ya Achebe ya Things Fall Apart ni mchango mkubwa sana na kimemsaidia sana. Anafurahi kunifahamisha vile vile kuwa ananukuu kitabu changu katika tasnifu yake ya uzamifu kuhusu jinsia katika riwaya za Ngugi wa Thiong'o. Jina langu litatajwa katika orodha ya watu waliochangia tasnifu hii. Anahitimisha kwa kusema, "Asante sana....Tunakupenda sana."

Ujumbe wowote kutoka kwa wasomaji makini una manufaa kwangu kama mwandishi. Ninayachukulia maanani maoni yao, hasa nikijua kuwa wametumia hela zao kununua kitabu changu. Kuna wengine ambao ninakuwa nimewapa nakala ya bure. Hao wanaponiandikia maoni yao juu ya kitabu ninaona kama wamelipa fadhila. Maoni yao ni muhimu kwangu kuliko hela.

Kitabu hiki na vingine vinapatikana hapa

Tuesday, May 30, 2017

Likizo Inaanza: Ni Kujisomea Vitabu na Kuandika

Tumemaliza muhula wa mwisho wa mwaka wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Tunamalizia kusahihisha mitihani na matokeo yatakuwa yamekamilika tarehe 5 Juni. Kuanzia pale tutakuwa na miezi mitatu ya likizo. Lakini kwetu waalimu, likizo si likizo, bali fursa ya kujisomea, kufanya utafiti, na kuandika, bila kuhusika na ufundishaji darasani.

Mpango wangu kwa likizo hii ni kutumia wiki sita za mwanzo katika kujisomea vitabu na kuandika, halafu wiki sita zitakazofuata nitafundisha kozi ya fasihi ya Afrika. Kufundisha kipindi hiki cha likizo ni jambo la hiari. Mwalimu anatangaza kozi anayotaka kufundisha na wanafunzi wanaohitaji wanajisajili. Wanafunzi huwa wachache. Ni fursa nzuri kwa mwalimu kujaribisha mambo mapya.

Wakati huu ninavyoandika ujumbe huu, ninafadhaika katika kuamua nisome vitabu vipi. Maktaba yangu ina vitabu vingi ambavyo sijavisoma. Kwa likizo hii, nimewazia nisome tamthilia za William Shakespeare, au George Bernard Shaw, au Sean O'Casey, au Anton Chekhov, au riwaya za Orhan Pamuk ili niweze kupata mwanga juu ya huyu mwandishi maarufu aliyejipatia tuzo ya Nobel mwaka 2006 na ambaye nimekuwa nikimtaja katika blogu hii. Nimewazia pia kusoma hadithi fupi na riwaya za Ernest Hemingway, zile ambazo sijazisoma.

Ningependa kuonja uandishi wa Svetlana Alexievich, ambaye nimemgundua wiki iliyopita. Nilijipatia kitabu chake, Secondhand Time: The Last of the Soviets, cha bure, hapa chuoni. Sikuwa ninamfahamu mwandishi huyu mwanamke m-Rusi, ambaye alipata tuzo ya Nobel mwaka 2015, "for her polyphonic writings, a monument to suffering and courage in our time," kwa mujibu wa kamati ya tuzo.

Wafuatiliaji wa nadharia ya fasihi wanafahamu kuwa dhana ya "polyphony" katika fasihi ilifafanuliwa vizuri na mwanafalsafa na mhakiki m-Rusi Mikhail Bakhtin akimaanisha sauti na mitazamo mbali mbali inayounda kazi ya fasihi. Nimefurahi kumfahamu mwandishi huyu mwanamke kutoka u-Rusi. Amenifanya nimkumbuke mwandishi mwanamke m-Rusi, Anna Akhmatova, mshairi maarufu. Nina dukuduku ya kujua kama waandishi hao wawili wanaweza kulinganishwa.

Hakuna kazi ya fasihi inayozuka katika ombwe. Inatokana na jadi fulani na mfumo mpana wa kazi za fasihi, na kazi yoyote mpya inachangia jadi na mfumo wa fasihi. Dhana hiyo ilielezwa vizuri na T.S. Eliot, mshairi na mwanafasihi maarufu, katika insha yake, "Tradition and the Individual Talent."

Ninapowazia waandishi wa fasihi wanawake waliopata tuzo ya Nobel, majina yanayonijia akilini hima ni Sigrid Undset wa Norway, Nadine Gordimer wa Afrika Kusini, Toni Morrison wa Marekani, Alice Munro wa Canada, na Doris Lessing wa Zimbabwe na Uingereza. Ninashawishika na wazo la kutunga na kufundisha kozi juu ya maandishi ya wanawake waliopata tuzo ya Nobel katika fasihi.

Papo hapo, katika likizo hii ninataka kuendelea kuandika makala ambayo nilianza kuiandika miezi kadhaa iliyopita, "Folkloric Discourse in Ama Ata Aidoo's The Dilemma of a Ghost." Azma ya kuendelea kuandika makala hii ni kubwa, kwani ninaamini kuwa hii itakuwa makala bora kabisa.

Hizi ndizo ndoto zangu. Ni ajenda kubwa, kielelezo cha namna akili yangu inavyohangaika kutokana na kutambua kuwa vitu vy kusoma na kuandika ni vingi kuliko muda unavyoruhusu. Sitaweza kufanya yote ninayowazia kwa likizo hii, lakini si neno. Nitatumia muda wangu vizuri na kufanya nitakachoweza.

Thursday, May 18, 2017

Vitabu Nilivyonunua Jana

Jana nilinunua vitabu vitatu katika duka la vitabu la chuoni St. Olaf. Viwili, Two Years Eight Months and Twenty-Eight Nights cha Salman Rushdie na A Strangeness in my Mind cha Orhan Pamuk, niliviona juzi. Cha tatu, Why Homer Matters, kilichotungwa na Adam Nicolson, nilikiona hiyo hiyo jana.

Nilipoingia dukani, nilikumbuka makala niliyoisoma juzi usiku, kuhusu vitabu halisi na vitabu pepe. Makala hii, sawa na nyingine nyingi, inatafakari iwapo vitabu vya jadi vitasalimika katika himaya hii ya vitabu pepe. Lakini inahitimisha kuwa hakuna ushahidi kuwa vitabu vya jadi vitapoteza mvuto au kufifia.

Mimi ni mmoja wa wale ambao hatujabadilika. Bado tumezoea vitabu halisi, yaani vitabu vya jadi, na ndio maana sisiti kuvinunua, wala sisiti kuelezea tabia yangu hiyo. Hapa nitaelezea kifupi kwa nini nimenunua vitabu hivi vitatu.

Kitabu cha Salman Rushdie kilinivutia kwa sababu ya umaarufu wa mwandishi huyu. Bila shaka wengi watakumbuka kitabu chake, Satanic Verses, ambacho kilipigwa marufuku katika nchi nyingi kwa madai kuwa kinaukashifu u-Islam. Ayatollah Khomeini wa Iran alitangaza fatwa kuwa Salman Rushdie anapaswa kuuawa.

Duniani kote, na hata miongoni mwa wa-Islam wenyewe hukumu hii ilizua mjadala. Baadhi walisema kuwa fatwa haikupaswa kutolewa kabla ya Salman Rushdie kupewa fursa ya kujieleza na kukiri kosa lake. Watu wengine walisema kuwa zogo hili lilimpa Salman Rushdie umaarufu ambao hakustahili kwa kigezo cha ubora wa uandishi wake.

Ninavyo baadhi vitabu vya Salman Rushdie, kikiwemo hiki cha Satanic Verses. Nimemewahi kufundisha riwaya yake maarufu, Midnight's Children. Ninavutiwa na ubunifu wake katika kuelezea mambo, na uhodari wake wa kutumia lugha. Uandishi wake unasisimua na kufikirisha.

Orhan Pamuk ni mwandishi ambaye nimewahi kumtaja katika blogu hii. Nina vitabu vyake kadhaa, na nimekuwa na hamu ya kuvisoma, ila bado sijapata wasaa. Huyu amenivutia si tu kwa kuwa alipata tuzo ya Nobel, bali pia kwa sababu ninafahamu kiasi fulani kuhusu fasihi simulizi ya Uturuki, kama vile hadithi za Nasreddin Hodja na Dede Korkut.

Why Homer Matters nimekipenda kwa kuwa taaluma ya tendi nimeipenda na kuishughulikia kwa miaka mingi. Homer, ingawa taarifa zake hazijulikani vizuri, ndiye anayehusishwa na tendi maarufu za u-Griki ya kale, The Iliad na The Odyssey. Kwa kuangalia juu juu, niliona kuwa mwandishi wa Why Homer Matters ana uwezo mkubwa wa kuelezea masuala ya Homer na hizi tendi.

Sunday, May 14, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo nilikwenda tena Apple Valley, kwa muda mfupi, nikaingia katika duka la Half Price Books. Niliangalia kwanza sehemu vinapowekwa vitabu vya Hemingway au juu ya Hemingway. Kitabu cha pekee nilichokiona, ambacho nimekifahamu kwa miezi kadhaa ila sijakinunua, ni Hemingway's Boat: Everything He Loved in Life, And Lost, kilichotungwa na Paul Hendrickson.

Nilielekea sehemu ambapo huwekwa vitabu vya bei rahisi kabisa. Kwa kuwa sikuwa na muda mwingi, niliangalia haraka haraka, nikaona kitabu cha Matigari cha Ngugi wa Thiong'o, kilichotafsiriwa kwa ki-Ingereza na Wangui wa Goro. Ngugi alikuwa amekiandika kwa Kikuyu. Nilivutiwa kuona kuwa ni nakala ya jalada gumu, iliyochapishwa na Africa World Press. Nilichukua. Wasomaji wa Ngugi wanakumbuka kuwa tafsiri hii ilichapishwa kwanza na Heinemann.

Kisha, sehemu hiyo hiyo, katika kuchungulia chungulia, niliona kitabu Contagious Success: Spreading High Performance Throughout Your Organization, kilichoandikwa na Susan Lucia Annunzio. Nilivyoona kuwa kinahusu mbinu za kusambaza ufanisi katika makampuni na mashirika nilikichukua hima. Dhana ya maambukizi ya mafanikio ilinivutia.

Ninapenda kusoma vitabu vinavyohusu ujasiriamali na biashara, kwa sababu mimi mwenyewe ninajiona kama mjasiriamali jamii ("social enterpreneur"). Vile vile, ninavipenda vitabu hivi vinahusu masuala yenye uhusiano na taaluma ambazo nimezizoea, hasa saikolojia.

Sunday, April 2, 2017

Mhadhara Chuo Kikuu cha Minnesota Juu ya Kitereza

Juzi tarehe 31, Dr. Charlotte (Shoonie) Hartwig na mimi tulitoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Minnesota, juu ya mwandishi Aniceti Kitereza. Huyu ni mwandishi muhimu ambaye, hata hivyo, hafahamiki sana. Mama Shoonie amekuwa akiandika kitabu ambacho nami nimechangia, na mhadhara wetu ulihusu kitabu hiki ambacho tunategemea kukichapisha.

Kitereza alizaliwa mwaka 1896 katika kisiwa cha Ukerewe kilichomo katika Ziwa Victoria, upande wa Tanzania. Alisomea katika shule za wamisheni, na alipomaliza aliajiriwa kazi kadhaa. Alivyozidi kukua alipata dhamira ya kuhifadhi mila na desturi za zamani za wa-Kerewe, ili zisipotee. Kama sehemu ya juhudi hiyo aliandika riwaya katika lugha ya ki-Kerewe, ambao aliukamilisha mwanzoni mwa mwaka 1945. Andiko hili ni hazina ya mila na destruí za wa-Kerewe wa zamani, ila Kitereza aliandika kwa mtindo wa hadithi ya kubuni, ili wasomaji wasichoke kusoma.

Baada ya juhudi na mahangaiko ya miaka mingi ya kutafuta mchapishaji, na kufuatia ushauri wa marafiki zake wa-Marekani, Kitereza aliutafsiri mswada wake kwa ki-Swahili. Hata hivyo, aliendelea kungoja kwa miaka mingi hadi mwaka 1980 ambapo mswada ulichapishwa kama kitabu, Bwana Myombekere na Bibi Bugonoka na Ntulanalwo na Buliwhali.

Mama Shoonie ni mtu pekee aliyesalia mwenye taarifa za ndani za Kitereza, kwani yeye na mumewe, Dr. Gerald Hartwig, walimfahamu vizuri Kitereza baada ya kuonana naye kwa mara ya kwanza mwaka 1968 Ukerewe. Mbali ya kukutana naye mara kwa mara miaka ile ya mwanzo, waliendelea kuandikiana barua hadi miaka ya mwisho wa maisha yake. Kitereza alikuwa hodari wa kuandika barua; ananikumbusha waandishi kama Ernest Hemingway na Shaaban Robert.

Katika mhadhara wa juzi, Mama Shoonie alielezea maisha ya Kitereza na mambo aliyofanya kama mwandishi. Maelezo yake aliyaambatanisha na picha za Kitereza, mke wake, na familia nzima ya Hartwig. Watoto wa familia ya Hartwig walikuwa wadogo sana wakati huo. Mama Shoonie alielezea kuwa Kitereza alikuwa anajituma sana katika shughuli yake ya kuhifadhi mila na destruí za wahenga kwa kusukumwa na suali ambalo alilitunga mwenyewe, "Tunawajibika kuwafundisha nini watoto wetu?"

Ilipokuja zamu yangu, nilielezea kwa ufupi uandishi wa Kitereza kwa mujibu wa mtazamo wangu kama mwana fasihi. Nilisisitiza masuala kadhaa muhimu yanayojitokeza katika taaluma ya fasihi ya Afrika, hasa suala la uandishi katika lugha za ki-Afrika na suala la tafsiri. Niligusia jinsi riwaya ya Bwana Myombekere inavyoweza kutupa mtazamo mpya kuhusu historia ya riwaya ya ki-Afrika, na jinsi inavyoweza kuchambuliwa sambamba na kazi za waandishi kama Daniel O. Fagunwa na Amos Tutuola wa Nigeria, Gakaara wa Wanjau wa Kenya, na Shaaban Robert wa Tanzania. Huu utakuwa ni mtazamo wa fasihi linganishi.

Nimesoma tafsiri ya Kitereza ya riwaya yake. Ki-Swahili chake, ingawa kinatofautiana na ki-Swahili sanifu, kina ladha na mtiririko wa hadithi simulizi za lugha za ki-Bantu kama vile lugha yangu ya ki-Matengo. Kwa msingi huo, ninaipenda tafsiri ya Kitereza. Riwaya yake imetafsiriwa kwa ki-Faransa na ki-Jermani, lakini tafsiri hizo, kwa mujibu wa Profesa Gabriel Ruhumbika, zina walakini. Kauli ya Profesa Ruhumbika ina uzito sana, kwani lugha mama yake ni ki-Kerewe na pia yeye ni mashuhuri katika uwanja wa kutafsiri.

Profesa Ruhumbika mwenyewe ametafsiri kwa ki-Ingereza riwaya ya Kitereza kama ilivyoandikwa ki-Kikerewe, na tafsiri yake imechapishwa kama Mr. Myombekere and His Wife Bugonoka, Their Son Ntulanalwo and Daughter Buliwhali. Katika kuisoma tafsiri hii, nilivutiwa nayo, sawa na nilivyovutiwa na tafsiri ya ki-Swahili ya Kitereza mwenyewe. Ni tafsiri ambayo ninapendekeza isomwe na yeyote. Hivyo hivyo, ninakipendekeza kitabu cha Mama Shoonie kijacho. Ni kitabu chenye taarifa nyingi, zikiwemo barua na picha, ambazo ulimwengu haujaziona. 

Wednesday, March 22, 2017

Kitabu kwa Wasafiri Watokao Nebraska

Leo nimeona taarifa kutoka sinodi ya Nebraska ya Kanisa la Kiluteri la Marekani, kuhusu maandalizi ya safari za kwenda Tanzania. Safari hizo zimefanyika tangu miaka iliyopita. Kuna sehemu iitwayo "Preparatory Reading," na kama miaka iliyopita, katika sehemu hiyo kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimependekezwa kwa wasafiri hao:

For those persons wanting to more deeply explore cultural differences between Africans and Americans, the book Africans and Americans: Embracing Cultural Differences by Joseph Mbele is recommended. The book is available at www.africonxion.com.

Kwangu kama mwandishi, hii ni habari njema, ingawa si mpya. Viongozi wa programu kama hiyo ya Nebraska wana uzoefu wa miaka mingi wa kwenda Tanzania. Wana uzoefu wa utamaduni wa Tanzania. Kuendelea kwao kukipendekeza kitabu changu ni ushahidi kuwa wameona kinawafaa wa-Marekani wanaowapeleka Tanzania.

Watu kutoka Nebraska wanaosairi kwenda Tanzania nimewahi kuwataja katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Ninajisikia kama vile, kwa njia ya kitabu changu, nina uhusiano wa kudumu nao.

Nimeandika nilivyoandika, ingawa ninafahamu kuwa kwa mujibu wa utamaduni wa leo wa Tanzania, tunaogopa kuambiwa tunaringa. Ninaamini kuwa ni sahihi mtu kujivunia kazi yake na mafanikio yake, kama wafanyavyo wanamuziki wetu, ambao aghalabu tunawasikia wakitamba wanapoandaa albamu au wimbo wa kutupagawisha. Tunapowasikia wakisema hivyo, tunafurahi na kusubiri kwa hamu.

Lakini ni ajabu kuwa tunaona si sahihi kwa mwanataaluma kujivunia kazi yake. Lakini ninaona tujikumbushe kauli iliyomo katika "Azimio la Arusha" kuwa katika nchi yetu, kazi iwe ni kitu cha kujivunia; na uvivu, ulevi, na uzembe viwe ni vitu vya kuvionea aibu. "Azimio la Arusha" linazungumzia kila kazi yenye manufaa kwa mtu na jamii.

Kama kichekesho, ninakumbushia methali iliyomo katika riwaya ya Things Fall Apart ya Chinua Achebe: "The lizard that jumped from the high iroko tree to the ground said he would praise himself if no one else did," ambayo inamaanisha kuwa ukifanikisha jambo, usichelee kujisifu mwenyewe. Labda huo ndio utamaduni tunaouhitaji.

Thursday, March 16, 2017

Nimenunua "Two Thousand Seasons" (Ayi Kwei Armah)

Leo nilienda St. Paul, na wakati wa kurudi, nilipitia Apple Valley kuangalia vitabu katika duka la Half Price Books, kama ilivyo kawaida yangu. Hilo duka lina maelfu ya vitabu, na wateja wanapishana humo tangu asubuhi hadi jioni.

Kila ninapoingia katika duka la vitabu, ninajikuta nikianza kuangalia kama kuna vitabu vipya juu ya mwandishi Ernest Hemingway. Leo sikuona kitabu kipya juu ya Hemingway, nikaenda sehemu nyingine humo dukani, kwenye kona kabisa, ambapo sikosi kupitia.

Hapo, katikati ya msitu wa vitabu, niliona kitabu cha Ayi Kwei Armah, Two Thousand Seasons. Sikutegemea kukuta kitabu cha Armah. Nilikichukua hima, huku nikikumbuka enzi za ujana wangu Tanzania, kwani ni wakati ule ndipo nilianza kusikia habari za Ayi Kwei Armah.

Tangu nikiwa mwanafunzi sekondari, nilikuwa nafuatilia sana fasihi ya ki-Ingereza. Somo la fasihi ni somo nililolipenda na kuliweza sana. Nilipoingia Chuo kikuu cha Dar es Salaam, mwaka 1973, ndipo nilipofahamu kuwa Ayi Kwei Armah alikuwa anaishi Dar es Salaam. Alikuwa anafundisha chuo cha ualimu Chang'ombe, lakini tulishangaa kwa jinsi alivyokuwa hatumwoni kokote, hata chuo kikuu. Tulitegemea angejihusisha na chuo kikuu, lakini sidhani kama aliwahi hata kukanyaga pale.

Jambo hilo lilitushangaza, hasa kwa kuzingatia umaarufu wake kama mwandishi katika Afrika na ulimwenguni. Tulisoma riwaya yake, The Beautyful Ones Are Not Yet Born, na mimi binafsi nilisoma pia Fragments, Why are we So Blest?, na Two Thousand Seasons. Ayi Kwei Armah tulimfahamu pia kutokana na insha yake, "African Socialism: Utopian or Scientific?"

Nilijua tangu wakati ule kuwa wahakiki walikuwa wanalumbana kuhusu uandishi wa Armah. Baadhi walilalamika jinsi anavyoielezea Ghana katika The Beautyful Ones Are Not Yet Born. Anaelezea uozo wa kina namna. Wahakiki na wasomaji walishangaa kwa nini aliamua kuanika uozo huo machoni pa ulimwengu.

Two Thousand Seasons inahusu biashara ya utumwa iliyosababisha mamilioni ya wa-Afrika kupelekwa bara la Amerika kama watumwa. Armah kwa kushughulikia mada hii, alikuwa anaendeleza jadi ya waandishi wenzake wa Ghana, kama vile Ama Ata Aidoo katika tamthilia zake mbili: Dilemma of a Ghost na Anowa.

Sunday, February 19, 2017

Utungo wa Pushkin, "Eugene Onegin," Ni Mtihani

Siku chache zilizopita, niliandika katika blogu hii kuwa nilikuwa ninajiandaa kusoma Eugene Onegin, utungo maarufu wa Alexander Pushkin. Nilianza hima, na sasa ninaendelea.

Nilifahamu tangu zamani kuwa Pushkin alikuwa ameandika tungo zingine pia. Nilifahamu kuwa Eugene Onegin ndio utungo wake maarufu kuliko zingine. Nilifahamu kuwa utungo huo ni riwaya iliyoandikwa kwa mtindo wa kishairi.

Nilidhani kuwa ningesoma Eugene Onegin bila matatizo, kama ninavyosoma kazi za waandishi wengi. Baada ya kuanza kuusoma, na ninavyoendelea kusoma, ninajikuta kama vile niko katika mtihani. Eugene Onegin si rahisi kama nilivyodhani.

Pushkin ameusuka utungo wake kwa umahiri mkubwa, akitumia mbinu mbali mbali za kisanii, na pia taarifa za wasanii wa mataifa mbali mbali, kuanzia zama za kale, hadi zama zake. Humo kuna majina ya watunzi wa mataifa mbali mbali, kama vile Theocritus, Juvenal, Ovid, Racine, Chateaubriand, Lord Byron, pamoja na waandishi na waigizaji kadha wa kadha wa u-Rusi, wa wakati wa Pushkin na kabla yake, ambao hata mimi sikuwa ninawafahamu.

Kwa kufuatilia dondoo, dokezo, na maelezo yaliyomo, ninajifunza mambo mengi mapya. Mtindo huu wa Pushkin unanikumbusha ushairi wa Derek Walcott. Kusoma mashairi yake ni chemsha bongo. Unajikuta ukipelekwa sehemu nyingi katika historia, ikiwemo historia ya fasihi, sanaa, na falsafa.

Tafsiri ya Eugene Onegin ninayosoma ni ya Hofstadter. Katika kupambana na tafsiri yake, nimefikia uamuzi kuwa nikimaliza kusoma tafsiri, nisome tafsiri nyingine angalau moja ya mtu tofauti. Lakini ukweli utabaki kuwa ingekuwa bora zaidi kama ningekuwa ninakifahamu ki-Rusi, nikajisomea mwenyewe alichoandika Pushkin. Kama taaluma inavyotufundisha, hakuna tafsiri ambayo inaweza kuwa sawa na utungo unaotafsiriwa.

Mtu unaweza kujiuliza: Kwa nini ninajipitisha katika mtihani huu wa kusoma Eugene Onegin, badala ya kusoma vitabu rahisi? Jibu langu ni kuwa chemsha bongo ni muhimu kwa afya ya ubongo, kama vile mazoezi ya viungo yalivyo muhimu kwa afya ya binadamu. Utungo kama Eugene Onegin, kwa jinsi ulivyosheheni utajiri wa fikra na kumbukumbu za aina mbali mbali, ni njia bora ya kutajirisha akili. Nitajisikia mwenye furaha nitakapoweza kusema nimeusoma na kuutafakari kwa makini utungo huu mashuhuri wa Pushkin.

Wednesday, October 26, 2016

Miaka 80 ya "The Snows of Kilimanjaro"

Kwa mara nyingine tena, ninaandika ujumbe kuhusu kutimia kwa miaka 80 tangu hadithi ya Ernest Hemingway, 'The Snows of Kilimanjaro" ilipochapishwa kwa mara ya kwanza. Niliandika ujumbe wa aina hiyo katika blogu hii. Leo nimesoma tena ujumbe wangu, nikajiridhisha kwamba niliyosema ndiyo ninayoamini hadi sasa.

Jambo moja kubwa kabisa ni kuwa wa-Tanzania tunajipotezea fursa za wazi za kutumia hazina kama hii hadithi ya Hemingway kuitangaza nchi yetu. Niliandika katika ujumbe wangu baadhi ya mambo ambayo tungeyafanya mwaka huu wa kumbukumbu. Lakini mwaka unaelekea ukingoni, na hakuna tulichofanya. Hii ni hasara ya kukosa utamaduni wa kusoma vitabu. Tunashindwa hata kutumia fursa zilizo wazi.

Nimeona niandike ujumbe huu leo kwa sababu wiki hii, hapa katika Chuo cha St. Olaf ninapofundisha, litatokea jambo la pekee linalohusiana na Ernest Hemingway. Keshokutwa, tarehe 28, pataonyeshwa kwa mara ya kwanza filamu ya "Papa's Shadow," ambayo niliwahi kuielezea katika blogu hii.

Hiyo ni filamu iliyotokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwaka 2013 iitwayo Hemingway in East Africa. Nilisafiri na wanafunzi 29 wa Chuo cha St. Olaf, tukazunguka maeneo kadhaa ya Tanzania kaskazini, ambamo alipita Ernest Hemingway mwaka 1933-34. Katika safari hiyo, tulikuwa tunasoma maandishi ya Hemingway kuhusu maeneo hayo na maeneo mengine ambayo alipitia mwaka 1953-54.

Maandishi hayo ni pamoja na Green Hills of Africa na Under Kilimanjaro, ambavyo ni vitabu, kadhalika hadithi fupi mbili: "The Short Happy Life of Francis Macomber" na "The Snows of Kilimanjaro." Pia aliandika makala katika magazeti na barua nyingi akielezea aliyoyaona na kufanya katika safari zake. Kwa ujumla wake, maandishi haya ya Ernest Hemingway yanaitangaza nchi yetu na Afrika Mashariki kwa ujumla kwa namna ambayo sisi wenyewe hatujaweza kujitangaza.

Hiyo filamu ya "Papa's Shadow" inawasilisha vizuri mambo muhimu ya uhusiano wa Ernest Hemingway na Afrika Mashariki. Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway. Tunajadili kwa kina na mapana fikra za Ernest Hemingway kuhusu Afrika, uandishi, na maisha kwa ujumla.

Kwa kuwa hiyo filamu inaonyesha sehemu mbali mbali za Tanzania na maelezo kuhusu mambo yanayoifanya Tanzania kivutio kwa watalii, kama vile Mlima Kilimanjaro, na kwa kuwa filamu hii imejengeka katika maandishi ya Ernest Hemingway, mwandishi maarufu sana ulimwenguni, ni wazi kuwa filamu hii itakuwa chachu ya kuitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Taarifa zaidi Kuhusu "Papa's Shadow," zinapatikana kwenye tovuti ya Ramble Pictures.

Tuesday, February 23, 2016

"So Long a Letter" Katika Kozi ya "Muslim Women Writers"

Kozi yangu ya Muslim Women Writers inaendelea vizuri. Tulianzia India, na hadithi ya Sultana's Dream ya Rokeya Sakhawat Hossain. Baada ya hapo tunasoma So Long a Letter, utungo wa Mariama Ba wa Senegal, nchi mojawapo maarufu katika uwanja wa fasihi ya Afrika.

Senegal imetoa watunzi kama Leopold Sedar Senghor, Cheikh Hamidou Kane, Birago Diop, na Sembene Ousmane, kwa upande wa wanaume, na kwa upande wa wanawake kuna watunzi kama Aminata Sow Fall na Mariama Ba.

So Long a Letter ni utungo ulioandikwa kwa mtindo wa barua, ambayo mhusika mkuu anamwandikia mwanamke mwenzake, rafiki yake. Kwa hali hiyo, utungo huu unafuata jadi ambayo wanafasihi huiita "epistolary." Neno "epistolary" linatokana na neno la ki-Latini ambalo maana yake ni barua.

Suala moja muhimu linaloongelewa ni la wake wenza. Ni suala lenye chimbuko lake katika Qur'an, Sura iv aya 3:

     If ye fear that ye shall not
Bes able to deal justly
With the orphans,
Marry women of your choice,
Two, or three, or four;
But if ye fear that ye shall not
Be able to deal justly (with them),
Then only one, or (a captive)
That your right hand possess.
That will be more suitable,
To prevent you
From doing injustice.

Yusuf Ali, ambaye tafsiri yake ya Qur'an nimeinukuu hapa juu, anafafanua aya hii vizuri. Anakumbushia kwamba aya hii ilitokea katika mazingira maalum, ambamo kutokana na vita ya Uhud, jamii ya wa-Islam ilikuwa na wajane na yatima wengi, pamoja na mateka wa vita. Ilikuwa lazima watu hao watendewe kwa ubinadamu na haki kwa kiwango cha juu kabisa. Ruhusa ya kuwaoa wajane hao imewekewa masherti.

Kabla ya u-Islam, watu walikuwa wanaoa walivyopenda, lakini aya hii inaweka mipaka. Mtu anaweza kuoa hadi wake wanne, si zaidi, lakini kama Yusuf Ali anavyosema, "provided you could treat them with equality, in material things as well as in affection and immaterial things." Yaani masherti ni kwamba uweze kuwatendea wake hao kwa usawa katika mahitaji ya vitu, katika upendo, na mengine ya aina hiyo.

Kutokana na masherti hayo, Yusuf Ali anasema: "As this condition is most difficult to fulfill, I understand the recommendation to be towards monogamy." Yaani, kwa jinsi masherti yalivyo magumu kutekelezeka, nachukulia kwamba agizo hili linaegemea kwenye kuwa na mke moja.

Huu ndio msingi katika Qur'an wa suala la mitara. Wanawake wa-Islam wamekuwa wakilalamika kwamba fundisho la Qur'an limepotoshwa. Wanaume wamejitwalia mamlaka ya kupindisha mafundisho ya Qur'an na kuhalalisha mambo wanayoyapenda wao.  Hii ndio hali inayojitokeza katika So Long a Letter.

So Longer a Letter ni andiko linalohuzunisha kwa jinsi Ramatulaye anavyoelezea roho mbaya ya baadhi ya wanaume. Mume wake mwenyewe alijiolea binti kinyemela, na wanawake wengine wanakutana na adha za aina hiyo. Lakini, hasemi kuwa wanawake muda wote hawana dosari. Anakiri kuwa katika ndoa zingine, wanawake wanawatesa wanaume.

Hatimaye, So Long a Letter inaelezea matumaini ya kubadili mambo na kuwawezesha wanawake kushika nafasi wanazostahili katika jamii, wakitumia vipaji ambavyo wanavyo.

Tuesday, September 22, 2015

Nimenunua Kitabu cha Golding, "Lord of the Flies"

Zimepita siku nyingi kidogo tangu niandike ujumbe kuhusu vitabu nilivyonunua, au nilivyojipatia kwa namna nyingine. Viko vitabu kadhaa, hasa riwaya, ambavyo sikuvielezea.

Leo, baada ya kufundisha vipindi vyangu viwili, nilipita kwenye duka la vitabu la hapa chuoni. Niliangalia sehemu vinapouzwa vitabu kwa bei nafuu, nje ya duka, nikaona, kati ya vitabu vingi, kitabu cha William Golding, Lord of the Flies. Hapo hapo nilikumbuka miaka ya ujana wangu. Tulisoma kitabu hiki tulipokuwa kidatu tano Mkwawa High School, mjini Iringa. Huku nikikumbuka hayo yote, nilikinunua hima, ingawa nina hakika ninayo nakala nyingine niliyonunua zamani, ila itakuwa vigumu kuigundua ilipo katika utitiri wa vitabu vyangu.

Lord of the Flies ni riwaya niliyoipenda sana na ambayo ninaikumbuka sana. Ilinigusa kwa namna ya pekee kwa jinsi ilivyowachora wahusika, ambao ni watoto wa shule waliojikuta kwenye kisiwa peke yao baada ya ndege waliyokuwa wanasafiria kuanguka kisiwani humo na wao wakawa abiria pekee waliosalimika. Riwaya inaonyesha jinsi watoto hao, waliokulia katika jamii ya maadili na ustaarabu, walivyoanza kubadilika, wakawa wabaya na katili kupindukia.

Miaka ile, nilikuwa najikongoja katika uandishi wa hadithi fupi. Lord of the Flies ilinigusa kwa namna ya pekee, kwa ustadi wake wa kuelezea mazingira, ikachangia katika uandishi wa hadithi yangu, "A Girl in the Bus," ambayo ilichapishwa katika jarida la Busara. Hili lilikuwa ni jarida maarufu Afrika Mashariki, lililokuwa linachapishwa Nairobi.

Kuchapishwa kwa hadithi hii kulinipa furaha isiyoelezeka. Nilikuwa na mazoea ya kwenda katika maktaba ya mkoa Iringa, na daima nilikuwa napendezwa kuona jarida hili lenye hadithi yangu. Hata nilipoingia Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kusoma, mwaka 1973, nilikuwa najisikia raha kuliona jarida hili  katika maktaba.

Lord-Flies of the Flies ni riwaya iliyowagusa watu ulimwenguni. Wanadamu kwa ujumla tunaamini kuwa watoto wana silika ya wema na usafi wa moyo. Wanafalsafa kama Jean-Jacques Rousseau walichangia kujenga imani hiyo. Lakini William Golding, katika riwaya yake hii ameelezea jinsi watoto wanavyobadilika na kuwa wabaya. Ni hadithi iliyowashtua walimwengu kwa namna ilivyoihoji dhana ya kwamba watoto ni kama malaika.

Nikizingatia kuwa Lord of the Flies ni moja kati ya riwaya maarufu kabisa katika lugha ya ki-Ingereza, nitaisoma kwa furaha, nikikumbuka ilivyonigusa enzi za ujana wangu. Miaka ilivyopita, nimesoma hadithi na tamthilia mbali mbali ambazo zimeelezea dhamira hii ya watu waliopotelea kwenye kisiwa mbali na walimwengu. Mifano ni The Odyssey ya Homer, Robinson Crusoe ya Daniel Defoe, na mashairi kadhaa ya Derek Walcott, kama vile "The Castaway." Hata baadhi ya wanafalsafa wa mkondo wa "existentialism" wameongelea uwepo wetu hapa duniani kwa kuufananisha na upweke wa watu waliotupwa na kusahauliwa. Ni dhamira ambayo imekuwa na mashiko ya pekee katika fikra na hisia za wanadamu.

Tuesday, August 12, 2014

Nimemaliza Kusoma "The Pearl," Kitabu cha John Steinbeck

Leo asubuhi, nimemaliza kusoma The Pearl, kitabu cha John Steinbeck. Kitabu hiki kimeyagubika mawazo yangu siku nzima. Nilipomaliza kukisoma, nilibaki nimeduwaa, wala sikuweza kuandika ujumbe katika blogu yangu, ingawa nilitamani kufanya hivyo. Ni jioni hii, saa moja na kitu, ndipo nimeweza kuanza kuandika ujumbe huu.

Nirudi nyuma kidogo. Wiki kadhaa zilizopita, kitabu hiki nilikitaja katika blogu hii kuwa kimoja kati ya vitabu nilivyokuwa navisoma kwa mpigo. Sikuwa na haraka, bali niliamua mwenyewe muda gani nisome, na katika kusoma, niliamua mwenyewe niishie wapi, siku hadi siku. Mtindo huu naendelea nao kwa vitabu vingine.

Haiwezekani kuelezea nilivyojisikia wakati nasoma The Pearl. Ni kama kumwelezea mtu ambaye hajawahi kuumwa na jino au kula embe, jinsi jino linavyouma, au utamu wa embe. Hata hivi, naona nigusie tu kuhusu kitabu hiki,

Ni hadithi yenye mvuto wa pekee. Inasisimua, inasikitisha, na inatisha pia. Ni hadithi iliyoniteka, kama vile ndoto ya ajabu au jinamizi. Kisa chenyewe kinamhusu Kino, mvuvi anayebahatika kuokota lulu baharini, lulu kubwa, ya thamani isiyoelezeka. Jamii yake yote inapata habari hima, kuanzia walalahoi ambao ni majirani zake, mabepari wachuuzi wa lulu, padri, daktari, omba omba, kila mtu. Habari ya lulu hii inawasisimua wote hao kwa namna tofauti, wengi kwa wivu na tama ya kumwibia maskini mvuvi huyu. Kwa kutumia habari ya hii lulu, Steinbeck amefanikiwa kuanika tabia na hisia za binadamu.

Kino mwenyewe anajawa na ndoto za kuiwezesha familia yake kuondokana na maisha duni na kumpa fursa mtoto wake mdogo ya kusoma. Lakini pole pole, wasi wasi unaanza kumnyemelea Kino, na hofu pia, kuhusu usalama wa lulu yake na hata maisha yake, hasa pale watu wasiofahamika wanapomnyemelea usiku.

Hapo hadithi inaanza kutisha. Steinbeck ni mbunifu wa kiwango cha juu sana. Hadithi inaendelea hadi mwishoni Kino, mkewe, na mtoto wao wanahama mji usiku, kuinusuru lulu na maisha pia. Ajabu juu ya ajabu, baada ya kutembea kwa mwendo wa mbali usiku, na hatimaye kujificha porini, asubuhi Kino anawaona watu watatu wakija pole pole katika barabara ile ile aliyopitia. Ni wapelelezi makini, ambao wanaweza kutambua hata njia aliyopita mnyama kwenye miamba, ambako alama za nyayo hazionekani kwa binadamu wa kawaida.

Hapo nilijikuta nimeelemewa na hofu, ambayo iliongezeka kadiri nilivyoendelea kusoma kisa hiki. Naona nisiendelee, bali niseme tu kuwa hadithi inapoisha, watu kadhaa wamepoteza maisha, akiwemo mtoto wa Kino, na kwa jinsi lulu ilivyoandamana na mikosi, Kino na mkewe wanaenda ufukweni na kuitupilia mbali baharini.

Nina hakika nilikifahamu kitabu hiki tangu nilipokuwa nasoma sekondari, Seminari ya Likonde. Nilipomaliza kukisoma kitabu hiki, wazo moja kubwa lililokuwa akilini mwangu ni kuwa mara nitakapopata wasaa, nisome The Grapes of Wrath, kitabu kingine maarufu cha Steinbeck, ambacho nimetamani kukisoma kwa miaka mingi. Nimemaliza kusoma The Pearl nikiwa na masononeko, nikiwafikiria wa-Tanzania ambao hawajui ki-Ingereza, na mengi ya thamani yanawapitia mbali. Bado nimesononeka.

Thursday, July 11, 2013

Tumeanza Kusoma "Abyssinian Chronicles"

Baada ya kumaliza kitabu cha Half of a Yellow Sun, darasa langu la fasihi ya Afrika tumekuwa tukisoma Abyssinian Chronicles, riwaya ya Moses Isegawa.

Moses Isegawa ni kijana aliyezaliwa na kukulia Uganda. Lakini mwaka 1990 aliondoka Uganda akaenda kuishi Netherlands, akiwa amechukua uraia wa nchi ile.

Nilikuwa nimesikia habari za kitabu chake hiki kwa miaka kadhaa. Nilinunua nakala, ila sikupata fursa ya kukisoma, ingawa nilikipitia juu juu. Hata hivyo katika kukipitia hivyo, niliona wazi kabisa kuwa ni kitabu murua, kilichoelezea kwa ufasaha na mvuto mkubwa maisha ya leo ya watu wa Uganda, kuanzia kijijini hadi mjini.

Nilipokuwa naandaa kozi yangu hii, miezi michache iliyopita, niliamua kitabu hiki kiwemo katika orodha yangu. Tumesoma karibu kurasa 100 tu,  wakati kitabu kina kurasa 480. Kiasi tulichosoma kimetupa fursa ya kuongelea dhamira mbali mbali zinazojitokeza, kama vile mila na desturi za arusi, masuala ya wahusika, na sanaa.

Kwa upande wangu, nimekuwa nikiwaambia wanafunzi kuwa maelezo ya maisha ya vijijini yamenikumbusha maisha yangu mwenyewe, maana nilizaliwa na kukulia nilikulia kijijini.

Moses Isegawa alikiandika kitabu hiki kwa lugha ya kidachi (Dutch), na jina lake lilikuwa Abessijnse kronieken, ambacho kilichapishwa Amsterdam mwaka 1998. Nakala 100,000 ziliuzwa hima, ingawa idadi ya watu wa nchi ile ni yapata milioni 16 tu.

Mwandishi alikiweka kitabu chake hiki katika lugha ya ki-Ingereza. Kwa kawaida, tunasema alikitafsiri. Lakini kwa mujibu wa falsafa za leo, dhana ya tafsiri ni dhana tata, na kile tunachokiita tafsiri sio tafsiri kwa kweli, bali utungo mpya. Huo ndio mtazamo wangu kuhusu Abyssinian Chronicles.

Muhula wetu umeisha leo, na mategemeo yangu ni kuwa wanafunzi na mimi mwenyewe tutaendelea kukisoma kitabu hiki hadi ukurasa wa mwisho. Sioni kama kuna tatizo kufikia mwisho wa muhula bila kumaliza kusoma kitabu. Dhana ya kumaliza kusoma kitabu nayo ni dhana tata na naweza kusema ni dhana muflisi. Kwa kutafakari kwa undani maana ya kusoma ni nini, na nini kinafanyika tunaposema tunasoma kitabu, nimejionea kuwa huwezi kumaliza kusoma kitabu chochote, hata kama umefika ukurasa wa mwisho na sentensi ya mwisho. Hilo ni suala jingine la falsafa, ambalo nalifafanua wakati wa kufundisha fasihi.

Abyssinian Chronicles ni kitabu kinachoelezea mambo ya miaka ya karibuni, ya sabini na kitu hadi themanini na kitu. Kinavutia sana. Ni ushahidi mwingine wa jinsi wenzetu wa nchi jirani, na wa nchi zingine za Afrika, walivyo katika anga za juu sana katika uandishi kwa lugha hizi za kigeni.

Tuesday, June 4, 2013

Sikujua Mwandishi Legson Kayira Alifariki

Leo katika kupitapita mtandaoni, nimeona taarifa kuwa mwandishi Legson Kayira alifariki mwaka jana, tarehe 14 Oktoba. Sikuwa nimepata taarifa hii ya kifo chake.

Kilichonifanya nikatafuta habari za Kayira ni kuwa siku chache zilizopita, niliongea na mzee mmoja m-Marekani na katika maongezi na mzee mmoja m-Marekani, mzee huyu alikumbushia kuhusu mwandishi fulani, na kutokana na maelezo yake, nikahisi anamwazia Legson Kayira. Nilipomtajia, pamoja na jina la kitabu chake maarufu cha I Will Try, mzee huyu alikubali kuwa ni yeye aliyekuwa anamwazia.

Basi leo, katika kuangalia mtandaoni, nimesoma kuwa kumbe mwandishi huyu alifariki mwaka jana, akiwa na miaka 70. Taarifa hii imenikumbusha miaka ya ujana wetu, tulipokuwa sekondari. Tulikipenda sana kitabu cha I Will Try.

Habari ya kijana fukara Legson Kayira kuamua kutembea kwa mguu kutoka kijijini kwake Malawi ili akafike Marekani kusoma, ilikuwa ni habari ya kusisimua, iliyotutia hamasa ya kuwa wakakamavu katika kufuatilia malengo bora ya maisha. Kwa kweli nashukuru tulielimishwa kwa namna ile, ya kuthamini juhudi na ustahimilivu, sio mambo ya mkato.

Miaka yetu ile tulikuwa tunapenda kusoma vitabu. Tulisoma vitabu vilivyohitajika kwa masomo darasani, lakini tulisoma pia vitabu nje ya mahitaji ya darasani. Kayira alikuwa mmojawapo wa waandishi waliotuvutia. Binafsi, pamoja na kusoma I Will Try, nilisoma pia kitabu chake kilichofuatia, kiitwacho Jingala. Sina hakika, lakini huenda nilisoma pia The Looming Shadow.Le3o nimeona pia taarifa kuwa kitabu cha I Will Try sasa kinapatikana kama kitabu pepe mtandaoni.

Sambamba na Kayira, waandishi wengine kutoka Malawi waliokuwa wakisifika walikuwa Aubrey Kachingwe na David Rubadiri. Hao wote ni kama makamanda waliojenga misingi ya uandishi wa ki-Kingereza Malawi. Leo Malawi iko mbali sana katika uwanja huo. Na kwa jinsi wa-Tanzania tunavyoendekeza uzembe na visingizio elfu, hatutawafikia.

Tuesday, March 26, 2013

Ufundishaji Wangu wa Maandishi ya Achebe

Nimefundisha maandishi ya Chinua Achebe kuanzia miaka ya sabini na kitu. Kabla sijahitimu na shahada ya kwanza Chuo Kikuu Dar es Salaam, mwaka 1976, huenda nilifundisha Things Fall Apart katika shule za sekondari nilikopelekwa kufanya mazoezi ya kufundisha, yaani sekondari ya wasichana Iringa, 1974, na sekondari ya Kinondoni, 1975. Sina hakika.

Lakini baada ya kuhitimu shahada ya kwanza, mwaka 1976, nilipata fursa za kufundisha Things Fall Apart, nikianzia na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambapo nilikuwa mhadhiri. Mwaka 1980, chini ya mkataba wa ushirikiano baina ya Tanzania na Burundi, nilifundisha kwa wiki kadhaa katika Chuo Kikuu cha Burundi. Kitabu kimojawapo kilikuwa Things Fall Apart

Uzoefu huu ulinifanya niandike mwongozo wa Things Fall Apart, ili kuelezea mambo ambayo waandishi wengine hawajayaweka wazi.  Ilikuwa ni fursa kwangu kuwaelezea wanafunzi na walimwengu namna ninavyoichukulia riwaya hii ya Things Fall Apart. Kwa maelezo zaidi ya historia hii, soma hapa. Sihitaji kuficha ukweli kwamba mwongozo huu ni maarufu na wengi wanautumia.

Baada ya kuja kufundisha chuo cha St. Olaf, mwaka 1991, nimefundisha Things Fall Apart na maandishi mengine ya Achebe. Kuna muhula fulani nilitunga kozi nzima juu ya maandishi ya Achebe tu. Tulisoma riwaya zake kadhaa, na pia insha baadhi ya insha zake, zikiwemo "The Novelist at Teacher," "Colonialist Criticism," na "An Image of Africa." Tulisikiliza pia baadhi ya mahojiano yake. Ingekuwa muda unaruhusu, tungesoma pia mashairi yake.

Ni wazi kwamba Things Fall Apart ni moja ya riwaya ambazo nimezifundisha sana. Kila ninapoifundisha, nazua masuala mapya na tafakari mpya. Hiyo ni tabia ya fasihi. Hata misahafu ina tabia hiyo, ingawa wako watu wanaodai kuwa misahafu haibadiliki. Binafsi, kutokana na uzoefu wangu wa kusoma na kutafakari fasihi na maandishi mengine, siamini kwamba kuna andiko lolote, hata msahafu, ambalo haliguswi na mabadiliko, kuanzia na mabadiliko ya lugha na maana zake, ambayo hayakwepeki. Nimegusia suala hilo katika mwongozo wangu.

Friday, March 22, 2013

Buriani, Chinua Achebe

Msiba mzito umetufika leo, wasomaji wa fasihi na walimwengu kwa ujumla. Chinua Achebe amefariki, akiwa na umri wa miaka 82.

Maarufu kama muasisi wa fasihi ya ki-Ingereza katika Afrika, Chinua Achebe ametoa mchango mkubwa katika uandishi, mchango ambao uliiweka Afrika mahala pazuri katika ramani ya fasihi ya dunia.

Tangu alipochapisha riwaya yake maarufu, Things Fall Apart, hadi kufariki kwake, Achebe ameandika riwaya, hadithi fupi, na insha kuhusu fasihi, uandishi, siasa na utamaduni. Amefanya mahojiano mengi, ambayo, kwa bahati nzuri yanapatikana mtandaoni au katika vitabu na majarida.

Achebe aliamini kwa dhati kuwa jukumu la msanii ni kuwa mwalimu wa jamii. Yeye mwenyewe amezingati wajibu huo tangu ujana wake, alipochapisha Things Fall Apart, hadi kurariki kwake. Amewafundisha waAfrika mengi kuhusu jamii yao, udhaifu na uwezo wao, na amewafundisha walimwengu kuwaona wa-Afrika kwa mtazamo tofauti na ule wa wakoloni. Amewafundisha walimwengu maana ya ubinadamu, ambayo inavuka mipaka ya kabila, taifa, dini, jinsia au nchi.

Sikupata fursa ya kukutana uso kwa uso na Chinua Achebe, bali nimesoma na kufundisha maandishi yake mara kwa mara. Nashukuru pia kuwa nilipata wazo la kuandika mwongozo wa Things Fall Apart. Kwa namna hiyo ya kusoma na kutafakari maandishi yake, najiona kama vile nami nimekutana na mwandishi huyu. Nimalizie tu kwa kusema kwamba kwa mchango wake mkubwa kwa walimwengu, Achebe atakumbukwa daima.

Wednesday, October 26, 2011

Mwandishi Nuruddin Farah Katutembelea

Jana jioni, mwandishi maarufu Nuruddin Farah, mzaliwa wa Somalia, alikuja chuoni Carleton, hapa Northfield, kuongea na wadau kuhusu riwaya yake mpya, Crossbones, ambayo imechapishwa mwaka huu.









Nilienda kumsikiliza. Kama ilivyo kawaida katika shughuli za aina hii, vitabu vyake vilikuwepo, vinauzwa. Kwa vile ninavyo vitabu vyake vingine, nilinunua hiki kipya. Hapa pichani mwandishi anasaini nakala yangu. Bei yake ni dola 27.95, yapata shilingi 50,000 za Tanzania. Hiki ni kiasi kidogo sana ukifananisha na hela tunazotumia wa-Tanzania kwenye ulabu na makamuzi mengine. Bora kununua kitabu.




Ingawa bado sijaisoma riwaya ya Crossbones, kwa kufuatilia mazungumzo ya jana na kuiangalia kijuu juu, ni riwaya inayohusu Somalia kabla tu na baada ya uvamizi wa kijeshi uliofanywa na Ethipia miaka michache iliyopita. Ni riwaya inayoelezea athari za matukio hayo katika maisha ya wahusika.













Kwa bahati, nimeshamwona Nuruddin Farah mara kadhaa akihutubia, hapa Marekani. Vile vile, nimepata kufundisha baadhi ya maandishi yake. Mara ya kwanza ilikuwa ni mwaka 1974. Nilikuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na kwa vile nilikuwa nasomea ualimu, nilienda shule ya wasichana ya Iringa kufanya mazoezi ya kufundisha. Kitabu cha Nuruddin Farah From a Crooked Rib kilikuwa kinatumika katika somo la "Literature."

Miaka ya hivi karibuni, hapa chuoni St. Olaf, nimefundisha pia riwaya zingine za Nuruddin Farah. Ni mmoja wa waandishi bora kabisa kutoka Afrika, ambaye ameshapata tuzo nyingi kwa uandishi wake.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...