Thursday, March 16, 2017

Nimenunua "Two Thousand Seasons" (Ayi Kwei Armah)

Leo nilienda St. Paul, na wakati wa kurudi, nilipitia Apple Valley kuangalia vitabu katika duka la Half Price Books, kama ilivyo kawaida yangu. Hilo duka lina maelfu ya vitabu, na wateja wanapishana humo tangu asubuhi hadi jioni.

Kila ninapoingia katika duka la vitabu, ninajikuta nikianza kuangalia kama kuna vitabu vipya juu ya mwandishi Ernest Hemingway. Leo sikuona kitabu kipya juu ya Hemingway, nikaenda sehemu nyingine humo dukani, kwenye kona kabisa, ambapo sikosi kupitia.

Hapo, katikati ya msitu wa vitabu, niliona kitabu cha Ayi Kwei Armah, Two Thousand Seasons. Sikutegemea kukuta kitabu cha Armah. Nilikichukua hima, huku nikikumbuka enzi za ujana wangu Tanzania, kwani ni wakati ule ndipo nilianza kusikia habari za Ayi Kwei Armah.

Tangu nikiwa mwanafunzi sekondari, nilikuwa nafuatilia sana fasihi ya ki-Ingereza. Somo la fasihi ni somo nililolipenda na kuliweza sana. Nilipoingia Chuo kikuu cha Dar es Salaam, mwaka 1973, ndipo nilipofahamu kuwa Ayi Kwei Armah alikuwa anaishi Dar es Salaam. Alikuwa anafundisha chuo cha ualimu Chang'ombe, lakini tulishangaa kwa jinsi alivyokuwa hatumwoni kokote, hata chuo kikuu. Tulitegemea angejihusisha na chuo kikuu, lakini sidhani kama aliwahi hata kukanyaga pale.

Jambo hilo lilitushangaza, hasa kwa kuzingatia umaarufu wake kama mwandishi katika Afrika na ulimwenguni. Tulisoma riwaya yake, The Beautyful Ones Are Not Yet Born, na mimi binafsi nilisoma pia Fragments, Why are we So Blest?, na Two Thousand Seasons. Ayi Kwei Armah tulimfahamu pia kutokana na insha yake, "African Socialism: Utopian or Scientific?"

Nilijua tangu wakati ule kuwa wahakiki walikuwa wanalumbana kuhusu uandishi wa Armah. Baadhi walilalamika jinsi anavyoielezea Ghana katika The Beautyful Ones Are Not Yet Born. Anaelezea uozo wa kina namna. Wahakiki na wasomaji walishangaa kwa nini aliamua kuanika uozo huo machoni pa ulimwengu.

Two Thousand Seasons inahusu biashara ya utumwa iliyosababisha mamilioni ya wa-Afrika kupelekwa bara la Amerika kama watumwa. Armah kwa kushughulikia mada hii, alikuwa anaendeleza jadi ya waandishi wenzake wa Ghana, kama vile Ama Ata Aidoo katika tamthilia zake mbili: Dilemma of a Ghost na Anowa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...