Showing posts with label Malawi. Show all posts
Showing posts with label Malawi. Show all posts

Tuesday, June 4, 2013

Sikujua Mwandishi Legson Kayira Alifariki

Leo katika kupitapita mtandaoni, nimeona taarifa kuwa mwandishi Legson Kayira alifariki mwaka jana, tarehe 14 Oktoba. Sikuwa nimepata taarifa hii ya kifo chake.

Kilichonifanya nikatafuta habari za Kayira ni kuwa siku chache zilizopita, niliongea na mzee mmoja m-Marekani na katika maongezi na mzee mmoja m-Marekani, mzee huyu alikumbushia kuhusu mwandishi fulani, na kutokana na maelezo yake, nikahisi anamwazia Legson Kayira. Nilipomtajia, pamoja na jina la kitabu chake maarufu cha I Will Try, mzee huyu alikubali kuwa ni yeye aliyekuwa anamwazia.

Basi leo, katika kuangalia mtandaoni, nimesoma kuwa kumbe mwandishi huyu alifariki mwaka jana, akiwa na miaka 70. Taarifa hii imenikumbusha miaka ya ujana wetu, tulipokuwa sekondari. Tulikipenda sana kitabu cha I Will Try.

Habari ya kijana fukara Legson Kayira kuamua kutembea kwa mguu kutoka kijijini kwake Malawi ili akafike Marekani kusoma, ilikuwa ni habari ya kusisimua, iliyotutia hamasa ya kuwa wakakamavu katika kufuatilia malengo bora ya maisha. Kwa kweli nashukuru tulielimishwa kwa namna ile, ya kuthamini juhudi na ustahimilivu, sio mambo ya mkato.

Miaka yetu ile tulikuwa tunapenda kusoma vitabu. Tulisoma vitabu vilivyohitajika kwa masomo darasani, lakini tulisoma pia vitabu nje ya mahitaji ya darasani. Kayira alikuwa mmojawapo wa waandishi waliotuvutia. Binafsi, pamoja na kusoma I Will Try, nilisoma pia kitabu chake kilichofuatia, kiitwacho Jingala. Sina hakika, lakini huenda nilisoma pia The Looming Shadow.Le3o nimeona pia taarifa kuwa kitabu cha I Will Try sasa kinapatikana kama kitabu pepe mtandaoni.

Sambamba na Kayira, waandishi wengine kutoka Malawi waliokuwa wakisifika walikuwa Aubrey Kachingwe na David Rubadiri. Hao wote ni kama makamanda waliojenga misingi ya uandishi wa ki-Kingereza Malawi. Leo Malawi iko mbali sana katika uwanja huo. Na kwa jinsi wa-Tanzania tunavyoendekeza uzembe na visingizio elfu, hatutawafikia.

Saturday, February 6, 2010

Wamarekani Safarini Malawi

Leo nilikwenda mjini Chippewa Falls, katika jimbo la Wisconsin, umbali wa maili 123 kutoka Northfield, ambapo naishi. Nilienda kuongea na kikundi cha wa-Marekani wanaojiandaa kwenda Malawi kwa shughuli za kujitolea. Nilialikwa na Mama Diane Kaufmann, ambaye anaonekana kushoto kwangu, katika picha hapa juu. Yeye ameenda Malawi mara kadhaa, katika wadhifa wake kama mratibu wa mpango wa ushirikiano baina ya dayosisi ya Kanisa la kiLuteri Kaskazini Magharibi ya Wisconsin na Malawi. Ana uzoefu wa kupeleka vikundi vya wanadayosisi Malawi katika mpango huo. Vile vile tumeshirikiana kwa miaka kadhaa katika kuendesha mafunzo kwenye kituo cha Luther Point.
Kikundi nilichoenda kukutana nacho leo kinaenda Malawi kuwashughulikia watu wenye matatizo ya macho, na kuwagawia miwani. Wanatarajia kufanya shughuli hizo Karonga na Chitipa.
Baadhi yao wameshaenda Malawi, na kwa wengine hii itakuwa ni mara yao ya kwanza. Mama Kaufmann aliniita niongee nao kuhusu masuala ninayoongelea katika kitabu changu cha Africans and Americans. Alinieleza kabla kuwa washiriki wote watakuwa wamekisoma kitabu hiki kabla ya ujio wangu. Kama kawaida, mazungumzo na watu waliojiandaa namna hii yanakuwa ya kina, kwani yanalenga katika kufuatilia yale ambayo wamesoma.
Walifurahi kuwa nami, kwani walijisikia kama vile wameshanifahamu, kutokana na ninavyojieleza kitabuni. Nami nilifurahi kuwa nao na kuwasisitizia mambo ya msingi kuhusu kuishi au kushughulika na watu wa utamaduni tofauti na wetu. Kwa vile hao wanaenda kwa shughuli za matibabu, mazungumzo yetu yalilenga zaidi kwenye hali halisi ya kushughulika na watu katika hospitali. Tofauti za tamaduni zinajitokezaje katika mazingira ya hospitali.
Kwa bahati nzuri haya ni mambo ambayo nimeyawazia kwa muda mrefu, na katika kitabu changu nimeyagusia. Vile vile, nimekuwa nikijipatia uzoefu katika mazungumzo na wanafunzi wa masomo ya uuguzi wanapojiandaa kwenda Tanzania kimasomo.

Baadhi ya wasafiri hao walisoma katika chuo cha St. Olaf, na tulipata fursa ya kuongelea na kupiga soga kuhusu maisha chuoni hapa. Baadhi wamesoma maandishi yangu mengine, kama vile Matengo Folktales na Notes on Achebe's Things Apart. Niliona wazi kuwa hao ni watu makini ambao wanajishughulisha kufahamu habari za huko waendako.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...