Showing posts with label barua. Show all posts
Showing posts with label barua. Show all posts

Saturday, August 5, 2017

Shukrani ya Global Minnesota kwa Mhadhara Wangu

Tarehe 12 Julai, nilitoa mhadhara Global Minnesota, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Nimepata barua ya shukrani kutoka Global Minnesota, iliyoandikwa tarehe 20 Julai, ambayo ni kumbukumbu nzuri kwangu. Imeandikwa:

Dear Dr. Mbele

On behalf of Global Minnesota, I would like to thank you for speaking at the Global Conversations program on "African Folktales to Contemporary Authors" at the Minneapolis Central Library on July 12.

Your extensive knowledge and skillful storytelling captured and kept our audience's attention throughout the program. The program was both informative and entertaining, and the feedback we received from the attendees and our partners was extremely positive.

We were also so pleased that you brought your daughters to the program and rekindled an old MIC/GLobal Minnesota connection.

Thank you for partnering with us on this program and helping us in our mission to bring greater awareness and appreciation of African culture to the general public in Minnesota. We look forward to engaging with you again on future Global Minnesota programs!

Kwanza kabisa, mimi nina tabia ya kujitathmini mwenyewe. Pamoja na kusikiliza namna watu wengine wanavyotathmini kazi zangu, tathmini yangu mwenyewe ndiyo inayonisukuma zaidi. Kuna wakati ambapo watu wanaweza kusifia kazi yangu lakini mimi mwenyewe nikawa na mtazamo tofauti.

Pamoja na sifa nilizomwagiwa na Global Minnesota, mimi mwenyewe niliona kuwa muda wa mhadhara ulikuwa mfupi. Kwa hivyo, nilishaamua kuwafahamisha wanipangie siku nyingine na mada nyingine, niweze kuteremsha nondo za kufa mtu, kama wasemavyo wa-Tanzania vijiweni. Sasa, kwa kuwa katika barua yao nao wanapendekeza tuendelee kushirikiana katika programu zao, fursa hiyo sitailazia damu.

Napenda nihitimishe ujumbe wangu kwa kuelezea falsafa inayoniongoza. Jambo la msingi ni kwamba Global Minnesota waliponiuliza kama nitaweza kwenda kutoa mhadhara, nilikubali bila kusita. Ninatambua kuwa mimi ni mwalimu, na ufundishaji hauishii darasani bali unahitajika pia katika jamii nje ya chuo. Vipaji nilivyo navyo nilipewa na Mungu kwa ajili ya wanadamu, si kwa ajili yangu.

Sijivunii vipaji hivyo, bali ninamshukuru Mungu na kumwomba anisaidie kuvitumia kwa namna anavyotaka. Kwamba ninaamka kila asubuhi nikiwa mzima na akili timamu, ni baraka ya Mungu, kuniwezesha kufanya wajibu wangu. Ndio maana, sitilii maanani suala la malipo ninapoalikwa kwenda kutoa mhadhara, kama nilivyowahi kuelezea katika blogu hii. Ninazingatia ufanisi wa hali ya juu katika shughuli ninazofanya. Mengine ni matokeo.

Sunday, April 2, 2017

Mhadhara Chuo Kikuu cha Minnesota Juu ya Kitereza

Juzi tarehe 31, Dr. Charlotte (Shoonie) Hartwig na mimi tulitoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Minnesota, juu ya mwandishi Aniceti Kitereza. Huyu ni mwandishi muhimu ambaye, hata hivyo, hafahamiki sana. Mama Shoonie amekuwa akiandika kitabu ambacho nami nimechangia, na mhadhara wetu ulihusu kitabu hiki ambacho tunategemea kukichapisha.

Kitereza alizaliwa mwaka 1896 katika kisiwa cha Ukerewe kilichomo katika Ziwa Victoria, upande wa Tanzania. Alisomea katika shule za wamisheni, na alipomaliza aliajiriwa kazi kadhaa. Alivyozidi kukua alipata dhamira ya kuhifadhi mila na desturi za zamani za wa-Kerewe, ili zisipotee. Kama sehemu ya juhudi hiyo aliandika riwaya katika lugha ya ki-Kerewe, ambao aliukamilisha mwanzoni mwa mwaka 1945. Andiko hili ni hazina ya mila na destruĂ­ za wa-Kerewe wa zamani, ila Kitereza aliandika kwa mtindo wa hadithi ya kubuni, ili wasomaji wasichoke kusoma.

Baada ya juhudi na mahangaiko ya miaka mingi ya kutafuta mchapishaji, na kufuatia ushauri wa marafiki zake wa-Marekani, Kitereza aliutafsiri mswada wake kwa ki-Swahili. Hata hivyo, aliendelea kungoja kwa miaka mingi hadi mwaka 1980 ambapo mswada ulichapishwa kama kitabu, Bwana Myombekere na Bibi Bugonoka na Ntulanalwo na Buliwhali.

Mama Shoonie ni mtu pekee aliyesalia mwenye taarifa za ndani za Kitereza, kwani yeye na mumewe, Dr. Gerald Hartwig, walimfahamu vizuri Kitereza baada ya kuonana naye kwa mara ya kwanza mwaka 1968 Ukerewe. Mbali ya kukutana naye mara kwa mara miaka ile ya mwanzo, waliendelea kuandikiana barua hadi miaka ya mwisho wa maisha yake. Kitereza alikuwa hodari wa kuandika barua; ananikumbusha waandishi kama Ernest Hemingway na Shaaban Robert.

Katika mhadhara wa juzi, Mama Shoonie alielezea maisha ya Kitereza na mambo aliyofanya kama mwandishi. Maelezo yake aliyaambatanisha na picha za Kitereza, mke wake, na familia nzima ya Hartwig. Watoto wa familia ya Hartwig walikuwa wadogo sana wakati huo. Mama Shoonie alielezea kuwa Kitereza alikuwa anajituma sana katika shughuli yake ya kuhifadhi mila na destruĂ­ za wahenga kwa kusukumwa na suali ambalo alilitunga mwenyewe, "Tunawajibika kuwafundisha nini watoto wetu?"

Ilipokuja zamu yangu, nilielezea kwa ufupi uandishi wa Kitereza kwa mujibu wa mtazamo wangu kama mwana fasihi. Nilisisitiza masuala kadhaa muhimu yanayojitokeza katika taaluma ya fasihi ya Afrika, hasa suala la uandishi katika lugha za ki-Afrika na suala la tafsiri. Niligusia jinsi riwaya ya Bwana Myombekere inavyoweza kutupa mtazamo mpya kuhusu historia ya riwaya ya ki-Afrika, na jinsi inavyoweza kuchambuliwa sambamba na kazi za waandishi kama Daniel O. Fagunwa na Amos Tutuola wa Nigeria, Gakaara wa Wanjau wa Kenya, na Shaaban Robert wa Tanzania. Huu utakuwa ni mtazamo wa fasihi linganishi.

Nimesoma tafsiri ya Kitereza ya riwaya yake. Ki-Swahili chake, ingawa kinatofautiana na ki-Swahili sanifu, kina ladha na mtiririko wa hadithi simulizi za lugha za ki-Bantu kama vile lugha yangu ya ki-Matengo. Kwa msingi huo, ninaipenda tafsiri ya Kitereza. Riwaya yake imetafsiriwa kwa ki-Faransa na ki-Jermani, lakini tafsiri hizo, kwa mujibu wa Profesa Gabriel Ruhumbika, zina walakini. Kauli ya Profesa Ruhumbika ina uzito sana, kwani lugha mama yake ni ki-Kerewe na pia yeye ni mashuhuri katika uwanja wa kutafsiri.

Profesa Ruhumbika mwenyewe ametafsiri kwa ki-Ingereza riwaya ya Kitereza kama ilivyoandikwa ki-Kikerewe, na tafsiri yake imechapishwa kama Mr. Myombekere and His Wife Bugonoka, Their Son Ntulanalwo and Daughter Buliwhali. Katika kuisoma tafsiri hii, nilivutiwa nayo, sawa na nilivyovutiwa na tafsiri ya ki-Swahili ya Kitereza mwenyewe. Ni tafsiri ambayo ninapendekeza isomwe na yeyote. Hivyo hivyo, ninakipendekeza kitabu cha Mama Shoonie kijacho. Ni kitabu chenye taarifa nyingi, zikiwemo barua na picha, ambazo ulimwengu haujaziona. 

Tuesday, February 23, 2016

"So Long a Letter" Katika Kozi ya "Muslim Women Writers"

Kozi yangu ya Muslim Women Writers inaendelea vizuri. Tulianzia India, na hadithi ya Sultana's Dream ya Rokeya Sakhawat Hossain. Baada ya hapo tunasoma So Long a Letter, utungo wa Mariama Ba wa Senegal, nchi mojawapo maarufu katika uwanja wa fasihi ya Afrika.

Senegal imetoa watunzi kama Leopold Sedar Senghor, Cheikh Hamidou Kane, Birago Diop, na Sembene Ousmane, kwa upande wa wanaume, na kwa upande wa wanawake kuna watunzi kama Aminata Sow Fall na Mariama Ba.

So Long a Letter ni utungo ulioandikwa kwa mtindo wa barua, ambayo mhusika mkuu anamwandikia mwanamke mwenzake, rafiki yake. Kwa hali hiyo, utungo huu unafuata jadi ambayo wanafasihi huiita "epistolary." Neno "epistolary" linatokana na neno la ki-Latini ambalo maana yake ni barua.

Suala moja muhimu linaloongelewa ni la wake wenza. Ni suala lenye chimbuko lake katika Qur'an, Sura iv aya 3:

     If ye fear that ye shall not
Bes able to deal justly
With the orphans,
Marry women of your choice,
Two, or three, or four;
But if ye fear that ye shall not
Be able to deal justly (with them),
Then only one, or (a captive)
That your right hand possess.
That will be more suitable,
To prevent you
From doing injustice.

Yusuf Ali, ambaye tafsiri yake ya Qur'an nimeinukuu hapa juu, anafafanua aya hii vizuri. Anakumbushia kwamba aya hii ilitokea katika mazingira maalum, ambamo kutokana na vita ya Uhud, jamii ya wa-Islam ilikuwa na wajane na yatima wengi, pamoja na mateka wa vita. Ilikuwa lazima watu hao watendewe kwa ubinadamu na haki kwa kiwango cha juu kabisa. Ruhusa ya kuwaoa wajane hao imewekewa masherti.

Kabla ya u-Islam, watu walikuwa wanaoa walivyopenda, lakini aya hii inaweka mipaka. Mtu anaweza kuoa hadi wake wanne, si zaidi, lakini kama Yusuf Ali anavyosema, "provided you could treat them with equality, in material things as well as in affection and immaterial things." Yaani masherti ni kwamba uweze kuwatendea wake hao kwa usawa katika mahitaji ya vitu, katika upendo, na mengine ya aina hiyo.

Kutokana na masherti hayo, Yusuf Ali anasema: "As this condition is most difficult to fulfill, I understand the recommendation to be towards monogamy." Yaani, kwa jinsi masherti yalivyo magumu kutekelezeka, nachukulia kwamba agizo hili linaegemea kwenye kuwa na mke moja.

Huu ndio msingi katika Qur'an wa suala la mitara. Wanawake wa-Islam wamekuwa wakilalamika kwamba fundisho la Qur'an limepotoshwa. Wanaume wamejitwalia mamlaka ya kupindisha mafundisho ya Qur'an na kuhalalisha mambo wanayoyapenda wao.  Hii ndio hali inayojitokeza katika So Long a Letter.

So Longer a Letter ni andiko linalohuzunisha kwa jinsi Ramatulaye anavyoelezea roho mbaya ya baadhi ya wanaume. Mume wake mwenyewe alijiolea binti kinyemela, na wanawake wengine wanakutana na adha za aina hiyo. Lakini, hasemi kuwa wanawake muda wote hawana dosari. Anakiri kuwa katika ndoa zingine, wanawake wanawatesa wanaume.

Hatimaye, So Long a Letter inaelezea matumaini ya kubadili mambo na kuwawezesha wanawake kushika nafasi wanazostahili katika jamii, wakitumia vipaji ambavyo wanavyo.

Wednesday, December 5, 2012

Barua za Ernest Hemingway, 1907-1922

Leo nimekipata kitabu cha barua za Hemingway ambacho nilikitaja katika blogu hii siku chache zilizopita. Kama nilivyoandika, nilikiona kwa mara ya kwanza katika duka la vitabu hapa Chuoni St. Olaf. Lakini nakala ile ilinunuliwa hima, ikabidi niagize.

Hemingway alikuwa mwandishi makini wa barua. Hata mwanae, Mzee Patrick Hemingway, amethibitisha hivyo. Kwa ujumla, Hemingway hakutaka wala kutarajia kuwa barua zake zichapishwe. Alikuwa na mazoea ya kuandika barua zake kwa uwazi na hata kutumia lugha ambayo inaonekana kali au yenye kukiuka maadili.

Baada ya Hemingway kufariki, mwaka 1961, suala la kuchapisha au kutochapisha maandishi ya Hemingway ambayo alikuwa hajayachapisha lilijitokeza na kuwa kubwa. Maandishi yake mengine alikuwa hajamaliza kuyarekebisha. Barua zake alikuwa hajaazimia zichapishwe. Suala likawa nini kifanyike.

Wasomaji wa maandishi ya Hemingway walisukumwa na kiu ya kutaka kusoma maandishi yake yote. Wahariri na watafiti walitaka hivyo pia. Familia yake ilikuwa katika mtihani mgumu. Lakini hatimaye, iliamuliwa kuwa bora kuchapisha maandishi hayo, hata barua zake. Ndivyo tulivyovipata vitabu vya Hemingway kama vile The Garden of Eden, Islands in the Stream, A Moveable Feast, na Under Kilimanjaro. Ni matokeo ya maamuzi magumu, na juhudi za wahariri kuhariri miswada aliyoicha Hemingway ikiwa haijakamilika, wakiongozwa na wazo kwamba bila shaka Hemingway mwenyewe angeafiki uhariri huo.

Tunaposoma vitabu hivi bado tunajiuliza iwapo kama Hemingway angeishi zaidi, angerekebisha vipi maandishi haya, hasa ikizingatiwa kuwa alikuwa mwandishi mwenye nidhamu ya hali isiyo ya kawaida katika kusahihisha na kuboresha maandishi yake. Alitaka kila neno liwe mahali pake na liwe kweli ni neno hilo, si jingine, na kila sentensi iwe imekamilika kwa kiwango cha juu kabisa.

Leo nilitaka nikumbushie pia kitabu cha barua za Shaaban Robert, ambacho niliandika habari zake katika blogu hii. Nilitaka nivijadili vitabu hivi vya barua kwa pamoja, kuelezea umuhimu wa vitabu vya aina hii, ambamo tunapata kuwafahamu waandishi hao maarufu kupitia njia ya barua walizoandika. Barua hizi ni kioo muhimu cha kutuwezesha kuyafahamu mambo ambayo pengine hatungeyafahamu kwa kuangalia tu vitabu vyao vingine. Nangojea nipate wasaa wa kuandika na kuzihusianisha barua za Hemingway na zile za Shaaban Robert.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...