Wednesday, December 5, 2012

Barua za Ernest Hemingway, 1907-1922

Leo nimekipata kitabu cha barua za Hemingway ambacho nilikitaja katika blogu hii siku chache zilizopita. Kama nilivyoandika, nilikiona kwa mara ya kwanza katika duka la vitabu hapa Chuoni St. Olaf. Lakini nakala ile ilinunuliwa hima, ikabidi niagize.

Hemingway alikuwa mwandishi makini wa barua. Hata mwanae, Mzee Patrick Hemingway, amethibitisha hivyo. Kwa ujumla, Hemingway hakutaka wala kutarajia kuwa barua zake zichapishwe. Alikuwa na mazoea ya kuandika barua zake kwa uwazi na hata kutumia lugha ambayo inaonekana kali au yenye kukiuka maadili.

Baada ya Hemingway kufariki, mwaka 1961, suala la kuchapisha au kutochapisha maandishi ya Hemingway ambayo alikuwa hajayachapisha lilijitokeza na kuwa kubwa. Maandishi yake mengine alikuwa hajamaliza kuyarekebisha. Barua zake alikuwa hajaazimia zichapishwe. Suala likawa nini kifanyike.

Wasomaji wa maandishi ya Hemingway walisukumwa na kiu ya kutaka kusoma maandishi yake yote. Wahariri na watafiti walitaka hivyo pia. Familia yake ilikuwa katika mtihani mgumu. Lakini hatimaye, iliamuliwa kuwa bora kuchapisha maandishi hayo, hata barua zake. Ndivyo tulivyovipata vitabu vya Hemingway kama vile The Garden of Eden, Islands in the Stream, A Moveable Feast, na Under Kilimanjaro. Ni matokeo ya maamuzi magumu, na juhudi za wahariri kuhariri miswada aliyoicha Hemingway ikiwa haijakamilika, wakiongozwa na wazo kwamba bila shaka Hemingway mwenyewe angeafiki uhariri huo.

Tunaposoma vitabu hivi bado tunajiuliza iwapo kama Hemingway angeishi zaidi, angerekebisha vipi maandishi haya, hasa ikizingatiwa kuwa alikuwa mwandishi mwenye nidhamu ya hali isiyo ya kawaida katika kusahihisha na kuboresha maandishi yake. Alitaka kila neno liwe mahali pake na liwe kweli ni neno hilo, si jingine, na kila sentensi iwe imekamilika kwa kiwango cha juu kabisa.

Leo nilitaka nikumbushie pia kitabu cha barua za Shaaban Robert, ambacho niliandika habari zake katika blogu hii. Nilitaka nivijadili vitabu hivi vya barua kwa pamoja, kuelezea umuhimu wa vitabu vya aina hii, ambamo tunapata kuwafahamu waandishi hao maarufu kupitia njia ya barua walizoandika. Barua hizi ni kioo muhimu cha kutuwezesha kuyafahamu mambo ambayo pengine hatungeyafahamu kwa kuangalia tu vitabu vyao vingine. Nangojea nipate wasaa wa kuandika na kuzihusianisha barua za Hemingway na zile za Shaaban Robert.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...