Friday, December 21, 2012

Habari Njema: Kitabu cha "Hemingway and Africa" Kimefika

Leo nina furaha sana. Kisa? Kitabu nilichoagiza, Hemingway and Africa, kimefika leo.

Kila ninapojipatia kitabu kipya ninafurahi. Ukizingatia kuwa hadi sasa nina vitabu zaidi ya elfu tatu, utaona kuwa nimekuwa mwenye furaha, tena na tena. Huenda nitaishi miaka kadhaa ya ziada kutokana na hiyo furaha.

Pamoja na hayo yote, hiki kitabu cha Hemingway and Africa ni cha pekee. Mwanzo kukiona ni pale nilipokiazima kutoka maktaba ya Chuo Kikuu cha Minnesota, nikakisoma. Kilinigusa kwa namna ya pekee, kwa jinsi kilivyosheheni taarifa na uchambuzi mpya, nikaamua lazima niwe na nakala.

Kama unavyoniona pichani, nimekishika kitabu hiki nikiwa nimefurahi sawa na mtu aliyejishindia kreti ya bia. Ninataja bia kwa makusudi. Kitabu hiki, chenye kurasa 398, bei yake ni dola 80 ambayo kwa madafu ni zaidi ya 120,000. Ukienda baa na hela hizo, unapata kreti mbili za bia, kuku mzima, na nauli ya teksi ya kukurudisha kwenu Mbagala. Kama wewe si mtu wa baa, hizo hela ni mchango tosha wa sherehe kama vile "send-off."

Sasa inakuwaje Krismasi yote hii mtu ufurahie kitabu cha bei mbaya, badala ya kujichana na bia? Ukweli ni kwamba kila mtu ana udhaifu wake. Udhaifu wangu mojawapo ni kuvipenda sana vitabu.

Kuhusu mwandishi Hemingway, ni kwamba kwa miaka na miaka nimekuwa msomaji na shabiki mkubwa wa maandishi yake: kuanzia riwaya na hadithi fupi, hadi insha na barua. Nayapenda kwa namna ya pekee maandishi yake yanayohusu uhusiano wake na Afrika, kwani alitembelea na kuishi miezi mingi Afrika Mashariki, hasa Kenya na Tanganyika. Aliandika kuhusu mazingira ya nchi hizo, kuhusu watu na tamaduni zao, na kuhusu wanyama katika mbuga za hifadhi, kwa kiwango cha ustadi ambacho sisi wenyewe hatujakifikia. Alituachia hazina kubwa katika maandishi yake, hazina ambayo hatujafunguka macho na kuitumia.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...