Showing posts with label u-Islam. Show all posts
Showing posts with label u-Islam. Show all posts

Thursday, May 18, 2017

Vitabu Nilivyonunua Jana

Jana nilinunua vitabu vitatu katika duka la vitabu la chuoni St. Olaf. Viwili, Two Years Eight Months and Twenty-Eight Nights cha Salman Rushdie na A Strangeness in my Mind cha Orhan Pamuk, niliviona juzi. Cha tatu, Why Homer Matters, kilichotungwa na Adam Nicolson, nilikiona hiyo hiyo jana.

Nilipoingia dukani, nilikumbuka makala niliyoisoma juzi usiku, kuhusu vitabu halisi na vitabu pepe. Makala hii, sawa na nyingine nyingi, inatafakari iwapo vitabu vya jadi vitasalimika katika himaya hii ya vitabu pepe. Lakini inahitimisha kuwa hakuna ushahidi kuwa vitabu vya jadi vitapoteza mvuto au kufifia.

Mimi ni mmoja wa wale ambao hatujabadilika. Bado tumezoea vitabu halisi, yaani vitabu vya jadi, na ndio maana sisiti kuvinunua, wala sisiti kuelezea tabia yangu hiyo. Hapa nitaelezea kifupi kwa nini nimenunua vitabu hivi vitatu.

Kitabu cha Salman Rushdie kilinivutia kwa sababu ya umaarufu wa mwandishi huyu. Bila shaka wengi watakumbuka kitabu chake, Satanic Verses, ambacho kilipigwa marufuku katika nchi nyingi kwa madai kuwa kinaukashifu u-Islam. Ayatollah Khomeini wa Iran alitangaza fatwa kuwa Salman Rushdie anapaswa kuuawa.

Duniani kote, na hata miongoni mwa wa-Islam wenyewe hukumu hii ilizua mjadala. Baadhi walisema kuwa fatwa haikupaswa kutolewa kabla ya Salman Rushdie kupewa fursa ya kujieleza na kukiri kosa lake. Watu wengine walisema kuwa zogo hili lilimpa Salman Rushdie umaarufu ambao hakustahili kwa kigezo cha ubora wa uandishi wake.

Ninavyo baadhi vitabu vya Salman Rushdie, kikiwemo hiki cha Satanic Verses. Nimemewahi kufundisha riwaya yake maarufu, Midnight's Children. Ninavutiwa na ubunifu wake katika kuelezea mambo, na uhodari wake wa kutumia lugha. Uandishi wake unasisimua na kufikirisha.

Orhan Pamuk ni mwandishi ambaye nimewahi kumtaja katika blogu hii. Nina vitabu vyake kadhaa, na nimekuwa na hamu ya kuvisoma, ila bado sijapata wasaa. Huyu amenivutia si tu kwa kuwa alipata tuzo ya Nobel, bali pia kwa sababu ninafahamu kiasi fulani kuhusu fasihi simulizi ya Uturuki, kama vile hadithi za Nasreddin Hodja na Dede Korkut.

Why Homer Matters nimekipenda kwa kuwa taaluma ya tendi nimeipenda na kuishughulikia kwa miaka mingi. Homer, ingawa taarifa zake hazijulikani vizuri, ndiye anayehusishwa na tendi maarufu za u-Griki ya kale, The Iliad na The Odyssey. Kwa kuangalia juu juu, niliona kuwa mwandishi wa Why Homer Matters ana uwezo mkubwa wa kuelezea masuala ya Homer na hizi tendi.

Saturday, April 29, 2017

Tamasha la Mataifa Limefana Rochester, Minnesota.

Leo tamasha la mataifa limefanyika mjini Rochester, Minnesota. Niliweka tangazo la tamasha hili katika blogu hii. Binti yangu Zawadi na mimi tulishiriki. Ni mwendo wa saa moja kutoka hapa Northfield ninapoishi.

Tulipanga vitabu vyangu na machapisho mengine mezani, tukatundika ukutani bendera ya Tanzania ambayo nilinunua siku zilizopita. Saa nne ilipotimia, ambayo ndiyo saa ya kufunguliwa tamasha, watu walianza kuja. Na hapo kwenye meza yetu tulianza kutembelewa na watu tangu dakika zile za mwanzo. Tuliongea nao, tukajibu masuali kuhusu vitabu hivyo na mambo mengine mengi, nao wakatueleza mambo mbali mbali.


Baada ya nusu saa hivi, ilianza shughuli ya kupeperusha bendera. Watu walielekezwa zilipowekwa bendera ili wachukue bendera ya nchi yao na kujiunga katika maandamano wakiwa wamebeba bendera. Nilikwenda nikaikuta bendera ya Tanzania, nikaibeba katika maandamano.

Tuliendelea kuongea na watu wa mataifa mbali mbali hapo kwenye meza yetu, tukapata pia fursa ya kuzunguka kwenye meza za wengine, na kupiga picha. Kwa namna ya pekee ninakumbuka tulivyozungumza na mama mmoja Mmarekani, kuhusu tofauti za tamaduni akatueleza yaliyomkuta Japani. Mila na desturi alizozizoea Marekani ziliwashangaza wenyeji. Nasi tulimweleza yanayotokea pale wa-Afrika wanapokuwa na wa-Marekani, kama nilivyoelezea katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Ninakumbuka pia nilivyoongea na mama anayeonekana pichani hapa kushoto amevaa hijab. Nilikumbuka kuwa nilimwona katika tamasha mwaka jana, ila hatukufahamiana. Jana tulipata hiyo fursa, mezani pake, ambapo aliweka machapisho ya ki-Islam, kama vile The Message of the Qur'an cha Muhammad Asad, Who Speaks for Islam cha John L. Esposito na Dalia Mogahed, na Wisdom for Life & The Afterlife: A Selection of Prophet Mohammad's Sayings, ambavyo vyote ninavyo.

Nilimwambia kuwa mimi ni mwalimu katika chuo cha St. Olaf; nimetunga kozi, "Muslim Women Writers." na sababu za kuitunga. Naye alinielezea kuhusu kipindi anachoendesha kiitwacho Faith Talk Show, tukakubaliana nije kuhojiwa katika kipindi hicho siku zijazo.

Baada ya kurejea kutoka kwenye tamasha, nimeangalia mtandaoni, nikaona taarifa za mama huyu kama vile hii hapa. Ninawazia kumwalika darasani kwangu nitakapofundisha tena kozi yangu.

Muda wote wa tamasha kulikuwa na vikundi vya burudani jukwaani na pia vyakula vya nchi mbali mbali. Ninaleta hapa baadhi ya picha za tamasha.





Wednesday, January 18, 2017

Vitabu Nilivyojipatia Leo

Leo, baada ya wiki nyingi kidogo, nimeona nirejee tena kwenye mada ambayo nimekuwa nikiiandikia tena na tena katika blogu hii. Ni juu ya vitabu ninavyojipatia, iwe ni kwa kununua, au kwa namna nyingine.

Leo asubuhi, kama kawaida, nilienda chuoni St. Olaf kufundisha. Nilipoingia katika jengo la maktaba, ambamo pia ni makao ya idara yangu ya ki-Ingereza, nilipita kwenye meza ambapo huwekwa vitabu na makabrasha kwa ajili ya yeyote anayehitaji. Niliona meza imejaa vitabu kuliko siku nyingine yoyote iliyopita, nikaamua kuviangalia.

Niliona kuwa vyote vilikuwa vitabu vya taaluma, hasa masuala ya wanawake na jinsia. Niliamua kujichukulia vitatu, baada ya kuangalia ndani na kuona maelezo ya vitabu hivi. Kitabu kimojawapo ni Sex & Power, kilichotungwa na Susan Estrich. Niliona maelezo kuwa mwandishi alikuwa profesa wa sheria katika Chuo Kikuu cha Harvard na baadaye profesa wa sheria katika Chuo Kikuu cha California ya Kusini. Ameandika vitabu kadhaa na makala mbali mbali. Alikuwa mwanamke wa kwanza kuwa rais wa Harvard Law Review. Huenda msomaji wa taarifa hii utakumbuka kuwa hiki ni cheo ambacho Barack Obama aliwahi kushika. Kutokana na mada ya kitabu, na orodha ya sura zake niliona kuwa kitabu hiki kitanielimisha sana kuhusu nafasi ya wanawake katika jamii.

Kitabu cha pili kilichonivutia kwa namna ya pekee ni Globalization: The Making of World Society, ambacho kimetungwa na Frank J. Lechner. Kama tunavyofahamu, mada ya utandawazi inavuma sana miongoni mwa wanataaluma, wanasiasa, na jamii kwa ujumla. Hata hivi, mitazamo kuhusu nini maana ya utandawazi, chimbuko lake, faida na hasara zake, ni masuala ambayo yanajadiliwa na yamegubikwa na utata.

Mimi mwenyewe, kwa miaka kadhaa, nimetafakari suala la utandawazi, nikilihusisha na tofauti za tamaduni. Nimewahi hata kuendesha warsha kadhaa, nchini Tanzania, katika miji ya Arusha, Dar es Salaam, na Tanga. Kwa hivi, nilipokiona kitabu cha Globalization: The Making of World Society, nilikuwa na hamu ya kukisoma. Hiki kitaongeza idadi ya vitabu vyangu kuhusu utandawazi.

Kitabu cha tatu, Behind the Veil in Arabia: Women in Oman, kilichoandikwa na Unni Wikan, kilinivutia pengine zaidi ya hivi vingine. Nilipoona jina la kitabu hiki, nilikumbuka mara majina ya vitabu vingine, kama vile Beyond the Veil, cha Fatima Mernissi wa Morocco. Suala la wanawake katika nchi za ki-Arabu limeshika nafasi ya pekee kichwani mwangu kutokana na kozi niliyoanzisha na ninaifundisha, "Muslim Women Writers."

Simaanishi, na mtu asidhani, kwamba wa-Arabu wote ni wa-Islam, bali kuna suala la jinsi utamaduni unavyoingiliana na dini kiasi kwamba pamoja na tofauti za dini, kuna mambo kama mila, desturi, na lugha, ambayo yanawaungamisha wa-Arabu.

Katika kufundisha kozi ya "Muslim Women Writers" imedhihirika kuwa vazi kama hijab ni suala la utamaduni zaidi kuliko dini. Qur'an inasema wanawake wajisitiri na wainamishe macho, lakini haisemi wavae nini. Hili ni suala la kila utamaduni, na ndio maana mavazi ya wanawake wa ki-Islam katika tamaduni mbali mbali yanahitilafiana.

Maktaba yangu imetajirika leo kwa kuongezewa vitabu hivi muhimu. Ni raha iliyoje kujipatia hazina kubwa namna hii bila gharama yoyote kwa upande wangu.

Wednesday, October 19, 2016

Nimepata Vitabu Vipya vya Uislam

Leo nimepata vitabu kadhaa vya u-Islam kutoka kwa profesa Nadia Mohamed wa Minneapolis Community and Technical College. Huyu profesa, mzaliwa wa Misri, tulifahamiana mwaka jana. Muhula uliopita nilimwalika kutoa mhadhara katika darasa langu, Muslim Women Writers. Nilimwalika tena, na amekuja leo.


Katika vitabu alivyonipa leo, kuna nakala za Quran, yaani tafsiri tofauti. Kabla, nilikuwa na tafsiri mbili: moja ya Abdallah Yusuf Ali, yenye maelezo ya kina, ambayo nimekuwa nayo kwa miaka mingi, na ya pili aliyonipa Profesa Nadia Mohamed alipotembelea darasa langu muhula uliopita, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Lakini leo, amenipa The Message of the Quran, iliyotafsiriwa na kufafanuliwa na Muhammad Asad. Humo kuna Quran kwa hati ya ki-Arabu, na hicho ki-Arabu kipo pia kwa hati ya ki-Rumi. Na kuna tafsiri ya ki-Ingereza, pamoja na maelezo ya kina. Nakala ya Abdallah Yusuf Ali ina sura mbili: hati ya ki-Arabu na tafsiri ya ki-Ingereza.

Profesa Nadia Mohammed amenipa nakala zingine mbili za Quran, tafsiri ya Abdallah Yusuf Ali, ila ni tofauti na ile niliyokuwa nayo tangu zamani, kwa kuwa hii ni tafsiri tu bila yale maelezo. Hizi nakala ni vitabu vidogo kwa ukubwa, na kwa hivi ni rahisi kubebwa popote. Zinaonekana pichani hapa kushoto, zikiwa na majalada tofauti.

Kuna uzuri wa kuwa na tafsiri mbali mbali za Quran. Tunaambiwa kwamba ki-Arabu cha Quran ni cha pekee, sio rahisi kukitafsiri kwa lugha yoyote. Maneno yake mengi yana utajiri wa maana na ladha ambao ni mtihani mkavu kwa yeyote anayejaribu kutafsiri. Kutokana na ukweli huo, ambao unahusika pia katika tafsiri ya lugha yoyote, ni bora kusoma tafsiri mbali mbali. Nilimwambia hivyo Profesa Nadia Mohamed, ambaye ni mtaalamu, akaafiki.

















Vitabu vingine alivyonipa ni viwili vidogo vidogo. Kimoja kinaitwa A Brief Illustrated Guide to Understanding Islam na mtunzi ni I.A. Ibrahim. Cha pili ni Wisdom for Life & The Afterlife: A Selection of Prophet Muhammad's Sayings, ambacho ni mkusanyiko wa mafundisho ya Mtume Muhammad, yaliyotafsiriwa na Samir Saikali kwa ki-Ingereza, kutoka ki-Arabu, na kuchapishwa na Islamic Literacy Project.




Tuesday, December 1, 2015

Nilitembelea Duka la Vitabu la Amkal

Tarehe 23 Mei, 2015, nilitembelea duka la vitabu la Amkal mjini Minneapolis, kama nilivyoripoti katika blogu hii. Ni duka la wa-Somali ambalo linauza zaidi vitabu vinavyohusu dini ya ki-Islam. Siku hiyo nilinunua kitabu kiitwacho Jesus: Prophet of Islam. Ninapenda kuongelea, kwa kifupi na wepesi kabisa, mawazo yanayonijia ninapokumbuka ziara yangu katika duka lile.

Jambo la msingi kwamba katika kuishi kwangu hapa Marekani, nimeona jinsi wa-Afrika wa nchi mbali mbali wanavyovithamini vitabu. Kwa mfano, nimewahi kuwaongelea wa-Kenya.

Wa-Somali ni mfano mwingine. Nimekutana na wa-Somali wanaoishi hapa Minnesota ambao wanaandika vitabu. Nimejionea wanavyojitokeza kuwasikiliza waandishi wa vitabu wa ki-Somali. Mfano ni Nuruddin Farah, ambaye huonekana hapa Minnesota mara kwa mara, ingawa makao yake kwa miaka hii ni Afrika Kusini. Wanamheshimu kwa jinsi anavyowakilisha taifa lao katika ulimwengu wa uandishi.

Kwa ujumla, hao wa-Somali ni wakimbizi au wahamiaji. Lakini pamoja na kadhia hiyo, pamoja machungu waliyoyapitia, wameshikilia umuhimu wa vitabu na elimu. Katika vyuo vya hapa Minnesota, kama vile Chuo Kikuu cha Minnesota, Metropolitan State University. Mankato State University, South Central College, na Minneapolis Community and Technical College, wanafunzi wa ki-Somali ni wengi. Wanawekeza katika elimu. Wanajijengea mtaji ambao wataweza kuutumia kwa maendeleo ya nchi yao.

Suala la elimu wanalishughulika kwa namna nyingine pia, kama vile magazeti na vituo vya televisheni. Hali hii nimeiona pia miongoni mwa wa-Afrika wengine, kama vile wa-Kenya na wa-Ethiopia. Kwa kutumia njia hizo, wanazitangaza nchi zao na shughuli zao, kama vile biashara. Ninawaona ni mfano wa kuigwa.

Sunday, September 27, 2015

Tumechangia Kanisa la Venezuela

Leo kanisani kwetu hapa mjini Northfield, kanisa Katoliki, tulikuwa na padri ambaye anatumikia kanisa fulani nchini Venezuela. Huyu padri ni m-Marekani, na kwa miaka yapata arobaini, mapadri wa-Marekani wamekuwa wamisionari katika kanisa hilo la Venezuela. Hata paroko wetu aliwahi kutumikia kanisa hilo kwa miaka mitano. Ananivutia kwa jinsi anavyoijua lugha ya ki-Hispania, na anawahudumia waumini hapa Northfield wanaotumia lugha hiyo.

Huyu padri mgeni alitoa mafundisho mazuri, na katika kuelezea utume wake Venezuela alituhimiza kwa maneno matatu: "Pray, say, pay." Alifafanua kwamba tusali kuwaombea waumini wa kanisa lile la Venezuela, tuwaeleze wengine kuhusu hali halisi na mahitaji ya kanisa lile, na tutoe mchango kulisaidia kanisa lile.

Niliguswa na maelezo yake, nikangojea muda wa kutoa mchango. Kilipopitishwa kijikapu cha mchango, nilikuwa tayari nimekwangua vijihela vilivyokuwemo katika pochi yangu nikavitumbukiza humo. Nilijisikia faraja na furaha kwamba vijihela hivyo vitakuwa na manufaa kwa kanisa lile la Venezuela, hasa kwa kuzingatia kuwa dola, hata zikawa chache, zinakuwa ni hela nyingi kwenye nchi kama Venezuela au Tanzania.

Mimi kama muumini wa dini, naiheshimu dini yangu, na dini zote. Ninafahamu kwamba zote ni njia wanazotumia wanadamu kuelekea kwa Mungu. Ni safari, kama safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro. Kuna njia kadhaa za kufikia kileleni Kilimanjaro. Na itakuwa ni wendawazimu kwa watu wanaochukua njia tofauti kuanza kugombana na kupigana hadi kuuana kwa msingi wa tofauti za njia wanazochukua. Kwa mtazamo wangu, ni wendawazimu kwa watu wa dini mbali mbali kubezana au kugombana.

Ninaziheshimu nyumba za ibada za kila dini. Niliwahi kuelezea katika blogu hii nilivyozuru nyumba za ibada za wa-Hindu, nchini India. Leo nimechangia kanisa lililoko Venezuela. Lakini sibagui. Kuna wakati niliona taarifa kuwa wa-Islam wa sehemu fulani Tanzania walikuwa wanachangisha fedha za kukarabatia msikiti wao. Nilipeleka mchango wangu, kwa moyo mkunjufu, ingawa mimi si mu-Islam bali m-Katoliki. Nitaendelea kufanya hivyo.

Ninachojali ni kuwa wanadamu wote wameumbwa na Mungu, na Mungu hana ubaguzi, kama nilivyoandika katika blogu hii. Ninafurahi kumiliki blogu, kitu ambacho kinaniwezesha kueneza mawazo yangu na kupambana na mawazo ambayo nayaona ni sumu, hata kama yanaenezwa kwa jina la dini.

Thursday, June 11, 2015

Kesi ya Raif Badawi: Mwanablogu wa Saudi Arabia

Raif Badawi ni mwanablogu wa Saudi Arabia ambaye anafahamika sana duniani kutokana na kuhukumiwa kifungo cha miaka kumi gerezani na viboko 1000. Alihukumiwa kwa kile kilichoitwa kuitukana dini ya u-Islam. Amekaa gerezani miaka miwili na tayari alishapigwa viboko 50 nje ya msikiti mjini Jeddah. Adhabu hiyo si nyepesi; inaweza kusababisha kifo.

Watu wengi duniani wanalaani hukumu hiyo. Wengi hawaoni ni kwa vipi Raif Badawi ameutukana u-Islam. Wengi wamechukizwa na hukumu hiyo kwa kuwa ni hujuma dhidi ya uhuru wa kutoa mawazo.

 Mawazo ya Raif Badawi yaliyosababisha hukumu dhidi yake ni ya kawaida sana kwa vigezo vyetu wa-Tanzania na wengine duniani. Lakini wahusika nchini Saudi Arabia wameendelea kusisitiza kuwa Raif Badawi anastahili hukumu hiyo. Kuna tetesi kuwa huenda akashtakiwa upya ili apewe hukumu kali zaidi, kukatwa kichwa, hukumu ambayo hutekelezwa sana Saudi Arabia.

Kesi ya Raif Badawi imeibua masuala ya ukiukwaji wa haki za binadamu nchini Saudi Arabia. Kuna mengi yanayoongelewa. Kwa mfano, ni marufuku Saudi Arabia kutoa mawazo yanayopingana na yale ya watawala na viongozi wa dini. Ni marufuku kwa watu wasio wa-Islam kujenga nyumba za ibada zao, kama vile makanisa, katika ardhi ya Saudi Arabia. Ni marufuku kuhubiri dini tofauti na u-Islam. Ni marufuku kwa wanawake kuendesha gari. Ni marufuku kwa wanawake kusafiri bila kibali cha mume au ndugu wa kiume.

Kuna kampeni kubwa sehemu mbali mbali duniani kulaani hukumu dhidi ya Raif Badawi. Sisi wanablogu wa Tanzania tunasimama wapi? Ni vema kukumbushana kuwa ukiona mwenzako ananyolewa, wewe tia maji.

Saturday, March 16, 2013

Dunia Bila U-Islam

Wiki hii nimenunua vitabu kadhaa. Kimojawapo ni A World without Islam, kilichotungwa na Graham E. Fuller. Na hiki ndicho kitabu ninachotaka kukiongelea hapa.

Nilipokiona kitabu hiki katika duka la vitabu la hapa chuoni St. Olaf, nilivutiwa na jina la kitabu, nikajiwa na duku duku ya kufahamu ni kitabu cha aina gani, na kinaongelea nini. Dhana ya dunia isiyokuwa na u-Islam ilikuwa ngeni kwangu, kwa kuzingatia jinsi dunia ya leo ilivyo na jinsi u-Islam ulivyo na nguvu duniani. Dunia bila u-Islam ingekuwaje?

Ninahisi kuwa hadi hapo, wewe msomaji nawe tayari umeshapata mawazo au hisia fulani. Kama wewe ni mu-Islam, labda umeshaanza kuhisi kuwa kitabu hiki kimeandikwa na adui wa u-Islam. Labda unahisi kuwa kitabu hiki ni mwendelezo wa vita vya Msalaba ("Crusades"). Labda unahisi kuwa ni njama za makafiri dhidi ya u-Islam. Na kama wewe ni mmoja wa wale wanaoitwa wa-Islam wenye msimamo mkali, labda tayari unatamani yafanyike maandamano kulaani kitabu hiki, kama yalivyofanyika maandamano dhidi ya kitabu cha Satanic Verses cha Salman Rushdie.

Kama wewe si mu-Islam, labda ni m-Kristu, huenda una hisia zako pia. Na mimi kama m-Kristu nilikuwa na hisia zangu. Kusema kweli, nilipokiona hiki kitabu, nilihisi kuwa kitakuwa kimeandikwa na mtu ambaye ana ugomvi na u-Islam, na kwamba labda anataka kutueleza kuwa dunia ingekuwa bora endapo u-Islam haungekuwepo.

Hakuna ubaya kuwa na hisia au duku duku, ili mradi mtu uwe na tabia ya kufuatilia ili kujua ukweli. Unapokiona kitabu kama hiki, na hujakisoma, wajibu wako ni kukisoma ili ujue kinasema nini. Sio jambo jema katika taaluma kwa mtu kukumbana na kitu usichokifahamu, halafu ukaendelea na maisha yako bila duku duku ya kujua. Dukuduku hii huitwa "intellectual curiosity" kwa ki-Ingereza.

Duku duku hii ndio inayomtofautisha mtu aliyeelimika na yule asiyeelimika. Mtu aliyeelimika ni yule anayejitambua kuwa upeo wake ni finyu, na kuwa anawajibika kutafuta elimu muda wote. Nimeanza kukisoma kitabu hiki, na tayari nimegundua kuwa anachosema mwandishi si kile nilichodhania, ni tofauti kabisa na kile ambacho labda nawe ulidhania.

Kati ya hoja zake muhimu ni hizi: a) Vita vya Msalaba ("Crusades") vingekuwepo kwa vyo vyote vile, hata bila u-Islam. b) Ukristu wa ki-Orthodox wa Mashariki ungeinukia kuwa na nguvu sana na ungepambana na nchi za Magharibi. c) "Magaidi" wanaojilipua kwa mabomu wangekuwepo, kwani ingawa wengi wanahusisha jambo hili na wa-Islam, ukweli ni kuwa walioanzisha jambo hili ni Tamil Tigers, ambao ni wa-Hindu, kule Sri Lanka.

Inavyoonekana, hiki ni kitabu kimojawapo ambacho kinaelimisha sana. Kinatoa tahadhari mbali mbali kwa wale wanaouwazia u-Islam kwa ubaya.  Kwenye jalada lake, kitabu kimesifiwa sana na maprofesa Akbar S. Ahmed, Reza Aslan, na John L. Esposito, ambao ni wataalam wakubwa wa masuala hayo. Napendekeza tukisome kitabu hiki, kama ninavyopendekeza vitabu vingine katika blogu hii.

Friday, April 8, 2011

Nasoma Vitabu vya Dini Mbali Mbali

Kati ya mambo ya manufaa kabisa maishani ni kujielimisha. Nami husoma vitabu kila siku kama njia mojawapo ya kujielimisha. Pamoja na vitabu vya taaluma mbali mbali, hadithi, mashairi, na kadhalika, hupenda kusoma vitabu vya dini.

Nina vitabu vya dini mbali mbali, hasa u-Hindu, u-Islam, na u-Kristu. Nina vitabu kama vile Bhagavad-Gita, Upanishads, Quran, na Biblia. Nina vitabu kuhusu watu muhimu wa dini hizo, kama vile Yesu Kristu, Muhammad na Swami Vivekananda. Vyote hivyo ninavipitia, angalau mara moja moja.

Mimi ni m-Katoliki; habari ndio hiyo. Kwa msingi wa dini yangu, nawajibika kuwajali na kuwapenda wanadamu wote. Yesu alifafanua amri kuu kuliko zote kuwa ni kumpenda Mungu kwa uwezo wetu wote, akili yetu yote, na nafsi yetu yote; kumpenda jirani yetu vile vile, na kuwapenda maadui zetu vile vile. Huu ndio mtihani aliotuachia Yesu.

Sasa kwa vile ukweli ndio huo, ninajiuliza ni njia ipi ya kufuata ili niweze kufaulu mtihani huo. Nimeamua kuwa ni wajibu kujielimisha: kuwafahamu wanadamu, maisha yao, fikra zao, na imani zao. Ni wajibu kuzifahamu dini zao. Naamini tungechangia kujenga mahusiano mema duniani iwapo tungekuwa na utamaduni huu wa kuviheshimu na kuvisoma vitabu vya dini zetu na vile vya dini za wenzetu. Ni muhimu vile vile kusoma vitabu vya wale wasioamini dini, na kuwaheshimu.

Sunday, February 13, 2011

Kitabu Kuhusu Mtume Muhammad

Kati ya vitabu ninavyosoma wakati huu ni Muhammad: A Biography of the Prophet, kilichoandikwa na Karen Armstrong. Ni kitabu murua kwa jinsi kinavyoelezea mazingira aliyoishi Mtume Muhammad na harakati alizopitia katika kutimiza majukumu yake kama Mtume.

Kitabu hiki kinagusa na kuelimisha sana sio tu kuhusu historia ya u-Islam, bali pia kuhusu upekee wa Mtume Muhammad, kama Karen Armstrong anavyosema:

If we could view Muhammad as we do any other important historical figure we would surely consider him to be one of the greatest geniuses the world has known
(uk.52). (Tafsiri yangu: Kama tungemtazama Muhammad kwa namna tunayowatazama watu wengine muhimu katika historia, ni wazi tungemtambua kama mmoja wa watu wenye vipaji vya ajabu kabisa ambao dunia imepata kuwafahamu).

Karen Armstrong ni maarufu kwa msimamo wake kuhusu u-Islam. Anaelezea sana historia ya zile anazoziita hisia potofu kuhusu u-Islam na zilivyoanza na kuenea. Lakini, pamoja na kutafiti na kuandika sana kuhusu u-Islam, Karen Armstrong ni mtafiti wa dini zingine pia, kama vile u-Kristu u-Juda, na u-Buddha. Ni mmoja wa watu wanaoongoza hapa duniani kwa umakini wa kuandika kuhusu dini.

Pamoja na kusoma kitabu cha Muhammad na kufuatilia maandishi mengine ya Karen Armstrong, na pamoja na kufuatilia mihadhara na mahojiano aliyotoa sehemu mbali mbali za dunia, nafuatilia pia maandishi na matamshi ya wengine kuhusu mchango wa Karen Armstrong. Nimebaini kuwa kuna malumbano kuhusu mchango wake, ambalo ni jambo la kutegemewa katika taaluma.

Kitabu cha Muhammad ni kizuri na muhimu sana. Nafurahi kukisoma, kwani kinanifungulia milango ya kuyafahamu maisha na mchango wa mtu ambaye ametoa mchango mkubwa sana duniani. Ni kitabu muhimu kwa yeyote mwenye nia ya kumwelewa Mtume Muhammad na kuuelewa u-Islam.

Karen Armstrong, ambaye alikuwa sista katika Kanisa Katoliki, ambalo ndilo dhehebu langu, anatuonyesha mfano mzuri, kwa kujibidisha katika kuzifahamu dini za wengine. Naamini kuwa iwapo sote tungefanya hivyo, kungekuwa na maelewano mazuri baina ya watu wa dini mbali mbali.

Wednesday, February 2, 2011

Kauli ya Mufti Simba Kuhusu wa-Islam na Elimu

Nimesoma kwa furaha taarifa kuwa Mufti wa Tanzania, Shekhe Mkuu Issa Shaban Simba, amewataka wa-Islam Tanzania wajibidishe na elimu ili kujikomboa kimaisha. Amenukuliwa akisema, "Huu ni muda mwafaka kwa waislam kuanza kujikita na kukazania zaidi suala la elimu, na si kubaki kulialia pekee kuomba kuchaguliwa na kupewa vyeo serikalini, hivyo tuchangamke tusiendelee kubaki nyuma tupige hatua kama wenzetu." Soma taarifa hii hapa.

Nilikuwa njiani kuandika makala kuhusu suala la elimu katika historia ya u-Islam, ili kuiweka katika blogu hii. Baadhi ya mambo niliyopangia kusema ni kwamba u-Islam, tangu mwanzo, ulihimiza suala la elimu katika taaluma mbali mbali. Mtume Muhammad alisisitza suala hilo na waumini wakafuata kwa makini. Anayosema Mufti Simba ndio ukweli kwa mujibu wa dini ya ki-Islam.

Makala yangu inakuja. Kwa leo napenda tu kusema kuwa msisitizo wa Mufti Simba kuhusu elimu unatuhusu sisi wote, si wa-Islam peke yao. Ninaandika sana kuhusu suala hilo kwenye blogu na sehemu zingine, kama vile kitabu cha CHANGAMOTO, nikilalamika kuhusu uvivu uliokithiri miongoni mwa wa-Tanzania katika suala la elimu. Kwa hivi namwunga mkono na kumpongeza Mufti Simba kwa kusimama kidete kuongelea suala hilo. Yeye kama kiongozi wa wa-Islam amewataja wao, lakini ukweli ni kuwa nasaha zake zina manufaa kwa wa-Tanzania wote.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...