Showing posts with label wa-Hindu. Show all posts
Showing posts with label wa-Hindu. Show all posts

Friday, July 3, 2015

Mungu (Allah) Hana Ubaguzi

Blogu yangu hii ni uwanja huru kwa fikra na mijadala, ikiwemo mijadala kuhusu dini. Leo, kwa kifupi na lugha rahisi, napenda kuibua suala la dini na ubaguzi.

Laiti sisi tunaosema tuna dini tungetambua kuwa Mungu hana ubaguzi. Mungu, ambaye kulingana na tofauti za lugha, huitwa kwa majina mbali mbali, anathibitisha jinsi anavyowapenda wanadamu, wa dini zote, na wasio na dini.

Mungu anateremsha baraka zake bila ubaguzi. Anawapa uzazi watu wenye dini, sawa na wasio na dini. Wa-Islam wanazaa, wa-Kristu wanazaa, wa-Hindu wanazaa, na wa dini zingine kadhalika. Wasio na dini wanazaa.

Mungu anateremsha mvua kuotesha mbegu katika mashamba ya wa-Islamu, ya wa-Hindu, ya wa-Kristu, na ya wengine, hata wasio na dini. Kuku wa mu-Islam anataga mayai na kuangua vifaranga, sawa na kuku wa m-Kristu, sawa na kuku wa asiye na dini. Mungu hana ubaguzi katika kuteremsha neema zake.

Sasa basi, kwa nini wanadamu wengi wanaosema wana dini ni wabaguzi? Kwa nini wanatumia kigezo cha dini kujifanya wao ni bora kuliko wengine? Wanapobaguana namna hii, wanafuata njia ya Mungu au ya shetani?

Wednesday, April 3, 2013

Nitafundisha "Midnight's Children," Kitabu cha Salman Rushdie

Nimefundisha fasihi ya India mara nyingi sana, hapa Chuoni St. Olaf, kuanzia mwaka 1991. Nimefundisha maandishi ya watu kama Rabindranath Tagore, Mulk Raj Anand, Raja Rao, R.K. Narayan, Ruth Prawer Jhabvala, Nayantara Sahgal, Anita Desai, na Kamala Markandaya.

Sijawahi kufundisha maandishi ya Salman Rushdie, ambaye ni mwandishi maarufu sana, sambamba na hao niliowataja. Suali moja ambalo nimejiuliza miaka ya karibuni ni je, utafundishaje fasihi ya India bila kumjumlisha Salman Rushdie? Utaachaje kufundisha kitabu cha Rushdie kiitwacho Midnight's Children, ambacho kilipata tuzo maarufu ya Booker?

Mwezi Juni hadi Julai nitafundisha kozi ya wiki sita, katika somo liitwalo "Post-colonial Literature." Nimeamua kufundisha kitabu hiki cha Rushdie. Ni kitabu muhimu kwa namna nyingi, sio tu kwa upande wa sanaa, bali pia kwa jinsi kinavyojumlisha masuala na dhamira mbali mbali ambazo ni muhimu katika fasihi ya India. Ni kitabu chenye upekee kihistoria na kisiasa kwa jinsi kilivyofungamana na tukio moja muhimu sana katika karne ya ishirini, yaani kupatikana kwa uhuru kwa nchi iitwayo India.

Tukio hili la uhuru wa India lilitokea mwaka 1947. Ila kwa bahati mbaya sana, ni tukio lililoandamana na mgawanyiko uliosababisha kuwepo kwa nchi mbili, yaani India na Pakistan. Ni tukio lililoandamana na uhasama, mauaji na ukimbizi wa idadi kubwa sana ya watu, mtafaruku ambao ulikuwa baina ya wa-Hindu na wa-Islam. Tukio hili linakumbukwa kwa majonzi, na limeelezwa sana na waandishi kutoka India na Pakistan.

Kwa vile kitabu cha Midnight's Children kina kurasa nyingi sana, nimeona kuwa nisiweke vitabu vingi katika kozi hii ya wiki sita.  Nawazia kutumia vitabu vingine viwili au vitatu, ambavyo navyo vina kurasa nyingi. Nimeamua tu kutumia haya mavitabu makubwa nione itakuwaje. Kimoja ninachowazia sana ni Half of a Yellow Sun, cha Chimamanda Ngozi Adichie, wa Nigeria. Kingine ni Abyssinian Chronicles cha Moses Isegawa wa Uganda. Bado nina muda wa kufikia uamuzi wa mwisho. Huenda nikatumia The Famished Road, cha Ben Okri, au Wizard of the  Crow, cha Ngugi wa Thiong'o. Uamuzi kamili nitafikia katika siku kadhaa zijazo.

Saturday, March 16, 2013

Dunia Bila U-Islam

Wiki hii nimenunua vitabu kadhaa. Kimojawapo ni A World without Islam, kilichotungwa na Graham E. Fuller. Na hiki ndicho kitabu ninachotaka kukiongelea hapa.

Nilipokiona kitabu hiki katika duka la vitabu la hapa chuoni St. Olaf, nilivutiwa na jina la kitabu, nikajiwa na duku duku ya kufahamu ni kitabu cha aina gani, na kinaongelea nini. Dhana ya dunia isiyokuwa na u-Islam ilikuwa ngeni kwangu, kwa kuzingatia jinsi dunia ya leo ilivyo na jinsi u-Islam ulivyo na nguvu duniani. Dunia bila u-Islam ingekuwaje?

Ninahisi kuwa hadi hapo, wewe msomaji nawe tayari umeshapata mawazo au hisia fulani. Kama wewe ni mu-Islam, labda umeshaanza kuhisi kuwa kitabu hiki kimeandikwa na adui wa u-Islam. Labda unahisi kuwa kitabu hiki ni mwendelezo wa vita vya Msalaba ("Crusades"). Labda unahisi kuwa ni njama za makafiri dhidi ya u-Islam. Na kama wewe ni mmoja wa wale wanaoitwa wa-Islam wenye msimamo mkali, labda tayari unatamani yafanyike maandamano kulaani kitabu hiki, kama yalivyofanyika maandamano dhidi ya kitabu cha Satanic Verses cha Salman Rushdie.

Kama wewe si mu-Islam, labda ni m-Kristu, huenda una hisia zako pia. Na mimi kama m-Kristu nilikuwa na hisia zangu. Kusema kweli, nilipokiona hiki kitabu, nilihisi kuwa kitakuwa kimeandikwa na mtu ambaye ana ugomvi na u-Islam, na kwamba labda anataka kutueleza kuwa dunia ingekuwa bora endapo u-Islam haungekuwepo.

Hakuna ubaya kuwa na hisia au duku duku, ili mradi mtu uwe na tabia ya kufuatilia ili kujua ukweli. Unapokiona kitabu kama hiki, na hujakisoma, wajibu wako ni kukisoma ili ujue kinasema nini. Sio jambo jema katika taaluma kwa mtu kukumbana na kitu usichokifahamu, halafu ukaendelea na maisha yako bila duku duku ya kujua. Dukuduku hii huitwa "intellectual curiosity" kwa ki-Ingereza.

Duku duku hii ndio inayomtofautisha mtu aliyeelimika na yule asiyeelimika. Mtu aliyeelimika ni yule anayejitambua kuwa upeo wake ni finyu, na kuwa anawajibika kutafuta elimu muda wote. Nimeanza kukisoma kitabu hiki, na tayari nimegundua kuwa anachosema mwandishi si kile nilichodhania, ni tofauti kabisa na kile ambacho labda nawe ulidhania.

Kati ya hoja zake muhimu ni hizi: a) Vita vya Msalaba ("Crusades") vingekuwepo kwa vyo vyote vile, hata bila u-Islam. b) Ukristu wa ki-Orthodox wa Mashariki ungeinukia kuwa na nguvu sana na ungepambana na nchi za Magharibi. c) "Magaidi" wanaojilipua kwa mabomu wangekuwepo, kwani ingawa wengi wanahusisha jambo hili na wa-Islam, ukweli ni kuwa walioanzisha jambo hili ni Tamil Tigers, ambao ni wa-Hindu, kule Sri Lanka.

Inavyoonekana, hiki ni kitabu kimojawapo ambacho kinaelimisha sana. Kinatoa tahadhari mbali mbali kwa wale wanaouwazia u-Islam kwa ubaya.  Kwenye jalada lake, kitabu kimesifiwa sana na maprofesa Akbar S. Ahmed, Reza Aslan, na John L. Esposito, ambao ni wataalam wakubwa wa masuala hayo. Napendekeza tukisome kitabu hiki, kama ninavyopendekeza vitabu vingine katika blogu hii.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...