Showing posts with label Rushdie. Show all posts
Showing posts with label Rushdie. Show all posts

Friday, September 5, 2014

Leo Nimeanza Tena Kufundisha

Baada ya kuumwa kwa miezi mingi, na kuwa katika likizo ya matibabu, leo nimeanza tena kufundisha. Hali yangu inaendelea kuimarika, na ingawa naendelea na matibabu kidogo kidogo, madaktari wameridhia ombi langu kuwa nirudi darasani. Wameniwekea sharti kuwa nisibebe mzigo mkubwa wa kozi za kufundisha, na nisihusishwe na shughuli nyingine ambazo walimu huzifanya, kama vile ushiriki katika kamati mbali mbali na mikutano. Hiyo picha hapa kushoto nimejipiga mwenyewe leo, baada ya kutoka darasani.

Hali itakuwa hiyo kwa muhula mzima, ambao umeanza leo, na utamalizika katikati ya mwezi Desemba. Ninafundisha kozi mbili, ya kwanza ni "South Asian Literature," na ya pili ni "Writing." Katika hiyo kozi ya kwanza, ambayo niliitunga miaka michache iliyopita, nafundisha riwaya kutoka India, Pakistan, na Sri Lanka. Riwaya hizo ni, Untouchable, iliyoandikwa na Mulk Raj Anand (India); Twilight in Delhi, iliyoandikwa na Ahmed Ali (India); The Crow Eaters, iliyoandikwa na Bapsi Sidhwa (Pakistan); Shalimar the Clown, iliyoandikwa na Salman Rushdie (India); na Reef, iliyoandikwa na Romesh Gunesekera (Sri Lanka).

Ninapangia kufundisha pia mashairi kutoka katika nchi hizo. Kwa wakati huu, katika kujiandaa, ninasoma kitabu cha mashairi ya Michael Ondaatje kiitwacho The Cinnamon Peeler. Michael Ondaatje alizaliwa Sri Lanka, ila anaishi Canada. Ninafanya pia uchunguzi wa vitabu vya mashairi ambayo nitaweza kuyatumia. Kila ninapofundisha kozi hii, nabadilisha, kwa kiasi fulani, vitabu au waandishi.

Fasihi ya hiyo sehemu ya dunia imejengeka katika historia, siasa, dini, tamaduni, na harakati za watu wa kule tangu miaka elfu tano au zaidi iliyopita hadi kwenye kipindi cha ukoloni, na baada ya kupata uhuru. Waandishi wengi wa India na Pakistan, kwa mfano, wanaelezea janga kubwa lililotokea kabla tu ya kupata uhuru na wakati nchi ilipogawanyika na kuwa nchi hizi mbili, mwaka 1947.

Katika kozi ya "Writing," ninafundisha uandishi bora wa ki-Ingereza. Kadiri miaka ilivyokwenda, nami kujijengea uzoefu zaidi na zaidi wa kufundisha kozi hii, nimekuwa nikitafuta mbinu mpya za kufundisha. Leo nimewaambia wanafunzi kuwa, tofauti na miaka yote iliyopita, na tofauti na wanavyofanya waalimu wengine, muhula huu tutatumia vitabu viwili tu. Kitabu kimoja ni The Trickster, kilichoandikwa na Paul Radin, na kingine ni The Elements of Style, kilichoandikwa na William Strunk Jr. na E.B. White.

Lengo langu katika hii kozi ya uandishi ni kuwafundisha kwanza kabisa namna ya kuandika sentensi bora kabisa ya ki-Ingereza, kama alivyoelekeza mwandishi maarufu Ernest Hemingway, na baada ya hapo tutaendelea hadi kuweza kuandika insha bora kabisa. Nimewaeleza wanafunzi kwamba uandishi bora ni jambo la lazima kwa mafanikio maishani mwao, nikatoa mifano mbali mbali ya namna watakavyohitaji uwezo wa kuandika ipasavyo. Wameona uzito wa hoja na mifano niliyotoa.

Nimefurahi kuwa nimefikia hali ya kuweza kuingia tena darasani, nikizingatia hali yangu kiafya ilivyokuwa mbaya kabla sijalazwa hospitalini. Kwa mara nyingine tena, namshukuru Mungu, na nawashukuru madaktari na wauguzi, familia yangu, marafiki, na wote wanaonitakia mema. Mungu awabariki wote.

Wednesday, April 3, 2013

Nitafundisha "Midnight's Children," Kitabu cha Salman Rushdie

Nimefundisha fasihi ya India mara nyingi sana, hapa Chuoni St. Olaf, kuanzia mwaka 1991. Nimefundisha maandishi ya watu kama Rabindranath Tagore, Mulk Raj Anand, Raja Rao, R.K. Narayan, Ruth Prawer Jhabvala, Nayantara Sahgal, Anita Desai, na Kamala Markandaya.

Sijawahi kufundisha maandishi ya Salman Rushdie, ambaye ni mwandishi maarufu sana, sambamba na hao niliowataja. Suali moja ambalo nimejiuliza miaka ya karibuni ni je, utafundishaje fasihi ya India bila kumjumlisha Salman Rushdie? Utaachaje kufundisha kitabu cha Rushdie kiitwacho Midnight's Children, ambacho kilipata tuzo maarufu ya Booker?

Mwezi Juni hadi Julai nitafundisha kozi ya wiki sita, katika somo liitwalo "Post-colonial Literature." Nimeamua kufundisha kitabu hiki cha Rushdie. Ni kitabu muhimu kwa namna nyingi, sio tu kwa upande wa sanaa, bali pia kwa jinsi kinavyojumlisha masuala na dhamira mbali mbali ambazo ni muhimu katika fasihi ya India. Ni kitabu chenye upekee kihistoria na kisiasa kwa jinsi kilivyofungamana na tukio moja muhimu sana katika karne ya ishirini, yaani kupatikana kwa uhuru kwa nchi iitwayo India.

Tukio hili la uhuru wa India lilitokea mwaka 1947. Ila kwa bahati mbaya sana, ni tukio lililoandamana na mgawanyiko uliosababisha kuwepo kwa nchi mbili, yaani India na Pakistan. Ni tukio lililoandamana na uhasama, mauaji na ukimbizi wa idadi kubwa sana ya watu, mtafaruku ambao ulikuwa baina ya wa-Hindu na wa-Islam. Tukio hili linakumbukwa kwa majonzi, na limeelezwa sana na waandishi kutoka India na Pakistan.

Kwa vile kitabu cha Midnight's Children kina kurasa nyingi sana, nimeona kuwa nisiweke vitabu vingi katika kozi hii ya wiki sita.  Nawazia kutumia vitabu vingine viwili au vitatu, ambavyo navyo vina kurasa nyingi. Nimeamua tu kutumia haya mavitabu makubwa nione itakuwaje. Kimoja ninachowazia sana ni Half of a Yellow Sun, cha Chimamanda Ngozi Adichie, wa Nigeria. Kingine ni Abyssinian Chronicles cha Moses Isegawa wa Uganda. Bado nina muda wa kufikia uamuzi wa mwisho. Huenda nikatumia The Famished Road, cha Ben Okri, au Wizard of the  Crow, cha Ngugi wa Thiong'o. Uamuzi kamili nitafikia katika siku kadhaa zijazo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...