Showing posts with label India. Show all posts
Showing posts with label India. Show all posts

Wednesday, April 3, 2013

Nitafundisha "Midnight's Children," Kitabu cha Salman Rushdie

Nimefundisha fasihi ya India mara nyingi sana, hapa Chuoni St. Olaf, kuanzia mwaka 1991. Nimefundisha maandishi ya watu kama Rabindranath Tagore, Mulk Raj Anand, Raja Rao, R.K. Narayan, Ruth Prawer Jhabvala, Nayantara Sahgal, Anita Desai, na Kamala Markandaya.

Sijawahi kufundisha maandishi ya Salman Rushdie, ambaye ni mwandishi maarufu sana, sambamba na hao niliowataja. Suali moja ambalo nimejiuliza miaka ya karibuni ni je, utafundishaje fasihi ya India bila kumjumlisha Salman Rushdie? Utaachaje kufundisha kitabu cha Rushdie kiitwacho Midnight's Children, ambacho kilipata tuzo maarufu ya Booker?

Mwezi Juni hadi Julai nitafundisha kozi ya wiki sita, katika somo liitwalo "Post-colonial Literature." Nimeamua kufundisha kitabu hiki cha Rushdie. Ni kitabu muhimu kwa namna nyingi, sio tu kwa upande wa sanaa, bali pia kwa jinsi kinavyojumlisha masuala na dhamira mbali mbali ambazo ni muhimu katika fasihi ya India. Ni kitabu chenye upekee kihistoria na kisiasa kwa jinsi kilivyofungamana na tukio moja muhimu sana katika karne ya ishirini, yaani kupatikana kwa uhuru kwa nchi iitwayo India.

Tukio hili la uhuru wa India lilitokea mwaka 1947. Ila kwa bahati mbaya sana, ni tukio lililoandamana na mgawanyiko uliosababisha kuwepo kwa nchi mbili, yaani India na Pakistan. Ni tukio lililoandamana na uhasama, mauaji na ukimbizi wa idadi kubwa sana ya watu, mtafaruku ambao ulikuwa baina ya wa-Hindu na wa-Islam. Tukio hili linakumbukwa kwa majonzi, na limeelezwa sana na waandishi kutoka India na Pakistan.

Kwa vile kitabu cha Midnight's Children kina kurasa nyingi sana, nimeona kuwa nisiweke vitabu vingi katika kozi hii ya wiki sita.  Nawazia kutumia vitabu vingine viwili au vitatu, ambavyo navyo vina kurasa nyingi. Nimeamua tu kutumia haya mavitabu makubwa nione itakuwaje. Kimoja ninachowazia sana ni Half of a Yellow Sun, cha Chimamanda Ngozi Adichie, wa Nigeria. Kingine ni Abyssinian Chronicles cha Moses Isegawa wa Uganda. Bado nina muda wa kufikia uamuzi wa mwisho. Huenda nikatumia The Famished Road, cha Ben Okri, au Wizard of the  Crow, cha Ngugi wa Thiong'o. Uamuzi kamili nitafikia katika siku kadhaa zijazo.

Friday, May 20, 2011

"Mama m-Katoliki" (shairi kutoka India)

Uandishi wa ki-Ingereza wa India unafahamika zaidi katika tanzu ya riwaya na hadithi fupi, ingawa waandishi wa mashairi pia wapo, kama vile Kamala Das, Nissim Ezekiel na Jayanta Mahapatra. Leo wanafunzi wangu wa somo la fasihi ya Asia Kusini walifanya mtihani wa mwisho, na suali moja nililowapa lilihusu shairi la "Catholic Mother," lililotungwa na Eunice de Souza.

Suali nililowapa ni hili: "Discuss the poem, "Catholic Mother," by Eunice de Souza. Say what you want about it. In addition, compare the woman in this poem with Anil, a key character in Michael Ondaatje's Anil's Ghost."

Sijui kwa nini, baada ya mtihani kumalizika, nimepata wazo la kulitafsiri shairi hili na kuliweka hapa kwenye blogu yangu. Ingawa lugha aliyotumia mtunzi inaonekana ni ya kawaida tu, ameingiza tamathali za usemi kiurahisi, lakini kwa uhodari na kufikirisha. Amepenyeza na kuchochea uchambuzi wa masuala muhimu ya jamii, kama vile dini, udini na jinsia.

Vile vile, nimekuwa nikiangalia jinsi anavyotumia herufi kubwa na wakati mwingine herufi ndogo. Hili nalo ni suala la kufikiriwa. Kuna kejeli nzuri na ucheshi fulani ndani yake.

Kutafsiri kazi ya fasihi--iwe ni hadithi, riwaya, au shairi--ni suala tata na mtihani mkubwa. Ninajua ninalosema, kutokana na kusoma mawazo ya watalaam na pia kutokana na uzoefu wangu. Kwa kweli, dhana yenyewe ya tafsiri ni ndoto, kwani lugha zinatofautiana, na tafsiri yoyote ni lazima itofautiane kwa namna mbali mbali na utungo unaotafsiriwa. Hali hiyo inajitokeza katika tafsiri yangu ya shairi la "Catholic Mother."

Msomaji ambaye anafahamu vizuri ki-Ingereza na ki-Swahili ataweza kutambua namna ambayo yeye angetafsiri shairi hili. Ingekuwa vizuri kuona wengine wangetafsiri vipi shairi hili, nami nakaribisha michango hiyo.

Mimi kama m-Mkatoliki nimevutiwa na shairi hili. Nimejikuta nikitabasamu kwa jinsi mshairi anavyotusanifu sisi wa-Katoliki. Mshairi Eunice de Souza ni mwanamke, na ni m-Katoliki kutoka jamii ya wa-Goa. Alizaliwa Pune, India, mwaka 1940. Amestaafu kazi ya ualimu wa ki-Ingereza katika chuo cha Mtakatifu Xavier, mjini Mumbai. Soma hilo shairi lake, na tafsiri yangu:


Catholic Mother

Francis X. D’Souza
father of the year.
Here he is top left
the one smiling.
By the Grace of God he says
we’ve had seven children
(in seven years)
We’re One Big Happy Family
God Always Provides
India will Suffer for
her Wicked Ways
(these Hindu buggers got no ethics)

Pillar of the Church
says the parish priest
Lovely Catholic Family
says Mother Superior

the pillar's wife
says nothing.

---------------------------

Mama m-Katoliki

Francis X. D’Souza
baba wa mwaka.
Yuko hapa juu kushoto
anayetabasamu.
Kwa Neema ya Mungu anasema
tumejaaliwa watoto saba
(katika miaka saba)
Sisi ni Familia Moja Kubwa Yenye Furaha
Mungu Daima Anaruzuku
India Itateseka
kwa Mwenendo Wake Mbaya
(hao wa-Hindu mabwege hawana maadili)

Ni Nguzo ya Kanisa
asema baba paroko
Familia Murua ya ki-Katoliki
asema Mkuu wa Masista

mkewe nguzo
hasemi lolote.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...