Tuesday, December 1, 2015

Nilitembelea Duka la Vitabu la Amkal

Tarehe 23 Mei, 2015, nilitembelea duka la vitabu la Amkal mjini Minneapolis, kama nilivyoripoti katika blogu hii. Ni duka la wa-Somali ambalo linauza zaidi vitabu vinavyohusu dini ya ki-Islam. Siku hiyo nilinunua kitabu kiitwacho Jesus: Prophet of Islam. Ninapenda kuongelea, kwa kifupi na wepesi kabisa, mawazo yanayonijia ninapokumbuka ziara yangu katika duka lile.

Jambo la msingi kwamba katika kuishi kwangu hapa Marekani, nimeona jinsi wa-Afrika wa nchi mbali mbali wanavyovithamini vitabu. Kwa mfano, nimewahi kuwaongelea wa-Kenya.

Wa-Somali ni mfano mwingine. Nimekutana na wa-Somali wanaoishi hapa Minnesota ambao wanaandika vitabu. Nimejionea wanavyojitokeza kuwasikiliza waandishi wa vitabu wa ki-Somali. Mfano ni Nuruddin Farah, ambaye huonekana hapa Minnesota mara kwa mara, ingawa makao yake kwa miaka hii ni Afrika Kusini. Wanamheshimu kwa jinsi anavyowakilisha taifa lao katika ulimwengu wa uandishi.

Kwa ujumla, hao wa-Somali ni wakimbizi au wahamiaji. Lakini pamoja na kadhia hiyo, pamoja machungu waliyoyapitia, wameshikilia umuhimu wa vitabu na elimu. Katika vyuo vya hapa Minnesota, kama vile Chuo Kikuu cha Minnesota, Metropolitan State University. Mankato State University, South Central College, na Minneapolis Community and Technical College, wanafunzi wa ki-Somali ni wengi. Wanawekeza katika elimu. Wanajijengea mtaji ambao wataweza kuutumia kwa maendeleo ya nchi yao.

Suala la elimu wanalishughulika kwa namna nyingine pia, kama vile magazeti na vituo vya televisheni. Hali hii nimeiona pia miongoni mwa wa-Afrika wengine, kama vile wa-Kenya na wa-Ethiopia. Kwa kutumia njia hizo, wanazitangaza nchi zao na shughuli zao, kama vile biashara. Ninawaona ni mfano wa kuigwa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...