Saturday, December 26, 2015

Jólabókaflóð: Mafuriko ya Vitabu Nchini Iceland

Nchi ya Iceland inaongoza ulimwenguni kwa usomaji wa vitabu, na pia kwa asilimia ya watu wanaochapisha vitabu. Hilo linatosha kuipambanua nchi ile. Lakini kuna pia jadi iitwayo Jólabókaflóð, yaani mafuriko ya vitabu, ambayo hutokea majira ya Krismasi.

Kila mwaka, kuanzia mwezi Septemba hadi Desemba, pilika pilika zinazohusiana na vitabu zinapamba moto. Wachapishaji wa vitabu wanaongeza juhudi ya kutangaza vitabu, na jamii nzima huwa katika heka heka ya kununua vitabu. Mazungumzo na malumbano kuhusu vitabu hushamiri kila mahali.

Mwezi Novemba, katalogi kubwa ya vitabu iitwayo bókatíðindi inachapishwa na kugawiwa bure karibu kila nyumba. Katalogi hii huorodhesha vitabu karibu vyote vilivyochapishwa katika mwaka husika. Kadiri Krismasi inavyokaribia, shughuli ya kuzawadiana vitabu inapamba moto. Kilele huwa ni tarehe 24 Desemba, ambayo ni mkesha wa Krismasi. Watu hutumia mkesha wa Krismasi wakisoma vitabu.

Taarifa hizo sikuwa ninazifahamu, hadi leo. Sikujua kuwa utamaduni wa Iceland umefungamana na vitabu kiasi hicho. Nimejikuta ninawazia hali ilivyo nchini mwangu Tanzania. Nimekumbuka makala niliyoandika katika blogu hii nikiwazia ingekuwaje iwapo wa-Tanzania tungeanzisha utamaduni wa kupeana vitabu kama zawadi ya Idd el Fitr au Krismasi.

Je, sisi wa-Tanzania tunaweza kuthubutu kuwapelekea wa-Tanzania wenzetu vitabu kama zawadi ya sikukuu au ya sherehe kama arusi? Tafakari mwenyewe.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...