Showing posts with label tofauti za tamaduni. Show all posts
Showing posts with label tofauti za tamaduni. Show all posts

Wednesday, May 2, 2018

Wadau Niliokutana Nao Wikii Hii

Katika siku saba zilizopita, nimekutana na wadau wengi wa vitabu vyangu. Kwanza, nilipata barua pepe kutoka kwa mtu aliyejitambulisha kuwa ni m-Marekani anayefundisha ki-Ingereza Mwanza kwa kujitolea. Ameandika kuhusu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences:

Nimemaliza kitabu chako kuhusu tofauti za tamaduni zetu na nilikifurahia sana. Ulinichekesha mara nyingi. Aidha ukanieleza mambo mengi.

Aprili tarehe 28, niliongea na wanafunzi wa somo la Global Semester ambao watasafiri na kukaa sehemu mbali mbali za dunia, ikiwemo Arusha, Tanzania, ambako watakaa kwa mwezi moja. Profesa wao aliniomba nikawaeleze masuala ya tofauti za tamaduni. Yeye mwenyewe amesoma Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Tarehe 28 Aprili, nilikuwa Rochester, Minnesota, kushiriki tamasha la kimataifa linaloandaliwa kila mwaka na Rochester International Association. Hapo nilikutana na hao ndugu wawili wanaoonekana pichani hapa juu. Huyu wa kushoto ni daktari katika hospitali maarufu ya Mayo, mwenye asili ya Uganda, na huyu wa kulia ni m-Kenya ambaye alikuwa mwanafunzi wetu chuoni St. Olaf. Tuliongea kirefu. Daktari ndiye aliyetaka tupige hiyo picha tukiwa tumeshika vitabu vyangu.

Friday, April 27, 2018

Madaktari Wanafundishia Kitabu Hiki

Nilivyoandika kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, sikuwazia kingetumika kwa namna nyingi kama ilivyotokea baadaye. Kilichonishtua zaidi ni pale waalimu wa uuguzi wa chuo cha Gustavus Adolphus walipoamua kukitumia kufundishia, wakaanza, kila wanapofundisha kozi hiyo, kunialika kuongea na wanafunzi.

Baada ya muda si mrefu, Dr. Randy Hurley mwanzilishi na mhusika mkuu wa  na programu ya hospitali ya Ilula, mkoani Iringa, alinialika kuhutubia mkutano wa mwaka wa wadau wa hospitali hiyo. Ulikuwa ni mkutano wa kuchangisha fedha za kuendelezea programu. Hapo ndipo nikajua kuhusu programu ya kuelimisha wauguzi ambayo inafanyika Ilula, ikiwahusisha wa-Marekani na wa-Tanzania.

Nilijua kuwa wanatumia kitabu changu, bali sikuwa na taarifa zaidi. Lakini siku chache zilizopita nimeona jinsi kitabu hicho kinavyotajwa katika silabasi mpya ya kozi yao. Wanafunzi wanahimizwa kukisoma. Kwa kuwa mimi si mtaalam wa masuala ya uuguzi na matibabu, nilijiuliza masuali, kwa sababu baadhi ya mambo niliyoandika kitabuni ni tofauti na taaluma ya uuguzi na matibabu. Dukuduku yangu hii niliigusia katika blogu hii.

Hatimaye, nilikuja kuelewa vizuri mantiki ya madkatari na waalimu wa uuguzi kukitumia kitabu hiki. Ni kwa sababu kinaelezea utamaduni hauwezi kutenganishwa na masuala ya matibabu ba uuguzi. Madaktari na wauguzi wanatakiwa kuwafahamu wale wanaowahudumia, katika vipengele kama jadi, tabia, matarajio, miiko, imani, na hisia. Ni muhimu kwa muuguzi au daktari kuyafahamu na kuyazingatia wakati anatoa huduma. Kwa hivyo, sasa ninavyosikia kitabu kinatumiwa na watu katika taaluma hizo, sina masuali bali ninashukuru kwamba nimeweza kutoa mchango fulani wa manufaa.

Thursday, October 12, 2017

Profesa Amekifurahia Kitabu

Ni kawaida yangu, kuchapisha maoni ya wasomaji wa vitabu vyangu. Leo nimepata ujumbe kutoka kwa profesa moja ambaye alihudhuria mkutano wa Africa Network nilioshiriki kuuandaa hapa chuoni St. Olaf.

Profesa huyu Mmarekani anawapeleka wanafunzi wa ki-Marekani Kenya na Rwanda. Katika mkutano wetu, aliongelea programu hiyo, akielezea jinsi tofauti za tamaduni zinavyojitokeza.

Nilivutiwa na mhadhara wake, kwa kuwa nami ni mzoefu wa programu hizi za kupeleka wanafunzi Afrika, ikiwemo Tanzania. Nilimpelekea kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, naye ameniandika ujumbe huu:

Dear Joseph,
There were several wonderful things that came from my attending the Africa Network conference. Meeting you and learning more is one. I just finished your book and enjoyed it so much. It made me laugh out loud and understand my Kenyan teaching colleague even more. I have been both to Rwanda and Kenya many times and am aware of many of the situations and misunderstandings you describe. I’ve shared my thoughts with Kitito and we hope to use your book in some way for our spring Cultural Identity course. 
Thanks again.

Ninashukuru kwamba kitabu hiki kinatoa mchango ambao nilipangia nilipokiandika, ikiwemo kuwaelimisha wanaohusika na programu za kupeleka wanafunzi Afrika. Msukumo wa kukiandika ulitoka katika mikutano ya jumuia ya vyuo iitwayo Associated Colleges of the Midwest (ACM), na baada ya kukichapisha, wahusika wa programu zingine nao wanakitumia. Mifano ni programu ya  chuo kikuu cha Wisconsin-Oshkosh na pia program ya chuo cha Gustavus Adolphus, ambayo nimeitaja mara kwa mara katika blogu hii.


Friday, June 2, 2017

Kitabu Kimependekezwa na Africa International University

Nimeona leo kuwa kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimependekezwa na Africa International University (AIU) kwa ajili ya wanafunzi wa kigeni. Chuo hiki kiko Karen, nchini Kenya.

Nimevutiwa na maelezo yaliyotolewa kama Information for International Students juu ya hali halisi anayokumbana nayo mtu anapojikuta katika utamaduni wa kigeni:

Moving to a different cultural environment is a very stressful experience – that’s why it is sometimes referred to as “culture shock”. You will likely go through a difficult period of adjustment and homesickness after the initial excitement wears off. This is normal. As you learn your way around the campus and its unique culture, you will be more comfortable at AIU. Soon you will be helping other new international students adjust to AIU and Kenya. If you are willing to learn, you will learn a great deal about yourself and others who are different from you. You will leave here enriched and transformed.

Still, it is wise to take time before coming to prepare yourself and your family for the cultural adjustments that will be necessary. By reading as much as you can about cultural adjustment and talking to other international students, you can learn what to expect. Then you will better understand the feelings and frustrations you deal with as you adjust to your new environment. Since academics will demand a great deal of you at AIU, any preparation you can do before coming will help all of your adjustments once you arrive on campus....Due to cultural differences, you may feel somewhat confused when talking with fellow students. “What do they mean?” Communication in Africa is inferential rather than direct, so you will need to become adept at listening for what is being communicated between the lines.... Students at AIU are coming from all over Africa and the world. They will appreciate the time you invest in learning about the uniqueness of their own cultures—e.g. what communicates respect.

Maelezo na mawaidha haya yanahusiana na yaliyomo katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ni masuala yasiyokwepeka, hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Yanawahusu sio tu wanafunzi, bali pia wafanya biashara, wanadiplomasia, na kadhalika, kama ninavyoelezea mara kwa mara katika blogu hii.

Saturday, April 29, 2017

Tamasha la Mataifa Limefana Rochester, Minnesota.

Leo tamasha la mataifa limefanyika mjini Rochester, Minnesota. Niliweka tangazo la tamasha hili katika blogu hii. Binti yangu Zawadi na mimi tulishiriki. Ni mwendo wa saa moja kutoka hapa Northfield ninapoishi.

Tulipanga vitabu vyangu na machapisho mengine mezani, tukatundika ukutani bendera ya Tanzania ambayo nilinunua siku zilizopita. Saa nne ilipotimia, ambayo ndiyo saa ya kufunguliwa tamasha, watu walianza kuja. Na hapo kwenye meza yetu tulianza kutembelewa na watu tangu dakika zile za mwanzo. Tuliongea nao, tukajibu masuali kuhusu vitabu hivyo na mambo mengine mengi, nao wakatueleza mambo mbali mbali.


Baada ya nusu saa hivi, ilianza shughuli ya kupeperusha bendera. Watu walielekezwa zilipowekwa bendera ili wachukue bendera ya nchi yao na kujiunga katika maandamano wakiwa wamebeba bendera. Nilikwenda nikaikuta bendera ya Tanzania, nikaibeba katika maandamano.

Tuliendelea kuongea na watu wa mataifa mbali mbali hapo kwenye meza yetu, tukapata pia fursa ya kuzunguka kwenye meza za wengine, na kupiga picha. Kwa namna ya pekee ninakumbuka tulivyozungumza na mama mmoja Mmarekani, kuhusu tofauti za tamaduni akatueleza yaliyomkuta Japani. Mila na desturi alizozizoea Marekani ziliwashangaza wenyeji. Nasi tulimweleza yanayotokea pale wa-Afrika wanapokuwa na wa-Marekani, kama nilivyoelezea katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Ninakumbuka pia nilivyoongea na mama anayeonekana pichani hapa kushoto amevaa hijab. Nilikumbuka kuwa nilimwona katika tamasha mwaka jana, ila hatukufahamiana. Jana tulipata hiyo fursa, mezani pake, ambapo aliweka machapisho ya ki-Islam, kama vile The Message of the Qur'an cha Muhammad Asad, Who Speaks for Islam cha John L. Esposito na Dalia Mogahed, na Wisdom for Life & The Afterlife: A Selection of Prophet Mohammad's Sayings, ambavyo vyote ninavyo.

Nilimwambia kuwa mimi ni mwalimu katika chuo cha St. Olaf; nimetunga kozi, "Muslim Women Writers." na sababu za kuitunga. Naye alinielezea kuhusu kipindi anachoendesha kiitwacho Faith Talk Show, tukakubaliana nije kuhojiwa katika kipindi hicho siku zijazo.

Baada ya kurejea kutoka kwenye tamasha, nimeangalia mtandaoni, nikaona taarifa za mama huyu kama vile hii hapa. Ninawazia kumwalika darasani kwangu nitakapofundisha tena kozi yangu.

Muda wote wa tamasha kulikuwa na vikundi vya burudani jukwaani na pia vyakula vya nchi mbali mbali. Ninaleta hapa baadhi ya picha za tamasha.





Friday, February 17, 2017

Umuhimu wa Kuzifahamu Tamaduni za Wengine

Mada ya tofauti za tamaduni na athari zake duniani ninaishughulikia sana. Kwa mfano, nimeandika kitabu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nimeongelea suala hilo pia katika kitabu changu kiitwacho CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Vile vile ninaliongelea mara kwa mara katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza.

Umuhimu wa kuzifahamu tofauti za tamaduni unaonekana wazi wazi wakati tunapokumbana na matatizo katika mahusiano yetu na watu wa tamaduni ambazo si zetu. Tusijidanganye kwamba jambo hilo ni la kinadharia tu na kwamba halituhusu. Miaka michache iliyopita, wafanya biashara wa Tanzania walikwenda Oman kushiriki maonesho ya biashara. Walipata shida kutokana na kutojua utamaduni wa watu wa Oman. Taarifa hiyo iliandikwa katika blogu ya Michuzi.

Suala hili haliwahusu wafanya bashara tu, bali wengine pia, kama vile wanafunzi wanaokwenda nchi za nje, wanadiplomasia, watu wanaokwenda mikutanoni, na kadhalika. Kwa kuzingatia hayo, na kwa kuwa nimekuwa nikifanya utafiti katika masuala hayo, nimekuwa nikipata mialiko ya kutoa ushauri kwa jumuia na taasisi mbali mbali hapa Marekani. Vyuo vya Marekani, kwa mfano, vinapopeleka wanafunzi nchi za nje, kama vile nchi za Afrika, vinazingatia suala la kuwaandaa wanafunzi kwa kuwaelimisha kuhusu utamaduni wa huko waendako. Mwaka hadi mwaka nimealikwa kutoa elimu hiyo.

Nimewahi pia kuendesha semina Tanzania, kwenye miji ya Arusha, Tanga, na Dar es Salaam. Vile vile, kwa kuombwa na ubalozi wa Marekani nchini Tanzania, niliwahi kutoa mihadhara Zanzibar na Pemba, juu ya utamaduni wa Marekani, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Kwa jinsi ninayofahamu umuhimu wa suala hili, nimekuwa nikikumbushia mara kwa mara kila ninapoweza. Kwa mfano, uhusiano ulipoanza kuimarika baina ya Tanzania na u-Turuki, nilikumbushia suala hilo katika blogu hii. Ningependa kuona suala hili la athari za tofauti za tamaduni linapewa kipaumbele katika maisha yetu kwani kulipuuzia ni kujitakia matatizo yasiyo ya lazima. Hii ndio sababu iliyonifanya nianzishe kampuni ya kutoa elimu na ushauri iitwayo Africonexion: Cultural Consultants.

Thursday, December 1, 2016

Maandalizi ya Wanachuo wa Gustavus Adolphus Waendao Tanzania

Jana nilipata ujumbe kutoka kwa Profesa Barbara Zust wa Chuo cha Gustavus Adolphus akiulizia iwapo nitaweza kwenda kuongea na wanafunzi wanaojiandaa kwenda naye Tanzania kwa safari ya kimasomo. Ameniambia kuwa watakuwa na kikao cha maandalizi ya safari tarehe 2 na 3 Januari, katika kituo cha mikutano cha Mount Olivet. Nimefanya mazungumzo hayo tena na tena miaka iliyopita.

Katika ujumbe wake, Profesa Zust amekumbushia kuwa, kama ilivyo jadi, wanafunzi hao watakuwa wameshasoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Pia amekumbushia jinsi wanafunzi wanavyoshukuru na kufurahia kwamba wanapokuwa Tanzania wanakutana na yale ambayo ninakuwa nimewaeleza kitabuni na katika mazungumzo.

Taarifa hii ni muhimu kwangu, na ndio maana ninaiweka hapa katika blogu yangu, kama kumbukumbu. Kwa kuzingatia umuhimu wa suala hili, nimeitika mwaliko wa Profesa Zust na kumwambia kuwa nitakwenda kukutana nao tarehe 2 Januari. Kama kawaida, panapo majaliwa, nitaandika taarifa katika blogu hii.

Wednesday, February 22, 2012

Nilivyoanza Kupeleka Wanafunzi Tanzania

Nimetoka mbali, katika suala la kuwapeleka Tanzania wanafunzi wa vyuo vya Marekani. Mara baada ya kuja kufundisha katika Chuo Cha St. Olaf, nilianza kujishughulisha na masuala ya programu zinazowapeleka wanafunzi Afrika. Kama mmoja wa washauri wa programu hizo nilijifunza mengi. Baada ya miaka michache, nilianza kuwapeleka wanafunzi Tanzania.

Hapa kushoto niko na wanafunzi kwenye chuo kilichokuwa kinaitwa Danish, eneo la Usa River. Hii ilikuwa ni programu ya vyuo vilivyomo katika mtandao wa LCCT. Nadhani hiyo ilikuwa ni mwaka 1997. Hapo Danish, tulikuwa tunawapa wanafunzi mafunzo kuhusu masuala mbali mbali ya Tanzania, kwa wiki moja na kidogo. Baada ya hapo, kwa mujibu wa programu hii, niliwapeleka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kusoma kwa muhula mmoja.



Hapa kushoto niko na wanafunzi wale wale katika nyumba niiyokuwa naishi pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, sehemu iitwayo "Research Flats."

Kadiri miaka ilivyopita, nimejijengea uzoefu na ufahamu mkubwa wa programu hizi. Nafahamu mikakati, mahitaji, changamoto, na faida za programu hizo kwa wahusika wa pande zote. Uzoefu wa kuwaandaa wanafunzi wa ki-Marekani kuishi katika utamaduni wa kigeni uliniwezesha kuandika kitabu kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nilikiandika mahsusi kuchangia programu hizo, na walimu wengine wanaopeleka wanafunzi Afrika wanakitumia, bila kuwataja watu wanaoenda Afrika kwa utalii, shughuli za kujitolea, na kadhalika.

Tuesday, November 30, 2010

Asante, Joseph Mbele

Jioni hii, katika kuzurura mtandaoni, mitaa ya Google, nimekumbana na makala kwenye blogu fulani, ambayo inanitaja. Soma hapa.

Sikuwa nimeiona makala hii ambayo inataja ziara niliyofanya College of St. Benedict/St. John's University mwaka jana. Nilialikwa kutoa mihadhara. Katika darasa la Profesa Lisa Ohm, niliongelea hadithi na utamaduni, kufuatia maelezo yaliyomo katika kitabu cha Matengo Folktales, ambacho walikuwa wanakitumia. Soma hapa.

Mhadhara wa pili niliutoa kwa wanafunzi na walimu waliokuwa wanajiandaa kwenda Tanzania na Afrika ya Kusini, lakini ulihudhuriwa na wengi wengine. Lengo lilikuwa kuwaarifu kuhusu tofauti za msingi baina ya tamaduni wa mw-Afrika na ule wa m-Marekani, kama nilivyoeleza katika kitabu cha Africans and Americans.

Nakumbuka jinsi ukumbi ulivyojaa watu kwenye mhadhara huu, na kwenye meza nyuma ya umati walikuwa wameweka nakala nyingi za vitabu hivi viwili, kama ilivyo desturi hapa Marekani, wanapowaita waandishi kuzungumzia vitabu na uandishi. Soma hapa.

Nimefurahi kuona kuwa mazungumzo yangu kwa hao wa-Marekani yameelezwa kama ilivyoelezwa na mwandishi huyu. Nimefurahi jinsi anavyokiri kuwa yale niliyowaambia ndiyo aliyoyakuta Afrika Kusini. Huwa nakutana na wa-Marekani wengi wanaosema hivyo hivyo, wanaporudi kutoka Afrika. Nami nafanya juhudi nijielimishe zaidi kuhusu tofauti za tamaduni hizi, ili niweze kuboresha mafunzo na mawaidha ninayotoa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...