Friday, February 17, 2017

Umuhimu wa Kuzifahamu Tamaduni za Wengine

Mada ya tofauti za tamaduni na athari zake duniani ninaishughulikia sana. Kwa mfano, nimeandika kitabu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nimeongelea suala hilo pia katika kitabu changu kiitwacho CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Vile vile ninaliongelea mara kwa mara katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza.

Umuhimu wa kuzifahamu tofauti za tamaduni unaonekana wazi wazi wakati tunapokumbana na matatizo katika mahusiano yetu na watu wa tamaduni ambazo si zetu. Tusijidanganye kwamba jambo hilo ni la kinadharia tu na kwamba halituhusu. Miaka michache iliyopita, wafanya biashara wa Tanzania walikwenda Oman kushiriki maonesho ya biashara. Walipata shida kutokana na kutojua utamaduni wa watu wa Oman. Taarifa hiyo iliandikwa katika blogu ya Michuzi.

Suala hili haliwahusu wafanya bashara tu, bali wengine pia, kama vile wanafunzi wanaokwenda nchi za nje, wanadiplomasia, watu wanaokwenda mikutanoni, na kadhalika. Kwa kuzingatia hayo, na kwa kuwa nimekuwa nikifanya utafiti katika masuala hayo, nimekuwa nikipata mialiko ya kutoa ushauri kwa jumuia na taasisi mbali mbali hapa Marekani. Vyuo vya Marekani, kwa mfano, vinapopeleka wanafunzi nchi za nje, kama vile nchi za Afrika, vinazingatia suala la kuwaandaa wanafunzi kwa kuwaelimisha kuhusu utamaduni wa huko waendako. Mwaka hadi mwaka nimealikwa kutoa elimu hiyo.

Nimewahi pia kuendesha semina Tanzania, kwenye miji ya Arusha, Tanga, na Dar es Salaam. Vile vile, kwa kuombwa na ubalozi wa Marekani nchini Tanzania, niliwahi kutoa mihadhara Zanzibar na Pemba, juu ya utamaduni wa Marekani, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Kwa jinsi ninayofahamu umuhimu wa suala hili, nimekuwa nikikumbushia mara kwa mara kila ninapoweza. Kwa mfano, uhusiano ulipoanza kuimarika baina ya Tanzania na u-Turuki, nilikumbushia suala hilo katika blogu hii. Ningependa kuona suala hili la athari za tofauti za tamaduni linapewa kipaumbele katika maisha yetu kwani kulipuuzia ni kujitakia matatizo yasiyo ya lazima. Hii ndio sababu iliyonifanya nianzishe kampuni ya kutoa elimu na ushauri iitwayo Africonexion: Cultural Consultants.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...