
Matangazo yalitayarishwa na kubandikwa sehemu mbali mbali Zanzibar na Pemba. Nilisindikizwa kwenye ziara hii na Bwana David Colvin, ofisa utamaduni katika Ubalozi wa Marekani. Yeye ndiye aliyekuwa ananitambulisha kwa wenyeji wangu, kwani alikuwa amewazoea. Mhadhara wa kwanza ulifanyika katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar.


Walikuja watu wengi. Kwa bahati nzuri baadhi nilikuwa nawafahamu, tangu walipokuwa wanafunzi wangu katika chuo kikuu cha Dar es Salaam. Walikuwepo pia wanafunzi kutoka Ulaya, waliokuwa wanasoma kiSwahili hapo Chuoni. Mhadhara wangu ulitokana na yale niliyoandika katika Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ilikuwa fursa nzuri ya kuwaleza waTanzania mambo kadhaa yanayoweza kuleta matatizo ya kutoelewana baina ya waTanzania na waMarekani. Baada ya mhadhara, kilifuata kipindi cha masuali. Jambo mojawapo lililoleta msisimko ni jinsi dhana ya tabia njema au heshima ilivyo katika jamii ya kiMarekani, na jamii ya kiTanzania.

Nililala Zanzibar na siku ya pili nikaenda Pemba. Nilipokelewa uwanja wa ndege na bwana mmoja ambaye alinikumbusha kuwa alikuwa mwanafunzi wangu Chuo Kikuu cha Dar es Salaama miaka iliyopita. Tulienda hadi mjini Chake Chake, na hapo nilipokelewa kwa ngoma ya Msewe.


Mhadhara wangu ulikuwa sawa na ule wa Zanzibar. Watu walijaa ukumbini, na wengi walilazimika kusikiliza wakiwa nje ya ukumbi.


Hii ni kati ya ziara ambazo sitazisahau. Pamoja na yote niliyoweza kuongea kuhusu waMarekani, nilifurahi kupata bahati ya kuiona Pemba kwa mara ya kwanza maishani. Nawajibika kutoa shukrani kwa Ubalozi wa Marekani Tanzania kwa kunipa fursa hii ya kuiona sehemu ya nchi yangu. Namshukuru sana Bwana David Colvin kwa kunipa picha nyingi, zikiwemo nilizotumia hapa.
No comments:
Post a Comment