
Leo ninapenda kumtambulisha Charles Chanda Dennis, raia wa Liberia ambaye anaishi hapa Marekani, jimbo la Minnesota. Huyu ni mtu maarufu, hasa katika jamii ya wa-Afrika na wa-Marekani Weusi. Ni mtangazaji na mwendeshaji wa kipindi kiitwacho African Roots Connection katika KMOJ Radio.
Sikumbuki ni lini nilifahamiana na Charles, lakini nadhani ni miaka karibu kumi iliyopita. Aliwahi kunialika kama mgeni katika kipindi chake tukahojiana juu ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Wiki chache zilizopita, alinialika tena, tukafanya mahojiano marefu na ya kina ambayo unaweza kuyasikiliza hapa:
https://www.dropbox.com/home?preview=Story+Telling.mp3
Miaka yapata mitano iliyopita, Charles alialikwa na wanafunzi hapa chuoni St. Olaf kutoa mhadhara juu ya historia ya mahusiano na harakati za watu wa asili ya Afrika. Nilihudhuria mhadhara ule. Charles alithibitisha kuwa ni msomi wa uhakika, mwenye uwezo mkubwa wa kuchambua mambo. Anafahamu vizuri njia waliyopitia watu weusi barani Afrika na nje ya Afrika, hasa Marekani.
Alivyonialika kwenye mahojiano safari hii, hatukuongelea angenihoji kuhusu nini hasa, bali nilihisi kuwa alitaka kufuatilia masuala ambayo ninashughulika nayo katika jamii, kama mwalimu na mtoa ushauri kuhusu tamaduni. Niliguswa na masuali yake, kama inavyosikika katika ukanda wa mahojiano niliyoweka hapa juu.
Niliguswa kwa namna ya pekee jinsi Charles alivyonitambulisha kwa wasikilizaji, akinipigia debe kwa bidii na kuwahamasisha watu wasome Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ninamshukuru kwa hilo, nikizingatia umaarufu wa kipindi chake cha African Roots Connection na KMOJ Radio kwa ujumla.
No comments:
Post a Comment