Tuesday, February 21, 2017

Kitabu Nilichonunua Leo: "The Fundamentals of Tawheed"

Leo nilikuwa mjini Minneapolis. Baada ya shughuli zangu, niliamua kwenda kwenye duka la vitabu vya dini ya Uislam liitwalo Akmal Bookstore. Niliwahi kulitembelea duka hilo, kama nilivyoandika katika blogu hii.

Kama nilivyoona mara ya kwanza, duka hili lina vitabu vingi vya Uislam. Leo nilitumia muda kuvipitia. Hatimaye niliamua kununua The Fundamentals of Tawheed: Islamic Monotheism, cha Dr. Abu Ameenah Bilal Philips. Huyu nilifahamu habari zake tangu miaka kadhaa iliyopita. Alizaliwa Jamaica, lakini alikulia Canada, ambako alisilimu mwaka 1972. Nimesikiliza hotuba zake mtandaoni. Ni mmoja wa watu wanaosifika kwa ufahamu wao wa dini ya Uislam.

Kama nilivyowahi kuandika tena na tena katika blogu hii, ninasoma vitabu vya Uislam na dini zingine kwa ajili ya kujielimisha, sio kwa ajili ya kubadili dini. Nina dini yangu, na nitabaki hivyo. Ninaiheshimu dini yangu, na ninaziheshimu dini za wengine. Ninategemea wengine nao wafanye hivyo, vinginevyo sisiti kuwakabili kwa hoja.

Vile vile, kwa kuwa ninafundisha kozi niliyoitunga iitwayo Muslim Women Writers, na mara kwa mara katika kozi zingine za fasihi ninafundisha maandishi ya wa-Islam, ni muhimu nijielimishe juu ya Uislam. Mwalimu wa somo lolote ana wajibu wa kujielimisha daima. Katika kufundisha tunachambua mambo, hatufundishi kama wafanyavyo katika nyumba za ibada, kwa lengo la kuimarisha imani ya dini au kuwavuta watu wawe waumini wa dini. Darasa langu si kanisa au msikiti. Hoja zozote zinakaribishwa na kutafakariwa kwa uhuru kamili, hata zile zinazokosoa au kupinga dini.

Kwa mtazamo wangu, kila mtu ana wajibu wa kujielimisha kuhusu dini za wengine. Kujielimisha kuhusu dini mbali mbali ni sawa na kujielimisha juu ya tamaduni mbali mbali. Ni hatua muhimu katika kujenga maelewano duniani, kama ninavyoelezea katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

2 comments:

Anonymous said...

Hi Professor.....love your comments on diversity and learning about other religions. This is wonderful, for when we know and understand other religions then we can choose the one which resonates with us most closely, and also have less bad judgement about someone else and their beliefs. Thank you for your expansive views on this. With respect..Merri

Mbele said...

Thank you, Merri, for your comments. I am very pleased that you have a way to read my Swahili postings and thereby follow what I am saying. Best wishes.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...