Monday, January 2, 2012

Maongezi na Wanafunzi wa Gustavus Adolphus

Leo nimeongea na wanafunzi wa Chuo cha Gustavus Adolphus ambao wanaenda Tanzania wiki hii kujifunza masuala ya afya na matibabu katika utamaduni tofauti na ule wa Marekani.

Kama nilivyoelezea katika blogu hii, nilialikwa na Profesa Barbara Zust, nikaongee na wanafunzi hao kuhusu masuala ninayoongelea katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences". Pichani kushoto, Profesa Zust ni kati ya waliosimama, wa nne kutoka kulia.

Profesa Zust ni mmoja wa walimu hapa Marekani ambao wanakipenda na kukitegemea kitabu hiki. Nami nashukuru kwa jinsi kinavyowasaidia walimu na wanafunzi wao. Mimi mwenyewe kama mwalimu siwezi kukaa na kutulia, bali natambua na kuzingatia wajibu wa kuendelea kutafiti na kuandika.

Leo, nilianza kwa kujitambulisha kwa kuelezea maisha yangu kwa ufupi hadi nilivyosoma Marekani na nikazingatia zaidi mchakato ulionifikisha kwenye kuandika kitabu hiki. Wale waliokisoma watakumbuka kuwa nimeelezea kiasi mchakato huo mwanzoni mwa kitabu.

Nilisisitiza mambo mhimu niliyojifunza katika kuandika kitabu hiki, kwa mfano umuhimu wa kuachana na dhana ya kuwa yale tuliyozoea katika jamii tuliyokulia ndio kigezo cha kufuatwa na watu wengine duniani. Nilielezea pia ugumu nilioupata katika kuandika kitabu hiki, nikiwa na lengo la kukifanya kiwe rahisi kusomwa, nikaelezea pia taabu niliyoipata katika kujieleza kwa hadhira mbili tofauti, yaani wa-Afrika na wa-Marekani, kwa wakati mmoja.

Baada ya utangulizi huo, kilifuata kipindi cha masuali, na hapo ndipo tulipotumia muda wetu mwingi. Kwa vile wanafunzi hao huwa wamekisoma kitabu, wanakuwa na masuali mengi ya kunitaka nifafanue vipengele mbali mbali. Maongezi yetu yalidumu kwa zaidi ya saa tatu. Nimeongea na makundi mbali mbali ya wadau hapa Marekani kuhusu kitabu hiki, lakini leo imekuwa ni rekodi, kwa maana ya kutumia muda mrefu namna hii.

Mkutano wa leo tulifanyia Mount Olivet Conference and Retreat Center, mwendo wa nusu saa tu kutoka Northfield ninapoishi. Ni kituo chenye ukumbi wa mikutano na vyumba vya kulala. Vyakula vinandaliwa hapa pia. Picha mbili zifuatazo nilipiga wakati wa chakula cha mchana.



No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...