Friday, January 20, 2012

Kitabu cha m-Tanzania Kuhusu Usimamizi wa Fedha

Hatimaye, nimejipatia na kusoma nakala ya kitabu kiitwacho Taking Control of Your Money, kilichoandikwa na Juanita Puja Kilasara. Huyu ni binti m-Tanzania ambaye amejipambanua katika fani ya uhasibu na masuala ya fedha kwa ujumla. Habari za kitabu chake hiki niliziona kwanza katika tovuti ya wavuti, kwani kwenye ukurasa wa mbele pana sehemu inayotangaza vitabu vya wa-Tanzania.

Kitabu hiki kinaeleza kwa njia rahisi masuala mbali mbali ya kuzalisha fedha na matumizi ya fedha kwa namna ya kumsaidia mtu kuwa mwangalifu na kumfanya asonge mbele kimaisha. Kuna mawaidha mengi ya manufaa, hata katika masuala ya kuanzisha na kuendesha biashara na shughuli zingine za kujipatia kipato.

Kwa kuzingatia mabadiliko ya dunia, hasa katika tekinolojia ya mawasiliano, kitabu hiki kinatoa dokezo mbali mbali za kumwezesha mtu kutumia fursa zilizopo mtandaoni. Ingekuwa vijana wa Tanzania wana mazoea ya kusoma vitabu, wakawa wanasoma vitabu kama hiki, hata suala la ajira wangeliangalia kwa upeo tofauti, kwani ni aina ya kitabu kinachofungua milango ya ujasiriamali. Nina jambo moja tu la kushauri, kwamba ingefaa kitafsiriwe pia katika ki-Swahili.

Unaweza kumsikiliza Juanita akiongelea kitabu chake hapa. Kitabu hiki kinapatikana sehemu mbali mbali, kama ilivyoelezwa hapa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...