Showing posts with label Saudi Arabia. Show all posts
Showing posts with label Saudi Arabia. Show all posts

Saturday, February 11, 2017

Ninamwazia Mwandishi Alexander Pushkin

Kwa wiki yapata mbili, nimekuwa nikimwazia sana Alexander Pushkin, mwandishi maarufu wa u-Rusi. Nimefahamu tangu ujana wangu kuwa wa-Rusi wanamwenzi kama baba wa fasihi ya u-Rusi. Miaka ya baadaye, nilikuja kufahamu kuwa Pushkin alikuwa na asili ya Afrika, na kwamba hata katika baadhi ya maandishi yake aliongelea suala hilo.

Nilisoma makala za profesa moja wa Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, nikafahamu zaidi suala hilo. Katika kufuatilia zaidi, niliguswa na mengi, hasa maelezo juu ya kipaji cha Pushkin cha ajabu katika matumizi ya lugha ya ki-Rusi na ubunifu wake, na pia jinsi alivyokufa. Aliuawa katika ugomvi akiwa na umri wa miaka 37 tu.


Siku kadhaa zilizopita, nilitoa mhadhara katika darasa la Nu Skool, kuhusu umuhimu wa Afrika na wa-Afrika katika historia ya ulimwengu. Kati ya watu maarufu wenye asili ya Afrika ambao niliwataja kwa mchango wao ni Antar bin Shaddad wa Saudi Arabia na Pushkin. Antar bin Shaddad ni mshairi aliyeishi kabla ya Mtume Muhammad, na ambaye tungo zake zinakumbukwa kama hazina isiyo kifani katika lugha ya ki-Arabu. Pushkin ni hivyo hivyo; wa-Rusi wanakiri kuwa umahiri wake katika kuimudu lugha yao hauna mfano.

Kutokana na hayo nimekuwa na hamu ya kumsoma Pushkin, nikakumbuka kuwa nilishanunua kitabu chake maarufu, Eugene Onegin, ambayo ni hadithi iliyoandikwa kishairi. Ninajiandaa kuisoma.

Wednesday, January 18, 2017

Vitabu Nilivyojipatia Leo

Leo, baada ya wiki nyingi kidogo, nimeona nirejee tena kwenye mada ambayo nimekuwa nikiiandikia tena na tena katika blogu hii. Ni juu ya vitabu ninavyojipatia, iwe ni kwa kununua, au kwa namna nyingine.

Leo asubuhi, kama kawaida, nilienda chuoni St. Olaf kufundisha. Nilipoingia katika jengo la maktaba, ambamo pia ni makao ya idara yangu ya ki-Ingereza, nilipita kwenye meza ambapo huwekwa vitabu na makabrasha kwa ajili ya yeyote anayehitaji. Niliona meza imejaa vitabu kuliko siku nyingine yoyote iliyopita, nikaamua kuviangalia.

Niliona kuwa vyote vilikuwa vitabu vya taaluma, hasa masuala ya wanawake na jinsia. Niliamua kujichukulia vitatu, baada ya kuangalia ndani na kuona maelezo ya vitabu hivi. Kitabu kimojawapo ni Sex & Power, kilichotungwa na Susan Estrich. Niliona maelezo kuwa mwandishi alikuwa profesa wa sheria katika Chuo Kikuu cha Harvard na baadaye profesa wa sheria katika Chuo Kikuu cha California ya Kusini. Ameandika vitabu kadhaa na makala mbali mbali. Alikuwa mwanamke wa kwanza kuwa rais wa Harvard Law Review. Huenda msomaji wa taarifa hii utakumbuka kuwa hiki ni cheo ambacho Barack Obama aliwahi kushika. Kutokana na mada ya kitabu, na orodha ya sura zake niliona kuwa kitabu hiki kitanielimisha sana kuhusu nafasi ya wanawake katika jamii.

Kitabu cha pili kilichonivutia kwa namna ya pekee ni Globalization: The Making of World Society, ambacho kimetungwa na Frank J. Lechner. Kama tunavyofahamu, mada ya utandawazi inavuma sana miongoni mwa wanataaluma, wanasiasa, na jamii kwa ujumla. Hata hivi, mitazamo kuhusu nini maana ya utandawazi, chimbuko lake, faida na hasara zake, ni masuala ambayo yanajadiliwa na yamegubikwa na utata.

Mimi mwenyewe, kwa miaka kadhaa, nimetafakari suala la utandawazi, nikilihusisha na tofauti za tamaduni. Nimewahi hata kuendesha warsha kadhaa, nchini Tanzania, katika miji ya Arusha, Dar es Salaam, na Tanga. Kwa hivi, nilipokiona kitabu cha Globalization: The Making of World Society, nilikuwa na hamu ya kukisoma. Hiki kitaongeza idadi ya vitabu vyangu kuhusu utandawazi.

Kitabu cha tatu, Behind the Veil in Arabia: Women in Oman, kilichoandikwa na Unni Wikan, kilinivutia pengine zaidi ya hivi vingine. Nilipoona jina la kitabu hiki, nilikumbuka mara majina ya vitabu vingine, kama vile Beyond the Veil, cha Fatima Mernissi wa Morocco. Suala la wanawake katika nchi za ki-Arabu limeshika nafasi ya pekee kichwani mwangu kutokana na kozi niliyoanzisha na ninaifundisha, "Muslim Women Writers."

Simaanishi, na mtu asidhani, kwamba wa-Arabu wote ni wa-Islam, bali kuna suala la jinsi utamaduni unavyoingiliana na dini kiasi kwamba pamoja na tofauti za dini, kuna mambo kama mila, desturi, na lugha, ambayo yanawaungamisha wa-Arabu.

Katika kufundisha kozi ya "Muslim Women Writers" imedhihirika kuwa vazi kama hijab ni suala la utamaduni zaidi kuliko dini. Qur'an inasema wanawake wajisitiri na wainamishe macho, lakini haisemi wavae nini. Hili ni suala la kila utamaduni, na ndio maana mavazi ya wanawake wa ki-Islam katika tamaduni mbali mbali yanahitilafiana.

Maktaba yangu imetajirika leo kwa kuongezewa vitabu hivi muhimu. Ni raha iliyoje kujipatia hazina kubwa namna hii bila gharama yoyote kwa upande wangu.

Thursday, June 11, 2015

Kesi ya Raif Badawi: Mwanablogu wa Saudi Arabia

Raif Badawi ni mwanablogu wa Saudi Arabia ambaye anafahamika sana duniani kutokana na kuhukumiwa kifungo cha miaka kumi gerezani na viboko 1000. Alihukumiwa kwa kile kilichoitwa kuitukana dini ya u-Islam. Amekaa gerezani miaka miwili na tayari alishapigwa viboko 50 nje ya msikiti mjini Jeddah. Adhabu hiyo si nyepesi; inaweza kusababisha kifo.

Watu wengi duniani wanalaani hukumu hiyo. Wengi hawaoni ni kwa vipi Raif Badawi ameutukana u-Islam. Wengi wamechukizwa na hukumu hiyo kwa kuwa ni hujuma dhidi ya uhuru wa kutoa mawazo.

 Mawazo ya Raif Badawi yaliyosababisha hukumu dhidi yake ni ya kawaida sana kwa vigezo vyetu wa-Tanzania na wengine duniani. Lakini wahusika nchini Saudi Arabia wameendelea kusisitiza kuwa Raif Badawi anastahili hukumu hiyo. Kuna tetesi kuwa huenda akashtakiwa upya ili apewe hukumu kali zaidi, kukatwa kichwa, hukumu ambayo hutekelezwa sana Saudi Arabia.

Kesi ya Raif Badawi imeibua masuala ya ukiukwaji wa haki za binadamu nchini Saudi Arabia. Kuna mengi yanayoongelewa. Kwa mfano, ni marufuku Saudi Arabia kutoa mawazo yanayopingana na yale ya watawala na viongozi wa dini. Ni marufuku kwa watu wasio wa-Islam kujenga nyumba za ibada zao, kama vile makanisa, katika ardhi ya Saudi Arabia. Ni marufuku kuhubiri dini tofauti na u-Islam. Ni marufuku kwa wanawake kuendesha gari. Ni marufuku kwa wanawake kusafiri bila kibali cha mume au ndugu wa kiume.

Kuna kampeni kubwa sehemu mbali mbali duniani kulaani hukumu dhidi ya Raif Badawi. Sisi wanablogu wa Tanzania tunasimama wapi? Ni vema kukumbushana kuwa ukiona mwenzako ananyolewa, wewe tia maji.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...