Showing posts with label sanaa. Show all posts
Showing posts with label sanaa. Show all posts

Saturday, March 11, 2017

Mashairi ya Robert Frost

Leo nina jambo la kusema, kuhusu mashairi ya Robert Frost, ambayo nimekuwa nikiyasoma sambamba na kazi zingine za fasihi au taaluma. Ni mazoea yangu kusoma kiholela, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.

Mashairi ya Frost ninayoongelea yamo katika kitabu kiitwacho Robert Frost: Selected Poems, ambacho binti yangu alininunulia. Wakati ule, nilijitahidi kuyasoma, lakini ninayafurahia zaidi wakati huu, labda ni kwa kuwa akili yangu imetulia kuliko wakati ule.

Leo, kwa mfano, nimesoma shairi liitwalo "The Black Cottage." Tunaelezwa kuhusu watu wawili wanavyoijongea nyumba ndogo iliyofichika nyuma ya miti na nyasi mbali na barabara. Wanaikaribia na kuchungulia ndani. Mmoja wao, ambaye ni mchungaji, anafahamu habari za nyumba hii ambayo sasa haina watu.

Anamweleza mwenzake kuwa bibi kizee aliyeishi humu alifariki, na watoto wake, wote wanaume, wanaishi mbali, ila hawataki kuiuza nyumba wala chochote kilichomo. Walipangia kuwa wanakuja mara moja kwa mwaka, lakini mwaka huu hawajaja. Baba yao alikufa katika vita ya wa-Marekani wenyewe kwa wenyewe ("Civil War"), eneo la Fredericksburg au Gettysburg.

Sehemu kubwa inayobaki ya shairi hili inaelezea fikra za marehemu bibi kizee kuhusu masuala mbali mbali yatokanayo na vita ile, kama vile malengo ya vita, na usawa wa binadamu. Mchungaji anaonesha kuwa fikra na mitazamo ya bibi kizee yule ilikuwa ya pekee na pia ya kutatanisha.

Hata mimi siwezi kusema nimeelewa vizuri mtazamo wa bibi kizee huyu, ingawa nimelisoma shairi hili na kulirudia. Itanibidi nilisome tena na tena. Vile vile, nimeona itakuwa jambo jema kufanya utafiti ili nione kama kuna tahakiki za shairi hili ambazo zimechapishwa. Daima, hii njia bora ya kujipanua upeo kuhusu utungo wa fasihi.

Kama kawaida, Frost anaandika kwa mtindo unaokufanya msomaji ujisikie kuwa anafanya nawe maongezi ya kina. Unawajibika kumsikiliza huku ukitafakari asemayo. Kusoma shairi hili, kama mashairi mengine ya Frost kunahitaji akili  tulivu.

Jambo moja linalonivutia katika kusoma mashairi haya ya Frost ni kuwa ninasoma alichoandika yeye mwenyewe, sio tafsiri. Ni bahati kuwa na uhusiano wa moja kwa moja na mwandishi namna hiyo. Ninakuwa na fursa kamili ya kuguswa na umahiri wa mwandishi katika kuelezea mambo, kuanzia hisia na fikra zake na za wahusika, hadi vitu na mazingira.

Sunday, February 19, 2017

Utungo wa Pushkin, "Eugene Onegin," Ni Mtihani

Siku chache zilizopita, niliandika katika blogu hii kuwa nilikuwa ninajiandaa kusoma Eugene Onegin, utungo maarufu wa Alexander Pushkin. Nilianza hima, na sasa ninaendelea.

Nilifahamu tangu zamani kuwa Pushkin alikuwa ameandika tungo zingine pia. Nilifahamu kuwa Eugene Onegin ndio utungo wake maarufu kuliko zingine. Nilifahamu kuwa utungo huo ni riwaya iliyoandikwa kwa mtindo wa kishairi.

Nilidhani kuwa ningesoma Eugene Onegin bila matatizo, kama ninavyosoma kazi za waandishi wengi. Baada ya kuanza kuusoma, na ninavyoendelea kusoma, ninajikuta kama vile niko katika mtihani. Eugene Onegin si rahisi kama nilivyodhani.

Pushkin ameusuka utungo wake kwa umahiri mkubwa, akitumia mbinu mbali mbali za kisanii, na pia taarifa za wasanii wa mataifa mbali mbali, kuanzia zama za kale, hadi zama zake. Humo kuna majina ya watunzi wa mataifa mbali mbali, kama vile Theocritus, Juvenal, Ovid, Racine, Chateaubriand, Lord Byron, pamoja na waandishi na waigizaji kadha wa kadha wa u-Rusi, wa wakati wa Pushkin na kabla yake, ambao hata mimi sikuwa ninawafahamu.

Kwa kufuatilia dondoo, dokezo, na maelezo yaliyomo, ninajifunza mambo mengi mapya. Mtindo huu wa Pushkin unanikumbusha ushairi wa Derek Walcott. Kusoma mashairi yake ni chemsha bongo. Unajikuta ukipelekwa sehemu nyingi katika historia, ikiwemo historia ya fasihi, sanaa, na falsafa.

Tafsiri ya Eugene Onegin ninayosoma ni ya Hofstadter. Katika kupambana na tafsiri yake, nimefikia uamuzi kuwa nikimaliza kusoma tafsiri, nisome tafsiri nyingine angalau moja ya mtu tofauti. Lakini ukweli utabaki kuwa ingekuwa bora zaidi kama ningekuwa ninakifahamu ki-Rusi, nikajisomea mwenyewe alichoandika Pushkin. Kama taaluma inavyotufundisha, hakuna tafsiri ambayo inaweza kuwa sawa na utungo unaotafsiriwa.

Mtu unaweza kujiuliza: Kwa nini ninajipitisha katika mtihani huu wa kusoma Eugene Onegin, badala ya kusoma vitabu rahisi? Jibu langu ni kuwa chemsha bongo ni muhimu kwa afya ya ubongo, kama vile mazoezi ya viungo yalivyo muhimu kwa afya ya binadamu. Utungo kama Eugene Onegin, kwa jinsi ulivyosheheni utajiri wa fikra na kumbukumbu za aina mbali mbali, ni njia bora ya kutajirisha akili. Nitajisikia mwenye furaha nitakapoweza kusema nimeusoma na kuutafakari kwa makini utungo huu mashuhuri wa Pushkin.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...