Showing posts with label Makala. Show all posts
Showing posts with label Makala. Show all posts

Tuesday, May 30, 2017

Likizo Inaanza: Ni Kujisomea Vitabu na Kuandika

Tumemaliza muhula wa mwisho wa mwaka wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Tunamalizia kusahihisha mitihani na matokeo yatakuwa yamekamilika tarehe 5 Juni. Kuanzia pale tutakuwa na miezi mitatu ya likizo. Lakini kwetu waalimu, likizo si likizo, bali fursa ya kujisomea, kufanya utafiti, na kuandika, bila kuhusika na ufundishaji darasani.

Mpango wangu kwa likizo hii ni kutumia wiki sita za mwanzo katika kujisomea vitabu na kuandika, halafu wiki sita zitakazofuata nitafundisha kozi ya fasihi ya Afrika. Kufundisha kipindi hiki cha likizo ni jambo la hiari. Mwalimu anatangaza kozi anayotaka kufundisha na wanafunzi wanaohitaji wanajisajili. Wanafunzi huwa wachache. Ni fursa nzuri kwa mwalimu kujaribisha mambo mapya.

Wakati huu ninavyoandika ujumbe huu, ninafadhaika katika kuamua nisome vitabu vipi. Maktaba yangu ina vitabu vingi ambavyo sijavisoma. Kwa likizo hii, nimewazia nisome tamthilia za William Shakespeare, au George Bernard Shaw, au Sean O'Casey, au Anton Chekhov, au riwaya za Orhan Pamuk ili niweze kupata mwanga juu ya huyu mwandishi maarufu aliyejipatia tuzo ya Nobel mwaka 2006 na ambaye nimekuwa nikimtaja katika blogu hii. Nimewazia pia kusoma hadithi fupi na riwaya za Ernest Hemingway, zile ambazo sijazisoma.

Ningependa kuonja uandishi wa Svetlana Alexievich, ambaye nimemgundua wiki iliyopita. Nilijipatia kitabu chake, Secondhand Time: The Last of the Soviets, cha bure, hapa chuoni. Sikuwa ninamfahamu mwandishi huyu mwanamke m-Rusi, ambaye alipata tuzo ya Nobel mwaka 2015, "for her polyphonic writings, a monument to suffering and courage in our time," kwa mujibu wa kamati ya tuzo.

Wafuatiliaji wa nadharia ya fasihi wanafahamu kuwa dhana ya "polyphony" katika fasihi ilifafanuliwa vizuri na mwanafalsafa na mhakiki m-Rusi Mikhail Bakhtin akimaanisha sauti na mitazamo mbali mbali inayounda kazi ya fasihi. Nimefurahi kumfahamu mwandishi huyu mwanamke kutoka u-Rusi. Amenifanya nimkumbuke mwandishi mwanamke m-Rusi, Anna Akhmatova, mshairi maarufu. Nina dukuduku ya kujua kama waandishi hao wawili wanaweza kulinganishwa.

Hakuna kazi ya fasihi inayozuka katika ombwe. Inatokana na jadi fulani na mfumo mpana wa kazi za fasihi, na kazi yoyote mpya inachangia jadi na mfumo wa fasihi. Dhana hiyo ilielezwa vizuri na T.S. Eliot, mshairi na mwanafasihi maarufu, katika insha yake, "Tradition and the Individual Talent."

Ninapowazia waandishi wa fasihi wanawake waliopata tuzo ya Nobel, majina yanayonijia akilini hima ni Sigrid Undset wa Norway, Nadine Gordimer wa Afrika Kusini, Toni Morrison wa Marekani, Alice Munro wa Canada, na Doris Lessing wa Zimbabwe na Uingereza. Ninashawishika na wazo la kutunga na kufundisha kozi juu ya maandishi ya wanawake waliopata tuzo ya Nobel katika fasihi.

Papo hapo, katika likizo hii ninataka kuendelea kuandika makala ambayo nilianza kuiandika miezi kadhaa iliyopita, "Folkloric Discourse in Ama Ata Aidoo's The Dilemma of a Ghost." Azma ya kuendelea kuandika makala hii ni kubwa, kwani ninaamini kuwa hii itakuwa makala bora kabisa.

Hizi ndizo ndoto zangu. Ni ajenda kubwa, kielelezo cha namna akili yangu inavyohangaika kutokana na kutambua kuwa vitu vy kusoma na kuandika ni vingi kuliko muda unavyoruhusu. Sitaweza kufanya yote ninayowazia kwa likizo hii, lakini si neno. Nitatumia muda wangu vizuri na kufanya nitakachoweza.

Saturday, April 23, 2016

Ujumbe Mzuri Kutoka kwa Mwanafunzi

Leo nimepata ujumbe mzuri kutoka kwa m-Tanzania ambaye simfahamu. Amejitambulisha kwamba alipokuwa mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule ya sekondari ya Namtumbo, alisoma mwongozo wangu juu ya Things Fall Apart na Song of Lawino. Nimefurahi kusikia habari hii ya kusomwa maandishi yangu sehemu ya mbali kama Namtumbo ambayo iko njiani baina ya Songea na Tunduru.

Inawezekana kuwa huyu mtu alimaanisha kijitabu changu ambacho kilikuwa na mwongozo wa Things Fall Apart na The African Child, ambao niliuelezea katika blogu hii. Ni hivi karibuni tu nimechapisha mwongozo wa Song of Lawino. Si hoja, ili mradi watu wasome ninayoandika.

Mimi ni mwalimu, na dhana yangu ya ufundishaji ni pana. Inajumlisha ninavyofundisha darasani, ninavyoandika na kuchapisha vitabu na makala, ninavyoblogu, ninavyoshiriki matamasha ya vitabu na utamaduni, ninavyoongea na watu ana kwa ana, kama vile mitaani, ninavyoendesha warsha, ninavyoshiriki mijadala mitandaoni, na kadhalika.

Mwalimu si mtu wa kuficha mawazo na mitazamo yake. Hachelei kujieleza. Ni wajibu wake. Mwalimu wa Chuo kikuu ana wajibu wa pekee wa  kufanya utafiti na kuandika vitabu na makala ili kuchangia taaluma. Anawajibika kwa wanataaluma wenzake na pia kwa jamii. Huu wajibu mpana ndio unanifanya nijishughulishe na jamii katika nyanja kama magazeti, blogu, mitandao. Miongozo ninayoandika juu ya kazi za fasihi ni sehemu ya azma hii ya kuisogeza taaluma katika jamii.

Mwongozo wangu wa Things Fall Apart alioongelea huyu mtu inaonekana ni wa mwanzo mwanzo. Nilifanya juhudi kuuboresha. Uthibitisho wa ubora wake ni kwamba unapendekezwa kwa wanafunzi hapa Marekani wanaosoma Things Fall Apart, kama ilivyofanywa na Chuo Kikuu cha Cornell. Ninafurahi kwamba ninatoa mchango wangu kwa namna hiyo, kuanzia Marekani hadi Namtumbo.

Thursday, December 3, 2015

Kuhusu Kublogu

Nimekuwa mwanablogu tangu mwaka 2008. Ninaendesha blogu hii ya Hapa Kwetu na nyingine ya ki-Ingereza. Kublogu kuna mambo mengi. Kublogu kunanipa fursa ya kujieleza kwa uhuru. Hili ni jambo la msingi, kama alivyoelezea mwanablogu Christian Bwaya.

Lakini kublogu kuna matokeo yenye manufaa. Kumeniwezesha kuwafikia watu mbali mbali ambao wanatembelea blogu zangu. Siwezi kujua wanapata ujumbe gani katika maandishi yangu. Kama taaluma inayotufundisha, hili ni suala tata.

Ujumbe wa andiko ni zao la kazi anayofanya msomaji juu ya andiko. Na kwa kuwa wasomaji wana akili zinazotofautiana, na wana nidhamu na uzoefu tofauti wa kusoma, kila mmoja anaibuka na ujumbe tofauti, kwa kiwango kidogo au kikubwa.

Niliwahi kuelezea kwa nini ninablogu, lakini sidhani kama nilikuwa na majibu ya uhakika. Baadaye, katika kutafakari suala hili, nilifikia hatua ya kutamka kwamba ninablogu kwa ajili yangu mwenyewe. Labda huu ndio ukweli wa mambo.

Imani iliyojengeka katika jamii ni kuwa mwandishi anawaandikia wasomaji. Tumezoea kuona waandishi wakiulizwa wanamwandikia nani, nao wanaelezea walengwa wao. Jadi hii na imani hii imekosolewa kwa uhodari na Roland Barthes katika makala yake, "The Death of the Author."

Makala hii ya Barthes naona inaipa uzito hoja yangu kuwa ninapoblogu ninajiandikia mwenyewe. Sijui ni nani atasoma au anasoma ninachoandika. Kusema kwamba ninawaandikia wasomaji ni kama kuota ndoto. Ni kujiridhisha kwa jambo ambalo halina uhakika bali ni bahati nasibu. Nikisema ninajiandikia mwenyewe ninasema jambo la uhakika.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...