Tuesday, February 6, 2018

Mteja Anapokupigia Debe

Tarehe 3 Februari, nilipata ujumbe wa barua pepe kutoka kwa dada au mama ambaye amejitambulisha kwa jina la Cynthia, ila simjui. Ameandika kuulizia kitabu changu namna hii:

Hello,

I am planning a trip to Tanzania and someone recommended your book about cultural differences between Africans and Americans. How can I purchase your book? Thank you very much.

Kwa wasiojua ki-Ingereza, tafsiri yake ni hii:

Habari

Ninapanga safari ya kwenda Tanzania na mtu fulani alikipendekeza kitabu chako juu ya tofauti za tamaduni za wa-Afrika na wa-Marekani. Nitakinunuaje kitabu chako? Shukrani sana.

Kwa mwandishi, habari ya aina hii ni habari njema. Kwamba mtu fulani ambaye alitumia hela zake kununulia kitabu chako alikisoma akaridhika au kufurahi kiasi cha kukipendekeza kwa mwingine, si jambo jepesi. Mtu anapopendekeza kitu kwa mwingine namna hii, anajiweka katika hali ya kueleweka vibaya, iwapo kile anachopendekeza hakitamridhisha huyu mwingine. Tunapendekeza vitu kwa marafiki zetu tukiwa na uhakika na hicho tunachopendekeza.

Sisi wote ni wateja wa hiki au kile, iwe ni vitu au huduma. Muda wote tunawashawishi wenzetu wakanunue kitu fulani au wanapohitaji huduma, tunawaelekeza sehemu ambayo tunaiamini. Tunapopendekeza kitu au huduma tunatoa tamko kuhusu ubora wa kile tunachopendekeza. Nimekuwa nikielezea masuala haya katika blogu hii.

Muda wote sisi binadamu tunafanya hii shughuli ya kupiga debe bila malipo. Tunafanya hiki kibarua kisicho na malipo bila hata kujitambua. Ni sehemu ya mazungumzo yetu na marafiki au watu wengine. Mwenye kuuza bidhaa au kutoa huduma anafaidika bila kutumia hela kulipia matangazo.

Hayo ni baadhi ya mawazo yangu wakati huu ninapotafakari suala la huyu mpiga debe asiyejulikana ambaye amekipendekeza kitabu changu kwa mtu huyu aitwaye Cynthia, ambaye naye simjui. Nimemjibu Cynthia nikamwambia sijui mahali alipo, lakini kitabu anaweza kukipata mtandaoni.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...