Saturday, May 9, 2015

Neno Jingine Kuhusu Uandishi na Uchapishaji

Mimi ni mwandishi wa vitabu. Ninaandika vitabu vya tahakiki ya fasihi, juu ya masuala ya jamii, fasihi simulizi, na masuala ya athari za tofauti za tamaduni, hali halisi ya uandishi wa vitabu, mbinu za kujichapishia vitabu. Naandika kuhusu utangazaji na uuzaji wa vitabu, na kuhusu hali halisi ya usomaji wa vitabu Tanzania na ughaibuni.

Ninatoa ushauri kwa wengine kupitia blogu hii na katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Yeyote anayetaka kujifunza kutoka kwangu anaweza kufanya hivyo, bila kipingamizi. Lakini namtegemea aanze kwa kusoma nilichoandika, mawasiano ya ziada yafuate baadaye.

Siwezi kuwasiliana na kila mtu na kuongelea hata yale ambayo tayari nimeshaandika. Nina kazi yangu na majukumu mengine kila siku. Nikisema niwasiliane na kila mtu hata kwa yale ambayo nimeshaandika, nitashindwa kufanya kazi zangu zinazoniwezesha kuishi, kulipia nyumba, matibabu, na mahitaji mengine.

Labda niache kazi niliyoajiriwa kufanya, nijiajiri kama mshauri. Ikiwa hivyo, kila anayetafuta ushauri kwangu atatakiwa alipie. Ndivyo wanavyofanya watoa ushauri. Nami ujuzi na uzoefu ninao, kama inavyodhihirika katika taarifa ninazoandika katika blogu hii ya hapakwetu na blogu ya ki-Ingereza.

Suali ambalo ninaulizwa tena na tena ni kuhusu mikakati ya kuchapisha miswada. Ni wazi kuwa watu bado wana fikra za jadi kuhusu uchapishaji. Nawashauri waondokane na fikra za kuwateemea wachapishaji. Badala yake, waingie katika ulimwengu wa kujichapishia vitabu.

Wafanyeje au waanzie wapi ndio aima ya masuala ninayoongelea katika blogu na katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Kama mtu anataka mafanikio, ni lazima awekeze katika elimu inayohusiana na shughuli anayotaka kufanya. Kununua vitabu na kuvisoma ni uwekezaji, sawa na uwekezaji wa kununua trekta ya kilimo au nyavu za kuvulia samaki.

 Suala la kujichapishia vitabu ni tata, hasa kwa upande wa wanataaluma. Jadi iliyopo katika kuchapisha vitabu vya kitaaluma au makala za kitaaluma imekuwa ya kuzingatia umuhimu wa wanataaluma tofauti na mwandishi kufanya uhakiki na udhibiti wa andiko kabla ya kuchapishwa. Ninapangia kuandika zaidi kuhusu suala hilo.  

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...