Tuesday, May 26, 2015

Mwaliko Chuo Kikuu cha Winona

Nimepata mwaliko kutoka Chuo Kikuu cha Winona, Minnesota, kwenda kutoa mhadhara tarehe 23 Juni. Huu utakuwa ni mchango wangu katika semina ya mafunzo kwa wanafunzi kutoka sehemu mbali mbali itakayofanyika Juni 17-27. Kama ilivyo kawaida yangu, nimeona niweke kumbukumbu hapa.

Mafunzo haya yatalenga kuwaandaa wanafunzi hao kwa masomo ya juu, waweze kuifahamu hali halisi ya maisha ya chuoni na taratibu za taaluma, waweze kujijengea hali ya kujitambua na uwezo wa uongozi.

Mratibu wa mafunzo, Alexander Hines, ambaye anafahamu kiasi shughuli zangu,  aliniambia tuangalie ni kipi kati ya vitabu vyangu viwili kitafaa zaidi kwa semina hii: Africans and Americans: Embracing Cultural Differences au Matengo Folktales. Nilishauri kwamba hicho cha pili kingeendana vizuri zaidi na dhamira kuu ya semina.

Tumekubaliana. Tumekubaliana nikaelezee ni nini tunaweza kujifunza kutokana na tamaduni za jadi za Afrika katika masuala haya ya kujitambua, falsafa ya maisha, na uongozi katika dunia ya leo na kesho.

Kama ilivyo kawaida yangu, huwa napokea mialiko ya kutoa mchango wa mawazo kufuatana na mahitaji ya wale wanaonialika. Itabidi nitafakari na kuandaa mawazo yatakayotoa mchango unaohitajika katika semina. Wazo la kutumia kitabu cha Matengo Folktales kama msingi ni wazo muafaka, kwani masimulizi haya ya jadi yanathibitisha jinsi wahenga wetu walivyoyatafakari masuala muhimu ya maisha, mahusiano, na mengine yanatuhusu leo na yataendelea kuwa muhimu daima.
 

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...