Showing posts with label bodi. Show all posts
Showing posts with label bodi. Show all posts

Friday, August 11, 2017

Mkutano wa Bodi ya Rochester International Association

Tarehe 8 Agosti, nilikwenda Rochester, Minnesota, kuhudhuria mkutano wa bodi ya Rochester International Association (RIA). Tunakutana mara moja kwa mwezi. Katika ajenda ya tarehe 8, yalikuwepo mambo yanayonihusu moja kwa moja, ambayo ninapenda kuyaelezea hapa.

Moja ni kuwa wanabodi tuliohudhuria tuliulizwa na rais wa bodi, Brian Faloon, iwapo tutapenda kuendelea kuwa wajumbe mwaka ujao. Wote tulikubali. Mimi kama mwanabodi mpya kuliko wote, nilivutiwa na jinsi wajumbe walivyo na moyo wa kujitolea. Nilikubali kwa sababu ninathamini mchango wa RIA katika jamii. Kwa upande wangu, kutumikia RIA kumeniwezesha kufahamika katika mji wa Rochester. Kwa mfano, kupitia RIA niliweza kutoa mhadhara chuo kikuu cha Minnesota Rochester.

 Pili ni kuwa RIA imesisitiza kuafiki pendekezo nililotoa siku zilizopita la kuonyesha filamu ya Papa's Shadow mjini Rochester. Bodi ilipendekeza kwamba onesho lifanyike kupitia maktaba ya Rochester. Tutafuatilia, ili filamu ionyeshwe hivi karibuni.

Jambo jingine ni kuwa mwanabodi Kristin Faloon aliwaeleza wanabodi kuhusu mhadhara niliotoa katika kikuu cha Winona, ambao yeye na mumewe Brian walihudhuria. Sikutegemea Kristin angeongelea tukio lile, lakini ilionekana wazi kuwa walifurahishwa na mhadhara ule, akasema kuwa walijifunza mengi. Kwa kuzingatia hadhi ya Brian na Kristin katika jamii, maoni yao yana uzito mkubwa. Nimewaandikia ujumbe kwamba sitawaangusha katika mihadhara ya baadaye.

Zaidi ya hayo, mkutano wa RIA umenifungua macho kuhusu taasisi zinazofanya shughuli zinazofanana na zangu katika kuendeleza maelewano baina ya watu wa tamaduni mbali mbali. Mbali ya Diversity Council-Rochester, ambayo niliifahamu, niligundua pia kuwa kuna kitengo katika Mayo Clinic kinachoshughulika na masuala ya kujenda na kustawisha mahusiano baina ya watu wa tamaduni mbali mbali. Ninatarajia kuwa tutakuwa na fursa ya kushirikiana kwa namna moja au nyingine.

Thursday, April 27, 2017

Bendera ya Tanzania Kupepea Rochester, Minnesota

Kwa mara ya kwanza bendera ya Tanzania itapeperushwa katika tamasha la kimataifa mjini Rochester, Minnesota, tarehe 29 mwezi huu. Hili ni tamasha linaloandaliwa na Rochester International Association (RIA) kila mwaka. Nimewahi kuelezea kuhusu tamasha hili katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza.

Napenda kuelezea mchakato uliowezesha bendera ya Tanzania kupewa hadhi hiyo. Mwaka jana wa-Kenya wawili, Olivia Njogu na Kennedy Ombaye, ambao ni wanabodi wa RIA, waliniambia kuwa wangependa nijiunge nao. Niliguswa na wazo lao, nikaafiki. Waliwasilisha ujumbe kwa mwenyekiti wa bodi, Brian Faloon, nami nikawasiliana naye kumthibitishia utayari wangu wa kujiunga. Wazo lilipitishwa na bodi, nami nikajiunga.

Wiki chache zilizopita, bodi ilianza kujadili mipango ya tamasha la kimataifa kwa mwaka huu. Wakati suala la bendera lilipojadiliwa, mwanabodi Olivia Njogu aliniambia kuwa iwepo bendera ya Tanzania. Kwa kuwa sikuelewa utaratibu wa bendera ukoje, Olivia na wanabodi wengine walinihakikishia kuwa sitahitaji kuileta bendera, bali wataipata kwa muuzaji. Nilifahamu kuwa utaratibu wa tamasha ni kuwa linapoanza, panakuwa na maandamano ya watu wakiwa wamebeba bendera za nchi mbali mbali.

Mwaka jana niliposhiriki tamasha hili, nilikuwa na bendera ya Tanzania, ambayo nilikuwa nimeinunua mwaka juzi, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Lakini kwa kuwa nilikuwa bado mgeni katika tamasha hili, sikuwa nimefanya utaratibu wa kuijumlisha katika maandamano ya bendera. Niliitandaza kwenye meza yangu, kama inavyoonekana pichani hapa kushoto.

Ninawashukuru tena wa-Kenya kwa urafiki na ukarimu ambao wamenionyesha tangu nilipokwenda nchini kwao kufanya utafiti, kuanzia mwaka 1989, hadi miaka yote niliyoishi huku Marekani. Jambo hili nimekuwa nikilitaja katika blogu hii.

Sunday, November 13, 2016

Nimeteuliwa Kwenye Bodi ya Rochester International Association

Mwezi huu nimeteuliwa kujiunga na bodi ya Rochester International Association, ambayo makao yake ni mjini Rochester, Minnesota. Rochester International Association inashughulika na program mbali mbali za kujenga mahusiano mema miongoni mwa watu wa mataifa na tamaduni mbali mbali.

Moja ya programu hizo ni tamasha liitwalo World Festival, linalofanyika kila mwaka. Nimewahi kushiriki tamasha hili mara mbili, nikaelezea habari zake katika blogu yangu ya ki-Ingereza, na blogu hii ya hapakwetu.

Shughuli za bodi ni za kujitolea. Kwa miaka yote niliyoishi hapa Marekani, nimejionea jinsi wa-Marekani wanavyozijali shughuli za kujitolea, nami nimekuwa nikishiriki shughuli za aina hiyo, kama vile katika programu zinazowapeleka wanafunzi Afrika. Kujitolea kwa manufaa ya jamii kunaleta faraja na furaha moyoni.

Kushiriki kwangu katika Rochester International Association kutaniwezesha kuchangia mawazo katika masuala ya tamaduni kama nilivyoyaelezea katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kwa bahati nzuri, baadhi ya wanabodi wa Rochester International Association wamesoma kitabu hiki na ndio maana wamenipokea kwa msisimko.

Kushiriki shughuli za Rochester International Association ni jambo la manufaa kwangu katika kujijenga katika shughuli zangu za kutoa ushauri ambazo ninafanya chini ya mwavuli wa kampuni ndogo ya Africonexion: Cultural Consultants. Vile vile ni fursa ya kuiwakilisha Tanzania na Afrika huku mbali Marekani.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...