Thursday, April 27, 2017

Bendera ya Tanzania Kupepea Rochester, Minnesota

Kwa mara ya kwanza bendera ya Tanzania itapeperushwa katika tamasha la kimataifa mjini Rochester, Minnesota, tarehe 29 mwezi huu. Hili ni tamasha linaloandaliwa na Rochester International Association (RIA) kila mwaka. Nimewahi kuelezea kuhusu tamasha hili katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza.

Napenda kuelezea mchakato uliowezesha bendera ya Tanzania kupewa hadhi hiyo. Mwaka jana wa-Kenya wawili, Olivia Njogu na Kennedy Ombaye, ambao ni wanabodi wa RIA, waliniambia kuwa wangependa nijiunge nao. Niliguswa na wazo lao, nikaafiki. Waliwasilisha ujumbe kwa mwenyekiti wa bodi, Brian Faloon, nami nikawasiliana naye kumthibitishia utayari wangu wa kujiunga. Wazo lilipitishwa na bodi, nami nikajiunga.

Wiki chache zilizopita, bodi ilianza kujadili mipango ya tamasha la kimataifa kwa mwaka huu. Wakati suala la bendera lilipojadiliwa, mwanabodi Olivia Njogu aliniambia kuwa iwepo bendera ya Tanzania. Kwa kuwa sikuelewa utaratibu wa bendera ukoje, Olivia na wanabodi wengine walinihakikishia kuwa sitahitaji kuileta bendera, bali wataipata kwa muuzaji. Nilifahamu kuwa utaratibu wa tamasha ni kuwa linapoanza, panakuwa na maandamano ya watu wakiwa wamebeba bendera za nchi mbali mbali.

Mwaka jana niliposhiriki tamasha hili, nilikuwa na bendera ya Tanzania, ambayo nilikuwa nimeinunua mwaka juzi, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Lakini kwa kuwa nilikuwa bado mgeni katika tamasha hili, sikuwa nimefanya utaratibu wa kuijumlisha katika maandamano ya bendera. Niliitandaza kwenye meza yangu, kama inavyoonekana pichani hapa kushoto.

Ninawashukuru tena wa-Kenya kwa urafiki na ukarimu ambao wamenionyesha tangu nilipokwenda nchini kwao kufanya utafiti, kuanzia mwaka 1989, hadi miaka yote niliyoishi huku Marekani. Jambo hili nimekuwa nikilitaja katika blogu hii.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...